Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endelea Kutarajia!

Endelea Kutarajia!

“Hata yakikawia, endelea kuyatarajia!”—HAB. 2:3.

NYIMBO: 128, 45

1, 2. Kwa muda mrefu waabudu wa Yehova wamekuwa na mtazamo gani?

KWA muda mrefu, waabudu wa Yehova wametazamia kutimizwa kwa unabii ulioongozwa na roho ya Mungu. Kwa mfano, Yeremia alitabiri kwamba Yuda lingeachwa ukiwa, na jambo hilo lilitekelezwa na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K. (Yer. 25:8-11) Isaya, aliyetabiri kwamba Yehova angewarudisha Wayahudi kutoka uhamishoni, alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wote wanaoendelea kumtarajia.” (Isa. 30:18) Mika pia alitoa unabii kuhusu watu wa Mungu, naye aliazimia hivi: “Nitaendelea kumtazamia Yehova.” (Mika 7:7) Kwa miaka mingi, watumishi wa Mungu walitarajia pia kutimizwa kwa unabii uliomhusu Masihi au Kristo.—Luka 3:15; 1 Pet. 1:10-12. *

2 Leo pia, watumishi wa Mungu wanaendelea kutarajia kutimizwa kwa unabii unaomhusu Masihi. Hivi karibuni, Yehova atatumia Ufalme wa Kimasihi kuondoa mateso ya wanadamu kwa kuwaharibu waovu na kuwaokoa watu wake kutoka katika ulimwengu huu unaotawaliwa na Shetani. (1 Yoh. 5:19) Kwa hiyo, acheni tuendelee kuwa macho na kukumbuka kwamba mwisho wa mfumo huu unakaribia sana.

3. Huenda wengine wakajiuliza swali gani baada ya kusubiri mwisho kwa miaka mingi?

3 Tukiwa watumishi wa Yehova, tunatamani sana kuona mapenzi ya Mungu ‘yakitendeka duniani kama ilivyo mbinguni.’ (Mt. 6:10) Hata hivyo, baada ya kutarajia mwisho wa mfumo huu kwa miaka mingi, huenda wengine wakajiuliza, ‘Je, bado kuna sababu za msingi za kuendelea kutarajia?’ Acheni tuone.

KWA NINI TUENDELEE KUTARAJIA?

4. Ni sababu gani ya msingi inayotuchochea tuendelee kukesha?

4 Biblia inatueleza waziwazi mtazamo tunaopaswa kuwa nao tunapokaribia mwisho wa mfumo huu wa mambo. Yesu aliwaambia wafuasi wake ‘waendelee kukesha.’ (Mt. 24:42; Luka 21:34-36) Hiyo pekee ni sababu nzuri ya kuendelea kutarajia mwisho wa mfumo huu. Tengenezo la Yehova limeweka mfano mzuri kuhusiana na jambo hilo. Mara nyingi machapisho yetu yametuhimiza tuendelee ‘kungoja na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova,’ huku tukitumaini kuishi katika ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu.—Soma 2 Petro 3:11-13.

5. Kwa nini ni muhimu kuendelea kukesha hasa katika siku zetu?

5 Ingawa Wakristo walioishi katika karne zilizopita walihitaji kuendelea kutarajia, jambo hilo ni muhimu hata zaidi kwetu. Kwa nini? Kwa sababu tunaishi wakati wa kuwapo kwa Kristo. Ishara ya kuwapo kwake imeonekana tangu mwaka wa 1914. Ishara hiyo, inayohusisha kuzorota kwa hali za ulimwengu na kuhubiriwa kwa habari njema duniani kote, inaonyesha kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 24:3, 7-14) Yesu hakutaja urefu wa siku za mwisho, hivyo ni muhimu sana kuwa macho na kuendelea kukesha.

6. Tunajuaje kwamba hali za ulimwengu zitazidi kuwa mbaya kadiri mwisho unavyokaribia?

6 Huenda ukajiuliza: Je, inawezekana maneno “umalizio wa mfumo wa mambo” yanarejelea wakati ujao hali za ulimwengu zitakapokuwa mbaya zaidi? Biblia inaonyesha kwamba uovu utaongezeka sana “katika siku za mwisho.” (2 Tim. 3:1, 13; Mt. 24:21; Ufu. 12:12) Kwa hiyo, tunaweza kutarajia kwamba hali za ulimwengu zitazidi kuzorota na kuwa mbaya zaidi.

7. Andiko la Mathayo 24:37-39 linaonyesha nini kuhusu hali za ulimwengu katika siku za mwisho?

7 Unafikiri hali za ulimwengu zitakuwa mbaya kiasi gani kabla ya “dhiki kuu”? (Ufu. 7:14) Kwa mfano, je, unafikiri kwamba kutakuwa na vita kwenye kila nchi, upungufu wa chakula kila mahali, na magonjwa katika kila familia? Chini ya hali hizo, basi hata wale wanaotilia shaka unabii wa Biblia wataamini kwamba unatimizwa. Hata hivyo, Yesu alisema kwamba watu wengi ‘hawangejali’ kuwapo kwake na wangeendelea na shughuli za kawaida za maisha mpaka itakapokuwa kuchelewa mno. (Soma Mathayo 24:37-39.) Kwa hiyo, Maandiko yanaonyesha kwamba hali za ulimwengu hazitakuwa mbaya kupindukia, kiasi cha kumfanya kila mtu aamini kwamba mwisho umekaribia.—Luka 17:20; 2 Pet. 3:3, 4.

8. Ni jambo gani ambalo wale wanaoendelea kukesha wanaona waziwazi?

8 Kwa upande mwingine, utimizo wa ishara ya Yesu unapaswa kuonekana waziwazi kwa wafuasi wake wanaotii himizo la ‘kuendelea kukesha.’ (Mt. 24:27, 42) Kuanzia mwaka wa 1914 na kuendelea, ishara hiyo imekuwa ikitimizwa kwa njia mbalimbali. Ni wazi kwamba sasa tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo,” yaani, kipindi kifupi kinachoongoza kwenye uharibifu wa mfumo huu mwovu.

9. Kwa nini tunapaswa kuendelea kutarajia mwisho wa mfumo huu?

9 Kwa nini tunapaswa kuendelea kutarajia mwisho? Kwa sababu tunamtii Yesu Kristo na tunatambua ishara ya kuwapo kwake. Matarajio yetu hayategemei kuamini jambo bila msingi, bali yanategemea msingi thabiti wa Kimaandiko unaotuchochea kuwa macho na kukesha, huku tukitazamia mwisho wa mfumo huu mwovu.

MPAKA WAKATI GANI?

10, 11. (a) Kwa nini Yesu aliwaambia wanafunzi wake ‘waendelee kukesha’? (b) Yesu aliwaambia wafuasi wake wafanye nini ikiwa mwisho usingekuja haraka kama walivyotarajia? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 14.)

10 Wengi wetu tumekuwa macho kiroho kwa miaka mingi. Hata hivyo, kupita kwa muda hakupaswi kudhoofisha azimio letu la kuendelea kukesha. Tunapaswa kuwa tayari Yesu anapokuja kutekeleza hukumu dhidi ya mfumo huu wa mambo. Kumbuka kwamba Yesu aliwahimiza hivi wafuasi wake: “Endeleeni kutazama, endeleeni kukesha, kwa maana hamjui wakati uliowekwa ni gani. Ni kama mtu anayesafiri kwenda ng’ambo, ambaye aliacha nyumba yake na kuwapa mamlaka watumwa wake, kila mmoja kazi yake, na kumwamuru mtunza-mlango aendelee kukesha. Kwa hiyo endeleeni kukesha, kwa maana hamjui bwana wa nyumba anakuja wakati gani, kama ni wakati wa jioni au katikati ya usiku au anapowika jogoo au asubuhi na mapema; ili anapofika kwa ghafula, asiwakute mkiwa mmelala usingizi. Lakini lile ninalowaambia ninyi ninawaambia wote, endeleeni kukesha.”—Marko 13:33-37.

11 Baada ya kutambua kwamba kuwapo kwa Kristo kulianza mwaka wa 1914, wafuasi wa Yesu walijitayarisha kwa ajili ya mwisho ambao walidhani ungekuja karibuni. Walifanya hivyo kwa kuongeza bidii katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Yesu alisema kuwa anaweza kuja wakati “anapowika jogoo au asubuhi na mapema.” Hivyo, alionyesha kwamba huenda muda fulani ungepita kabla hajaja. Ikiwa hilo lingetokea, wafuasi wake wangepaswa kufanya nini? Alisema hivi: “Endeleeni kukesha.” Kwa hiyo, hata ikiwa wamesubiri kwa muda mrefu, hawapaswi kufikiri kwamba mwisho uko mbali sana au kwamba hautakuja.

12. Habakuki alimuuliza Yehova swali gani? Na Mungu alimjibuje?

12 Mfikirie nabii Habakuki, aliyeagizwa atabiri kuhusu uharibifu wa Yerusalemu. Kufikia wakati alipoanza huduma yake, tayari manabii wengine walikuwa wametangaza ujumbe huo kwa miaka mingi. Hali ilikuwa mbaya hivi kwamba ‘mwovu alimzingira mwadilifu na haki ilipotoshwa.’ Kwa hiyo, haishangazi kwamba Habakuki aliuliza hivi: “Ee Yehova, nililie msaada mpaka wakati gani?” Badala ya kujibu swali hilo moja kwa moja, Yehova alimhakikishia nabii huyo mwaminifu kwamba uharibifu uliotabiriwa ‘hautachelewa.’ Mungu alimwambia Habakuki ‘aendelee kutarajia.’—Soma Habakuki 1:1-4; 2:3.

13. Habakuki angeweza kusitawisha mtazamo gani, lakini kwa nini ingekuwa hatari kufanya hivyo?

13 Wazia ikiwa Habakuki angekata tamaa na kuwaza hivi: ‘Nimesikia kuhusu uharibifu wa Yerusalemu kwa miaka mingi. Vipi ikiwa bado uko mbali sana? Sidhani kama ninapaswa kuendelea kutoa unabii kana kwamba jiji litaharibiwa ghafla hivi karibuni. Acha wengine wafanye kazi hiyo.’ Ikiwa Habakuki angewaza hivyo, basi angepoteza kibali cha Yehova, na huenda angeuawa Yerusalemu lilipoharibiwa na Wababiloni.

14. Kwa nini inafaa tuendelee kutarajia mwisho wa mfumo huu?

14 Kufikia wakati tutakapoingia katika ulimwengu mpya, unabii wote kuhusu umalizio wa mfumo wa mambo utakuwa umetimizwa. Kutafakari jinsi mambo yalivyokuwa kutaimarisha imani yetu kwa Yehova na ahadi zake. (Soma Yoshua 23:14.) Tutamshukuru sana Mungu, ‘aliyeweka nyakati na majira katika mamlaka yake mwenyewe,’ kwa kutuhimiza tuendelee kuwa macho ‘mwisho wa mambo yote ulipokuwa ukikaribia.’—Mdo. 1:7; 1 Pet. 4:7.

ENDELEA KUHUBIRI UNAPOSUBIRI MWISHO

Je, unahubiri habari njema kwa bidii? (Tazama fungu la 15)

15, 16. Kwa nini tunapaswa kuhubiri kwa bidii katika siku hizi za mwisho?

15 Tengenezo la Yehova litaendelea kutukumbusha kwamba tunapaswa kumtumikia Mungu tukiwa na hisi ya uharaka. Vikumbusho hivyo vinatusaidia kuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Mungu na kuwa macho kutambua utimizo wa ishara ya kuwapo kwa Kristo. Ni jambo gani muhimu sana tunalopaswa kufanya wakati huu? Tunapaswa kuutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu kwa kuhubiri habari njema kwa bidii.—Mt. 6:33; Marko 13:10.

16 Dada mmoja alisema hivi: “Kwa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, tunaweza . . . kuwasaidia watu waokoke mwisho wa ulimwengu huu.” Anajua umuhimu wa jambo hilo, kwa kuwa yeye na mume wake waliokoka janga baya sana kuwahi kutokea katika historia, yaani, kuzama kwa meli ya Wilhelm Gustloff mwaka wa 1945. Meli hiyo ilipokuwa ikizama, watu wengine walihangaikia mambo yasiyo na maana. Mwanamke mmoja aliomboleza hivi: “Begi langu! Begi langu! Vito vyangu! Vito vyangu vyote viko kwenye chumba cha chini. Nimepoteza kila kitu!” Hata hivyo, baadhi ya abiria wenye huruma walihatarisha maisha yao kwa kujitahidi kuwaokoa watu wengine. Kama abiria hao wasio na ubinafsi, sisi tunafanya yote tuwezayo kuwasaidia watu. Tunahubiri tukiwa na hisi ya uharaka na tunawasaidia watu ili waokoke mwisho wa mfumo huu kabla haijawa kuchelewa mno.

Je, unafanya maamuzi ya hekima ili usikengeushwe na kupoteza hisi ya uharaka? (Tazama fungu la 17)

17. Kwa nini tunaamini kwamba mwisho unaweza kuja wakati wowote?

17 Matukio ya ulimwengu yanaonyesha kwamba unabii wa Biblia unatimizwa na mwisho wa mfumo huu mwovu uko karibu sana. Kwa hiyo, hatupaswi kufikiri kwamba bado wakati mwingi unahitajika ili hali za ulimwengu zifikie hatua ya kuzilazimu “zile pembe kumi” na “yule mnyama-mwitu” wa Ufunuo 17:16 kumgeukia Babiloni Mkubwa, yaani, milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo. Kumbuka kwamba Mungu ‘atatia hilo ndani ya mioyo yao’ ili kuharibu dini ya uwongo—hilo linaweza kutokea ghafla na wakati wowote! (Ufu. 17:17) Mwisho wa mfumo huu wa mambo hauko mbali. Kwa hiyo tunapaswa kutii onyo hili la Yesu: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego.” (Luka 21:34, 35; Ufu. 16:15) Acheni tuazimie kumtumikia Yehova tukiwa na hisi ya uharaka, huku tukiamini kwamba ‘anatenda kwa ajili ya mtu anayeendelea kumtarajia.’—Isa. 64:4.

18. Tutazungumzia jambo gani katika makala inayofuata?

18 Tunapongojea mwisho wa mfumo huu mwovu, acheni tutii maneno haya ambayo Yuda aliandika kwa mwongozo wa roho: “Wapendwa, kwa kujijenga wenyewe juu ya imani yenu iliyo takatifu zaidi, na kusali mkiwa na roho takatifu, jitunzeni katika upendo wa Mungu, huku mkiingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa kutazamia uzima wa milele.” (Yuda 20, 21) Hata hivyo, tunawezaje kujitayarisha kwa ajili ya ulimwengu mpya na kuonyesha kwamba tunatarajia mwisho utakuja hivi karibuni? Tutazungumzia jambo hilo katika makala inayofuata.

^ fu. 1 Ili kuona baadhi ya unabii kumhusu Masihi na utimizo wake, tazama kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?, ukurasa wa 200.