Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jihadhari na Mashirika Mabaya Katika Siku Hizi za Mwisho

Jihadhari na Mashirika Mabaya Katika Siku Hizi za Mwisho

“Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.”—1 KOR. 15:33.

NYIMBO: 73, 119

1. Tunaishi katika kipindi gani cha wakati?

TUNAISHI katika nyakati ngumu sana. Biblia inaonyesha kwamba “siku za mwisho” zilianza mwaka wa 1914. Katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,’ kumekuwa na hali mbaya zaidi ambazo hazijawahi kutokea kabla ya mwaka huo. (2 Tim. 3:1-5) Isitoshe, hali zitazidi kuwa mbaya ulimwenguni, kwa kuwa Biblia ilitabiri kwamba “watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi.”—2 Tim. 3:13.

2. Watu wengi wanafurahia burudani gani? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

2 Watu wengi hujiburudisha kwa kutazama au kufanya mambo ambayo Mungu huchukia, kama vile jeuri, ngono haramu, na kuwasiliana na pepo. Kwa mfano, Intaneti, vipindi vya televisheni, sinema, magazeti, na vitabu vya hadithi huonyesha kwamba ujeuri na ukosefu wa maadili ni mambo yanayofaa. Katika baadhi ya maeneo, mambo fulani yamehalalishwa ingawa mwanzoni hayakukubalika. Lakini hilo halimaanishi kwamba mambo hayo yanakubalika machoni pa Mungu.—Soma Waroma 1:28-32.

3. Watu wanawaonaje wale wanaofuata viwango vya Mungu maishani mwao?

3 Wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza waliepuka burudani chafu. Walikashifiwa na kuteswa kwa sababu ya mwenendo wao mzuri. Mtume Petro aliandika hivi: “Kwa sababu ninyi [Wakristo] hamwendelei kukimbia pamoja nao katika mwendo huo kwenda kwenye dimbwi lilelile la chini la upotovu, wao wanashangaa na kuendelea kuwatukana ninyi.” (1 Pet. 4:4) Leo pia, ulimwengu unawaona wale wanaofuata viwango vya Mungu maishani mwao kuwa watu wa ajabu. Zaidi ya hayo, “wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.”—2 Tim. 3:12.

“MASHIRIKA MABAYA HUHARIBU TABIA NZURI”

4. Maandiko yanatushauri nini kuhusu ulimwengu huu?

4 Maandiko yanawashauri wale wanaotaka kumfurahisha Mungu wasiupende ulimwengu wala mazoea yake. (Soma 1 Yohana 2:15, 16.) Shetani Ibilisi, “mungu wa mfumo huu wa mambo,” anatumia dini, siasa, vyombo vya habari na mashirika ya kibiashara ya ulimwengu huu ili kuwapotosha watu. (2 Kor. 4:4; 1 Yoh. 5:19) Hivyo, tukiwa Wakristo, tunahitaji kuepuka mashirika mabaya. Neno la Mungu linaonya hivi waziwazi: “Msipotoshwe. Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.”—1 Kor. 15:33.

5, 6. Tunapaswa kuepuka kushirikiana na watu gani, na kwa nini?

5 Ili tusiharibu tabia zetu nzuri, ni lazima tuepuke kushirikiana na watu wenye mazoea ya kufanya mambo mabaya. Hilo linahusisha kuepuka kushirikiana na watu wasio Mashahidi ambao wana mazoea ya kufanya mambo mabaya, na vilevile wale wanaodai kumwabudu Yehova lakini wanavunja sheria zake kimakusudi. Ikiwa Wakristo hao wanafanya dhambi nzito na hawatubu, basi tunaacha kushirikiana nao.—Rom. 16:17, 18.

6 Tukishirikiana na watu ambao hawatii sheria za Mungu, tunaweza kusitawisha mwelekeo wa kufanya yale wanayofanya ili watukubali. Kwa mfano, tukishirikiana kwa ukaribu na waasherati, huenda tukashawishiwa kufanya uasherati. Baadhi ya Wakristo waliojiweka wakfu wamepatwa na jambo hilo, na wengine kati yao wametengwa na ushirika kwa sababu hawakutubu. (1 Kor. 5:11-13) Ikiwa hawatatubu, hali yao inaweza kuwa kama ile iliyoelezwa na Petro.—Soma 2 Petro 2:20-22.

7. Ni nani wanaopaswa kuwa rafiki zetu wa karibu?

7 Ingawa tunawatendea kwa fadhili wale ambao hawatii sheria za Mungu, hatupaswi kuwa rafiki zao wa karibu. Hivyo, ni kosa kwa Shahidi wa Yehova mseja kuanzisha urafiki wa kimapenzi na mtu ambaye hajajiweka wakfu na si mwaminifu kwa Yehova, na ambaye haheshimu viwango vya maadili vya Mungu. Kukubaliwa na Yehova ni muhimu zaidi kuliko kupendwa na watu wengi ambao hawaishi kulingana na sheria za Yehova. Tunapaswa kushirikiana kwa ukaribu na wale wanaofanya mapenzi ya Mungu. Yesu alisema, “Yeyote yule anayefanya mapenzi ya Mungu, huyo ndiye ndugu yangu na dada yangu na mama yangu.”—Marko 3:35.

8. Mashirika mabaya yaliwaathirije Waisraeli?

8 Waisraeli walipatwa na maafa kwa sababu ya kushirikiana na watu wabaya. Yehova alipowakomboa kutoka utumwani Misri na kuwaongoza kwenda Nchi ya Ahadi, aliwaambia hivi kuhusu wakazi wa nchi hiyo: “Usiinamie miungu yao wala kuchochewa kuitumikia, wala usifanyize chochote kilicho kama kazi zao, bali lazima utawaangusha nawe lazima uzivunje nguzo zao takatifu. Nanyi mtamtumikia Yehova Mungu wenu.” (Kut. 23:24, 25) Hata hivyo, Waisraeli wengi hawakutii maagizo ya Mungu. (Zab. 106:35-39) Kwa sababu waliacha kuwa waaminifu kwa Mungu, baadaye Yesu aliwaambia hivi: “Tazama! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mt. 23:38) Yehova aliwakataa Waisraeli, naye akachagua kutaniko jipya la Kikristo.—Mdo. 2:1-4.

JIHADHARI NA MAMBO UNAYOSOMA NA UNAYOTAZAMA

9. Kwa nini vyombo vya habari vya ulimwengu huu vinaweza kuwa hatari?

9 Mambo mengi yaliyo kwenye vyombo vya habari vya ulimwengu huu yanaweza kuhatarisha hali ya kiroho ya Wakristo. Mambo hayo hayatusaidii tumwamini Yehova na ahadi zake. Badala yake, yamekusudiwa kuwachochea watu wapende mambo mabaya na wautumaini ulimwengu mwovu wa Shetani. Hivyo, tunapaswa kuepuka kutazama, kusoma, au kusikiliza mambo yanayoweza kuamsha “tamaa za kilimwengu.”—Tito 2:12.

10. Habari zote zisizofaa zitapatwa na nini?

10 Hivi karibuni, habari zote zisizofaa hazitakuwepo tena. Mambo yote hayo yatatoweka ulimwengu wa Shetani utakapoharibiwa. Neno la Mungu linasema hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yoh. 2:17) Vilevile, mtunga-zaburi aliimba hivi: “Watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia.” Kisha akaongeza: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” Kwa muda gani? “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zab. 37:9, 11, 29.

11. Mungu huandaaje chakula kizuri cha kiroho kwa ajili ya watu wake?

11 Tofauti na ulimwengu wa Shetani, tengenezo la Yehova hutupatia habari zinazotuchochea tuwe na mwenendo utakaotusaidia tupate uzima wa milele. Yesu alisali hivi kwa Yehova: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yoh. 17:3) Baba yetu wa mbinguni anatupatia chakula kingi cha kiroho chenye kujenga kupitia tengenezo lake. Ni baraka iliyoje kuwa na magazeti, broshua, vitabu, video na makala mbalimbali kwenye Intaneti zinazoendeleza ibada ya kweli! Pia, tengenezo la Yehova huandaa mikutano katika makutaniko zaidi ya 110,000 ulimwenguni pote. Katika mikutano hiyo na pia kwenye makusanyiko, tunajifunza habari zinazotegemea Biblia ambazo hutusaidia kumwamini Mungu na ahadi zake.—Ebr. 10:24, 25.

KUOA AU KUOLEWA “KATIKA BWANA TU”

12. Ushauri wa Biblia kuhusu kuoa au kuolewa “katika Bwana tu” unamaanisha nini?

12 Wakristo waseja wanaotaka kufunga ndoa wanapaswa kuwa waangalifu sana inapohusu watu wanaoshirikiana nao. Neno la Mungu linashauri hivi waziwazi: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini. Kwa maana kuna ushirika gani kati ya uadilifu na uasi-sheria? Au nuru ina ushirika gani na giza?” (2 Kor. 6:14) Biblia inawashauri watumishi wa Mungu wanaotafuta mwenzi, wafunge ndoa “katika Bwana tu,” yaani, waoe au waolewe na mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu na kubatizwa na anayeishi kupatana na mafundisho ya Biblia. (1 Kor. 7:39) Wakristo wanapofunga ndoa na waumini wenzao, wanapata wenzi waliojiweka wakfu kwa Yehova, na ambao watawasaidia kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu.

13. Mungu aliwapa Waisraeli amri gani kuhusu ndoa?

13 Yehova anajua mambo yanayowafaa watumishi wake, na maoni yake kuhusu ndoa hayajabadilika. Fikiria amri hii iliyo wazi ambayo aliwapa Waisraeli kupitia Musa. Aliwaamuru hivi kuhusiana na mataifa jirani, yaani, watu ambao hawakumwabudu Yehova: “Usifanye mapatano yoyote ya ndoa pamoja nao. Binti yako usimpe mwana wake, wala binti yake usimchukue kwa ajili ya mwana wako. Kwa maana atamgeuza mwana wako aache kunifuata, nao watatumikia miungu mingine; na hasira ya Yehova itawaka kwelikweli juu yenu, naye hakika atakuangamiza haraka.”—Kum. 7:3, 4.

14, 15. Sulemani aliathiriwaje kwa kupuuza amri ya Yehova?

14 Mwanzoni mwa utawala wake, Sulemani aliomba apewe hekima, na Yehova akajibu sala yake. Hivyo, Mfalme Sulemani alijulikana sana kuwa mtawala mwenye hekima wa taifa la Israeli. Kwa mfano, malkia wa Sheba alisema hivi alipojionea hekima ya Sulemani: “Nami sikuyaamini maneno hayo mpaka nilipokuja ili nijionee kwa macho yangu mwenyewe; na tazama! sikuwa nimeambiwa hata nusu. Umezidi katika hekima na mafanikio, mambo yale niliyoyasikia.” (1 Fal. 10:7) Lakini Sulemani akaja kuwa mfano mbaya unaoonyesha matokeo ya kupuuza amri ya Mungu inayokataza kuoa au kuolewa na mtu ambaye hamwabudu Yehova.—Mhu. 4:13.

15 Licha ya mambo yote ambayo Yehova alimfanyia, Sulemani alipuuza amri ya Mungu iliyokataza kuoa wanawake kutoka mataifa jirani, yaani watu ambao hawakumwabudu Yehova. Sulemani “akawapenda wake wengi wageni” na hatimaye akawa na wake 700 na masuria 300. Alipata matokeo gani? Katika siku zake za uzeeni, wake zake wapagani waliugeuza “moyo wake ukaifuata miungu mingine, . . . na Sulemani akaanza kufanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.” (1 Fal. 11:1-6) Mashirika mabaya yaliathiri hekima ya Sulemani na kumfanya aache ibada ya kweli. Hilo ni onyo kwa Wakristo wanaofikiria kuoa au kuolewa na mtu ambaye hampendi Yehova.

16. Biblia inashauri nini kuhusu mtu aliye na mwenzi asiye mwamini?

16 Namna gani ikiwa mtu amekuwa mwabudu wa Yehova ilhali mwenzi wake si Shahidi wa Yehova? Biblia inasema hivi: “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao.” (1 Pet. 3:1) Ingawa maneno hayo yanawahusu wake Wakristo, kanuni hiyo inawafaa pia ndugu wenye wake wasio waamini. Ushauri wa Biblia uko wazi: Uwe mwenzi mzuri, na uishi kupatana na viwango vya Mungu vya ndoa. Wenzi wengi wasio waamini wamekubali kweli kwa sababu ya mwenendo mzuri wa waume au wake zao.

SHIRIKIANA NA WALE WANAOMPENDA YEHOVA

17, 18. Kwa nini Noa aliokoka Gharika? Na ni nini kilichowasaidia Wakristo wa karne ya kwanza kuokoka uharibifu wa Yerusalemu?

17 Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri, lakini mashirika mazuri yatakusaidia uwe na sifa nzuri. Mfikirie Noa aliyeishi katika ulimwengu uliopotoka lakini hakutamani kufanya urafiki wa karibu na watu wa siku zake. Katika siku hizo, Yehova aliona kuwa “ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani na kila mwelekeo wa fikira za moyo wake ulikuwa mbaya tu wakati wote.” (Mwa. 6:5) Hivyo, Mungu aliazimia kuharibu mfumo huo mwovu na watu wake kupitia gharika. Lakini “Noa alikuwa mtu mwadilifu. Alionekana kuwa mtu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake. Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.”—Mwa. 6:7-9.

18 Bila shaka, Noa hakushirikiana kwa ukaribu na watu wasiomwabudu Mungu. Yeye na watu saba wa familia yake waliendelea kufanya kazi waliyopewa na Mungu, iliyohusisha kujenga safina. Wakati huohuo, Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Pet. 2:5) Kazi ya kuhubiri, kujenga safina, na kushirikiana kwa ukaribu na familia yake kulimsaidia aendelee kufanya mapenzi ya Mungu. Matokeo ni kwamba Noa na familia yake waliokoka Gharika. Tunathamini kwamba Noa, mke wake, watoto wake, na wake zao walimtumikia Yehova kwa uaminifu, na sisi sote ni wazao wao. Vivyo hivyo, ushikamanifu na utii wa Wakristo wa karne ya kwanza uliwafanya wawe tofauti na watu wasiomwogopa Mungu, nao wakaokoka uharibifu wa Yerusalemu na mfumo wa mambo wa Kiyahudi mwaka wa 70 W.K.—Luka 21:20-22.

Ushirika mzuri na waumini wenzetu ni kionjo tu cha maisha tutakayofurahia katika ulimwengu mpya? (Tazama fungu la 19)

19. Tunapaswa kufanya nini ili tupate kibali cha Mungu?

19 Tukiwa waabudu wa Yehova, tunapaswa kumwiga Noa, familia yake, na Wakristo waaminifu wa karne ya kwanza. Ni lazima tujitenge na ulimwengu huu mwovu na tushirikiane na mamilioni ya ndugu na dada zetu waaminifu. Kushikamana na wale wanaoongozwa na hekima ya Mungu kutatusaidia ‘tusimame imara katika imani.’ (1 Kor. 16:13; Met. 13:20) Hebu wazia tumaini letu! Ikiwa tutaendelea kujihadhari na mashirika mabaya katika siku hizi za mwisho, tutaokoka mwisho wa mfumo huu mwovu, na kuingia katika ulimwengu mpya wenye uadilifu ulio karibu sana.