Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitayarishe Sasa Kuishi Katika Ulimwengu Mpya

Jitayarishe Sasa Kuishi Katika Ulimwengu Mpya

‘Uwape maagizo watende mema, ili waushike imara uzima ulio wa kweli.’ —1 TIM. 6:17-19.

NYIMBO: 125, 40

1, 2. (a) Unatazamia nini katika Paradiso? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Ni jambo gani litakalotupatia shangwe zaidi?

“UZIMA ULIO WA KWELI.” Maneno hayo yanatukumbusha tumaini letu la uzima wa milele duniani. Mtume Paulo alihusianisha “uzima wa milele” na “uzima ulio wa kweli.” (Soma 1 Timotheo 6:12, 19.) Tunatazamia kuishi maisha yanayoridhisha na yenye shangwe kwa umilele wote. Hebu wazia jinsi utakavyohisi kila siku utakapoamka ukiwa na hali nzuri ya kimwili, kiakili, na kihisia! (Isa. 35:5, 6) Fikiria shangwe utakayopata kwa kushirikiana na wale uwapendao, pamoja na wale watakaofufuliwa. (Yoh. 5:28, 29; Mdo. 24:15) Pia, tutakuwa na nafasi ya kujifunza kwa kina sayansi, muziki, usanifu majengo na mengineyo.

2 Ingawa tunatazamia mambo mengi mazuri katika ulimwengu mpya, mambo ya kiroho ndiyo yatakayotuletea shangwe zaidi. Tutafurahia sana kwa kuwa jina la Mungu litakuwa limetakaswa na enzi yake kuu kutetewa. (Mt. 6:9, 10) Itasisimua sana kuona Yehova akitimiza kusudi lake kwa dunia na wanadamu. Hebu wazia jinsi itakavyokuwa rahisi kumkaribia Yehova kadiri tutakavyokuwa tukifikia ukamilifu!—Zab. 73:28; Yak. 4:8.

3. Tunapaswa kujitayarisha kwa ajili ya nini sasa?

3 Tutafurahia baraka hizo kwa kuwa Yesu alisema, “kwa Mungu mambo yote yanawezekana.” (Mt. 19:25, 26) Ikiwa tunatazamia kuishi katika ulimwengu mpya, na kuendelea kuwepo baada ya Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu Moja, tunapaswa ‘kuushika imara’ uzima wa milele sasa. Tunapaswa kuishi huku tukitazamia mwisho wa ulimwengu huu mwovu, na tunahitaji kuchukua hatua sasa ili kujitayarisha kuishi katika ulimwengu mpya. Tunawezaje kufanya hivyo wakati bado tunaishi katika mfumo huu mwovu?

JINSI YA KUJITAYARISHA

4. Toa mfano unaoonyesha jinsi tunavyoweza kujitayarisha kuishi katika ulimwengu mpya.

4 Tunawezaje kujitayarisha kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu? Wazia kwamba unapanga kuhamia nchi nyingine. Utajitayarishaje? Unaweza kuanza kujifunza lugha inayozungumzwa katika nchi hiyo. Pia, utafaidika ukijifunza desturi zao. Huenda ukajaribu kula baadhi ya vyakula vyao. Kwa kadiri fulani unaishi kama utakavyoishi katika nchi hiyo, kwa kuwa hivyo ndivyo utakavyoishi utakapofika huko. Vivyo hivyo, tunaweza kujitayarisha sasa kuishi katika ulimwengu mpya kwa kufanya juu chini kuishi kama tutakavyoishi wakati huo. Jinsi gani? Fikiria mifano ifuatayo.

5, 6. Kutii mwongozo wa kitheokrasi kunatuzoezaje kuishi katika ulimwengu mpya?

5 Katika ulimwengu mpya, enzi kuu ya Yehova itaungwa mkono kikamili. Hali zitakuwa tofauti kabisa na ulimwengu huu unaotawaliwa na Shetani. Shetani anachochea roho ya ubinafsi. Hivyo, watu wengi hawaoni haja ya kumtegemea Mungu na wanasisitiza kwamba maoni yao ndiyo bora zaidi. Kumekuwa na matokeo gani? Kupuuza mwongozo wa Mungu kumesababisha mateso, taabu, na hata majanga. (Yer. 10:23) Tunatazamia kwa hamu sana wakati ambapo wanadamu wote wataunga mkono enzi kuu ya Yehova!

6 Katika ulimwengu mpya, tutafurahia sana kufuata mwongozo wa Yehova tutakaposhiriki kuigeuza dunia kuwa paradiso, kuwafundisha watakaofufuliwa, na kufanya mapenzi ya Yehova. Lakini itakuwaje tukiambiwa tufanye jambo ambalo halituvutii? Je, tutatii kwa kufanya yote tuwezayo ili kutimiza na kufurahia mgawo huo? Huenda wengi wetu tukajibu ndiyo! Lakini, je, tunatii mwongozo wa kitheokrasi sasa? Ikiwa tunafanya hivyo, basi tunajitayarisha kuishi chini ya utawala wa Yehova.

7, 8. (a) Kwa nini tunapaswa kuwa na ushirikiano? (b) Wakristo fulani wamekabili mabadiliko gani? (c) Tunaweza kuwa na uhakika gani kuhusu maisha katika ulimwengu mpya?

7 Ili kujitayarisha kuishi katika ulimwengu mpya, haitoshi tu kutii mwongozo wa tengenezo la Yehova. Tunapaswa pia kujifunza kuridhika na kushirikiana. Ikiwa tunashirikiana na wale wanaoongoza, labda kwa kukubali na kufurahia migawo mipya ya utumishi, inaelekea tutakuwa na mtazamo huohuo katika ulimwengu mpya. (Soma Waebrania 13:17.) Katika Nchi ya Ahadi, Waisraeli waligawiwa urithi kwa kura. (Hes. 26:52-56; Yos. 14:1, 2) Hata hivyo, sisi hatujui tutapangiwa kuishi wapi katika mfumo mpya. Ushirikiano utatusaidia kuridhika na kufurahia sana kufanya mapenzi ya Yehova haidhuru tutaishi wapi.

8 Jitihada zozote tunazofanya ili kushirikiana na tengenezo la Yehova na kutimiza migawo ya kitheokrasi si za bure, kwa kuwa tutapata baraka nyingi sana chini ya utawala wa Ufalme. Bila shaka, hali zinabadilika siku baada ya siku. Kwa mfano, baadhi ya washiriki wa familia ya Betheli ya Marekani wamepata mgawo wa kwenda shambani na sasa wanafurahia baraka nyingi katika utumishi huo. Baadhi ya waangalizi wamepewa mgawo wa kuwa mapainia wa pekee kwa sababu ya umri au mambo mengine. Ikiwa tutaridhika katika utumishi wetu, huku tukifanya yote tuwezayo na kumtegemea Yehova, tutapata shangwe na baraka hata katika siku hizi za mwisho. (Soma Methali 10:22.) Vipi kuhusu wakati ujao? Huenda tumeanza kufikiria tutaishi wapi katika ulimwengu mpya, hata hivyo inawezekana tukapangiwa kuishi mahali tofauti. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutapata shangwe na kuridhika haidhuru tutatumikia wapi na tutafanya nini.—Neh. 8:10.

9, 10. (a) Huenda tukahitaji kuwa na subira kuhusiana na mambo gani katika ulimwengu mpya? (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna subira?

9 Wakati mwingine tutahitaji kuwa na subira katika ulimwengu mpya. Kwa mfano, huenda tukasikia wengine wakifurahia sana ufufuo wa ndugu na rafiki zao. Lakini huenda sisi binafsi tukahitaji kusubiri wapendwa wetu wafufuliwe. Jambo hilo likitokea, je, tutashangilia pamoja na wengine na kuonyesha subira? (Rom. 12:15) Kuwa na subira kuhusiana na utimizo wa ahadi za Yehova sasa kutatusaidia kuwa na subira wakati huo.Mhu. 7:8.

10 Pia, tunaweza kujitayarisha kuishi katika ulimwengu mpya kwa kuwa na subira kuhusu kufunuliwa kwa kweli ya Biblia. Je, tunajifunza kwa bidii na kuwa na subira kadiri uelewaji wetu unavyoboreshwa hatua kwa hatua? Ikiwa ndivyo, basi haitakuwa vigumu kwetu kuwa na subira Yehova atakapokuwa akifunua matakwa yake katika ulimwengu mpya.—Met. 4:18; Yoh. 16:12.

11. Kwa nini tunapaswa kujifunza kuwasamehe wengine?

11 Sifa nyingine itakayotutayarisha kuishi katika ulimwengu mpya ni kusamehe. Chini ya Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu Moja, huenda ikachukua muda kwa waadilifu na wasio waadilifu kufikia ukamilifu. (Mdo. 24:15) Je, tutatendeana kwa upendo wakati huo? Tukijifunza kusamehe kwa hiari na kuepuka kuwekeana kinyongo, basi itakuwa rahisi kufanya hivyo wakati huo.—Soma Wakolosai 3:12-14.

12. Kuna uhusiano gani kati ya maisha yetu ya sasa na tumaini letu la wakati ujao?

12 Kuishi katika ulimwengu mpya hakumaanishi kwamba mara zote tutapata kile tunachotaka wakati tunaotaka. Badala yake, tutahitaji kuwa wenye shukrani na kuridhika huku tukifaidika kwa kuunga mkono enzi kuu ya Yehova. Tutahitaji kuwa na sifa zilezile ambazo Yehova anatufundisha sasa. Tunapojitayarisha kuishi katika ulimwengu mpya, tunasitawisha sifa zitakazotusaidia kwa umilele wote. Jambo hilo linaimarisha imani na kufanya matarajio yetu ya kuishi katika “dunia yenye kukaliwa inayokuja” kuwa halisi zaidi. (Ebr. 2:5; 11:1) Tukifanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunatamani sana kuishi milele katika dunia mpya yenye uadilifu.

TANGULIZA MALENGO YA KIROHO

Hubiri kwa bidii

13. Tutatanguliza nini katika ulimwengu mpya?

13 Acheni tufikirie njia nyingine ya kujitayarisha kwa ajili ya uzima ulio wa kweli. Ingawa tutapata chakula kingi na mahitaji mengine muhimu katika ulimwengu mpya, mambo ya kiroho ndiyo yatakayotupatia shangwe zaidi. (Mt. 5:3) Tutatanguliza mambo ya kiroho, nasi tutapata furaha tele katika Yehova. (Zab. 37:4) Ikiwa tunatanguliza mambo ya kiroho sasa, basi tunajitayarisha kwa ajili ya uzima ulio wa kweli wakati ujao.—Soma Mathayo 6:19-21.

14. Ni malengo gani ya kiroho yatakayowasaidia vijana kujitayarisha kwa ajili ya uzima wa milele?

14 Tunawezaje kuongeza shangwe yetu katika mambo ya kitheokrasi? Njia moja ni kujiwekea malengo ya kiroho. Ikiwa wewe ni kijana na unafikiria kwa uzito kumtumikia Yehova, kwa nini usifanye utafiti kuhusu utumishi mbalimbali wa wakati wote na kujiwekea lengo fulani katika utumishi? * Unaweza kuzungumza na watumishi wa wakati wote ambao wamemtumikia Yehova kwa muda mrefu. Ukitumia maisha yako kumtumikia Mungu, utapata uzoefu na mazoezi ya kitheokrasi yatakayokusaidia katika ulimwengu mpya.

Shiriki katika shughuli za kitheokrasi

15. Tunaweza kujiwekea malengo gani ya kiroho?

15 Tunaweza kujiwekea malengo gani ya kiroho? Tunaweza kuwa na lengo la kuboresha ustadi wetu katika huduma. Au tunaweza kujitahidi kuboresha uelewaji wetu wa kanuni za Biblia na jinsi ya kuzitumia. Zaidi ya hayo, tunaweza kuboresha ustadi wetu wa kufundisha na kusoma mbele ya watu au kutoa maelezo mikutanoni. Bila shaka kuna mambo mengine mengi. Jambo kuu ni hili: Kujiwekea malengo ya kiroho kutakufanya ufurahie zaidi mambo ya kitheokrasi, na kukutayarisha kuishi katika ulimwengu mpya.

FURAHIA BARAKA ZA YEHOVA SASA!

Thamini chakula cha kiroho

16. Kwa nini kumtumikia Yehova ndiyo njia bora zaidi ya maisha?

16 Je, kutumia wakati wetu kujitayarisha kwa ajili ya ulimwengu mpya kunamaanisha kwamba hatutaishi maisha bora na yenye kuridhisha sasa? La hasha! Kumtumikia Yehova ndiyo njia bora zaidi ya maisha. Hatufanyi hivyo kwa lazima au ili tu tuokoke dhiki kuu, bali kufanya hivyo kunatuletea shangwe kubwa, kwa kuwa tumeumbwa tukiwa na uhitaji huo. Kufuata mwongozo wa Yehova na kuwa na urafiki wa karibu pamoja naye ni bora zaidi kuliko kitu kingine chochote. (Soma Zaburi 63:1-3.) Bila shaka, hatuhitaji kusubiri mpaka tufike kwenye ulimwengu mpya ili tufurahie baraka za kumtumikia Yehova kwa moyo wote. Tunaweza kufurahia baraka hizo sasa! Kwa kweli, baadhi yetu tumefurahia baraka hizo kwa miaka mingi, na tuna uhakika kabisa kwamba hii ndiyo njia bora zaidi ya maisha.—Zab. 1:1-3; Isa. 58:13, 14.

Tafuta mwongozo wa Kimaandiko

17. Burudani na mambo mengine yatakuwa na nafasi gani katika Paradiso?

17 Tutakuwa na nafasi ya kufurahia burudani na mambo mengine ya kibinafsi katika ulimwengu mpya. Yehova hangetuumba tukiwa na tamaa ya kufanya hivyo ikiwa hangetaka tufurahie maisha. (Mhu. 2:24) Yehova ameahidi “kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” (Zab. 145:16) Burudani ni muhimu, lakini tunaifurahia zaidi tunapotanguliza uhusiano wetu na Yehova. Hivyo ndivyo itakavyokuwa katika dunia Paradiso. Kwa hiyo, ni muhimu sana kuwa na maoni yanayofaa kuhusu burudani, huku tukiutafuta kwanza Ufalme na kukazia fikira baraka za kiroho ambazo watu wa Mungu wanazifurahia.—Mt. 6:33.

18. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunajitayarisha kuishi milele katika Paradiso?

18 Katika Paradiso, tutafurahia maisha kwa kiwango ambacho hatujawahi kufurahia. Acheni tujitayarishe sasa ili kuonyesha kwamba tunatamani kupata uzima ulio wa kweli. Jitahidi kusitawisha sifa zinazompendeza Mungu na ufurahie kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Sikuzote na tufurahie kufanya mambo ya kiroho. Tukiwa na imani thabiti katika Yehova, acheni tujitayarishe sasa kuishi katika ulimwengu mpya!