Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tafakari Upendo wa Yehova

Tafakari Upendo wa Yehova

“Nitautafakari utendaji wako wote.”—ZAB. 77:12.

NYIMBO: 18, 61

1, 2. (a) Kwa nini unaamini kwamba Yehova anawapenda watu wake? (b) Wanadamu wameumbwa wakiwa na uhitaji gani?

KWA nini unaamini kwamba Yehova anawapenda watu wake? Kabla ya kujibu swali hilo, fikiria mifano ifuatayo: Kwa miaka mingi, dada aitwaye Taylene alishauriwa na waabudu wenzake awe na usawaziko na asitazamie kufanya mambo yaliyo nje ya uwezo wake. Anaeleza hivi: “Ikiwa Yehova hanipendi, basi hangeendelea kunishauri.” Brigitte ambaye aliwalea watoto wake wawili peke yake baada ya kufiwa na mume wake, anasema hivi: “Kulea watoto katika mfumo wa Shetani ni mojawapo ya mambo magumu sana, hasa kwa mzazi mmoja. Lakini ninaamini kwamba Yehova ananipenda kwa kuwa aliniongoza nilipokabili hali ngumu na huzuni, na hajawahi kuruhusu nikabili hali ambayo nisingeweza kuvumilia.” (1 Kor. 10:13) Sandra anaugua ugonjwa usio na tiba. Akiwa kusanyikoni, mke wa ndugu fulani alimjali sana. Mume wa Sandra anasema hivi: “Ingawa hatukumjua vizuri, shauku yake ilitupatia shangwe kubwa sana. Hata neno au jambo dogo ambalo ndugu na dada zetu wanatufanyia kwa sababu ya upendo, linanionyesha jinsi Yehova anavyotupenda sana.”

2 Wanadamu wameumbwa wakiwa na uhitaji wa kupenda na kupendwa. Hata hivyo, ni rahisi kuvunjika moyo uhitaji huo usipotoshelezwa, iwe ni kwa sababu ya matukio yasiyotazamiwa, kukata tamaa, afya mbaya, matatizo ya kiuchumi, au kukosa matokeo mazuri katika huduma. Tukianza kufikiri kuwa Yehova hatupendi, inafaa tukumbuke kwamba anatuthamini sana na yupo pamoja nasi ili ‘kuushika mkono wetu wa kuume’ na kutusaidia. Tukiwa waaminifu kwake, hatatusahau kamwe.—Isa. 41:13; 49:15.

3. Ni nini kinachoweza kutusaidia tuwe na uhakika zaidi kwamba Yehova anatupenda?

3 Mashahidi walionukuliwa awali walikuwa na uhakika kwamba Mungu alikuwa pamoja nao walipokabili hali ngumu. Sisi pia tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova yuko upande wetu. (Zab. 118:6, 7) Katika makala hii, tutazungumzia zawadi nne zinazothibitisha kwamba Yehova anatupenda, nazo ni (1) uumbaji wake, (2) Neno lake lililoongozwa na roho, (3) sala, na (4) fidia. Kutafakari mambo mazuri ambayo Yehova ametufanyia kunaweza kutusaidia tuthamini zaidi upendo wake.—Soma Zaburi 77:11, 12.

TAFAKARI UUMBAJI WA YEHOVA

4. Tunajifunza nini tunapotafakari uumbaji wa Yehova? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 9.)

4 Je, tunaweza kuona jinsi Yehova anavyotupenda tunapotazama uumbaji? Bila shaka, kwa kuwa uumbaji ni ishara ya upendo wa Mungu. (Rom. 1:20) Yehova aliumba dunia ikiwa na mifumo inayoendeleza uhai wetu. Hata hivyo, anataka tufanye mengi zaidi ya kuishi tu. Tunahitaji kula ili tuendelee kuwa hai. Yehova alihakikisha kwamba dunia inatokeza aina mbalimbali za mimea ambayo inaweza kutayarishwa na kuwa chakula kitamu. Ndiyo sababu tunafurahia sana kula chakula! (Mhu. 9:7) Dada aitwaye Catherine hufurahia sana kutazama uumbaji, hasa katika majira ya kuchipua nchini Kanada. Anasema hivi: “Kwa kweli inastaajabisha sana kuona jinsi ambavyo vitu viliumbwa—maua yanavyochipuka ardhini, ndege wanavyohama kutoka eneo moja hadi lingine, na ndege mdogo sana anayeitwa mvumaji anavyoweza kujua njia inayoelekea kwenye chombo cha chakula nje ya dirisha langu la jikoni. Yehova anatupenda sana ndiyo sababu ametupatia mambo mengi ya kufurahia.” Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anafurahia uumbaji wake, naye anataka sisi pia tuufurahie.—Mdo. 14:16, 17.

5. Yehova ameonyeshaje upendo wake kwa namna alivyowaumba wanadamu?

5 Yehova alituumba tukiwa na uwezo wa kufanya kazi nzuri na kuzifurahia. (Mhu. 2:24) Alikusudia wanadamu waijaze dunia, waitiishe, na watawale samaki, ndege, na viumbe hai wengine. (Mwa. 1:26-28) Pia, inapendeza kwamba Yehova alituumba tukiwa na uwezo wa kuiga sifa zake.—Efe. 5:1.

THAMINI NENO LA MUNGU

6. Kwa nini tunapaswa kuthamini sana Neno la Mungu?

6 Mungu ameonyesha upendo mkubwa kwa kutupatia Neno lake lililoongozwa na roho. Linafunua mambo tunayohitaji kujua kumhusu na jinsi anavyoshughulika na wanadamu. Kwa mfano, Maandiko yanatueleza jinsi alivyoshughulika na Waisraeli, ambao mara nyingi hawakumtii. Zaburi 78:38 inasema hivi: “Alikuwa mwenye rehema; akawa akilifunika kosa wala hakuharibu. Na mara nyingi akageuzia mbali hasira yake, naye akawa haiamshi ghadhabu yake yote.” Kutafakari mstari huo kunaweza kukusaidia kuona jinsi Yehova anavyokupenda na kukujali. Uwe na uhakika kwamba Yehova anakuthamini sana.—Soma 1 Petro 5:6, 7.

7. Kwa nini tunapaswa kuithamini sana Biblia?

7 Tunapaswa kuithamini sana Biblia kwa sababu ndiyo njia kuu ambayo Yehova anaitumia kuwasiliana nasi. Mawasiliano mazuri kati ya wazazi na watoto huwasaidia kutumainiana na kuimarisha upendo wao. Tutarajie nini kutoka kwa Yehova? Ingawa hatujawahi kumwona au kusikia sauti yake, “anaongea” nasi kupitia Neno lake lililoongozwa na roho, nasi tunahitaji kumsikiliza. (Isa. 30:20, 21) Yehova anatamani kutuongoza na kutulinda dhidi ya hatari yoyote, kwa kuwa tumejiweka wakfu kwake. Pia, anataka tumjue na kumtegemea.—Soma Zaburi 19:7-11; Methali 1:33.

Ingawa Yehu alilazimika kumshauri Yehoshafati, Yehova aliona “mambo mema” aliyokuwa amefanya (Tazama fungu la 8 na 9)

8, 9. Yehova anataka tujue nini? Toa mfano unaopatikana kwenye Biblia.

8 Yehova anataka tujue kwamba anatupenda sana, naye hakazii fikira kutokamilika kwetu. Anatafuta sifa nzuri tulizo nazo. (2 Nya. 16:9) Kwa mfano, alifanya hivyo katika kisa cha Mfalme Yehoshafati wa Yuda. Wakati fulani, Yehoshafati alifanya uamuzi usiofaa kwa kukubali kumsindikiza vitani Mfalme Ahabu wa Israeli ili kulikomboa jiji la Ramothi-gileadi kutoka mikononi mwa Wasiria. Ingawa manabii 400 wa uwongo walimhakikishia Ahabu kwamba angeshinda vita hivyo, nabii wa kweli wa Yehova, Mikaya, alitabiri kuwa angeshindwa. Ahabu alikufa vitani, na Yehoshafati aliponea chupuchupu kuuawa. Aliporudi Yerusalemu, alikaripiwa kwa sababu ya kushirikiana na Ahabu. Hata hivyo, Yehu, mwana wa Hanani, alimwambia hivi Yehoshafati: “Kuna mambo mema ambayo yameonekana kwako.”—2 Nya. 18:4, 5, 18-22, 33, 34; 19:1-3.

9 Mwanzoni mwa utawala wake, Yehoshafati aliwaagiza wakuu, walawi, na makuhani wasafiri katika majiji yote ya Yuda ili kuwafundisha raia zake Sheria ya Yehova. Kampeni hiyo ilikuwa na matokeo mazuri sana kwa kuwa watu wa mataifa jirani walianza kumwogopa Yehova. (2 Nya. 17:3-10) Ni kweli kwamba Yehoshafati alitenda kipumbavu, lakini Yehova hakusahau mambo mema aliyokuwa amefanya. Simulizi hilo linatufundisha kwamba licha ya kutokamilika kwetu, Yehova atatupenda daima ikiwa tunafanya yote tuwezayo ili kumfurahisha.

THAMINI ZAWADI YA SALA

10, 11. (a) Kwa nini sala ni zawadi ya pekee kutoka kwa Yehova? (b) Mungu hujibuje sala zetu?

10 Baba mwenye upendo huwa tayari kuzungumza na watoto wake wanapotaka kuongea naye. Anataka kujua hisia na mahangaiko yao kwa sababu anawajali sana. Baba yetu wa mbinguni, Yehova, hutusikiliza tunapomkaribia kupitia zawadi nzuri sana ya sala.

11 Tunaweza kusali kwa Yehova wakati wowote. Hajatuwekea vizuizi vyovyote. Yeye ni rafiki yetu ambaye sikuzote yuko tayari kutusikiliza. Taylene, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Unaweza kumweleza jambo lolote unalotaka.” Tunapomweleza Mungu mambo yaliyo moyoni mwetu, anaweza kutujibu kupitia Biblia, habari fulani kwenye magazeti, au waumini wenzetu. Yehova anasikia maombi yetu na anatuelewa hata kama wengine hawatuelewi. Anapojibu sala zetu anathibitisha kwamba anatupenda sana.

12. Kwa nini tunapaswa kutafakari sala zilizoandikwa kwenye Biblia? Toa mfano.

12 Tunaweza kujifunza mambo mengi kutoka kwenye sala zilizoandikwa katika Neno la Mungu. Tutafaidika sana tukichunguza sala hizo katika ibada ya familia. Kutafakari jinsi watumishi wa zamani wa Yehova walivyomweleza Mungu mawazo yao ya moyoni kunaweza kutusaidia tuboreshe sala zetu. Kwa mfano, fikiria sala ya toba aliyotoa Yona alipokuwa ndani ya tumbo la samaki mkubwa. (Yona 1:17–2:10) Fikiria pia sala aliyotoa Sulemani hekalu lilipokuwa likiwekwa wakfu. (1 Fal. 8:22-53) Tafakari sala ya mfano ambayo Yesu aliitoa kwa faida yetu. (Mt. 6:9-13) Zaidi ya yote, acheni “maombi yenu na yajulishwe Mungu.” Matokeo ni kwamba “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.” Hivyo, tutathamini zaidi upendo wa Yehova.—Flp. 4:6, 7.

THAMINI ZAWADI YA FIDIA

13. Fidia hutuwezesha kufanya nini?

13 Zawadi bora zaidi ya dhabihu ya Yesu ya fidia ilitolewa ili “tupate uzima.” (1 Yoh. 4:9) Alipokuwa akizungumzia upendo mkubwa wa Mungu, mtume Paulo alisema hivi: “Kristo alikufa wakati uliowekwa kwa ajili ya watu wasiomwogopa Mungu. Kwa maana ni vigumu kwa yeyote kufa kwa ajili ya mtu mwadilifu; kwa kweli, labda, mtu anaweza kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu mwema. Lakini Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Rom. 5:6-8) Zawadi ya fidia inaonyesha kwamba Mungu anawapenda sana wanadamu, nayo huwawezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova.

14, 15. Fidia inawanufaishaje (a) Wakristo watiwa-mafuta? (b) wale wenye tumaini la kuishi duniani?

14 Wanadamu wachache wanafurahia upendo wa Yehova kwa njia ya pekee sana. (Yoh. 1:12, 13; 3:5-7) Wametiwa mafuta kwa roho takatifu, hivyo wamekuwa “watoto wa Mungu.” (Rom. 8:15, 16) Ingawa baadhi ya Wakristo watiwa-mafuta bado wako duniani, Paulo alisema kwamba ‘wameinuliwa pamoja na kuketishwa pamoja katika mahali pa kimbingu katika muungano na Kristo Yesu.’ (Efe. 2:6) Wanapata wadhifa huo wa kiroho kwa sababu ‘walitiwa muhuri kwa roho takatifu iliyoahidiwa, ambayo ni rehani ya kimbele ya urithi wao,’ yaani, ‘tumaini ambalo limewekwa akiba kwa ajili yao mbinguni.’—Efe. 1:13, 14; Kol. 1:5.

15 Mamilioni ya wanadamu wengine ambao wana imani katika fidia, wanaweza kuwa marafiki wa Yehova na wana tumaini la kufanywa kuwa wana wa Mungu na kuishi milele katika dunia Paradiso. Hivyo, mpango wa fidia unaonyesha jinsi Yehova anavyowapenda sana wanadamu. (Yoh. 3:16) Ikiwa tuna tumaini la kuishi milele duniani na tunaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atatupatia maisha bora zaidi katika ulimwengu mpya. Kwa kweli, zawadi ya fidia ni uthibitisho ulio wazi kwamba Yehova anatupenda sana.

MPENDE SANA YEHOVA

16. Kutafakari upendo wa Mungu kunatuchochea kufanya nini?

16 Yehova ameonyesha anatupenda katika njia nyingi sana. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Jinsi mawazo yako yalivyo yenye thamani kwangu! Ee Mungu, jinsi jumla yake yote ilivyo kuu! Kama ningejaribu kuyahesabu, ni mengi kuliko hata chembe za mchanga. Nimeamka, na bado niko pamoja nawe.” (Zab. 139:17, 18) Kutafakari mambo hayo kutatuchochea tumpende sana Yehova na kufanya yote tuwezayo ili kumpa kilicho bora.

17, 18. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunampenda Mungu?

17 Tuna njia nyingi za kuonyesha tunampenda Yehova. Kwa mfano, tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu na jirani kwa kuwa wenye bidii katika kazi ya kuhubiri Ufalme. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Tunathibitisha kwamba tunampenda Yehova kutoka moyoni tunapovumilia majaribu ya imani na kuendelea kuwa waaminifu. (Soma Zaburi 84:11; Yakobo 1:2-5.) Ikiwa majaribu yanazidi kuwa makali, tuwe na uhakika kwamba Mungu anajua mateso yetu na atatusaidia, kwa kuwa anatujali sana.—Zab. 56:8.

18 Upendo wetu kwa Yehova unatuchochea tutafakari uumbaji wake na matendo yake mengine yenye kustaajabisha. Tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu na kulithamini sana Neno lake kwa kujifunza Biblia. Tunasali kwa ukawaida kwa sababu tunampenda Yehova na tunataka kuimarisha uhusiano wetu pamoja naye. Isitoshe, upendo wetu kwa Mungu unaimarika zaidi tunapotafakari dhabihu ya fidia aliyoitoa kwa ajili ya dhambi zetu. (1 Yoh. 2:1, 2) Hizo ni baadhi ya njia tunazoweza kuonyesha kwamba tunathamini sana upendo wake.