Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunaweza Kuonyeshaje Kwamba Tunampenda Yehova?

Tunaweza Kuonyeshaje Kwamba Tunampenda Yehova?

“Tunaonyesha upendo, kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.” —1 YOH. 4:19.

NYIMBO: 56,  138

1, 2. Kulingana na mtume Yohana, Yehova amefanya jambo gani linalotuchochea tumpende?

NJIA nzuri zaidi ya kuwafundisha watoto ni kuwawekea mfano mzuri. Mtume Yohana aliandika kwamba “sisi tunaonyesha upendo, kwa sababu [Mungu] alitupenda sisi kwanza.” (1 Yoh. 4:19) Ni wazi kwamba Yehova ametuwekea mfano mzuri sana wa upendo, na hilo linatuchochea kumpenda.

2 Ni kwa njia gani Mungu “alitupenda sisi kwanza”? Mtume Paulo alisema: “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Rom. 5:8) Yehova alimtoa Mwana wake ili awe fidia kwa ajili ya wanadamu wanaomwamini. Jambo hilo linaonyesha jinsi upendo wa kweli ulivyo. Mtu huonyesha upendo huo kwa kutoa kwa moyo mkunjufu au kwa kujidhabihu. Dhabihu ambayo Mungu alitoa inatuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye na inatuchochea kumpenda.—1 Yoh. 4:10.

3, 4. Tunaonyeshaje kwamba tunampenda Mungu?

3 Upendo ni sifa kuu ya Yehova. Hiyo ndiyo sababu Yesu alisema kwamba amri ya kwanza kutoka kwa Mungu ni hii: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Maneno ya Yesu yanatufundisha kwamba kumpenda Mungu kunaanzia moyoni. Yehova anataka tumpende kwa moyo wote. Hata hivyo, kumpenda Mungu kunahusisha mengi zaidi ya hisia tu. Yehova anataka pia tumpende kwa akili, nguvu, na nafsi yote. Hilo linamaanisha kwamba mambo yote tunayofanya, iwe ya kimwili au ya kiroho, yanahusika katika kumpenda Mungu.—Soma Mika 6:8.

4 Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunampenda kikweli Baba yetu wa mbinguni? Kwa kutanguliza utumishi wake maishani mwetu. Kama Yesu alivyosema, kila kitu kinahusika katika kumpenda Mungu—mwili wetu, hisia zetu, na mambo ya kiroho. Katika makala iliyopita tulizungumzia mambo manne yanayoonyesha kwamba Yehova anatupenda sana. Acheni sasa tuzungumzie jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunampenda Mungu, na jinsi tunavyoweza kuzidisha upendo huo.

MSHUKURU YEHOVA KWA ZAWADI ANAZOTUPATIA

5. Kufikiria yale ambayo Yehova ametufanyia kunatuchochea kufanya nini?

5 Huwa unafanya nini unapopewa zawadi? Bila shaka unamshukuru aliyekupa zawadi. Isitoshe, inaelekea utaithamini na kuitumia vizuri zawadi hiyo. Yakobo aliandika hivi: “Kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu, kwa maana hushuka kutoka kwa Baba wa mianga ya mbinguni, naye habadiliki, kama kugeuka kwa kivuli.” (Yak. 1:17) Yehova hutupatia kile tunachohitaji ili tuendelee kuwa hai na kufurahia maisha. Je, jambo hilo halikuchochei umpende?

6. Waisraeli walipaswa kufanya nini ili waendelee kupata baraka za Yehova?

6 Yehova aliwatunza Waisraeli kwa miaka mingi, naye aliwabariki kimwili na kiroho. (Kum. 4:7, 8) Hata hivyo, ili waendelee kupokea baraka hizo, walipaswa kutii Sheria ya Mungu, ambayo ilihusisha kumtolea Yehova kwa ukawaida ‘matunda ya kwanza yaliyo bora zaidi.’ (Kut. 23:19) Kwa kufanya hivyo, Waisraeli wangeonyesha kwamba wanathamini upendo na baraka za Yehova.—Soma Kumbukumbu la Torati 8:7-11.

7. Tunawezaje kutumia ‘vitu vyetu vyenye thamani’ kuonyesha kwamba tunampenda Yehova?

7 Sisi pia, tunaweza kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kwa kumpa “vitu vyetu vyenye thamani.” (Met. 3:9) Tunawezaje kufanya hivyo? Tunaweza kutumia vitu vyetu kuendeleza kazi ya Ufalme katika eneo letu na ulimwenguni pote. Hiyo ni njia nzuri ya kuonyesha kwamba tunampenda Yehova, iwe tuna vitu vingi au vichache. (2 Kor. 8:12) Hata hivyo, kuna njia nyingine za kuonyesha kwamba tunampenda Yehova.

8, 9. Kuna uhusiano gani kati ya kumpenda na kumtumaini Yehova? Toa mfano.

8 Kumbuka kwamba Yesu aliwaambia wafuasi wake wasihangaikie chakula na mavazi, bali waendelee kuutafuta kwanza Ufalme. Alisema kwamba Baba yetu wa mbinguni anajua kile tunachohitaji hasa. (Mt. 6:31-33) Tunamtumaini Yehova na tuna uhakika kwamba atatutimizia mahitaji yetu. Hatuwezi kumpenda mtu ambaye hatumtumaini. Kwa hiyo, kadiri tunavyomtumaini Yehova ndivyo tunavyoonyesha kwamba tunampenda zaidi. (Zab. 143:8) Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, malengo na maisha yangu yanaonyesha kwamba ninampenda kikweli Yehova? Je, mambo ninayofanya kila siku yanaonyesha kwamba ninaamini anaweza kutosheleza mahitaji yangu?’

9 Ndugu anayeitwa Mike alimpenda na kumtumaini Yehova. Alipokuwa kijana, alitamani sana kumtumikia Mungu katika nchi ya kigeni. Alifunga ndoa na akapata watoto wawili, lakini tamaa yake haikufifia. Makala na ripoti mbalimbali kuhusu kutumikia kwenye eneo lenye uhitaji mkubwa zilimchochea sana, hivyo yeye na familia yake waliamua kurahisisha maisha yao. Waliuza nyumba yao na kuhamia kwenye nyumba ndogo ya kupanga. Mike alipunguza ukubwa wa biashara yake na akajifunza jinsi ya kuisimamia kupitia Intaneti. Kisha yeye na familia yake wakahamia nchi nyingine. Mike alisema hivi baada ya kutumikia huko kwa miaka miwili: “Tumejionea ukweli wa maneno ya Yesu kwenye Mathayo 6:33.”

TAFAKARI MAMBO AMBAYO MUNGU ANATUFUNDISHA

10. Kwa nini ni muhimu kutafakari mambo tunayojifunza kumhusu Yehova?

10 Mfalme Daudi alitafakari uumbaji wa Yehova. Aliandika hivi akichochewa na yale aliyoona: “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; nalo anga linatangaza kazi ya mikono yake.” Pia, alisema hivi kuhusu Sheria ya Mungu: “Sheria ya Yehova ni kamilifu, huirudisha nafsi. Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, humfanya asiye na uzoefu awe na hekima.” Kutafakari mambo hayo kulikuwa na matokeo gani? Daudi aliendelea kusema: “Maneno ya kinywa changu na kutafakari kwa moyo wangu na yawe yenye kupendeza mbele zako, Ee Yehova Mwamba wangu na Mkombozi wangu.” Ni wazi kwamba Daudi alisitawisha uhusiano wa karibu sana na Mungu.—Zab. 19:1, 7, 14.

11. Tunaweza kutumiaje ujuzi ambao Yehova ametupatia ili kuonyesha kwamba tunampenda? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 23.)

11 Leo, tunaelewa mambo mengi kuhusu uumbaji wa Yehova na kutimizwa kwa kusudi lake. Ulimwengu unawachochea watu wafuatilie elimu ya juu. Lakini watu wengi ambao wamefuatilia jambo hilo wamepoteza imani na upendo wao kwa Mungu. Hata hivyo, Biblia inatuhimiza tujipatie ujuzi, hekima na uelewaji. Mungu anataka tujifunze jinsi ya kutumia ujuzi ambao ametupatia kwa faida yetu na ya wengine. (Met. 4:5-7) “Mapenzi [ya Mungu] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova tunapojitahidi kumweleza kila mtu habari njema ya Ufalme na kuwasaidia watu waelewe kusudi la Mungu kwa wanadamu.—Soma Zaburi 66:16, 17.

12. Kijana mmoja alisema nini baada ya kupokea zawadi kutoka kwa Yehova?

12 Hata vijana wanaweza kuonyesha kwamba wanampenda Yehova kwa kuthamini mambo ya kiroho. Shannon alipokuwa na umri wa miaka 11, na mdogo wake alipokuwa na umri wa miaka 10, walihudhuria kusanyiko lenye kichwa “Ujitoaji Kimungu” pamoja na wazazi wao. Katika kipindi kimoja cha kusanyiko hilo, vijana wote waliombwa waketi katika eneo maalum. Ingawa Shannon alikuwa na wasiwasi, alienda kuketi kwenye eneo hilo. Alishangaa sana vijana wote walipopewa kitabu kizuri sana kinachoitwa Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. Shannon alihisije baada ya kupokea zawadi hiyo? Anasema hivi: “Wakati huo ndipo nilipogundua kwamba Yehova ni halisi na ananipenda sana mimi binafsi.” Shannon anaongeza hivi: “Tunamshukuru sana Mungu wetu mkuu, Yehova, kwa kutupatia zawadi bora kama hizo!”

KUBALI USHAURI NA NIDHAMU YA YEHOVA

13, 14. Tunapaswa kutendaje Yehova anapotutia nidhamu, na kwa nini?

13 Biblia inatukumbusha hivi: “Yeye ambaye Yehova anampenda, humkaripia, kama vile baba anavyomkaripia mwana anayemfurahia.” (Met. 3:12) Tunapaswa kutendaje Yehova anapotutia nidhamu? Mtume Paulo alisema wazi kwamba “hakuna nidhamu inayoonekana kwa sasa kuwa yenye shangwe, bali ni yenye kuhuzunisha.” Paulo hakuwa akipunguza uzito au umuhimu wa nidhamu kwa kuwa aliendelea kusema hivi: “Lakini baadaye kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo huzaa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.” (Ebr. 12:11) Ikiwa tunampenda Yehova, basi tutakubali nidhamu yake kwa moyo mkunjufu badala ya kuweka kinyongo. Hata hivyo, si rahisi kwa wengine kufanya hivyo. Lakini kumpenda Mungu kunaweza kutusaidia sana.

14 Katika siku za Malaki, Wayahudi wengi hawakutilia maanani maagizo ya Mungu. Waliijua Sheria inayohusu kutoa dhabihu, lakini waliipuuza kiasi cha kumlazimu Yehova awakaripie. (Soma Malaki 1:12, 13.) Jambo hilo lilikuwa na matokeo gani? Yehova alisema hivi: “Nitaleta juu yenu laana, nami nitazilaani baraka zenu. Ndiyo, hata nimeilaani baraka, kwa sababu hamwitii [sheria yangu] moyoni.” (Mal. 2:1, 2) Kwa kweli, kupuuza kimakusudi au kuwa na mazoea ya kupuuza maagizo ya Yehova kunaweza kuleta madhara makubwa.

Fuata viwango vya Mungu badala ya viwango vya ulimwengu (Tazama fungu la 15)

15. Tunapaswa kuepuka mtazamo gani?

15 Watu wengi katika ulimwengu huu wana ubinafsi, na hawapendi kushauriwa au kurekebishwa. Hata wale wanaokubali ushauri au nidhamu, mara nyingi wanafanya hivyo kwa shingo upande. Lakini Wakristo wanahimizwa ‘waache kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo.’ Tunapaswa kufanya ‘mapenzi ya Mungu yaliyo makamilifu.’ (Rom. 12:2) Yehova anatumia tengenezo lake kutushauri kuhusu mambo mbalimbali maishani. Kwa mfano, tunakumbushwa kuhusu jinsi tunavyopaswa kushirikiana na watu wa jinsia tofauti, kuchagua watu wa kushirikiana nao, na kuchagua burudani inayofaa. Tunapokubali na kutumia miongozo hiyo kwa hiari, tunaonyesha kwamba tunamshukuru na kumpenda Yehova kutoka moyoni.—Yoh. 14:31; Rom. 6:17.

TEGEMEA ULINZI NA WOKOVU WA YEHOVA

16, 17. (a) Kwa nini tunapaswa kuzingatia mapenzi ya Mungu tunapofanya uamuzi? (b) Waisraeli walionyeshaje kwamba hawampendi wala kumtumaini Yehova?

16 Kwa kawaida, watoto wanapoona hatari huwakimbilia wazazi wao. Kadiri watoto wanavyokua, wanaanza kujitegemea na kujifanyia maamuzi. Hiyo ni ishara ya utu uzima. Hata hivyo, watoto wenye uhusiano wa karibu na wazazi wao, huwaomba ushauri kabla ya kufanya uamuzi. Hivyo ndivyo ilivyo katika uhusiano wetu na Baba yetu wa mbinguni. Yehova ametupatia roho yake, inayotuchochea kuwa na “nia na kutenda.” Hata hivyo, tunaonyesha kwamba hatumpendi wala kumtumaini Mungu tunapofanya uamuzi bila kuzingatia mapenzi yake.—Flp. 2:13.

17 Katika siku za Samweli, Waisraeli walishindwa walipopigana na Wafilisti. Watu wa Mungu walihitaji sana msaada na ulinzi. Walifanya nini? Walisema hivi: “Na tujichukulie kutoka Shilo sanduku la agano la Yehova, ili lije katikati yetu na kutuokoa kutoka mkononi mwa adui zetu.” Ikawaje? “Mauaji hayo yakawa makubwa sana, hivi kwamba katika Israeli wakaanguka watu 30,000 wenye kwenda kwa miguu. Nalo sanduku la Mungu likatekwa.” (1 Sam. 4:2-4, 10, 11) Huenda ikaonekana kwamba Waisraeli walikuwa wakitafuta msaada wa Yehova walipochukua sanduku la agano. Hata hivyo, ni wazi kwamba hawakutafuta mwongozo wa Yehova; walikuwa wakifuata mawazo yao wenyewe, na walipata matokeo mabaya sana.—Soma Methali 14:12.

18. Biblia inatufundisha nini kuhusu kumtegemea Yehova?

18 Mtunga-zaburi alikuwa na mtazamo mzuri. Aliandika hivi: “Mngojee Mungu, kwa maana bado nitamsifu kuwa ndiye wokovu wangu mkuu. Ee Mungu wangu, nafsi yangu mwenyewe imekata tamaa ndani yangu. Ndiyo sababu ninakukumbuka.” (Zab. 42:5, 6) Kwa kweli alimpenda sana Yehova! Je, unampenda na kumtegemea Yehova kama mtunga-zaburi? Hata ikiwa jibu lako ni ndiyo, bado una nafasi ya kumtegemea zaidi. Biblia inatueleza hivi: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”—Met. 3:5, 6.

19. Wewe binafsi utaonyeshaje kwamba unampenda Yehova?

19 Kwa kutupenda sisi kwanza, Yehova ametusaidia kujua jinsi tunavyoweza kumpenda. Sikuzote na tutafakari upendo wake. Naam, acheni tuendelee kumpenda Mungu kwa ‘moyo wetu wote na kwa nafsi yetu yote na kwa akili yetu yote na kwa nguvu zetu zote.’—Marko 12:30.