Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mtu Asiye na Uzoefu Huamini Kila Neno”

“Mtu Asiye na Uzoefu Huamini Kila Neno”

“Mtu ambaye hasomi magazeti ni mpumbavu; lakini mtu anayeamini mambo anayosoma kwa sababu tu yameandikwa gazetini ni mpumbavu zaidi.” —August von Schlözer, mwanahistoria na mwandishi wa habari Mjerumani (1735-1809).

IKIWA mtu hakupaswa kuamini kila kitu kilichoandikwa magazetini miaka zaidi ya 200 iliyopita, basi inapaswa kuwa hivyo kuhusu habari nyingi tunazosoma kwenye Intaneti katika karne hii ya 21. Teknolojia ya kisasa inatuwezesha kupata habari nyingi sana; habari za kweli na za uwongo, zinazofaa na zisizofaa, nzuri na hatari. Tunapaswa kuchagua kwa makini habari tunazosoma. Wale ambao hawana uzoefu wa kutumia mtandao wanaweza kuamini kwa urahisi ripoti au habari fulani, iwe mpya au isiyo ya kawaida, kwa sababu tu ipo mtandaoni au wametumiwa na rafiki zao kupitia barua pepe. Biblia inaonya hivi: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Met. 14:15.

Tunawezaje kuwa “werevu” na kutambua habari za uwongo, za ulaghai, au habari nyingine zisizofaa zinazopatikana kwenye mtandao? Kwanza, jiulize hivi: ‘Je, habari hii inatoka katika tovuti rasmi, blogu, au chanzo kisichojulikana? Je, habari hii imewekwa kwenye tovuti inayoorodhesha habari hatari?’ * Kisha, tumia “ufahamu.” (Met. 1:3) Ikiwa unatilia shaka habari fulani, basi inawezekana habari hiyo si sahihi. Zaidi ya hayo, iwapo habari fulani inawaharibia wengine sifa, fikiria ni nani atafaidika ikiwa habari hiyo itaenezwa na kusudi la wale waliotoa habari hiyo.

JE, UNAWATUMIA WENGINE KILA HABARI UNAYOPOKEA?

Baadhi ya watu wanapenda kuwa wa kwanza kusambaza habari na huwatumia rafiki zao wote habari hizo bila kufikiria chanzo chake au matokeo ya kuzisambaza. (2 Sam. 13:28-33) Hata hivyo, ikiwa sisi ni “werevu,” tutafikiria madhara yanayoweza kutokea. Kwa mfano, labda habari hizo zinaweza kuharibu sifa ya mtu au shirika fulani.

Jitihada zinahitajika ili kuhakikisha ikiwa habari fulani inafaa au haifai. Ndiyo sababu wengine huamua kuacha uamuzi huo mikononi mwa yule atakayepokea ujumbe. Lakini je, atakuwa na muda wa kufanya hivyo? Wakati ni mali. (Efe. 5:15, 16) Badala ya kutuma tu ujumbe hata kama una mashaka nao, ni bora kuwa na mtazamo huu: “Ikiwa ninautilia shaka, basi ninapaswa kuufuta.”

Jiulize hivi: ‘Je, mimi huwatumia wengine kila ujumbe ninaopokea? Je, nimewahi kulazimika kuwaomba wengine msamaha kwa sababu ya kuwatumia habari isiyo sahihi au ya uwongo? Je, kuna mtu yeyote amewahi kuniomba niache kumtumia ujumbe wa aina fulani?’ Kumbuka kwamba wale walio na anwani za barua pepe wanaweza pia kutumia Intaneti kutafuta habari wanazopenda bila msaada wako. Hawahitaji kulemewa na hadithi nyingi za vichekesho, video, au picha. Pia, si jambo la hekima kuwatumia wengine rekodi au maandishi ya hotuba. * Zaidi ya hayo, kuwatumia wengine habari ulizofanyia utafiti, maandiko uliyosoma katika funzo la kibinafsi, au majibu yatakayotumiwa katika mikutano kutapunguza thamani ya kujitayarisha kibinafsi.

Je, nitume ujumbe huu kwa mtu mwingine

Unapaswa kufanya nini ukiona habari za uwongo kuhusu tengenezo la Yehova kwenye Intaneti? Kataa kabisa habari hizo. Baadhi ya watu hufikiri kwamba wanapaswa kuwaonyesha wengine habari za aina hiyo ili kujua maoni yao, lakini kufanya hivyo hakuna faida yoyote zaidi ya kuendelea tu kueneza habari hatari. Ikiwa tunatatizwa na habari fulani kwenye Intaneti, tunapaswa kumwomba Yehova atupe hekima na kuongea na ndugu wakomavu kuhusu jambo hilo. (Yak. 1:5, 6; Yuda 22, 23) Yesu, ambaye alishtakiwa kwa uwongo, aliwaonya wafuasi wake kwamba maadui wangewatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu [yao].” (Mt. 5:11; 11:19; Yoh. 10:19-21) Tunahitaji kutumia “uwezo wa kufikiri” na “utambuzi” ili kujua “mtu anayesema mambo mapotovu” na wale ambao “mapito yao yamepotoka.”—Met. 2:10-16.

HESHIMU HAKI ZA WENGINE

Tunapaswa kuwa waangalifu pia kuhusu habari za kiroho au mambo yaliyoonwa tunayotumiwa na wengine. Hata kama habari hizo ni za kweli, mara nyingine si lazima tuzieneze. Wakati mwingine haifai au si haki kueneza habari fulani hata kama ni za kweli. (Mt. 7:12) Kwa mfano, hakuna faida ya kueneza porojo, hata ikiwa habari hizo ni sahihi. (2 The. 3:11; 1 Tim. 5:13) Habari fulani zinaweza kuwa za siri, na tunapaswa kuheshimu haki za wengine za kufunua habari hizo kwa wakati unaofaa na kwa njia inayofaa. Kueneza habari kabla ya wakati kunaweza kusababisha madhara makubwa.

Leo ni rahisi sana kueneza habari, iwe ni za kweli au za uwongo, zinazofaa au zisizofaa, nzuri au hatari. Hata hivyo, tambua kwamba ukituma barua pepe au ujumbe kwa mtu fulani, iwe ni kwa kukusudia au bila kukusudia, ujumbe huo unaweza kuenea duniani kote ndani ya muda mfupi sana. Hivyo, acheni tupinge kishawishi cha kuwa na haraka ya kutuma ujumbe fulani kwa kila mtu tunayemjua. Hatupaswi kuwa wajinga na kuamini kila habari mpya au yenye kusisimua. Zaidi ya yote, upendo utatusaidia kutoamini habari mbaya kuhusu tengenezo la Yehova au uwongo kuhusu ndugu zetu unaoenezwa na watu ambao ni watumwa wa “baba ya uwongo,” Shetani Ibilisi. (Yoh. 8:44; 1 Kor. 13:7) Uwezo wa kufikiri na utambuzi utatusaidia kuwa “werevu” na kutafakari jinsi tunavyotumia habari nyingi tunazopata kila siku. Biblia inasema, “wasio na uzoefu hakika watarithi upumbavu, lakini werevu watavaa ujuzi kama vazi la kichwani.”—Met. 14:18.

^ fu. 4 Uwe chonjo kwa sababu habari ambayo mwanzoni ilijulikana kuwa hatari au ya uwongo, inaweza kubadilishwa kwa njia fulani ili ionekane kuwa ya kweli.

^ fu. 8 Tazama Huduma Yetu ya Ufalme, Aprili 2010, “Sanduku la Swali.”