Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtumikie Yehova Bila Kukengeuka

Mtumikie Yehova Bila Kukengeuka

‘Maria aliendelea kulisikiliza neno lake Yesu. Martha alikengeushwa na kazi nyingi.’ —LUKA 10:39, 40.

NYIMBO: 94, 134

1, 2. Kwa nini Yesu alimpenda Martha? Lakini tunajuaje kwamba Martha hakuwa mkamilifu?

UNAFIKIRI Martha alikuwa mtu wa aina gani? Yeye ndiye mwanamke pekee anayetajwa kwa jina kwamba alipendwa na Yesu. Bila shaka, Yesu aliwapenda wanawake wengine waliomtumikia Mungu kama vile mama yake mpendwa na Maria dada ya Martha. (Yoh. 11:5; 19:25-27) Hata hivyo, kwa nini Yesu alimpenda Martha?

2 Yesu alimpenda Martha kwa sababu alikuwa mkarimu na mwenye bidii, na zaidi ya yote, alikuwa mwanamke wa kiroho. Aliamini kabisa mafundisho ya Yesu, na hakuwa na shaka hata kidogo kwamba Yesu alikuwa Masihi aliyeahidiwa. (Yoh. 11:21-27) Hata hivyo, Martha hakuwa mkamilifu kama tu wanadamu wengine. Wakati fulani, Yesu alipowatembelea nyumbani, Martha alimkasirikia dada yake kwa sababu ya jambo ambalo alifikiri si sawa na akamwambia Yesu amrekebishe. Martha alisema hivi: “Bwana, hujali kwamba dada yangu ameniacha peke yangu kushughulikia mambo? Kwa hiyo, mwambie aje anisaidie.” (Soma Luka 10:38-42.) Simulizi hilo linatufundisha nini?

MARTHA ALIKENGEUKA

3, 4. Ni kwa njia gani Maria alichagua “fungu jema,” na Martha alijifunza nini? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

3 Yesu alifurahia ukarimu wa Martha na Maria, naye alitaka kutumia nafasi hiyo kuwapa zawadi ya kiroho. Maria alitumia fursa hiyo kujifunza moja kwa moja kutoka kwa Mwalimu Mkuu, hivyo “aliketi miguuni pa Bwana na . . . , kulisikiliza neno lake.” Martha angeweza kufanya vivyo hivyo. Bila shaka, Yesu angempongeza ikiwa angefanya hivyo.

4 Hata hivyo, Martha alikuwa na shughuli nyingi akitayarisha mlo na kufanya kazi nyingine ili tukio hilo liwe la pekee. Lakini mambo hayo yalimsababishia mahangaiko yasiyo ya lazima, na kufanya amkasirikie Maria. Yesu alitambua kwamba Martha anahangaikia mambo mengi, hivyo akamwambia hivi kwa upole: “Martha, Martha, wewe unahangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi.” Kisha akasema kwamba hata mlo mmoja tu ungetosha. Halafu Yesu akamgeukia Maria na kumwondolea wasiwasi kwa kusema hivi: “Maria alichagua fungu jema, nalo halitaondolewa kwake.” Baada ya muda mfupi, Maria angesahau chakula walichokula wakati huo, lakini hangesahau kamwe pongezi na mambo aliyofundishwa na Yesu. Zaidi ya miaka 60 baadaye, mtume Yohana aliandika hivi: “Yesu alimpenda Martha na dada yake.” (Yoh. 11:5) Maneno hayo yanaonyesha kwamba Martha alikubali kurekebishwa na Yesu na akajitahidi kumtumikia Yehova kwa uaminifu maishani mwake.

5. Ulimwengu leo ukoje, na hilo linazusha swali gani?

5 Leo kuna mambo mengi sana yanayoweza kutukengeusha kuliko ilivyokuwa katika nyakati za Biblia. “Leo wanadamu wana mifumo bora sana ya mawasiliano kuliko wakati mwingine wowote katika historia, mashine za kuchapishia zenye kasi, magazeti yenye picha nyingi, redio, filamu, televisheni. . . . Kila siku tunapata mambo mapya yanayokengeusha . . . Miaka michache iliyopita, watu walifikiri kwamba hii ni ‘Enzi ya Elimu.’ Kadiri siku zinavyopita inakuwa ‘Enzi ya Vikengeusha Fikira.’” Maneno hayo yalisemwa zaidi ya miaka 60 iliyopita kwa kikundi cha wanafunzi nchini Marekani. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 1958 lilisema hivi: “Inaonekana mambo yanayokengeusha yatazidi kuongezeka kadiri ulimwengu huu unavyokaribia mwisho.” Maneno hayo ni ya kweli kabisa! Jambo hilo linazusha swali hili muhimu: Tunaweza kufanya nini ili tusikengeuke, na tuendelee kukazia fikira mambo ya kiroho kama Maria?

USIUTUMIE ULIMWENGU KWA UKAMILI

6. Watu wa Yehova wanatumiaje teknolojia ya ulimwengu?

6 Sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova inatumia vizuri teknolojia ya ulimwengu kuendeleza ibada ya kweli. Kwa mfano, kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, na wakati vita hivyo vikiendelea, mamilioni ya watu walionyeshwa sinema ya Photo-Drama of Creation.” Sinema hiyo ilikuwa na picha za rangi na muziki, na ilimalizia kwa kufafanua Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Yesu Kristo. Baadaye, ujumbe wa Ufalme ulienezwa kupitia redio za umma na kuwafikia mamilioni ya watu duniani kote. Leo, teknolojia ya kompyuta na Intaneti inatumiwa sana kueneza habari njema, na kuwafikia watu katika kila kona ya dunia.

Usiruhusu mambo yasiyo ya lazima yavuruge mambo ya kiroho (Tazama fungu la 7)

7. (a) Kwa nini ni hatari kuutumia ulimwengu kwa ukamili? (b) Tunapaswa kujihadhari na nini? (Tazama maelezo ya chini.)

7 Biblia inatuonya kuhusu hatari ya kuutumia ulimwengu kwa ukamili. (Soma 1 Wakorintho 7:29-31.) Mkristo anaweza kupoteza muda mwingi katika mambo ya ulimwengu ambayo huenda si mabaya; mambo kama vile burudani, kutazama televisheni, kutembelea maeneo yenye vivutio, kuzunguka madukani ili tu kuangalia bidhaa, na kutafuta vifaa vya kisasa vya elektroniki. Kutumia mitandao ya kijamii, kutumiana ujumbe mfupi, barua pepe, na kuangalia kila wakati habari mpya au matukio ya michezo kunaweza pia kupoteza muda na hata kuwa uraibu. * (Mhu. 3:1, 6) Ikiwa hatudhibiti muda tunaotumia kufanya mambo yasiyo ya lazima, tunaweza kuanza kupuuza jambo muhimu zaidi, yaani, kumwabudu Yehova.—Soma Waefeso 5:15-17.

8. Kwa nini tunashauriwa tusipende vitu vilivyo katika ulimwengu?

8 Shetani amekusudia ulimwengu wake utuvutie na kutukengeusha. Alifanya hivyo katika karne ya kwanza, na anafanya hivyo zaidi katika siku zetu. (2 Tim. 4:10) Hivyo, tunapaswa kufuata ushauri huu: ‘Msipende vitu vilivyo katika ulimwengu.’ Ikiwa tutajichunguza mara kwa mara na kufanya marekebisho yanayohitajika, hatutakengeuka na tutampenda zaidi Baba yetu wa mbinguni. Tukifanya hivyo, itakuwa rahisi kufanya mapenzi ya Mungu, naye atatubariki milele.—1 Yoh. 2:15-17.

USIKENGEUKE

9. Yesu aliwashauri nini wafuasi wake, naye alituwekea mfano gani?

9 Maneno ambayo Yesu alimwambia Martha yanapatana kabisa na mafundisho yake na mfano aliotuwekea. Yesu aliwatia moyo wafuasi wake wawe na jicho “rahisi” ili wasikengeuke wanapomtumikia Mungu. (Soma Mathayo 6:22, 33.) Yesu hakukengeushwa na vitu vya kimwili; hakuwa na nyumba wala shamba.—Luka 9:58; 19:33-35.

10. Yesu aliweka mfano gani mwanzoni mwa huduma yake?

10 Yesu hakuruhusu jambo lolote limkengeushe katika kazi ya kuhubiri. Mwanzoni mwa huduma yake, baada ya kuufundisha umati wa watu na kufanya miujiza huko Kapernaumu, watu walimsihi abaki katika jiji hilo. Yesu alitendaje? Alisema hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:42-44) Yesu alifanya kama alivyosema; alitembea huku na huku katika eneo la Palestina, akihubiri na kufundisha. Ingawa alikuwa mkamilifu, Yesu alikuwa na mahitaji ya kawaida ya kibinadamu na wakati mwingine alichoka sana.—Luka 8:23; Yoh. 4:6.

11. Yesu alimwambia nini mwanaume aliyekuwa na mgogoro wa kifamilia? Naye alitoa onyo gani?

11 Baadaye, Yesu alipokuwa akiwafundisha watu jinsi ya kukabiliana na upinzani, mtu mmoja alimkatiza kwa kusema hivi: “Mwalimu, mwambie ndugu yangu tugawane urithi.” Lakini Yesu alikataa kuingilia mgogoro huo. Alimjibu hivi: “Wewe mtu, nani aliyeniweka mimi kuwa mwamuzi au mgawaji juu yenu?” Kisha akaendelea kufundisha akiwaonya wasikilizaji wake kwamba tamaa ya vitu vya kimwili inaweza kuwakengeusha katika utumishi wao.—Luka 12:13-15.

12, 13. (a) Ni nini kilichowavutia Wagiriki wageuzwa imani? (b) Yesu alitendaje watu hao walipoomba kukutana naye?

12 Yesu alikuwa na mkazo mkubwa katika juma la mwisho la maisha yake duniani. (Mt. 26:38; Yoh. 12:27) Alikuwa na kazi nyingi, aliaibishwa na akauawa kikatili. Kwa mfano, fikiria kilichotokea Jumapili, Nisani 9, mwaka wa 33 W.K. Kama ilivyotabiriwa, Yesu aliingia Yerusalemu akiwa amepanda mwana-punda, na umati ulimsifu kwa kusema, ‘anayekuja ni Mfalme katika jina la Yehova.’(Luka 19:38) Siku iliyofuata, Yesu aliingia hekaluni na kuwafukuza wafanyabiashara wenye pupa waliokuwa wakiuza vitu kwa bei ghali na hivyo wakawa kama wanyang’anyi. —Luka 19:45, 46.

13 Kati ya umati uliokuwa Yerusalemu, kulikuwa na baadhi ya Wagiriki wageuzwa imani. Ni wazi kwamba walivutiwa sana na Yesu, hivyo wakamwomba Filipo awakutanishe naye. Lakini Yesu hakukengeuka; aliendelea kukazia fikira mambo muhimu zaidi yaliyokuwa mbele yake. Hakujaribu kujitafutia umaarufu ili aepuke kifo cha kidhabihu mikononi mwa adui za Mungu. Kwa hiyo, baada ya kueleza kuhusu kifo chake, aliwaambia hivi Andrea na Filipo: “Yule anayeipenda sana nafsi yake huiangamiza, lakini yule anayeichukia nafsi yake katika ulimwengu huu atailinda kwa ajili ya uzima wa milele.” Badala ya kukengeushwa na Wagiriki hao wenye udadisi, Yesu alipendekeza wafuate mfano wake wa kujidhabihu na akaahidi hivi: “Ikiwa yeyote anataka kunihudumia, Baba atamheshimu huyo.” Bila shaka Filipo aliwarudishia wale Wagiriki ujumbe huo muhimu. —Yoh. 12:20-26.

14. Ingawa Yesu alitanguliza kazi ya kuhubiri, tunajuaje kwamba alikuwa na usawaziko?

14 Ingawa Yesu hakukengeuka na alikazia fikira kuhubiri habari njema, hakufikiria tu kazi yake wakati wote. Alikubali mwaliko wa harusi angalau mara moja na akachangia furaha ya sherehe hiyo kwa kufanya muujiza wa kubadilisha maji kuwa divai. (Yoh. 2:2, 6-10) Pia, alialikwa kwenye milo pamoja na rafiki zake na watu wengine. (Luka 5:29; Yoh. 12:2) Jambo muhimu zaidi ni kwamba mara kwa mara Yesu alitenga wakati wa kusali, kutafakari, na kupumzika.—Mt. 14:23; Marko 1:35; 6:31, 32.

‘ONDOA KILA UZITO’

15. Mtume Paulo alitoa ushauri gani, naye aliwekaje mfano mzuri?

15 Mtume Paulo alilinganisha maisha ya Mkristo aliyejiweka wakfu na shindano la mbio linalohitaji uvumilivu. Naye aliandika hivi: “Acheni . . . tuondoe kila uzito.” (Soma Waebrania 12:1.) Paulo aliishi kulingana na yale aliyofundisha; aliacha kazi nzuri, katika dini ya kiyahudi, ambayo ingeweza kumpa utajiri na umaarufu. Alikazia fikira “mambo yaliyo ya maana zaidi” na alimtumikia Mungu, akisafiri mara nyingi huko Siria, Asia Ndogo, Makedonia, na Yudea. Paulo aliandika hivi kuhusu tumaini lake la kuishi mbinguni: “Nayasahau mambo ya nyuma na kujinyoosha kwenda mbele kuelekea mambo yaliyo mbele, ninafuatilia kuelekea ule mradi kwa ajili ya tuzo.” (Flp. 1:10; 3:8, 13, 14) Alitumia vizuri useja, naye akafanikiwa “kumhudumia Bwana daima bila kukengeushwa fikira.”—1 Kor. 7:32-35.

16, 17. Tunawezaje kufuata mfano wa Paulo, iwe tumefunga ndoa au waseja? Toa mfano.

16 Kama Paulo, baadhi ya watumishi wa Mungu wameamua kubaki waseja ili wasiwe na majukumu mengi ya familia na wafanye mengi katika kazi ya Ufalme. (Mt. 19:11, 12) Mara nyingi watumishi wa Mungu waliooa au kuolewa wana majukumu mengi zaidi ya familia. Hata hivyo, sisi sote, iwe tumefunga ndoa au waseja, tunaweza ‘kuondoa kila uzito’ ili tumtumikie Mungu bila kukengeuka  kadiri iwezekanavyo. Huenda hilo likahusisha kuacha mazoea fulani yanayopoteza wakati  na kutumia muda mwingi zaidi katika utumishi wa Mungu.

17 Wafikirie Mark na Claire, wenzi wa ndoa kutoka nchini Wales. Wote walianza upainia baada ya kumaliza shule na waliendelea na upainia baada ya kuoana. Mark anaeleza hivi: “Tulirahisisha zaidi maisha yetu kwa kuacha nyumba yetu yenye vyumba vitatu na kazi yetu, ili tujiunge na kazi ya ujenzi wa kimataifa.” Katika miaka 20 iliyopita, wamesafiri maeneo mbalimbali ya Afrika, wakisaidia kujenga Majumba ya Ufalme. Wakati fulani walibaki na dola 15 tu, lakini Yehova aliwategemeza. Claire anasema hivi: “Tunaridhika sana tunapotumia kila siku kumtumikia Yehova. Tumepata marafiki wengi sana na hatujakosa kitu chochote. Mambo machache  tuliyoacha hayawezi kulinganishwa  na shangwe ya kumtumikia Yehova wakati wote.” Watumishi wengi wa wakati wote wanahisi vivyo hivyo. *

18. Tunaweza kujiuliza maswali gani?

18 Namna gani wewe? Unaweza kufanya nini ukigundua kwamba umekengeuka na hufurahii kumtumikia Yehova kama zamani? Labda unahitaji kusoma na kujifunza Biblia kwa njia yenye manufaa zaidi. Jinsi gani? Makala inayofuata itafafanua jambo hilo.

^ fu. 7 Tazama makala yenye kichwa “Mtu Asiye na Uzoefu Huamini Kila Neno.”

^ fu. 17 Tazama simulizi la maisha la Hadyn na Melody Sanderson katika makala yenye kichwa “Kujua Yaliyo Sawa na Kuyatenda.” (Mnara wa Mlinzi, Machi 1, 2006) Waliacha biashara nzuri huko Australia na kuanza utumishi wa wakati wote. Soma kilichotokea baada ya wao kuishiwa pesa walipokuwa wamishonari huko India.