Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unauona Mkono wa Yehova Maishani Mwako?

Je, Unauona Mkono wa Yehova Maishani Mwako?

Mkono wa Yehova hakika utajulishwa kwa watumishi wake.” —ISA. 66:14.

NYIMBO: 65, 26

1, 2. Watu fulani wana maoni gani kumhusu Mungu?

WATU wengi hufikiri kwamba hakuna uhusiano kati mambo wanayofanya na yale ambayo Mungu anafanya. Baadhi yao wanaamini kuwa Mungu hawajali wanadamu. Kwa mfano, kimbunga Haiyan kiliposababisha uharibifu mkubwa nchini Ufilipino mnamo Novemba 2013, meya wa jiji moja alisema hivi: “Ni wazi kwamba Mungu hakuwa pamoja nasi.”

2 Watu wengine hutenda kana kwamba Mungu haoni mambo wanayofanya. (Isa. 26:10, 11; 3 Yoh. 11) Wanafanana na watu ambao mtume Paulo aliwazungumzia aliposema hivi: “Hawakukubali kumjua Mungu,” bali ‘walijawa na ukosefu wote wa uadilifu, uovu, tamaa, na ubaya.’—Rom. 1:28, 29.

3. (a) Tunaweza kujiuliza maswali gani? (b) Mara nyingi Biblia inamaanisha nini inapozungumzia kuhusu “mkono” wa Yehova?

3 Namna gani sisi? Tofauti na watu waliotajwa awali, tunajua kuwa Yehova anaona kila kitu tunachofanya. Lakini je, kweli tunaamini kwamba anatujali? Je, tunauona mkono wa Mungu maishani mwetu? Na zaidi ya yote, je, sisi ni miongoni mwa watu ambao Yesu alisema “watamwona Mungu”? (Mt. 5:8) Ili kupata majibu ya maswali hayo, acheni tuchunguze mifano ya watu wanaotajwa katika Biblia ambao waliuona mkono wa Mungu maishani mwao na wale ambao hawakuuona. Kisha tutajifunza jinsi tunavyoweza kuuona mkono wa Yehova maishani mwetu. Tunapochunguza mambo hayo, kumbuka kwamba Biblia inapozungumzia “mkono” wa Mungu, mara nyingi inamaanisha nguvu zake, ambazo anazitumia kuwasaidia watumishi wake na kuwashinda maadui.—Soma Kumbukumbu la Torati 26:8.

HAWAKUUONA MKONO WA MUNGU

4. Kwa nini maadui wa Israeli hawakuuona mkono wa Mungu?

4 Zamani, watu walikuwa na fursa ya kuona na kusikia jinsi Mungu alivyowasaidia Waisraeli. Yehova alitumia miujiza kuwaokoa watu wake kutoka Misri, na kisha akawashinda wafalme wengi katika Nchi ya Ahadi. (Yos. 9:3, 9, 10) Ingawa wafalme wengi waliotawala eneo la magharibi ya Yordani walisikia na kuona miujiza hiyo, walikusanyika pamoja ili “kupigana vita na Yoshua na Israeli.” (Yos. 9:1, 2) Wafalme hao walipokuwa wakipigana na Israeli, bado walikuwa na nafasi ya kuuona mkono wa Mungu. Kwa nguvu za Yehova, “jua likasimama tuli, mwezi nao ukasimama, mpaka taifa [la Israeli] lilipokuwa limelipiza kisasi juu ya adui zake.” (Yos. 10:13) Yehova aliacha mioyo ya adui za watu wake “iwe migumu ili watangaze vita juu ya Israeli.” (Yos. 11:20) Maadui hao walishindwa kwa sababu hawakutaka kukubali kwamba Mungu alikuwa akiwapigania watu wake.

5. Mfalme Ahabu hakutambua jambo gani?

5 Miaka mingi baadaye, Mfalme Ahabu alikuwa na fursa za kuuona mkono wa Mungu. Eliya alimwambia hivi: “Hakutakuwa na umande wala mvua, isipokuwa kwa agizo la neno langu!” (1 Fal. 17:1) Ingawa maneno hayo yalitoka kwa Yehova, Ahabu hakuyaamini. Baadaye, Ahabu aliona Yehova akijibu sala ya Eliya kwa kushusha moto ulioteketeza dhabihu. Kisha, Eliya alimwambia Ahabu kwamba Yehova angekomesha ukame, kwa kusema hivi: “Funga gari! Nawe ushuke ili mvua kubwa isikuzuie!” (1 Fal. 18:22-45) Ahabu aliona miujiza yote hiyo, lakini bado hakutambua kwamba alikuwa akiona nguvu za Mungu. Mifano hiyo miwili inatufundisha jambo muhimu sana: tunapaswa kuwa macho ili tutambue jinsi Yehova anavyotusaidia maishani mwetu.

WALIUONA MKONO WA YEHOVA

6, 7. Rahabu na Wagibeoni walitambua nini?

6 Tofauti na wafalme hao waovu, kuna watu ambao waliuona mkono wa Mungu, licha ya kwamba wote walikabili hali zinazofanana. Kwa mfano, Wagibeoni waliamua kufanya amani na Waisraeli badala ya kupigana nao. Kwa nini? Walisema hivi: “Watumishi wako wametoka nchi ya mbali sana kwa sababu ya jina la Yehova Mungu wako, kwa kuwa tumesikia sifa zake na mambo yote ambayo alitenda.” (Yos. 9:3, 9, 10) Kwa busara walitambua kwamba Yehova ndiye aliyekuwa akiwasaidia Waisraeli.

7 Rahabu pia aliuona mkono wa Yehova maishani mwake. Baada ya kusikia jinsi Yehova alivyowakomboa watu wake, aliwaambia hivi wapelelezi wawili Waisraeli: “Najua hakika ya kwamba Yehova atawapa nchi hii.” Ingawa ilikuwa hatari kuwaunga mkono Waisraeli, Rahabu aliamini kwamba Yehova angemwokoa yeye na familia yake.—Yos. 2:9-13; 4:23, 24.

8. Waisraeli fulani walitambuaje nguvu za Mungu?

8 Tofauti na Mfalme Ahabu ambaye alikuwa mwovu, Waisraeli wengine ambao walishuhudia Yehova akijibu sala ya Eliya, walitambua mkono wa Mungu. Walipoona moto kutoka mbinguni ukiteketeza dhabihu, walisema hivi: “Yehova ndiye Mungu wa kweli!” (1 Fal. 18:39) Waliona waziwazi uthibitisho wa nguvu za Mungu.

9. Tunawezaje kuuona mkono wa Yehova leo?

9 Mifano mizuri na mibaya ambayo tumezungumzia inatusaidia kuelewa maana ya kumwona Mungu au kuuona mkono wake maishani mwetu. Tunapoendelea kumjua Yehova na sifa zake, sisi pia tunaweza kuuona mkono wake kwa ‘macho ya moyo wetu.’ (Efe. 1:18) Kwa kweli, tunataka kuwaiga watu waaminifu ambao wameona jinsi Yehova anavyowasaidia watu wake. Hata hivyo, tuna uhakika gani kwamba Mungu anawasaidia watu leo?

UTHIBITISHO WA MKONO WA MUNGU LEO

10. Tuna uhakika gani kwamba Yehova anawasaidia watu leo? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

10 Tuna sababu nyingi za kuamini kwamba Yehova anaendelea kuwasaidia watu wake. Mara nyingi tumesikia masimulizi ya watu yanayoonyesha jinsi sala zao za kuomba msaada wa kiroho zilivyojibiwa. (Zab. 53:2) Allan alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba katika kisiwa fulani kidogo nchini Ufilipino, alikutana na mwanamke ambaye ghafla alianza kulia. Allan anaeleza hivi: “Siku hiyo asubuhi, alikuwa amesali ili Mashahidi wa Yehova wamtembelee. Alipokuwa kijana alijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, lakini hakuonana nao tena baada ya kuolewa na kuhamia katika kisiwa hicho. Mungu alijibu sala yake haraka na hilo lilimgusa moyo sana.” Alijiweka wakfu kwa Yehova mwaka huohuo.

Je, unaona jinsi Yehova anavyowasaidia watu wake leo? (Tazama fungu la 11-13)

11, 12. (a) Yehova anawasaidiaje watumishi wake? (b) Simulia jinsi Yehova alivyomsaidia Amy.

11 Watumishi wengi wa Mungu wamejionea jinsi alivyowasaidia kuacha tabia mbaya, kama vile kuvuta sigara, kutumia dawa za kulevya, au kutazama ponografia. Baadhi yao wanasema kwamba walijaribu tena na tena kuacha tabia hizo kwa jitihada zao lakini hawakufanikiwa. Hata hivyo, walipomwomba Yehova msaada, wakapata “nguvu zinazopita zile za kawaida,” na hatimaye wakashinda udhaifu wao.—2 Kor. 4:7; Zab. 37:23, 24.

12 Yehova amewasaidia watumishi wake wengi kukabiliana na hali ngumu. Kwa mfano, Amy alikabili changamoto nyingi alipopewa mgawo wa kusaidia kujenga Jumba la Ufalme na nyumba ya wamishonari katika kisiwa fulani kidogo cha Pasifiki. Anasema hivi: “Tulikaa kwenye hoteli ndogo, na kila siku tulitembea kwenye barabara zilizojaa maji ili kufika kwenye eneo la ujenzi.” Alihitaji kuzoea utamaduni tofauti, na kulikuwa na tatizo kubwa la umeme na maji. Amy anaongezea hivi: “Kwa kusikitisha, siku moja nilimfokea dada fulani niliyefanya naye kazi. Niliporudi nyumbani nilijihisi sifai kabisa. Nikiwa chumbani kwangu, nilimweleza Yehova yote yaliyokuwa moyoni, nikimwomba anisaidie.” Umeme uliporudi, Amy alisoma gazeti la Mnara wa Mlinzi lililokuwa na makala inayohusu mahafali ya Gileadi. Makala hiyo ilizungumzia mambo yote aliyokuwa akikabili, yaani, utamaduni mpya, kukumbuka nyumbani, na jinsi ya kuishi na watu ambao hakuwazoea. Anasema hivi: “Nilihisi Yehova alikuwa akiongea nami usiku huo. Jambo hilo lilinichochea niendelee na mgawo wangu.”—Zab. 44:25, 26; Isa. 41:10, 13.

13. Kuna uthibitisho gani unaoonyesha kwamba Yehova anawasaidia watu wake “kutetea na kuithibitisha kisheria” habari njema?

13 Uthibitisho mwingine wa mkono wenye nguvu wa Mungu ni mafanikio ambayo Mashahidi wa Yehova wamepata katika “kutetea na kuithibitisha kisheria” habari njema. (Flp. 1:7) Baadhi ya serikali zimejaribu kuzuia kabisa kazi ya watu wa Mungu. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wameshinda kesi 268 hivi katika mahakama za juu, zikiwemo kesi 24 katika Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu tangu mwaka 2000. Hilo linaonyesha wazi kwamba hakuna mtu anayeweza kuuzuia mkono wenye nguvu wa Mungu.—Isa. 54:17; soma Isaya 59:1.

14. Mkono wa Yehova unaonekana katika njia gani nyingine?

14 Kuhubiriwa kwa habari njema duniani kote ni uthibitisho mwingine wa msaada wa Yehova. (Mt. 24:14; Mdo. 1:8) Mbali na hilo, umoja na undugu wa ulimwenguni pote wa watu wa Yehova leo ni wa pekee sana hivi kwamba ulimwengu hauwezi kuiga. Kwa hiyo hatushangai watu wanaposema, “Kwa kweli Mungu yupo katikati yenu.” (1 Kor. 14:25) Hivyo, tukiwa kikundi, tuna uthibitisho mwingi sana unaoonyesha kwamba Mungu anawasaidia watu wake. (Soma Isaya 66:14.) Lakini namna gani wewe? Je, unauona mkono wenye nguvu wa Yehova maishani mwako?

JE, UNAUONA MKONO WA YEHOVA MAISHANI MWAKO?

15. Ni nini kinachoweza kufanya tusiuone mkono wa Yehova maishani?

15 Nyakati nyingine tunaweza kushindwa kuuona mkono wa Yehova maishani mwetu. Kwa nini? Kwa sababu changamoto za maisha zinaweza kutulemea. Chini ya hali hiyo, tunaweza kusahau jinsi ambavyo Yehova alitusaidia awali. Malkia Yezebeli alipotaka kumuua nabii Eliya, kwa muda fulani nabii huyo alisahau jinsi Mungu alivyomsaidia. Biblia inasema hivi kumhusu Eliya: “Akaanza kuomba kwamba nafsi yake ife.” (1 Fal. 19:1-4) Eliya angepata wapi suluhisho la tatizo lake? Alihitaji kumtegemea Yehova ili amwimarishe.—1 Fal. 19:14-18.

16. Tunaweza kufanya nini ili tuuone mkono wa Mungu kama Ayubu?

16 Mwanzoni, Ayubu alikengeushwa na mahangaiko yake hivi kwamba hakuona mambo kama Yehova alivyoyaona. (Ayu. 42:3-6) Nyakati fulani, huenda ikawa vigumu kwetu kuuona mkono wa Mungu kwa sababu ya matatizo tunayokabili. Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda hali hiyo? Tunahitaji kutafakari yale ambayo Maandiko yanasema kuhusu mambo tunayokabili. Kadiri tunavyoona jinsi Yehova anavyotusaidia, ndivyo anavyokuwa halisi zaidi kwetu. Mwishowe, sisi pia tunaweza kusema hivi kama Ayubu: “Nimesikia habari zako kwa fununu, lakini sasa jicho langu mwenyewe linakuona wewe.”

Je, Yehova anakutumia kuwasaidia wengine wauone mkono wake? (Tazama fungu la 17 na 18)

17, 18. (a) Tunawezaje kutambua msaada wa Yehova? (b) Simulia mfano unaoonyesha jinsi Yehova anavyotusaidia leo.

17 Tunawezaje kuuona mkono wa Yehova? Fikiria mifano ifuatayo: Labda unahisi kwamba Yehova ndiye aliyekusaidia kupata kweli. Huenda umewahi kusikia jambo fulani katika mikutano ya Kikristo na ukawaza hivi: “Kwa kweli habari hii inanihusu mimi.” Au je, umewahi kuona jinsi Yehova alivyojibu sala yako? Huenda ulikuwa na lengo la kuongeza utumishi wako na ulishangaa kuona jinsi Yehova alivyokusaidia kutimiza lengo hilo. Au labda wakati fulani uliacha kazi yako kwa ajili ya mambo ya kiroho na kisha ukajionea ukweli wa ahadi hii ya Mungu: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” (Ebr. 13:5) Tukiwa macho kiroho, tunaweza kutambua jinsi ambavyo Yehova ametusaidia kwa njia mbalimbali.

18 Sarah, anayeishi nchini Kenya, anaeleza hivi: “Nilisali kuhusu mwanafunzi fulani ambaye nilifikiri kwamba hafurahii kujifunza Biblia. Nilimwomba Yehova anisaidie kujua ikiwa ninapaswa kuendelea kumfundisha Biblia au la. Baada tu ya kusema ‘Amina,’ simu yangu ikaanza kuita. Mwanafunzi huyo alinipigia ili kuniuliza kama ninaweza kwenda naye mkutanoni! Nilishangaa sana!” Ukiwa macho, wewe pia utaona jinsi ambavyo Yehova anakusaidia kwa njia nyingi maishani mwako. Rhonna, dada anayeishi barani Asia, anasema kwamba tunahitaji kutafakari mambo tuliyopitia maishani ili tutambue jinsi Yehova alivyotusaidia. Anaongezea hivi: “Lakini baada kujionea jambo hilo, unastaajabu kutambua jinsi Yehova anavyotujali!”

19. Tunapaswa kufanya nini zaidi ili tujionee mkono wa Yehova?

19 Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio safi moyoni, kwa kuwa watamwona Mungu.” (Mt. 5:8) Tunawezaje kuwa “safi moyoni”? Tunapaswa kuwa na mawazo safi na kuacha mwenendo mbaya. (Soma 2 Wakorintho 4:2.) Tukiendelea kukua kiroho na kudumisha mwenendo mzuri, tutajionea mkono wa Mungu maishani mwetu. Katika makala inayofuata tutazungumzia jinsi imani inavyoweza kutusaidia kuuona mkono wa Yehova waziwazi zaidi.