Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tupe Imani Zaidi”

“Tupe Imani Zaidi”

“Unisaidie mahali ambapo ninahitaji imani!”—MARKO 9:24.

NYIMBO: 81, 135

1. Kwa nini ni muhimu sana kuwa na imani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

UMEWAHI kujiuliza hivi: ‘Je, Yehova ataniokoa wakati wa dhiki kuu na kuniingiza katika ulimwengu mpya?’ Kwa kweli, wokovu unahusisha mambo mengi, lakini mtume Paulo alitaja sifa moja muhimu sana tunayohitaji kusitawisha ili tuokolewe. Aliandika hivi: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza vema.” (Ebr. 11:6) Huenda jambo hilo likaonekana kuwa rahisi sana, lakini ukweli ni kwamba “imani si mali ya watu wote.” (2 The. 3:2) Maandiko hayo yanatusaidia kuelewa umuhimu wa kuimarisha imani yetu.

2, 3. (a) Andiko la 1 Petro 1:7 linatufundisha nini kuhusu umuhimu wa imani? (b) Tutajibu maswali gani katika makala hii?

2 Mtume Petro alizungumzia pia umuhimu wa imani “iliyojaribiwa.” (Soma 1 Petro 1:7.) Kwa kuwa dhiki kuu inakaribia sana, tunataka kuwa “namna ya watu walio na imani ya kuihifadhi hai nafsi.” (Ebr. 10:39) Hivyo, tunahitaji kufanya yote tuwezayo ili kuimarisha imani yetu. Lengo letu ni kuwa miongoni mwa wale watakaothawabishwa wakati Yesu Kristo, Mfalme wetu, atakapofunuliwa. Tukiwa na wazo hilo, sisi pia tunaweza kuomba kama yule mwanaume aliyesema hivi: “Unisaidie mahali ambapo ninahitaji imani!” (Marko 9:24) Au kama vile mitume wa Yesu, huenda sisi pia tukachochewa kusema: “Tupe imani zaidi.”—Luka 17:5.

3 Katika makala hii tutajibu maswali yafuatayo: Tunawezaje kuimarisha imani yetu? Tunawezaje kuonyesha kwamba tuna imani? Na tuna uhakika gani kwamba sala zetu za kuomba imani zaidi zitajibiwa?

IMARISHA IMANI YAKO

4. Ni mifano gani inayoweza kuimarisha imani yetu?

4 Tunaweza kujifunza mambo mengi katika masimulizi ya Biblia, kwa kuwa “mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha.” (Rom. 15:4) Tunaposoma habari za watu wanaotajwa katiba Biblia kama vile Abrahamu, Sara, Isaka, Yakobo, Musa, Rahabu, Gideoni, Baraka, na wengine wengi, tunachochewa kuchunguza imani yetu. (Ebr. 11:32-35) Isitoshe, masimulizi ya watumishi wa Yehova leo ambao wameonyesha imani thabiti, yanaweza kutuchochea tufanye kila tuwezalo kuimarisha imani yetu. *

5. Eliya alionyeshaje kwamba ana imani yenye nguvu? Na inafaa tujiulize swali gani?

5 Mfano mmoja katika Biblia ni nabii Eliya. Wazia matukio yafuatayo yanayoonyesha jinsi alivyomtumaini Yehova. Eliya alipomjulisha Mfalme Ahabu kwamba Yehova amekusudia kuleta ukame, alimweleza hivi kwa uhakika: “Kama anavyoishi Yehova . . . hakutakuwa na umande wala mvua, isipokuwa kwa agizo la neno langu!” (1 Fal. 17:1) Eliya aliamini kwamba Yehova angetosheleza mahitaji yake na ya wengine wakati wa ukame. (1 Fal. 17:4, 5, 13, 14) Alikuwa na uhakika kwamba Yehova angemfufua mwana wa mjane. (1 Fal. 17:21) Hakuwa na shaka kwamba moto wa Yehova ungeteketeza dhabihu yake kwenye Mlima Karmeli. (1 Fal. 18:24, 37) Wakati wa Yehova wa kumaliza ukame ulipofika, Eliya alimwambia hivi Ahabu hata ingawa hakukuwa na dalili yoyote ya mvua: “Panda ukale na kunywa; kwa maana kuna kishindo cha machafuko ya mvua kubwa.” (1 Fal. 18:41) Baada ya kuchunguza masimulizi hayo, inafaa tujiulize, ‘Je, nina imani thabiti kama Eliya?’

TUNAWEZAJE KUIMARISHA IMANI YETU?

6. Tunapaswa kufanya nini ili Yehova atusaidie kuimarisha imani yetu?

6 Hatuwezi kuimarisha imani kwa nguvu zetu. Kwa nini? Kwa sababu imani ni sifa ya tunda la roho takatifu ya Mungu. (Gal. 5:22) Hivyo, ni jambo la busara kuomba roho takatifu kwa kuwa Yesu anatuhakikishia kwamba Baba ‘huwapa roho takatifu wale wanaomwomba.’—Luka 11:13.

7. Toa mfano unaoonyesha jinsi tunavyoweza kudumisha imani thabiti.

7 Baada ya kuimarisha imani yetu, tunapaswa kuendelea kuidumisha. Tunaweza kulinganisha imani yetu na moto wa mkaa. Mkaa unapokolezwa, moto wake huwa mkali sana. Hata hivyo, mkaa usipoongezwa kwenye jiko, moto utafifia na mwishowe yatabaki majivu. Lakini ikiwa unaongeza mkaa, basi moto utaendelea kuwa mkali. Vivyo hivyo, imani yetu itaendelea kuwa hai ikiwa tunasoma kwa ukawaida Neno la Mungu. Tukijifunza Biblia kwa ukawaida tutampenda zaidi Yehova na Neno lake, na huo ni msingi mzuri wa kuimarisha imani yetu.

8. Ni jambo gani lingine linaloweza kutusaidia tuimarishe na kudumisha imani yetu?

8 Unaweza kufanya jambo gani lingine ili kuimarisha na kudumisha imani yako? Usiridhike tu kujua mambo uliyojifunza kabla ya ubatizo. (Ebr. 6:1, 2) Jifunze unabii mbalimbali ambao tayari umetimizwa kwa kuwa kufanya hivyo kutajenga na kuimarisha imani yako. Isitoshe, unaweza kutumia Neno la Mungu kupima imani yako ikiwa inafikia viwango vinavyotajwa katika Biblia.—Soma Yakobo 1:25; 2:24, 26.

9, 10. Imani yetu inawezaje kuimarishwa na (a) marafiki wazuri? (b) mikutano ya kutaniko? (c) utumishi wa shambani?

9 Mtume Paulo aliwaambia Wakristo wenzake kwamba wangekuwa na ‘ubadilishanaji wa kitia-moyo kati yao, kila mmoja kupitia imani ya mwingine.’ (Rom. 1:12) Tunaimarisha imani yetu na ya wengine pia tunaposhirikiana na waabudu wenzetu, hasa wale ambao tayari wameonyesha “sifa iliyojaribiwa” ya imani yao. (Yak. 1:3) Marafiki wabaya hubomoa imani, lakini marafiki wazuri huimarisha imani. (1 Kor. 15:33) Hiyo ndiyo sababu tunashauriwa tusiache “kukusanyika pamoja,” bali tuendelee ‘kutiana moyo.’ (Soma Waebrania 10:24, 25.) Isitoshe, mambo tunayojifunza katika mikutano huimarisha imani yetu. Jambo hilo linapatana na maneno haya ya Paulo: “Imani hufuata jambo lililosikiwa.” (Rom. 10:17) Je, tunahudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida?

10 Tunapohubiri na kuwafundisha watu habari njema, tunaimarisha imani yetu na kuwasaidia wengine wawe na imani. Kama Wakristo wa karne ya kwanza, tunajifunza kumtegemea kabisa Yehova na kuongea kwa ujasiri chini ya hali yoyote ile.—Mdo. 4:17-20; 13:46.

11. Kwa nini Kalebu na Yoshua walikuwa na imani thabiti, na tunawezaje kuwaiga?

11 Tunapoona jinsi Yehova anavyotusaidia maishani na kujibu sala zetu, imani yetu inaimarika. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Kalebu na Yoshua. Walikuwa na imani kwamba Yehova angewasaidia walipoenda kuipeleleza Nchi ya Ahadi. Hata hivyo, walipoendelea kuona jinsi Yehova alivyowaongoza maishani, imani yao iliimarika zaidi. Haishangazi kwamba Yoshua aliwaambia hivi Waisraeli: “Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi.” Baadaye aliongeza hivi: “Sasa mwogopeni Yehova na kumtumikia kwa njia isiyo na kosa na katika kweli . . . Lakini mimi na nyumba yangu, tutamtumikia Yehova.” (Yos. 23:14; 24:14, 15) Kadiri tunavyoonja wema wa Yehova, ndivyo tunavyozidi kuimarisha imani yetu.—Zab. 34:8.

TUNAWEZA KUONYESHAJE KWAMBA TUNA IMANI?

12. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna imani thabiti?

12 Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna imani thabiti? Mwanafunzi Yakobo anajibu hivi swali hilo: “Nitakuonyesha imani yangu kwa matendo yangu.” (Yak. 2:18) Matendo yetu yataonyesha kwamba tuna imani thabiti. Acheni tuchunguze mifano michache.

Wale wanaohubiri kwa bidii wanaonyesha kwamba wana imani thabiti (Tazama fungu la 13)

13. Tunapohubiri habari njema tunathibitisha nini, na kwa nini?

13 Kuhubiri habari njema ni njia bora ya kuthibitisha kwamba tuna imani. Kwa nini? Kwa sababu tunapohubiri, tunaonyesha kwamba tunaamini kuwa mwisho wa mfumo huu wa mambo uko karibu, na pia tunaamini ‘hautachelewa.’ (Hab. 2:3) Njia moja ya kupima imani yetu ni kwa kujiuliza maswali kama vile, ‘Kazi ya kuhubiri ni muhimu kadiri gani kwangu?’ Je, ninafanya yote niwezayo kuwahubiria wengine habari njema? Je, ninatafuta njia za kuongeza utumishi wangu kwa Yehova? (2 Kor. 13:5) Naam, kutoa “tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu” ni njia nzuri ya kuonyesha kwamba tuna imani thabiti.—Soma Waroma 10:10.

14, 15. (a) Tunaweza kuonyeshaje imani maishani mwetu? (b) Simulia mfano unaoonyesha jinsi familia moja ilivyotenda kwa imani.

14 Tunaweza pia kuonyesha imani tunapoendelea kukabiliana na changamoto za maisha. Iwe tunakabili hali ngumu ya kiuchumi, ugonjwa, kuvunjika moyo, huzuni, au tatizo lingine, tuna uhakika kwamba Yehova na Mwana wake watatupatia “msaada kwa wakati unaofaa.” (Ebr. 4:16) Mbali na kuomba atutimizie mahitaji yetu ya kiroho, tunaonyesha kwamba tuna imani tunaposali kuhusu mahitaji mengine pia. Yesu alisema kwamba tunaweza kumwomba Yehova vitu vya kimwili, kama vile “mkate wetu kwa ajili ya siku kulingana na mahitaji ya siku hiyo.” (Luka 11:3) Masimulizi ya Biblia yanatuhakikishia kwamba Yehova anaweza kutosheleza mahitaji yetu. Taifa la Israeli lilipokumbwa na ukame mkali, Yehova alimpatia Eliya chakula na maji. Biblia inasema kwamba “kunguru wakamletea mkate na nyama wakati wa asubuhi na mkate na nyama wakati wa jioni, naye akaendelea kunywa maji katika lile bonde la mto.” (1 Fal. 17:3-6) Sisi pia, tunaamini kwamba Yehova anaweza kutupatia mambo tunayohitaji.

Tunaonyesha imani tunapoendelea kukabiliana na changamoto za maisha (Tazama fungu la 14)

15 Tuna uhakika kwamba kutumia kanuni za Biblia maishani kunaweza kutusaidia tutimize mahitaji ya familia zetu. Rebecca, anayeishi barani Asia, alijionea ukweli wa jambo hilo katika familia yao. Wametumia kanuni ya Mathayo 6:33 na Methali 10:4 maishani mwao kwa kutanguliza masilahi ya Ufalme na kufanya kazi kwa bidii. Rebecca anasema kwamba wakati fulani mume wake alihisi kuwa kazi yake ya kimwili ingeweza kuhatarisha hali yao ya kiroho, hivyo akaamua kuiacha. Lakini walikuwa na watoto wanne waliohitaji kutunzwa. Rebecca anasema kilichotokea: “Tulianza kuuza vyakula mbalimbali. Baada ya kufanya kazi hiyo kwa miaka mingi, tunahisi kwamba Yehova hajawahi kamwe kutuacha. Hatujawahi kukosa chakula hata siku moja.” Je, umewahi kukabili hali kama hiyo ambayo iliimarisha imani yako?

16. Tutapata matokeo gani tukimtumaini Yehova?

16 Tunapaswa kuwa na uhakika kwamba tukifuata mwongozo wa Mungu, tutafanikiwa. Paulo alinukuu maneno ya Habakuki aliposema hivi: “Mwadilifu ataishi kwa sababu ya imani.” (Gal. 3:11; Hab. 2:4) Ndiyo sababu tunapaswa kumwamini Yule ambaye kwa kweli anaweza kutusaidia. Paulo anatukumbusha kwamba Mungu ndiye “anayeweza, kulingana na nguvu zake zinazotenda ndani yetu, kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri.” (Efe. 3:20) Watumishi wa Yehova wanafanya yote wawezayo ili kufanya mapenzi ya Mungu huku wakimtumaini kabisa Yehova abariki jitihada zao. Tunafurahi sana kujua kwamba Mungu wetu yuko pamoja nasi!

OMBI LA KUPEWA IMANI LAJIBIWA

17. (a) Ombi la mitume la kupewa imani zaidi lilijibiwa jinsi gani? (b) Kwa nini tunaweza kutarajia kujibiwa ombi letu la kupewa imani zaidi?

17 Baada ya kuzungumzia mambo hayo, huenda tunahisi kama mitume waliomwambia hivi Bwana wao: “Tupe imani zaidi.” (Luka 17:5) Ombi lao lilijibiwa, hasa katika Pentekoste ya 33 W.K. roho takatifu ilipomiminwa juu yao, nao wakapewa ufahamu wa kina wa kusudi la Mungu. Jambo hilo liliimarisha imani yao. Matokeo ni kwamba walifanikiwa kuhubiri habari njema katika maeneo mengi. (Kol. 1:23) Je, tunaweza kutarajia kujibiwa ombi letu la kupewa imani zaidi? Bila shaka! Biblia inatuhakikishia kwamba Yehova atasikiliza sala zetu ikiwa tunaomba “kulingana na mapenzi yake.”—1 Yoh. 5:14.

18. Yehova huwabariki jinsi gani wale wanaositawisha imani yao?

18 Ni wazi kwamba Yehova hufurahishwa sana na wale wanaomtumaini kwa moyo wote. Yehova atajibu sala yetu ya kuomba imani zaidi, na imani yetu itaimarika, hatimaye ‘tutahesabiwa kuwa tunastahili Ufalme wa Mungu.’—2 The. 1:3, 5.

^ fu. 4 Kwa mfano, soma simulizi la maisha la Lillian Gobitas Klose (Julai 22, 1993, Amkeni!), Feliks Borys (Februari 22, 1994, Amkeni!), na Josephine Elias (Septemba 2009 Amkeni!).