Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Baba Asiye na Kifani

Baba Asiye na Kifani

Mkaribie Mungu

Baba Asiye na Kifani

Mathayo 3:16, 17

“BABA.” Ni maneno machache yanayochochea hisia za ndani zaidi katika mioyo ya wanadamu kuliko neno hilo. Baba anayewapenda kwelikweli watoto wake anawasaidia wafanikiwe. Biblia ina sababu nzuri za kumwita Yehova Mungu “Baba.” (Mathayo 6:9) Yehova ni Baba wa aina gani? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze maneno ambayo Yehova alimwambia Yesu wakati Yesu alipobatizwa. Kwa kweli, namna ambavyo baba anazungumza na watoto wake inaonyesha vizuri yeye ni mzazi wa aina gani.

Mnamo Oktoba (Mwezi wa 10) mwaka wa 29 W.K., Yesu alienda kwenye Mto Yordani ili abatizwe. Biblia inasema kuhusu yale yaliyotukia: “Baada ya kubatizwa Yesu akapanda mara moja kutoka katika maji; na, tazama! mbingu zikafunguliwa, naye akaona roho ya Mungu ikishuka kama njiwa, ikija juu yake. Tazama! Kulikuwa pia na sauti kutoka mbinguni iliyosema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.’” * (Mathayo 3:16, 17) Maneno hayo mororo yaliyosemwa na Yehova mwenyewe yanatuambia mengi kuhusu Yeye ni Baba wa aina gani. Ona mambo matatu ambayo Yehova alimwambia Mwana wake.

Kwanza, kwa kusema “huyu ni Mwanangu,” kwa kweli, Yehova alikuwa akisema, ‘Ninajivunia kuwa Baba yako.’ Baba mwenye utambuzi anatosheleza tamaa ya watoto wake ya kuthaminiwa na kupewa uangalifu. Watoto wanahitaji kuhakikishiwa kwamba wanathaminiwa wakiwa washiriki muhimu wa familia. Wazia jinsi Yesu alivyohisi Baba yake alipomhakikishia kwamba anamthamini, hata ingawa alikuwa mtu mzima!

Pili, kwa kumwita Mwana wake, “mpendwa,” Yehova alionyesha waziwazi kwamba anampenda Yesu. Kwa maneno mengine, Baba alikuwa akisema, ‘Ninakupenda.’ Baba mzuri anawaambia watoto wake kwamba anawapenda sana. Maneno kama hayo yanapoambatana na upendo wa kweli, yanawasaidia watoto kusitawi. Yesu aliguswa moyo kama nini kumsikia Baba yake akisema kwamba anampenda!

Tatu, aliposema “nimekukubali,” Yehova alionyesha kwamba alimkubali Mwana wake. Ni kana kwamba Yehova alikuwa akisema, ‘Mwana, ninapendezwa na jambo ambalo umefanya.’ Baba mwenye upendo anatafuta nafasi za kuwajulisha watoto wake kwamba anapendezwa na mambo mazuri wanayosema au kufanya. Watoto wanatiwa nguvu na kupata ujasiri wazazi wao wanapowaeleza kwamba wanawakubali. Bila shaka, Yesu alitiwa moyo kusikia kwamba Baba yake anamkubali!

Kwa kweli, Yehova ni Baba asiye na kifani. Je, unatamani kuwa na baba kama huyo? Ikiwa ndivyo, utafarijiwa kujua kwamba unaweza kuwa na uhusiano kama huo pamoja na Yehova. Ikiwa una imani, unajifunza kumhusu, na unajitahidi kikweli kufanya mapenzi yake, Yehova ataitikia. Biblia inasema: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Ni nini kinachoweza kukufanya ujihisi salama zaidi kuliko kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu, ambaye ni Baba bora zaidi?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Kulingana na simulizi la Injili ya Luka, Yehova alitumia neno “wewe,” aliposema: “Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali wewe.”Luka 3:22.