Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Fundisho la Mageuzi Linapatana na Biblia?

Je, Fundisho la Mageuzi Linapatana na Biblia?

Je, Fundisho la Mageuzi Linapatana na Biblia?

JE, INAWEZEKANA kwamba Mungu alitumia mageuzi ili kuumba wanadamu kutokana na wanyama? Je, Mungu alifanya bakteria ikue ndani ya samaki na kuendelea kukua na kuwa wanyama wanaotambaa na wale wanaonyonyesha, hivi kwamba mwishowe sokwe au nyani wakawa wanadamu? Wanasayansi fulani na viongozi wa kidini wanadai kwamba wanaamini mafundisho ya mageuzi na ya Biblia. Wanasema kwamba kitabu cha Biblia cha Mwanzo kinaeleza mambo kwa njia ya mfano. Huenda umejiuliza, ‘Je, fundisho la kwamba mwanadamu alitokana na wanyama kupitia mageuzi linapatana na Biblia?’

Ili tuelewe sisi ni nani, tunaelekea wapi, na jinsi tunavyopaswa kuishi, ni jambo la maana sana kuelewa asili yetu. Hatuwezi kuelewa kwa nini Mungu anaruhusu mateso na kusudi lake kuhusu wakati ujao wa wanadamu tusipojua mwanadamu alitoka wapi. Hatuwezi kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu ikiwa hatuna uhakika wa kwamba yeye ndiye Muumba wetu. Hivyo basi, acheni tuchunguze yale ambayo Biblia inasema kuhusu asili ya mwanadamu, hali yake ya sasa, na wakati wake ujao. Kisha, tutaona ikiwa fundisho la mageuzi linapatana na Biblia.

Kulipokuwa na Mwanadamu Mmoja

Kwa kawaida, wanamageuzi wanadai kwamba wanyama walibadilika hatua kwa hatua na kuwa wanadamu, lakini wanakana kwamba wakati fulani kulikuwa na mwanadamu mmoja tu. Hata hivyo, Biblia inasema jambo tofauti kabisa. Inasema kwamba tunatokana na mwanadamu mmoja, Adamu. Masimulizi yake yanasema Adamu alikuwa mtu halisi. Inatujulisha majina ya mke na watoto wake. Inatuambia mengi kuhusu mambo aliyofanya, yale aliyosema, aliishi wakati gani, na alikufa wakati gani. Yesu hakuona masimulizi hayo kuwa hadithi tu ya watu wasio na elimu. Alipokuwa akizungumza na viongozi wa kidini wenye elimu ya juu, alisema hivi: “Je, hamkusoma kwamba yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke?” (Mathayo 19:3-5) Kisha, Yesu akanukuu maneno kuhusu Adamu na Hawa kwenye Mwanzo 2:24.

Luka, mwandikaji wa Biblia na mwanahistoria aliye makini sana, alionyesha kwamba Adamu alikuwa mtu halisi kama Yesu. Luka alionyesha ukoo wa Yesu kurudi nyuma mpaka kwa mwanadamu wa kwanza. (Luka 3:23-38) Pia, mtume Paulo alipozungumza mbele ya wasikilizaji waliotia ndani wanafalsafa ambao walisomea katika shule maarufu za Ugiriki, aliwaambia hivi: “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo . . . alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, ili wakae juu ya uso wa dunia nzima.” (Matendo 17:24-26) Kwa wazi, Biblia inafundisha kwamba tulitokana na “mtu mmoja.” Je, yale ambayo Biblia inasema kuhusu hali ya mwanzoni ya mwanadamu yanapatana na fundisho la mageuzi?

Mwanadamu Anapoteza Ukamilifu

Kulingana na Biblia, Yehova alimfanya mwanadamu wa kwanza akiwa mkamilifu. Je, Mungu anaweza kufanya vitu visivyo vikamilifu? Masimulizi ya uumbaji yanasema: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake . . . Kisha Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.” (Mwanzo 1:27, 31) Mtu mkamilifu alikuwa namna gani?

Mtu mkamilifu ana uhuru wa kuchagua na anaweza kuiga kabisa sifa za Mungu. Biblia inasema: “Mungu wa kweli aliwafanya wanadamu wakiwa wanyoofu, lakini wao wenyewe wametafuta mipango mingi.” (Mhubiri 7:29) Adamu aliamua kumwasi Mungu. Kwa kuasi, Adamu alipoteza ukamilifu kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya wazao wake. Kupoteza ukamilifu kunaonyesha kwa nini mara nyingi tunavunjika moyo, hata ingawa tunataka kufanya yaliyo mema. Mtume Paulo aliandika hivi: “Lile ninalolitaka, hilo sizoei kulifanya; bali lile ninalochukia ndilo ninalofanya.”—Waroma 7:15.

Kulingana na Biblia, mtu mkamilifu angeishi milele akiwa na afya kamilifu. Ni wazi kwamba kutokana na yale ambayo Mungu alimwambia Adamu, ikiwa mwanadamu huyo wa kwanza angemtii Mungu, hangekufa kamwe. (Mwanzo 2:16, 17; 3:22, 23) Yehova hangetangaza kwamba kuumbwa kwa mwanadamu kulikuwa ‘kwema sana’ ikiwa mwanadamu huyo alikuwa na mwelekeo wa kuwa mgonjwa au kuasi. Kupoteza ukamilifu kunaonyesha kwa nini mwili wa binadamu, ingawa umeumbwa kwa njia ya ajabu, unakuwa na kasoro na kupatwa na magonjwa. Kwa hiyo, fundisho la mageuzi halipatani na Biblia. Fundisho hilo linaonyesha kwamba mwanadamu wa kisasa ni mnyama anayeendelea kubadilika na kuwa bora. Biblia inaonyesha kwamba mwanadamu wa kisasa alitokana na mwanadamu mkamilifu naye anaendelea kudhoofika.

Wazo la kwamba Mungu alitumia mageuzi ili kutokeza mtu halipatani pia na yale ambayo Biblia inasema kuhusu utu wa Mungu. Ikiwa Mungu aliongoza utaratibu wa mageuzi, hilo lingemaanisha kwamba aliwaongoza pia wanadamu kuingia katika hali yao ya sasa ya magonjwa na mfadhaiko. Hata hivyo, Biblia inasema hivi kumhusu Mungu: “Yeye Mwamba, kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki; yeye ni mwadilifu na mnyoofu. Wametenda kwa uharibifu; wao si watoto wake, kasoro ni yao wenyewe.” (Kumbukumbu la Torati 32:4, 5) Kwa hiyo, mateso ya sasa ya wanadamu hayatokani na mageuzi yaliyoongozwa na Mungu. Ni matokeo ya mtu mmoja kupoteza ukamilifu kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya wazao wake kwa kumwasi Mungu. Kwa kuwa tumezungumza kumhusu Adamu, sasa tunaweza kuzungumza kumhusu Yesu. Je, fundisho la mageuzi linapatana na yale ambayo Biblia inasema kumhusu Yesu?

Je, Unaweza Kuamini Fundisho la Mageuzi Pamoja na Ukristo?

“Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu.” Kama vile ambavyo huenda unajua, hilo ni mojawapo ya mafundisho ya msingi ya Ukristo. (1 Wakorintho 15:3; 1 Petro 3:18) Ili kuelewa kwa nini fundisho la mageuzi halipatani na maneno hayo, kwanza tunahitaji kuelewa kwa nini Biblia inatuita watenda-dhambi na pia matokeo ya dhambi juu yetu.

Sisi sote ni watenda-dhambi katika maana ya kwamba hatuwezi kuiga kwa ukamilifu sifa tukufu za Mungu, kama vile upendo na haki yake. Kwa hiyo, Biblia inasema: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Biblia inafundisha kwamba dhambi ndiyo inayosababisha kifo. Andiko la 1 Wakorintho 15:56 linasema: “Mchomo unaotokeza kifo ni dhambi.” Pia, tunakuwa wagonjwa kwa sababu ya dhambi tuliyorithi. Yesu alionyesha kwamba kuna uhusiano kati ya magonjwa na hali yetu ya dhambi. Alimwambia hivi mtu fulani aliyepooza: “Dhambi zako zimesamehewa,” na mtu huyo akapona.—Mathayo 9:2-7.

Kifo cha Yesu kinatusaidia jinsi gani? Biblia inamtofautisha Adamu na Yesu Kristo kwa kusema hivi: “Kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.” (1 Wakorintho 15:22) Kwa kutoa uhai wake, Yesu alilipa bei kwa ajili ya dhambi ambayo tulirithi kutoka kwa Adamu. Hivyo, wote wanaomwamini Yesu na kumtii watapokea kile ambacho Adamu alipoteza, yaani, tarajio la kuishi milele.—Yohana 3:16; Waroma 6:23.

Hivyo basi, je, huoni kwamba fundisho la mageuzi halipatani na Biblia? Tukiwa na shaka kwamba “katika Adamu wote wanakufa,” tunaweza jinsi gani kuwa na tumaini kwamba “katika Kristo wote watafanywa kuwa hai”?

Kwa Nini Fundisho la Mageuzi Linawavutia Watu?

Biblia inaonyesha kwa nini mafundisho kama vile fundisho la mageuzi yanapendwa sana na watu wengi. Inasema: “Kutakuwa na kipindi cha wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe; nao watageuza masikio yao kutoka kwenye kweli, nao watageuzwa kando kufuata hadithi za uwongo.” (2 Timotheo 4:3, 4) Ingawa kwa kawaida fundisho la mageuzi linaelezwa kwa maneno ya kisayansi, kwa kweli ni fundisho la kidini. Linafundisha falsafa kuhusu uhai na mtazamo fulani kumwelekea Mungu. Mafundisho hayo yanawavutia kwa udanganyifu wanadamu wenye ubinafsi, na wenye mielekeo ya kujitegemea. Watu wengi wanaoamini fundisho la mageuzi wanasema kwamba wanamwamini Mungu pia. Hata hivyo, wanaona wana uhuru wa kufikiri kwamba Mungu hakuumba vitu vyote, haingilii mambo ya wanadamu, na kwamba hatawahukumu watu. Ni fundisho linalofurahisha masikio ya watu.

Walimu wa fundisho la mageuzi mara nyingi hawachochewi na mambo ya hakika, bali na “tamaa zao wenyewe,” labda tamaa ya kukubaliwa na jamii ya wanasayansi ambao wanaamini fundisho hilo. Michael Behe, profesa wa biokemia, ambaye kwa muda mrefu wa maisha yake amejifunza kuhusu utendaji tata ndani ya chembe zilizo hai, alieleza kwamba madai ya wale wanaofundisha mageuzi ya muundo wa chembe hayana msingi. Je, mageuzi yanaweza kutokea kwenye molekuli ndogo sana ya chembe? Aliandika hivi: “Mageuzi ya molekuli hayana msingi wa kisayansi. Hakuna kichapo cha kisayansi, iwe magazeti maarufu, magazeti ya kipekee, au vitabu vinavyoeleza jinsi mageuzi ya molekuli ya mfumo wowote halisi au ulio tata wa biokemia ulivyotokea au jinsi ambavyo ungetokea. . . . Madai ya Darwin kuhusu mageuzi ya molekuli ni ya kujitutumua tu.”

Ikiwa wanamageuzi hawawezi kuthibitisha madai yao, kwa nini wanatetea sana maoni yao. Behe anaeleza: “Watu wengi, kutia ndani wanasayansi wengi maarufu na wenye kuheshimika, hawataki tu kuamini kwamba kuna mtu aliye na nguvu zinazozidi za wanadamu aliyeumba kila kitu.”

Fundisho la mageuzi linavutia makasisi wengi ambao wanataka waonekane kuwa wenye hekima. Wanalingana na wale ambao mtume Paulo anazungumzia katika barua yake kwa Wakristo wa Roma. Paulo aliandika: “Yale yanayoweza kujulikana juu ya Mungu yamefunuliwa katikati yao . . . Sifa zake ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea. Kwa sababu, ijapokuwa walimjua Mungu, hawakumtukuza yeye kuwa Mungu wala hawakumshukuru, bali wakawa wajinga katika kufikiri kwao na moyo wao usio na ufahamu ukaingiwa na giza. Ijapokuwa walisisitiza kuwa ni wenye hekima, wakawa wapumbavu.” (Waroma 1:19-22) Unaweza kuepuka jinsi gani kudanganywa na walimu wa uwongo?

Uthibitisho Unaotegemea Imani Katika Muumba

Biblia inakazia umuhimu wa uthibitisho inapoeleza maana ya imani. Inasema hivi: “Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Imani ya kweli katika Mungu inapaswa kutegemea uthibitisho ambao unaonyesha ukweli wa kwamba kuna Muumba. Biblia inaonyesha ni wapi unaweza kupata uthibitisho huo.

Daudi, mwandikaji wa Biblia aliyeongozwa na roho aliandika hivi: “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha.” (Zaburi 139:14) Kutumia wakati kutafakari kuhusu ubuni wa ajabu wa mwili wetu na vitu vingine vilivyo hai kunatufanya tustaajabie hekima ya Mtengenezaji wetu. Kila sehemu ya maelfu ya mifumo ya mwili wetu ambayo inashirikiana ili kutusaidia kuwa hai imebuniwa kwa njia inayofaa kabisa. Pia, ulimwengu wote unathibitisha kwamba unafuata utaratibu na vipimo sahihi kabisa. Daudi aliandika: “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; nalo anga linatangaza kazi ya mikono yake.”—Zaburi 19:1.

Biblia yenyewe ina uthibitisho mwingi kuhusu Muumba. Ukichukua wakati na kuchunguza upatano wa vitabu vyake 66, ubora wa viwango vyake vya maadili, na unabii wake mbalimbali unaotimia kabisa utaona uthibitisho mwingi kwamba Muumba ndiye aliyeitunga Biblia. Pia, kuelewa mafundisho ya Biblia kutakupa uhakika wa kwamba kwa kweli Biblia ni Neno la Muumba. Kwa mfano, unapoelewa mafundisho ya Biblia kama vile kwa nini tunateseka, Ufalme wa Mungu, wakati ujao wa wanadamu, na jinsi ya kupata furaha, utaona uthibitisho ulio wazi wa hekima ya Mungu. Huenda ukahisi kama alivyohisi Paulo alipoandika: “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika!”—Waroma 11:33.

Kadiri unavyochunguza uthibitisho na imani yako inavyozidi kukua, ndivyo utakavyokuwa na uhakika kwamba unaposoma Biblia, unamsikiliza Muumba mwenyewe. Anasema: “Mimi mwenyewe nimeifanya dunia nami nimemuumba mwanadamu juu yake. Mimi—mikono yangu mwenyewe imezitandaza mbingu, nami nimeliamuru jeshi lake lote.” (Isaya 45:12) Kwa kweli, hutajuta kamwe kwa sababu ya kujitahidi kujithibitishia mwenyewe kwamba Yehova ndiye Muumba wa vitu vyote.

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Mtume Paulo aliwaambia hivi wasomi Wagiriki: “Mungu . . . alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu”

[Blabu katika ukurasa wa 15]

Fundisho la mageuzi linaonyesha mwanadamu wa kisasa ni mnyama anayeendelea kubadilika na kuwa bora. Biblia inaonyesha kwamba mwanadamu wa kisasa alitokana na mwanadamu mkamilifu naye anaendelea kudhoofika

[Blabu katika ukurasa wa 16]

“Mageuzi ya molekuli hayana msingi wa kisayansi”

[Blabu katika ukurasa wa 17]

Ubuni wa ajabu wa vitu vilivyo hai unatufanya tustaajabie hekima ya Mtengenezaji wetu