Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jenga Familia Yako kwa “Maneno Yenye Kupendeza”

Jenga Familia Yako kwa “Maneno Yenye Kupendeza”

Jenga Familia Yako kwa “Maneno Yenye Kupendeza”

KADIRI wakati ulivyopita, David alizidi kufadhaika. Aliendelea kuangalia saa huku akimngojea mke wake ndani ya gari. Mwishowe, mke wake, Diane, alipotoka ndani ya nyumba, David alimfokea kwa hasira.

“Kwa nini umenifanya nikungoje kwa muda huu wote?” alifoka. “Unachelewa sikuzote! Kwa nini huwezi hata siku moja kuwa tayari kwa wakati?”

Diane aliumizwa sana moyoni. Alianza kulia na kurudi haraka ndani ya nyumba. Papo hapo, David akatambua kosa lake. Kufoka kwake kwa hasira kulifanya tu mambo yawe mabaya zaidi. Sasa angefanya nini? Alizima gari, akashusha pumzi, na akamfuata polepole mke wake ndani ya nyumba.

Mfano huo unaonyesha hali halisi ambayo huenda wengi wamepitia. Je, umewahi kutaka kubadili maneno uliyosema? Tunapozungumza bila kufikiri, mara nyingi tunasema mambo ambayo yanatufanya tujute baadaye. Hivyo, Biblia ina sababu nzuri ya kusema: “Moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu.”—Methali 15:28.

Hata hivyo, inaweza kuwa vigumu kufikiri vizuri kabla ya kusema, hasa tukiwa na hasira, woga, au tunapoumizwa hisia. Inakuwa hivyo hasa kuhusiana na watu wa familia. Tunapojaribu kueleza hisia zetu tunaweza kwa urahisi kujikuta tukimlaumu au kumchambua-chambua mtu mwingine. Kwa kufanya hivyo, huenda tukaumiza hisia za mtu huyo au kutokeza mabishano.

Tunaweza kufanya nini ili kupata matokeo mazuri? Tunaweza jinsi gani kuzuia hisia zetu zisituongoze vibaya? Tunaweza kupata mashauri fulani yenye faida kutoka kwa mwandikaji wa Biblia, Sulemani.

Fikiria Mambo ya Kusema na Jinsi ya Kuyasema

Sulemani, mwandikaji wa kitabu cha Biblia cha Mhubiri, aliandika mambo mazito kuhusu ubatili wa maisha. Ni wazi kwamba alikuwa na hisia zenye nguvu kuhusu habari hiyo. Alisema hivi: “Nikauchukia uzima.” Pindi moja, alisema uzima ni “ubatili mkubwa zaidi.” (Mhubiri 2:17; 12:8) Hata hivyo, kitabu cha Mhubiri hakitaji mambo ambayo yalimfadhaisha Sulemani. Hakufikiria kwamba lilikuwa jambo linalofaa kuzungumza tu kuhusu mambo mabaya yanayotukia maishani. Akimalizia kitabu chake, Sulemani anaonyesha kwamba “alijitahidi kutafuta maneno yenye kupendeza na kuandika maneno sahihi ya kweli.” (Mhubiri 12:10) Tafsiri nyingine inasema kwamba “alijaribu kueleza mambo hayo katika njia iliyo bora na sahihi zaidi.”—Contemporary English Version.

Ni wazi kwamba Sulemani alitambua kuwa alihitaji kuzuia hisia zake. Ni kana kwamba alikuwa akijiuliza hivi: ‘Je, mambo ninayokusudia kusema ni ya kweli au sahihi? Nikitumia maneno haya, je, watu wengine watayaona kuwa yenye kupendeza, yenye kukubalika?’ Kwa kutafuta “maneno yenye kupendeza” ya kweli, aliweza kuzuia hisia zake zisivuruge mawazo yake.

Kwa sababu ya jitihada zake, kitabu cha Mhubiri kimeandikwa kwa njia bora kabisa, lakini pia kimejaa hekima kutoka kwa Mungu kuhusu kusudi la maisha. (2 Timotheo 3:16, 17) Je, namna Sulemani anavyozungumzia habari hiyo kwa hisia nyingi sana inaweza kutusaidia kuzungumza vizuri na wapendwa wetu? Fikiria mfano mmoja.

Jifunze Kuzuia Hisia Zako

Tuseme mvulana mmoja anarudi nyumbani kutoka shuleni akiwa na ripoti yake na anaonekana mwenye huzuni. Baba yake anachunguza ripoti hiyo na kuona kwamba kijana wake alianguka katika somo fulani. Papo hapo baba huyo anakasirika, akikumbuka mara nyingi ambazo mvulana huyo hakufanya kazi zake za shule. Baba huyo anahisi amfokee hivi: “Wewe ni mvivu tu! Ukiendelea kujiendesha hivyo, hutafanikiwa maishani!”

Kabla ya kuacha hisia zake ziongoze jibu lake, ni vizuri baba huyo ajiulize, ‘Je, kweli mambo ninayofikiri ni ya kweli au sahihi?’ Swali hilo linaweza kumsaidia kuona uhakika wa mambo badala ya kufuata tu hisia zake. (Methali 17:27) Je, ni kweli kwamba mwana wake hatafanikiwa maishani kwa sababu ameanguka somo moja tu? Je, kweli yeye ni mvivu katika kila jambo maishani, au hafanyi kazi zake za shule kwa sababu haelewi vizuri somo fulani? Biblia inakazia tena na tena umuhimu wa kuwa na maoni mazuri na yenye usawaziko kuhusu mambo. (Tito 3:2; Yakobo 3:17) ili kumtia moyo mtoto, mzazi anahitaji kusema “maneno sahihi ya kweli.”

Tafuta Maneno Yaliyo Sawa

Anapofikiria jambo la kusema, baba anapaswa kujiuliza, ‘Ninaweza jinsi gani kusema jambo hili kwa maneno ambayo mwanangu atayaona kuwa yenye kupendeza na yenye kukubalika?’ Ni kweli kwamba kupata maneno yaliyo sawa si jambo rahisi. Lakini wazazi wanapaswa kukumbuka kwamba mara nyingi vijana wana mwelekeo wa kufikiri kwamba wasipofanya mambo kwa ukamilifu wameshindwa kabisa. Huenda wakafikiria pindi ambazo walishindwa au kuwa dhaifu na hivyo kukazia udhaifu huo, hivi kwamba wanakuwa na maoni yasiyofaa kujihusu. Mzazi akikasirika kupita kiasi, huenda akamfanya mtoto wake azidi kuhisi kwamba yeye ni bure kabisa. Andiko la Wakolosai 3:21 linasema: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.”

Maneno kama “sikuzote” na “kamwe” kwa kawaida yanafanya jambo lionekane kuwa zoea au yanatilia chumvi uhakika wa mambo. Mzazi akisema, “Hutafanikiwa kamwe maishani,” je, mtoto huyo ataendelea kujiheshimu? Ikiwa mara nyingi mtoto anashutumiwa hivyo, huenda akaanza kujiona kuwa bure kabisa. Bila shaka, maneno hayo hayavunji moyo tu bali pia si ya kweli.

Kwa kawaida, ni vizuri zaidi kukazia mambo mazuri katika kila hali. Baba katika mfano wetu anaweza kusema hivi: “Mwanangu, ninaona umekasirika kwa sababu umeanguka somo hili. Hata hivyo, ninajua kwamba kwa ujumla unafanya kazi zako kwa bidii. Basi, acha tuzungumzie somo hili ili tuone jinsi unavyoweza kushinda matatizo yoyote ambayo huenda unakabili.” ili kujua ni njia gani nzuri ya kumsaidia mtoto wake, baba huyo anaweza pia kuuliza maswali hususa ili kuona ikiwa kuna matatizo yanayohusika.

Inaelekea kwamba badala ya kufoka kwa hasira, kuzungumzia mambo kwa njia nzuri kama hiyo kutakuwa na matokeo mazuri zaidi. Biblia inatuhakikishia kwamba “maneno yenye kupendeza” ni “matamu kwa nafsi na maponyo mifupani.” (Methali 16:24) Ndiyo, watoto, na washiriki wote wa familia, wanasitawi vizuri katika mazingira yenye amani na upendo.

“Kutokana na Wingi wa Moyo”

Fikiria tena mume ambaye alitajwa katika mfano ulio mwanzoni mwa habari hii. Je, haingekuwa vizuri ikiwa angechukua wakati wa kutafuta “maneno yenye kupendeza” ya kweli badala ya kumfokea kwa hasira mke wake? Ni vizuri mume aliye katika hali hiyo ajiulize hivi: ‘Hata ikiwa mke wangu anahitaji kujitahidi zaidi kutochelewa, je, ni kweli kwamba yeye anachelewa sikuzote? Je, huu ndio wakati mzuri zaidi wa kuzungumzia jambo hilo? Je, hasira au maneno ya kumchambua-chambua yatamchochea afanye mabadiliko?’ Kutua na kujiuliza maswali hayo kunaweza kutusaidia kuepuka kuumiza hisia za wapendwa wetu bila kukusudia.—Methali 29:11.

Namna gani ikiwa mazungumzo yetu katika familia mara nyingi yanaishia kuwa mabishano? Huenda tukahitaji kuchunguza mambo kwa undani zaidi, na kufikiria hisia zetu tunapochagua maneno yetu. Maneno tunayosema, hasa tukiwa tumefadhaika au tukiwa chini ya hali ngumu, yanaweza kweli kufunua mengi kuhusu hali yetu ya ndani. Yesu alisema: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mathayo 12:34) Kwa maneno mengine, usemi wetu mara nyingi unafunua mawazo yetu ya ndani, tamaa, na mitazamo yetu.

Je, mtazamo wetu maishani unapatana na akili na ni wenye kutumainia mazuri? Ikiwa ndivyo, inaelekea sauti yetu na mambo tunayozungumzia yataonyesha mtazamo huo. Je, tuna mwelekeo wa kuwa wagumu, wenye maoni mabaya, au wenye kuchambua-chambua? Ikiwa ndivyo, huenda tukawavunja wengine moyo iwe kwa yale tunayosema au kwa namna tunavyoyasema. Huenda tusitambue jinsi ambavyo mawazo au maneno yetu yamekuwa yenye kuvunja moyo. Tunaweza hata kuamini kwamba njia yetu ya kuona mambo ni sahihi. Lakini tunapaswa kujihadhari ili tusijidanganye wenyewe.—Methali 14:12.

Tunashukuru kwamba tuna Neno la Mungu. Biblia inaweza kutusaidia kuchunguza mawazo yetu na kuchanganua yale yaliyo sahihi na yale yanayohitaji kurekebishwa. (Waebrania 4:12; Yakobo 1:25) Hata iwe tumerithi mwelekeo gani au tumepata malezi gani, sote tunaweza kubadili njia yetu ya kufikiri na kutenda ikiwa kwa kweli tunataka kufanya hivyo.—Waefeso 4:23, 24.

Zaidi ya kutumia Biblia, tunaweza kufanya jambo lingine ili kuchanganua jinsi tunavyozungumza na wengine. Waulize wengine. Kwa mfano, muulize mwenzi wako wa ndoa au mtoto wako akuambie kwa unyoofu jinsi unavyozungumza. Zungumza na rafiki mkomavu ambaye anakujua vizuri. Utahitaji kuwa mnyenyekevu ili kukubali yale watakayosema na kufanya marekebisho yoyote ambayo huenda yakahitajiwa.

Fikiri Kabla ya Kusema!

Mwishowe, ikiwa kwa kweli tunataka kuepuka kuwaumiza wengine kwa maneno yetu, tunapaswa kufanya yale ambayo andiko la Methali 16:23 linasema: “Watu wenye akili [yaani, wenye hekima] wanafikiri kabla ya kusema; hivyo yale wanayosema yanakuwa yenye kushawishi zaidi.” (Today’s English Version) Huenda sikuzote isiwe rahisi kuzuia hisia zetu. Hata hivyo, tukijitahidi kuwaelewa wengine badala ya kuwashtaki au kuwafedhehesha wengine, itakuwa rahisi zaidi kupata maneno sahihi ya kueleza maoni yetu.

Bila shaka, hakuna mtu aliye mkamilifu. (Yakobo 3:2) Nyakati nyingine, sote tunasema bila kufikiri. (Methali 12:18) Lakini kwa msaada wa Neno la Mungu, tunaweza kujifunza kufikiri kabla ya kusema na hivyo kutanguliza hisia na faida za wengine. (Wafilipi 2:4) Acheni basi tuazimie kutafuta “maneno yenye kupendeza” ya kweli, hasa tunapozungumza na watu wa familia yetu. Tukifanya hivyo, maneno yetu hayatawaumiza wala kuwabomoa wapendwa wetu, badala yake yatawaponya na kuwajenga.—Waroma 14:19.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Unaweza kuepuka jinsi gani kusema jambo fulani ambalo litakufanya ujute baadaye?