Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupata Faraja Baada ya Kukosa Tumaini Ujanani

Kupata Faraja Baada ya Kukosa Tumaini Ujanani

Kupata Faraja Baada ya Kukosa Tumaini Ujanani

Limesimuliwa na Eusebio Morcillo

Mnamo Septemba (Mwezi wa 9) 1993, nilitembelea gereza lenye ulinzi mkali. Ilikuwa siku ya ubatizo wa mfungwa fulani, yaani, dada yangu mdogo, Mariví. Wafungwa fulani na maofisa wa gereza walitazama kwa heshima nilipokuwa nikimbatiza. Kabla sijaeleza jinsi mimi na dada yangu mdogo tulivyojikuta hapo, acheni nieleze jinsi maisha yangu ya mapema yalivyokuwa.

NILIZALIWA Hispania mnamo Mei 5, 1954 (5/5/1954), nami nilikuwa wa kwanza kati ya watoto wanane. Mariví alikuwa wa tatu. Nyanya yetu alitulea na kutusaidia kuwa Wakatoliki wenye kumcha Mungu, nami nina kumbukumbu nzuri za utotoni nilipokuwa nikijihisi kuwa mcha-Mungu nikiwa pamoja na Nyanya. Lakini hali ya familia yetu haikuwa ya kiroho. Kwa kawaida, Baba alitupiga pamoja na Mama. Tuliishi kwa woga, nami niliumia sana kumwona Mama akiteseka.

Nikiwa shuleni, nilikabili hali nyingine zenye kuvunja moyo. Mwalimu mmoja ambaye alikuwa kasisi, alivigongesha vichwa vyetu ukutani tulipotoa jibu lisilo sahihi. Kasisi mwingine aliwatendea watoto vibaya kingono alipokuwa akipitia pamoja nao kazi ya shule. Zaidi ya hayo, mafundisho ya Kikatoliki kama vile moto wa mateso yalinivuruga na kuniogopesha. Muda si muda niliacha kumcha Mungu.

Kunaswa Katika Maisha Yasiyo na Kusudi

Kwa kuwa sikuwa na mwongozo wowote wa kiroho, nilianza kushirikiana sana na watu wenye jeuri na maadili mapotovu katika majumba ya disko. Mara nyingi vita vilitokea, na vitu kama vile visu, minyororo, glasi, na stuli vilitumiwa kama silaha. Hata ingawa sikujihusisha na matendo hayo ya jeuri, pindi moja nilipigwa nikazimia.

Mwishowe nilichoshwa na mazingira hayo, hivyo nikatafuta majumba ya disko yenye utulivu zaidi. Hata katika majumba hayo, kwa kawaida kulikuwa na dawa za kulevya. Lakini badala ya kunistarehesha na kunipa amani ya akili, dawa za kulevya ziliniletea ndoto na mahangaiko.

Ingawa sikupata uradhi, nilimshawishi José Luis, mmoja wa ndugu zangu wadogo na Miguel rafiki yangu mkubwa, waishi maisha kama yangu. Wakati huo, sisi pamoja na vijana wengine wengi nchini Hispania, tulikuwa tumenaswa katika ulimwengu uliopotoka. Ningefanya chochote kile ili nipate pesa za kununua dawa za kulevya. Nilipoteza heshima kabisa.

Yehova Anatuokoa

Wakati huo, nilizungumza mara kadhaa na marafiki wangu kuhusu kuwapo kwa Mungu na kusudi la maisha. Nilianza kumtafuta Mungu kwa kumtafuta mtu ambaye ningemfunulia hisia zangu. Nilikuwa nimegundua kwamba Francisco, mmoja wa wafanyakazi wenzangu, alikuwa tofauti na wengine. Alionekana mwenye furaha, mnyoofu, na mwenye fadhili, hivyo nikaamua kumfunulia moyo wangu. Francisco alikuwa Shahidi wa Yehova, naye alinipa gazeti la Mnara wa Mlinzi lililokuwa na makala kuhusu dawa za kulevya.

Baada ya kusoma makala hiyo, nilimwomba Mungu anisaidie: “Bwana, ninajua kwamba upo, nami nataka kukujua na kufanya mapenzi yako. Tafadhali nisaidie!” Francisco na Mashahidi wengine walitumia Biblia kunitia moyo nao wakanipa vichapo vya Biblia ili nivisome. Nilikuja kutambua kwamba walikuwa wakinipa msaada niliokuwa nimemwomba Mungu. Punde si punde, nilianza kuzungumza na marafiki wangu na José Luis kuhusu mambo niliyokuwa nikijifunza.

Siku moja nilipokuwa nikitoka katika maonyesho ya muziki wa roki pamoja na marafiki fulani, nilijitenga nao. Niliwatazama nikiwa kando na kuona jinsi mwenendo wetu ulivyochukiza kwa sababu ya kutumia dawa za kulevya. Papo hapo niliamua kuacha mtindo huo wa maisha na kuwa Shahidi wa Yehova.

Nilimwomba Francisco Biblia, naye akanipa Biblia pamoja na kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. * Niliposoma kuhusu ahadi ya Mungu ya kufuta kila chozi na hata kuondoa kifo, nilisadiki kabisa kwamba nimeipata kweli inayoweza kuwaweka wanadamu huru. (Yohana 8:32; Ufunuo 21:4) Baadaye, nilihudhuria mkutano katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Urafiki na uchangamfu wao ulinivutia sana.

Kwa kuwa nilitamani sana kuwaambia wengine kuhusu yale niliyojionea katika Jumba la Ufalme, mara moja nilimwita José Luis na marafiki wangu na kuwaeleza mambo hayo. Siku kadhaa baadaye, sote tulihudhuria mkutano. Msichana mmoja aliyeketi mbele yetu alitutazama. Ni wazi kwamba alishangaa kuona kikundi cha watu wenye nywele ndefu, na alijihadhari sana asitutazame tena. Hapana shaka kwamba msichana huyo alishangaa alipotuona tena kwenye Jumba la Ufalme juma lililofuata, kwa kuwa tulirudi tukiwa tumevalia suti na tai.

Muda mfupi baadaye, mimi na Miguel tulihudhuria kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova. Hatukuwa tumewahi kujionea jambo kama hilo—undugu wa kweli kati ya watu wenye umri mbalimbali. Na la kushangaza hata zaidi ni kwamba kusanyiko lilifanyiwa katika jumba lilelile tulimokuwa tumehudhuria maonyesho ya muziki wa roki. Lakini pindi hii, mazingira na muziki tuliosikiliza ulituchangamsha sana.

Kikundi chetu chote kilianza kujifunza Biblia. Miezi minane hivi baadaye, mnamo Julai 26, 1974 (26/7/1974), mimi na Miguel tulibatizwa. Sote wawili tulikuwa na umri wa miaka 20. Watu wengine wanne katika kikundi chetu walibatizwa miezi michache baadaye. Mafundisho ya Biblia yalinichochea kuanza kumsaidia mama yangu aliyekuwa mstahimilivu kufanya kazi za nyumbani na kumjulisha kuhusu imani yangu mpya. Hivyo, tukawa na uhusiano wa karibu. Pia, nilitumia wakati mwingi kuwasaidia ndugu na dada zangu wadogo.

Muda si muda, mama yangu na ndugu na dada zangu wote kasoro mmoja walijifunza kweli ya Biblia nao wakabatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Katika mwaka wa 1977, nilimwoa Soledad. Huyo ndiye yule msichana aliyetutazama kwa mshangao tulipoenda katika Jumba la Ufalme mara ya kwanza. Baada ya miezi michache, sote wawili tukawa mapainia, yaani, Mashahidi wa Yehova ambao ni wahubiri wa wakati wote wa habari njema.

Mpendwa Anakombolewa

Mariví, dada yangu mdogo, alikuwa ametendewa vibaya kingono akiwa mtoto, na tukio hilo baya lilimwathiri sana. Akiwa kijana, aliishi maisha machafu kiadili, alitumia dawa za kulevya, aliiba, na kufanya ukahaba. Akiwa na umri wa miaka 23, alifungwa gerezani, ambamo aliendelea kuishi maisha yake mapotovu.

Kufikia wakati huo, nilikuwa mwangalizi wa mzunguko, yaani, mhudumu anayesafiri wa Mashahidi wa Yehova. Mnamo 1989, mimi na Soledad tulitumwa katika eneo ambako Mariví alikuwa amefungiwa. Muda mfupi uliotangulia, wenye mamlaka walikuwa wamemnyang’anya mtoto wake wa kiume, naye alikuwa amevunjika moyo sana na hakutaka kuendelea kuishi. Siku moja nilimtembelea na kupendekeza tujifunze Biblia pamoja, naye akakubali. Baada ya kujifunza kwa mwezi mmoja, aliacha kutumia dawa za kulevya na tumbaku. Nilisisimka sana kuona Yehova alimpa nguvu za kufanya mabadiliko hayo maishani mwake.—Waebrania 4:12.

Muda mfupi baada ya kuanza kujifunza, Mariví alianza kuwafundisha wafungwa wenzake na maofisa wa gereza kweli za Biblia. Ijapokuwa alihamishwa kutoka gereza moja hadi lingine, aliendelea kuhubiri. Katika gereza moja alihubiri seli kwa seli. Kadiri miaka ilivyopita, Mariví alianzisha mafunzo ya Biblia na wafungwa wengi katika magereza tofauti-tofauti.

Siku moja Mariví alinijulisha kwamba anatamani kuweka maisha yake wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Lakini hakuruhusiwa kutoka gerezani, wala hakuna aliyeruhusiwa kuingia gerezani ili kumbatiza. Aliendelea kuvumilia mazingira mapotovu ya gereza hilo kwa miaka mingine minne. Ni nini kilichomsaidia kudumisha imani yake? Kutaniko la eneo hilo lilipokuwa likifanya mkutano, wakati huohuo Marivi alikuwa akipitia habari hiyohiyo katika seli yake gerezani. Pia, alikuwa na programu ya kawaida ya kujifunza Biblia kibinafsi na kusali.

Muda si muda, Mariví alihamishiwa katika gereza lenye ulinzi mkali ambalo lilikuwa na dimbwi la kuogelea. Alihisi kwamba badiliko hilo lingemwezesha kubatizwa. Hivyo ndivyo ilivyokuwa. Mwishowe Mariví aliruhusiwa kubatizwa. Na hivyo ndivyo nilivyojikuta nikitoa hotuba yake ya ubatizo. Nilikuwa pamoja naye wakati wa tukio hilo muhimu zaidi katika maisha yake.

Kwa sababu ya mtindo wake wa zamani wa maisha, Mariví aliambukizwa UKIMWI. Hata hivyo, kwa sababu ya mwenendo wake mzuri, alifunguliwa mapema kutoka gerezani mnamo Machi (Mwezi wa 3) 1994. Aliishi nyumbani pamoja na Mama naye alikuwa Mkristo mwenye bidii mpaka kifo chake miaka miwili baadaye.

Kushinda Hisia Mbaya

Mimi pia sijaepuka kabisa matokeo mabaya ya maisha yangu ya zamani. Kutendwa vibaya na baba na pia mtindo wangu wa maisha nikiwa kijana ulikuwa na matokeo mabaya juu ya utu wangu. Katika maisha yangu nikiwa mtu mzima, mara kwa mara nimejihisi mwenye hatia na asiye na thamani. Nyakati nyingine ninashuka moyo sana. Lakini, Neno la Mungu limenisaidia sana kupambana na hisia hizo mbaya. Kadiri miaka inavyopita, kutafakari kwa ukawaida kuhusu maandiko kama vile Isaya 1:18 na Zaburi 103:8-13 kumeniwezesha kushinda hisia hizo za hatia zinazotokea mara kwa mara.

Sala ni silaha nyingine ya kiroho inayonisaidia kupambana na hisia za kujiona sina thamani. Mara nyingi macho yangu yanajaa machozi ninaposali kwa Yehova. Hata hivyo, maneno yaliyoandikwa katika 1 Yohana 3:19, 20 yananitia nguvu: “Kwa jambo hili tutajua kwamba sisi tunatokana na kweli, nasi tutaihakikishia mioyo yetu mbele zake kwa habari ya lolote ambalo huenda mioyo yetu ikatuhukumu kuwa na hatia, kwa sababu Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.”

Kwa kuwa ninamwomba Mungu kwa unyoofu nikiwa na moyo “uliovunjika na kupondwa,” ninatambua kwamba mimi si mbaya kama nilivyokuwa nikifikiri. Biblia inawahakikishia wote wanaomtafuta Yehova kwamba Yeye hawadharau wale wanaojuta kabisa kwa sababu ya mwenendo wao wa zamani na ambao sasa wanafanya mapenzi yake.—Zaburi 51:17.

Wakati wowote ninapokuwa na mashaka, ninajitahidi kufikiria mambo yanayofaa, mambo ya kiroho yanayotajwa katika Wafilipi 4:8. Nimeshika akilini maneno ya Zaburi 23 na Mahubiri ya Mlimani. Mawazo mabaya yanapoingia akilini mwangu, ninarudia-rudia maneno hayo yaliyo katika Maandiko. Kusafisha akili yangu kwa njia hiyo kumenisaidia sana hasa ninapokosa usingizi usiku.

Msaada mwingine ambao nimepata ni pongezi kutoka kwa mke wangu na Wakristo wengine wakomavu. Ijapokuwa mwanzoni ilikuwa vigumu kwangu kukubali maneno yao yenye kutia moyo, Biblia imenisaidia kuelewa kwamba upendo “huamini mambo yote.” (1 Wakorintho 13:7) Na bila shaka, pole kwa pole nimejifunza kukubali udhaifu na mipaka yangu.

Kuna faida ambayo nimepata kutokana na hisia hizo mbaya. Kupambana na hisia hizo mbaya kumenisaidia kuwa mwangalizi anayesafiri mwenye huruma. Mimi pamoja na mke wangu tumetumika tukiwa watumishi wa wakati wote wa habari njema kwa karibu miaka 30. Shangwe ninayopata kwa kuwatumikia wengine inanisaidia kusukumia mbali zaidi na zaidi hisia hizo mbaya na kumbukumbu za mambo mengi mabaya.

Sasa ninapotazama nyuma na kuona baraka zote ambazo Yehova amenipa, ninasukumwa kusema kama Mtunga-zaburi: “Mbariki Yehova, . . . yeye anayesamehe makosa yako yote, anayeponya magonjwa yako yote, anayeuokoa uhai wako kutoka katika shimo, anayekuvika taji la fadhili zenye upendo na rehema.”—Zaburi 103:1-4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini hakichapishwi tena.

[Blabu katika ukurasa wa 30]

Mara kwa mara nimejihisi mwenye hatia na asiye na thamani, lakini, Neno la Mungu limenisaidia sana kupambana na hisia hizo mbaya

[Picha katika ukurasa wa 27]

Ndugu yangu José Luis na rafiki yangu Miguel walifuata mfano wangu mbaya na mzuri pia

[Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Familia ya Morcillo mwaka wa 1973

[Picha katika ukurasa wa 29]

Mariví akiwa mfungwa

[Picha katika ukurasa wa 30]

Nikiwa na mke wangu, Soledad