Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ombi Lilelile Ulimwenguni Pote

Ombi Lilelile Ulimwenguni Pote

Ombi Lilelile Ulimwenguni Pote

WAZIA mamia ya mamilioni au hata mabilioni ya watu, wote wakiomba kitu kilekile. Wanamwomba mwenye mamlaka yote ulimwenguni atimize ombi fulani hususa. Hata hivyo, ni wachache sana kati yao wanaojua kile wanachoomba. Je, kweli ndivyo ilivyo? Kwa kweli, watu wanafanya hivyo kila siku. Watu hao wote wanaomba nini? Wanaomba Ufalme wa Mungu uje!

Kulingana na kadirio moja, kuna dini 37,000 hivi ambazo zinajiita za Kikristo, na zinadai kwamba Yesu Kristo ni Kiongozi. Dini hizo zina wafuasi zaidi ya bilioni mbili. Wengi wao wanatoa ile sala ambayo kwa kawaida inaitwa Sala ya Bwana. Je, unajua sala hiyo? Sala hiyo ambayo Yesu aliwafundisha wafuasi wake inaanza hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.

Kwa karne nyingi sasa, watu wamekuwa wakirudia-rudia maneno hayo wanapoabudu katika makanisa. Wamekuwa wakiyarudia pia wakiwa familia, mtu mmoja-mmoja, katika nyakati nzuri na mbaya. Wamesema maneno hayo kwa unyoofu na hata kwa hisia nyingi. Watu wengine wengi wameyaweka akilini nao wanayasema bila kufikiria maana yake. Watu wengine ambao si waamini wa dini zinazodai kuwa za Kikristo pia wametumaini na kuomba Ufalme wa Mungu uje.

Ombi Ambalo Halitegemei Dini

Katika dini ya Kiyahudi, kuna sala inayotolewa kila siku katika masinagogi au mtu anapofiwa na mtu wa karibu wa familia yake. Ingawa haitaji kifo au maombolezo moja kwa moja, kwa kawaida inasemwa mtu anapofiwa. Sala hiyo ina ombi hili: “[Mungu] na asimamishe Ufalme wake maishani mwako . . .  hata upesi zaidi.” * Sala nyingine ya zamani inayotolewa katika masinagogi inataja tumaini la Ufalme wa Masihi anayetoka katika nyumba ya Daudi.

Watu wa dini nyingine zisizo za Kikristo wamevutiwa na wazo la Ufalme wa Mungu. Gazeti fulani (The Times of India) linasema kwamba kiongozi mmoja mashuhuri wa dini ya Kihindu katika karne ya 19, ambaye alitaka sana kuunganisha pamoja dini ya Kihindu, Kiislamu, na Kikristo, alisema hivi: “Ufalme wa kweli wa Mungu hautapatikana isipokuwa upande wa mashariki uungane na wa magharibi.” Na hivi karibuni msimamizi wa chuo kimoja cha Kiislamu huko Strathfield, Australia, aliandika hivi katika gazeti fulani: “Ninaamini kama Waislamu wote [kwamba] Yesu atarudi na kusimamisha Ufalme wa kweli wa Mungu.”

Bila shaka, leo mabilioni ya watu wanasali na kuutumaini Ufalme wa Mungu. Lakini fikiria jambo hili lenye kupendeza.

Labda unajua kwamba sisi Mashahidi wa Yehova, ambao tunachapisha gazeti hili, tunaenda nyumba kwa nyumba katika eneo lenu na kuzungumza na watu kuhusu Biblia. Wakati huu habari hii inapoandikwa, tunafanya kazi hiyo ulimwenguni pote, katika nchi 236 na katika lugha zaidi ya 400. Kichwa kikuu cha mahubiri yetu ni Ufalme wa Mungu. Kwa kweli, ona kwamba kichwa kamili cha gazeti hili ni Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova. Mara nyingi tunawauliza watu ikiwa wanasali kuhusu Ufalme huo. Wengi wao wanajibu ndiyo. Hata hivyo, wanapoulizwa Ufalme huo ni nini, watu wengi wanajibu hivi, “sijui,” au wanajibu kwa njia isiyoeleweka na isiyo wazi.

Kwa nini watu wengi wanaomba kitu ambacho hawajui? Je, ni kwa sababu Ufalme wa Mungu haueleweki? Hapana. Ufalme huo unafafanuliwa kwa undani na waziwazi katika Biblia. Kwa kuongezea, ujumbe wa Biblia kuhusu Ufalme unaweza kukupa tumaini la kweli katika nyakati hizi zenye taabu. Katika habari inayofuata, tutaona Biblia inasema nini kuhusu tumaini hilo. Kisha, tutaona sala ya Yesu kuhusu kuja kwa Ufalme itajibiwa wakati gani.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kama ile sala ya kielelezo ambayo Yesu alitoa, sala ya Kiyahudi pia ina ombi la kwamba jina la Mungu litakaswe. Ingawa kuna ubishi kuhusu ikiwa sala hiyo ya Kiyahudi ilianza wakati wa Kristo au hata mapema zaidi, hatupaswi kushangaa kwamba inafanana na ile sala ya kielelezo. Sala ya Yesu haikukusudiwa iwe mpya na ya pekee. Sala hizo mbili zilitegemea kabisa Maandiko ambayo Wayahudi wote walikuwa nayo wakati huo. Yesu alikuwa akiwatia moyo Wayahudi wenzake wasali mambo ambayo walipaswa kuwa wakisali kabla ya yeye kuja duniani.