Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ufalme wa Mungu Ni Nini?

Ufalme wa Mungu Ni Nini?

Ufalme wa Mungu Ni Nini?

KICHWA kikuu cha mahubiri ya Yesu kilikuwa nini? Yesu mwenyewe alisema kwamba alihubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. (Luka 4:43) Watu walipomsikiliza, bila shaka walimsikia akitaja Ufalme mara nyingi. Je, walishangaa au kustaajabu? Je, walimuuliza Ufalme ni nini? Hapana. Vitabu vya Injili havina maswali kama hayo. Basi je, watu hao walijua Ufalme wa Mungu?

Ukweli ni kwamba, Maandiko ya zamani ambayo Wayahudi waliona kuwa matakatifu yalifafanua Ufalme huo, na kueleza waziwazi Ufalme huo ni nini na utatimiza nini. Vivyo hivyo leo, tunaweza kujifunza mengi hata zaidi kuhusu Ufalme huo kwa kusoma Biblia. Acheni tuzungumzie kweli saba ambazo tunajifunza katika Biblia kuhusu Ufalme. Wayahudi walioishi kabla na katika siku za Yesu wangeweza kujua kweli tatu za kwanza. Kweli nyingine tatu zilifunuliwa na Kristo au na mitume wake katika karne ya kwanza. Kweli ya mwisho imeonekana wazi katika wakati wetu.

1. Ufalme wa Mungu ni serikali halisi ambayo itadumu milele. Unabii wa kwanza wa Biblia ulifunua kwamba Mungu angemtuma mwokozi kwa wanadamu waaminifu. Mwokozi huyo aliyeitwa “uzao,” angeondoa kabisa matatizo yote ambayo yalisababishwa na uasi wa Adamu, Hawa, na Shetani. (Mwanzo 3:15) Baada ya muda mrefu kupita, Mfalme Daudi aliyekuwa mwaminifu aliambiwa jambo fulani lenye kusisimua kuhusu “uzao” huo, au Masihi. Angekuwa Mfalme wa Ufalme. Serikali hiyo ingekuwa tofauti na serikali nyingine zote. Ingedumu milele.—2 Samweli 7:12-14.

2. Ufalme wa Mungu utakomesha serikali zote za wanadamu. Nabii Danieli alipata maono kuhusu mfuatano wa serikali kuu za ulimwengu katika historia yote mpaka wakati wetu. Ona mwisho wenye kusisimua wa maono hayo: “Katika siku za wafalme hao [wa mwisho wa kibinadamu], Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” Kwa hiyo, falme au serikali zote za ulimwengu huu zitaharibiwa milele, na vita, uonevu, na ufisadi utakomeshwa. Kama unabii wa Danieli unavyoonyesha, hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaitawala dunia yote. (Danieli 2:44, 45) Ufalme huo ambao ni halisi, utakuwa serikali pekee inayotawala dunia. *

3. Ufalme wa Mungu utakomesha vita, magonjwa, njaa, hata kifo. Unabii wenye kusisimua wa Biblia unafunua mambo ambayo Ufalme wa Mungu utafanya hapa duniani. Serikali hiyo itafanya mambo ambayo hakuna serikali au shirika lolote la wanadamu limewahi kufanya au litawahi kufanya. Wazia silaha zote za vita zikiwa zimeharibiwa milele! “Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.” (Zaburi 46:9) Hakutakuwa tena na madaktari, hospitali, au magonjwa ya aina yoyote. “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Hakutakuwa tena na njaa, upungufu wa chakula, utapia-mlo, na watu hawatakufa njaa. “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani.” (Zaburi 72:16) Hakutakuwa na mazishi tena, makesha, makaburi, vyumba vya maiti, au mateso ya kufiwa. Kifo, adui yetu asiyechoka, kitakomeshwa milele. Mungu “kwa kweli atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.”—Isaya 25:8.

4. Ufalme wa Mungu una Mtawala ambaye amechaguliwa na Mungu. Masihi hakujichagua mwenyewe, wala hakuchaguliwa na wanadamu wasio wakamilifu. Amechaguliwa moja kwa moja na Yehova Mungu. Majina yake ya cheo, yaani, Masihi na Kristo yanathibitisha hilo. Maneno yote mawili yanamaanisha “Mtiwa-mafuta.” Kwa hiyo, Mfalme huyo ametiwa mafuta, au amechaguliwa katika cheo chake cha pekee na Yehova. Mungu anasema hivi kumhusu: “Tazama! Mtumishi wangu, ambaye ninamshika sana! Mchaguliwa wangu, ambaye nafsi yangu imemkubali! Nimetia roho yangu ndani yake. Yeye atawatolea mataifa haki.” (Isaya 42:1; Mathayo 12:17, 18) Ni nani anayejua vizuri zaidi aina ya Mtawala tunayehitaji isipokuwa Muumba wetu?

5. Mtawala wa Ufalme wa Mungu amewathibitishia wanadamu wote kwamba anastahili. Yesu wa Nazareti ndiye aliyekuwa Masihi aliyetabiriwa. Alizaliwa katika ukoo uliochaguliwa na Mungu. (Mwanzo 22:18; 1 Mambo ya Nyakati 17:11; Mathayo 1:1) Alipokuwa duniani, alitimiza unabii mwingi sana kumhusu Masihi ambao uliandikwa mamia ya miaka mapema. Alitambulishwa pia kutoka mbinguni kuwa Masihi. Jinsi gani? Mungu aliongea kutoka mbinguni, akimtambulisha kuwa Mwana Wake mwenyewe; malaika walifunua kwamba Yesu ndiye Masihi aliyetabiriwa; na mara nyingi mbele ya mamia au hata maelfu ya watu, Yesu alifanya miujiza ambayo kwa wazi ilitegemea nguvu za Mungu. * Yesu alionyesha mara nyingi sana angekuwa Mtawala wa aina gani. Mbali na kuwa na nguvu za kuwasaidia watu, alitamani pia kuwasaidia. (Mathayo 8:1-3) Alikuwa mwenye huruma, jasiri, na mnyenyekevu, naye hakuwa na ubinafsi. Watu wote wanaweza kusoma katika Biblia masimulizi ya maisha yake duniani.

6. Ufalme wa Mungu una watu wengine 144,000 ambao watatawala pamoja na Kristo. Yesu alisema kwamba wengine, kutia ndani mitume wake wangetawala pamoja naye mbinguni. Aliwaita “kundi dogo.” (Luka 12:32) Baadaye, mtume Yohana aliambiwa kwamba kundi hilo dogo lingekuwa na jumla ya watu 144,000. Wangekuwa na kazi yenye kusisimua huko mbinguni. Wangetawala pamoja na Kristo wakiwa wafalme na makuhani.—Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 3.

7. Ufalme wa Mungu unatawala mbinguni sasa, na hivi karibuni utaanza kutawala juu ya dunia yote. Kweli hii ya mwisho ni moja ya mambo yenye kusisimua sana ambayo tunaweza kujifunza. Biblia inatoa uthibitisho mwingi kwamba Yesu amepewa mamlaka akiwa Mfalme huko mbinguni. Sasa anatawala mbinguni, na hivi karibuni utawala wake utaenea duniani pote na kutimiza unabii mzuri sana ambao tumezungumzia. Lakini tunaweza jinsi gani kuwa na hakika kwamba Ufalme wa Mungu unatawala sasa? Na utaanza kuitawala dunia wakati gani?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Unabii kama huo unaonyesha kwamba Ufalme wa Mungu si kitu kilicho ndani ya mioyo yetu, kama wengi wanavyofundishwa. Ona habari yenye kichwa “Wasomaji Wetu Wanauliza,” kwenye ukurasa wa 13.