Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ufalme wa Mungu Utakuja Wakati Gani?

Ufalme wa Mungu Utakuja Wakati Gani?

Ufalme wa Mungu Utakuja Wakati Gani?

“BWANA, je, unarudishia Israeli ufalme wakati huu?” (Matendo 1:6) Mitume walitaka sana kujua wakati ambapo Yesu angesimamisha Ufalme wake. Leo, miaka 2,000 hivi tangu wakati huo, bado watu wanataka kujua: Ufalme wa Mungu utakuja wakati gani?

Kwa kuwa kichwa kikuu cha mafundisho ya Yesu kilikuwa Ufalme, huenda ukatazamia kwamba alijibu swali hilo. Na bila shaka alilijibu! Alizungumza kwa undani kuhusu kipindi cha pekee ambacho alikiita “kuwapo” kwake. (Mathayo 24:37) Kuwapo kwake kunahusiana sana na kusimamishwa kwa Ufalme wa Kimasihi. Kuwapo huko kunamaanisha nini? Acheni tuzungumzie kweli nne zinazofunuliwa na Biblia kuhusu kuwapo kwa Kristo.

1. Kuwapo kwa Kristo kungeanza muda mrefu baada ya kifo chake. Yesu alitoa mfano ambamo alijifananisha na mtu ambaye “alisafiri mpaka nchi ya mbali ili ajipatie mamlaka ya kifalme,” au apate ufalme. (Luka 19:12) Mfano huo wa kinabii ulitimizwa jinsi gani? Yesu alikufa na kufufuliwa; kisha akasafiri mpaka “nchi ya mbali,” yaani, mbinguni. Kama Yesu alivyotabiri katika mfano mwingine unaolingana na huo, angerudi katika mamlaka ya kifalme “baada ya muda mrefu.”—Mathayo 25:19.

Miaka fulani baada ya Yesu kupanda mbinguni, mtume Paulo aliandika hivi: “Mtu huyu [Yesu] alitoa dhabihu moja kwa ajili ya dhambi daima na kuketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu, tangu wakati huo na kuendelea akingojea mpaka adui zake wawekwe kuwa kiti cha miguu yake.” (Waebrania 10:12, 13) Kwa hiyo, baada ya kufika mbinguni, Yesu alihitaji kungoja kwa kipindi kirefu. Hatimaye, kipindi hicho cha kungoja kiliisha Yehova Mungu alipomfanya Mwana wake kuwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi uliokuwa umeahidiwa kwa muda mrefu. Kuwapo kwa Kristo kulianza wakati huo. Je, wanadamu wangeona tukio hilo la pekee wakiwa duniani?

2. Wanadamu hawawezi kuona kuwapo kwa Yesu kwa macho halisi. Kumbuka kwamba Yesu alizungumzia ishara ya kuwapo kwake. (Mathayo 24:3) Ikiwa wanadamu wangeona kihalisi kuwapo kwake, je, ishara ingehitajiwa? Kwa mfano: Wazia kwamba unaenda kuona bahari. Huenda ukaona ishara njiani zinazokuongoza kwenye bahari hiyo, lakini unapofika kwenye ufuo wake, na kusimama karibu kabisa na maji ya bahari hiyo kubwa sana, je, ungetazamia kuona ishara yenye neno “Bahari” na mshale mkubwa unaoelekeza iliko bahari hiyo? Bila shaka hapana! Je, kweli kuna haja ya ishara inayokuonyesha kitu ambacho tayari unaona kwa macho yako?

Yesu alieleza ishara ya kuwapo kwake ili awasaidie wanadamu kutambua jambo ambalo lingetukia mbinguni wala si jambo ambalo wangeweza kuona kwa macho yao. Kwa hiyo, Yesu alisema hivi: “Ufalme wa Mungu hautakuja kwa wonyesho wenye kutokeza sana.” (Luka 17:20) Hivyo basi, ishara hiyo ingewaonyesha jinsi gani wale walio duniani kwamba kuwapo kwa Kristo kumeanza?

3. Kungekuwa na matatizo makubwa sana hapa duniani wakati wa kuwapo kwa Yesu. Yesu alisema kwamba wakati wa kuwapo kwake akiwa Mfalme huko mbinguni, dunia ingekumbwa na vita, njaa, matetemeko ya nchi, tauni, na uasi-sheria. (Mathayo 24:7-12; Luka 21:10, 11) Matatizo hayo yote yangesababishwa na nini? Biblia inaeleza kwamba Shetani, “mtawala wa ulimwengu huu,” ana hasira kali kwa sababu anajua kwamba wakati wake ni mfupi sana kwa kuwa kuwapo kwa Kristo akiwa Mfalme kumeanza. (Yohana 12:31; Ufunuo 12:9, 12) Leo kuna uthibitisho mwingi ambao unaonyesha kuwapo kwa Kristo kumeanza na Shetani ana hasira kali. Uthibitisho huo umeongezeka sana ulimwenguni pote hasa tangu mwaka wa 1914, mwaka ambao wanahistoria wanatambua ulileta mabadiliko makubwa sana.

Huenda hizo zikaonwa kuwa habari mbaya tu, lakini sivyo ilivyo. Zinamaanisha kwamba Ufalme wa Kimasihi unatawala sasa huko mbinguni. Hivi karibuni, serikali hiyo itatawala juu ya dunia yote. Lakini watu watajua jinsi gani kuhusu Ufalme huo ili wakubali utawala wake na kuwa raia wake?

4. Kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ingefanywa wakati wa kuwapo kwa Yesu. Yesu alisema kwamba kuwapo kwake kungekuwa kama “siku za Noa.” * (Mathayo 24:37-39) Noa hakujenga safina tu; alikuwa pia “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5) Noa aliwaonya watu kwamba hukumu ya Mungu ilikuwa karibu. Yesu alisema kwamba wakati wa kuwapo kwake wafuasi wake duniani wangewaonya watu kama Noa alivyofanya. Alitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

Kama tulivyoona katika sura iliyotangulia, Ufalme wa Mungu utaharibu serikali zote za ulimwengu huu. Kazi ya kuhubiri inawaonya watu kwamba hivi karibuni serikali hiyo ya kimbingu itachukua hatua, na hivyo kuwapa wote nafasi ya kuokoka uharibifu unaokuja na kuwa raia wa Ufalme huo. Basi swali la maana zaidi ni, Utaitikia jinsi gani?

Je, Ufalme wa Mungu Utakuwa Habari Njema Kwako?

Ujumbe ambao Yesu alihubiri uliwapa watu tumaini lisilo na kifani. Baada ya uasi katika Edeni maelfu ya miaka iliyopita, Yehova Mungu alikusudia kuanzisha serikali ambayo ingenyoosha mambo na kuwarudishia wanadamu waaminifu maisha ambayo Mungu alikusudia wawe nayo hapo mwanzoni, maisha ya milele katika paradiso hapa duniani. Je, kuna jambo lenye kusisimua sana kuliko kujua kwamba serikali hiyo iliyoahidiwa zamani inatawala sasa huko mbinguni? Hilo si jambo la kuwaziwa tu ambalo si la kweli, ni jambo halisi kabisa!

Sasa, Mfalme aliyewekwa rasmi na Mungu anatawala katikati ya adui zake. (Zaburi 110:2) Katika ulimwengu huu uliopotoka ambao umetengwa mbali na Mungu, Masihi anatimiza tamaa ya Baba yake ya kuwatafuta watu wote wanaotaka kumjua Mungu kikweli na kumwabudu “kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Watu wa kila jamii, umri, na malezi wana nafasi ya kupata tumaini la kuishi milele chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. (Matendo 10:34, 35) Tunakuhimiza utumie nafasi nzuri ajabu ambayo unapewa. Jifunze kuhusu Ufalme wa Mungu sasa ili uweze kufurahia kuishi milele chini ya utawala wake wenye uadilifu!—1 Yohana 2:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Maneno hayo ya Yesu yanasaidia kurekebisha wazo lisilo sahihi ambalo linategemea jinsi tafsiri fulani zinavyotafsiri kimakosa neno “kuwapo.” Tafsiri fulani zinatafsiri neno hilo kuwa “kuja,” “kufika,” au “kurudi,” na maneno hayo yanamaanisha tukio la muda mfupi tu. Hata hivyo, ona kwamba Yesu hakulinganisha kuwapo kwake na Gharika ya siku za Noa, tukio la wakati mmoja, lakini alililinganisha na “siku za Noa,” kipindi fulani cha mwisho. Kama kipindi hicho cha zamani, kuwapo kwa Kristo kungekuwa kipindi cha wakati ambapo watu wangejishughulisha sana na maisha ya kila siku na kukosa kutambua onyo linalotolewa.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Habari mbaya tunazosikia kila siku zinathibitisha kwamba kutakuwa na mambo mazuri hivi karibuni

[Hisani]

Antiaircraft gun: U.S. Army photo