Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Mungu Anaruhusu Mateso?

Kwa Nini Mungu Anaruhusu Mateso?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Kwa Nini Mungu Anaruhusu Mateso?

Si Mungu anayesababisha mateso ya wanadamu. Biblia inasema hivi: “Hasha, Mungu wa kweli asitende kwa uovu!” (Ayubu 34:10) Hivyo basi, ni nani msababishaji mkuu wa mateso?

Yesu alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu.” (Yohana 14:30) Ni kweli kwamba Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Naye hatakiacha kamwe cheo hicho. Hata hivyo, kwa muda fulani, Mungu amemruhusu Shetani awatawale wanadamu wengi.—1 Yohana 5:19.

Shetani amekuwa mtawala wa aina gani? Shetani amekuwa muuaji na mdanganyifu tangu alipokutana na wanadamu kwa mara ya kwanza. Shetani anailetea jamii ya kibinadamu misiba katika njia nyingi. Yesu alimshutumu kwa maneno haya: “Huyo alikuwa muuaji alipoanza, naye hakusimama imara katika kweli, kwa sababu kweli haimo ndani yake. Anaposema uwongo, yeye husema kulingana na mwelekeo wake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.” (Yohana 8:44) Pia, Yesu alisema kwamba watu ambao walitafuta kumuua walikuwa watoto wa yule muuaji wa kwanza. Walijifanya wenyewe kuwa watoto wake kwa kutenda kama yeye. Ni kweli kwamba watoto wanawaiga baba zao.

Bado Shetani anachochea mitazamo ya uuaji katika mioyo ya wanadamu. Kwa mfano, R. J. Rummel, profesa aliyestaafu wa Chuo Kikuu cha Hawaii, Marekani, anakadiria kwamba tangu mwaka wa 1900 mpaka 1987, serikali mbalimbali ziliua watu 169,198,000 katika jitihada za kisiasa za kuondolea mbali serikali zisizopendwa na watu, maangamizi ya jamii nzima-nzima, na matendo ya jeuri ya kiholela. Vifo hivyo havitii ndani makumi ya mamilioni ambao wameuawa vitani katika kipindi hicho.

Ikiwa si Mungu anayesababisha mateso, kwa nini anayaruhusu? Kwa sababu masuala ya ulimwengu wote kuhusu mema na mabaya ambayo yalitokezwa zamani bado yanahitaji kutatuliwa. Acheni tuchunguze suala moja tu.

Mwanzoni mwa historia ya wanadamu, Adamu na Hawa walimuunga mkono Shetani. Walikataa utawala wa Mungu nao wakachagua kujitawala, na kwa kweli wakachagua utawala wa Ibilisi.—Mwanzo 3:1-6; Ufunuo 12:9.

Ili kutatua suala hilo kwa njia ya haki, Yehova aliruhusu wakati wa kutosha ili kukusanya uthibitisho. Mambo ya kweli yanaonyesha nini? Utawala wa wanadamu chini ya uvutano wa Shetani unaongoza tu kwenye mateso. Kwa kweli, wakati ambao Mungu ameruhusu umewafaidi wanadamu. Jinsi gani? Wale wanaochunguza uthibitisho huo na kuuamini wana nafasi ya kuonyesha kwamba wanakubali kutawaliwa na Mungu. Wale wanaojifunza viwango vya Mungu na kuishi kulingana navyo wana tumaini la kuishi milele.—Yohana 17:3; 1 Yohana 2:17.

Kwa kweli, sasa, Shetani anaongoza ulimwengu kwa uvutano wake mwovu. Lakini hataendelea kuuongoza. Hivi karibuni, Yehova atamtumia Mwana wake ‘kuzivunja kazi za Ibilisi.’ (1 Yohana 3:8) Chini ya uongozi wa Mungu, Yesu ataponya mioyo iliyovunjika na kuboresha maisha ya watu yaliyoharibika. Atawafufua na kuwarudisha kwenye uhai duniani mabilioni ya wanadamu ambao wameteseka na kufa kwa karne nyingi.—Yohana 11:25.

Ufufuo wa Yesu ni mfano wa ushindi wa Mungu juu ya kazi za Ibilisi, ishara ya mambo yanayokuja kwa ajili ya wanadamu ambao wanachagua utawala wa Mungu. (Matendo 17:31) Biblia inatusaidia kuelewa jinsi wakati huo utakavyokuwa kwa maneno haya yenye kufariji: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja [na wanadamu]. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4.