Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ananiongoza Katika Mapito ya Uadilifu”

“Ananiongoza Katika Mapito ya Uadilifu”

“Ananiongoza Katika Mapito ya Uadilifu”

Limesimuliwa na Olga Campbell

“Mtu ambaye ni mfano mzuri ni kama kengele inayowaita wengine,” akasema dada yangu Emily. “Ulipiga kengele, nami nikaitikia.” Alikuwa ameniandikia ili kunipongeza kwa kutimiza miaka 60 katika utumishi wa wakati wote. Acheni niwaeleze jinsi maisha yangu yalivyokuwa nilipokuwa kijana na jinsi nilivyoanza utumishi huo na kuufanya kuwa kazi yangu ya maisha.

NILIZALIWA Januari 19, 1927 (19/1/1927), katika shamba la familia moja kutoka Ukrainia karibu na Wakaw, Saskatchewan, magharibi mwa Kanada. Ndugu yangu pacha, Bill, alikuwa mtoto wa sita nami nilikuwa mtoto wa saba katika familia ya watoto wanane. Tukiwa watoto tulimsaidia baba yetu mwenye bidii kufanya kazi za shambani. Katika nyumba yetu ndogo, mama alitutunza vizuri ingawa alikuwa na maumivu makali ya ugonjwa wa baridi-yabisi, ambao mwishowe ulimuua. Alikufa akiwa na umri wa miaka 37 tu; wakati huo nilikuwa na umri wa miaka 4 tu.

Baba alioa tena miezi sita baada ya Mama kufa. Punde si punde, tulianza kuishi pamoja na dada zetu wa kambo watano, na nyumba yetu ikajaa mvurugo. Nilijitahidi kumheshimu mama yetu wa kambo, lakini haikuwa rahisi kwa ndugu yangu mkubwa John.

Mwishoni mwa miaka ya 1930, mimi na Bill tuliingia shule ya sekondari, ambako tungeweza kuepuka fujo iliyokuwa nyumbani. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokuwa vikikaribia, uzalendo ulipamba moto. Mwalimu wetu mpya alianzisha desturi ya kusalimu bendera, na msichana mmoja alikataa kufanya hivyo. Wanafunzi walimmwagia matusi. Hata hivyo, nilivutiwa na ujasiri wake na kumuuliza kwa nini hakusalimu bendera. Alieleza kwamba alikuwa Mwanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa nyakati fulani, na kwamba alikuwa upande wa Mungu tu.—Kutoka 20:2, 3; Matendo 5:29.

Ninatoka Nyumbani

Mwaka wa 1943, nilipata kazi ya kupakia mizigo kwenye malori huko Prince Albert na kusafirisha soda. Kwa kuwa nilitamani sana kupata mwongozo wa Mungu, nilinunua Biblia lakini nilishindwa kuielewa hivi kwamba nikalia kwa sababu ya kufadhaika. Katika Biblia nilijua tu Sala ya Baba Yetu.—Mathayo 6:9-13.

Jumapili moja (Siku ya Yenga), mama mwenye nyumba niliyokodi alieleza kwa kiburi kwamba alimsukuma “mwanamke wa Biblia” aliyekuja mlangoni pake. Nilijiuliza kwa nini alikuwa mkatili hivyo. Jumapili kadhaa baadaye, sikwenda kanisani kwa sababu nilikuwa mgonjwa. Siku hiyo, yule “mwanamke wa Biblia” alikuja.

Mwanamke huyo aliniuliza, “Je, wewe husali?”

Nilimjibu hivi: “Ninasali Sala ya Baba Yetu.”

Nilisikiliza kwa makini alipokuwa akifafanua maana ya maneno ya Yesu. Aliniahidi kurudi Jumatano (Siku ya 3).

Mwenye nyumba aliporudi, nilimweleza kwa shauku kuhusu yule “mwanamke wa Biblia,” ambaye alikuwa Shahidi wa Yehova. Inasikitisha kwamba mama huyo alinitisha kwa kusema, “Mwanamke huyo akirudi tena hapa Jumatano, nitawafukuza nyote wawili!”

Nilimtafuta sana Shahidi huyo, na baadaye nikajulishwa kwamba anaitwa Bi. Rampel. Nilipompata, nilimweleza tatizo langu na nikamwomba anieleze mambo yote anayojua kuhusu Biblia. Ni kana kwamba tulijifunza Biblia yote tangu kitabu cha Mwanzo mpaka Ufunuo! Alilinganisha wakati wetu na siku za Noa, Mungu alipoharibu ulimwengu usio na uadilifu na kumwokoa Noa na familia yake ili waishi katika dunia iliyosafishwa.—Mathayo 24:37-39; 2 Petro 2:5; 3:5-7, 12.

Bi. Rampel alisema hivi baada ya mazungumzo yetu marefu: “Ninaona kwamba umekubali mafundisho haya ya Biblia kuwa kweli. Majuma mawili tangu sasa, kutakuwa na kusanyiko la Mashahidi wa Yehova, na unapaswa kubatizwa.” Usiku huo nilikesha nikitafakari kuhusu mambo yote niliyojifunza. Ubatizo ulionekana kuwa hatua nzito sana. Hata hivyo, nilitaka kumtumikia Mungu! Ingawa sikuwa na ujuzi mwingi wa Biblia, nilibatizwa Oktoba 15, 1943 (15/10/1943) nikiwa na umri wa miaka 16.

Nahamia Mashariki Kutoka Magharibi

Mnamo Novemba (Mwezi wa 11), ndugu yangu Fred aliniomba niwe mfanyakazi wa nyumbani katika nyumba yake ya ghorofa tatu katika jiji la Toronto mashariki mwa Kanada. Nilikubali, nikitumaini kwamba nitapata uhuru mwingi zaidi wa kumwabudu Yehova huko. Kabla ya kuondoka, nilimtembelea dada yangu Ann, ambaye bado alikuwa anaishi karibu nami huko Saskatchewan. Alitaka kuniambia jambo fulani la kupendeza, yeye na Doris walikuwa wakijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, naye alinihimiza nifanye vivyo hivyo. Kisha, nikamwambia siri yangu, kwamba tayari nilikuwa Shahidi aliyebatizwa!

Mimi na dada yangu mdogo Emily tulipanda garimoshi la kwenda Toronto. Bill alikuja kutupokea kwenye kituo cha garimoshi naye akatupeleka katika nyumba ambamo aliishi pamoja na Fred na John. Nilimuuliza Fred ni nani mwingine aliyekuwa akiishi katika nyumba hiyo. “Hutaamini kamwe,” alisema. “Je, unamkumbuka Alex Reed kutoka nyumbani kwetu? Anaishi kwenye ghorofa ya juu, na mwendawazimu huyo anapendezwa na Wanafunzi wa Biblia!” Nilifurahi sana kusikia hilo.

Nilipanda haraka juu kwenda kumwona Alex na tukapanga kwenda kwenye mikutano usiku huohuo. Nilitaka kuanza kuhudhuria mikutano haraka iwezekanavyo ili ndugu zangu wasinizuie. Muda mfupi baadaye, hata ingawa sikuwa nimejifunza Biblia kirasmi, nilienda kuhubiri kwa mara ya kwanza. Nilifurahia kuzungumza na Waukrainia wengi, kwa kutumia lugha niliyojifunza nilipokuwa mtoto.

Bill alifurahia kusoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi, ambayo niliweka mara nyingi katika chumba chake. Baada ya Bill kuhamia British Columbia, magharibi mwa Kanada, nilimlipia ili awe akipokea magazeti ya Mnara wa Mlinzi. Ingawa si mzungumzaji sana, aliniandikia barua ya shukrani yenye kurasa kumi. Muda si muda, alijiweka wakfu kwa Yehova na kuwa mwangalizi Mkristo mwenye bidii. Nilifurahi kwamba watano kati ya ndugu na dada zangu, yaani, Bill, Ann, Fred, Doris, na Emily walikuja kuwa waabudu wa Yehova waliojiweka wakfu!

Mnamo Mei 22, 1945 (22/5/1945), serikali ya Kanada iliondoa marufuku juu ya kazi ya Mashahidi wa Yehova. * Kwa kweli, sikutambua kwamba tulikuwa tumepigwa marufuku mpaka niliposikia tangazo hilo. Mimi na rafiki yangu Judy Lukus tuliamua kuanza utumishi wa wakati wote tukiwa mapainia mbali zaidi upande wa mashariki huko Quebec, ambako lugha ya Kifaransa inazungumzwa. Dada zangu Doris na Emily waliposikia kuhusu mipango yetu, waliamua kufanya upainia huko Vancouver, British Columbia, upande mwingine wa bara.

Chuki ya Kidini Huko Quebec

Sikuhamia Quebec ili niwe tu katika mazingira mapya. Mashahidi wa huko walikuwa wakikabiliana na upinzani mkali katika kazi yao ya kuhubiri. * Tulifurahia kushiriki katika kazi ya kugawanya trakti ya Kiingereza yenye kichwa, Chuki Kali ya Quebec Kuelekea Mungu, Kristo, na Uhuru, Ni Aibu kwa Kanada Yote. Ujumbe huo mkali ulionyesha wazi chuki ya kidini kuelekea Mashahidi.

Kwa siku 16, tuliingiza kimyakimya trakti hiyo chini ya milango. Na tulifanya kazi hiyo kuanzia mwendo wa saa 8 usiku. Kwenye nyumba moja, tulipata habari kwamba polisi wanakuja kutushika. Tuliwaepa kwa kujificha katika njia moja nyembamba. Siku iliyofuata, tulienda tena barabarani kuwagawia watu Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kadiri miezi ilivyopita, polisi walitukamata mara nyingi sana. Ili kujitayarisha kukaa gerezani, sikuzote nilibeba mswaki na wanja.

Mnamo Novemba 1946, Nathan Knorr, ambaye alikuwa akiongoza kazi ya ulimwenguni pote ya Mashahidi, alitutembelea kutoka Brooklyn, New York. Alitualika mapainia 64 wa Quebec ili tuhudhurie darasa la tisa la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) huko South Lansing, New York. Katika shule hiyo, tulipokea mafundisho mengi ya Biblia kwa miezi mitano. Baada ya kuhitimu mnamo Agosti (Mwezi wa 8) 1947, tulitumwa katika miji mbalimbali ya Quebec ili kuanzisha makutaniko mapya.

Huduma Yenye Kuthawabisha

Wasichana wanne kati yetu tulitumwa katika jiji la Sherbrooke. Tulifanya mazoezi mengi ya kuzungumza Kifaransa. Tulirudia tena na tena maneno mbalimbali tulipokuwa tukienda na kutoka katika eneo letu la mahubiri. Nyakati nyingine, hatukuwa na pesa za chakula cha mchana. Hivyo, tulirudi nyumbani kujifunza. Mwenzangu, Kay Lindhorst, alijua lugha sana. Alinifundisha kwanza kanuni za lugha ya Kiingereza ili niweze kuelewa Kifaransa.

Wakati muhimu wa upainia wangu ulikuwa huko Victoriaville. Wakati huo, mji huo ulikuwa na watu karibu 15,000. Ni watu wachache sana waliozungumza Kiingereza. Hayo yalikuwa mazingira mazuri sana ya kuboresha Kifaransa chetu. Juma letu la kwanza lilikuwa lenye kusisimua sana. Watu walikubali vichapo vyetu kila mahali tulipoenda. Tuliporudi, milango yote na pia madirisha yalikuwa yamefungwa. Kwa nini?

Kasisi wa eneo hilo aliwaonya watu wasitusikilize. Hivyo, tulipoenda nyumba kwa nyumba, watoto walitufuata kwa mbali, wakitutupia mawe na mabonge ya theluji. Hata hivyo, watu wengi walitamani kusikiliza ujumbe wa Biblia. Mwanzoni, walikubali tuwatembelee usiku tu. Hata hivyo, walipopata ujuzi zaidi wa Biblia, walijifunza hadharani hata ingawa majirani wao hawakufurahi.

Katika miaka ya 1950, mimi na dada zangu tulirudi kutembea Wakaw. Kwenye mkutano mmoja, tulisimulia mambo tuliyoona tulipokuwa tukihubiri. Baadaye, mhudumu msimamizi alituambia hivi: “Mama yenu atafurahi sana atakapofufuliwa na kujua kwamba watoto wake walikuja kuwa Mashahidi wa Yehova!” Alieleza kwamba kabla mama yetu hajafa alijifunza Biblia na Shahidi mmoja. Tulitokwa na machozi tuliposikia kwamba Mama alijifunza kweli za Biblia na kwamba angetufundisha kweli hizo ikiwa hangekufa mapema.

Ndoa na Kushiriki Katika Huduma

Mwaka wa 1956, nilikutana na Merton Campbell, Shahidi mmoja aliyefungwa gerezani kwa miezi 27 wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu kwa sababu ya msimamo wake wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote. Alikuwa amefanya kazi kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn kwa karibu miaka kumi. Merton alikuwa na sifa nyingi nzuri za kiroho, na niliona kwamba angekuwa mume mzuri. Tuliandikiana kwa miezi fulani, tukaheshimiana na kupendana zaidi.

Mimi na Merton tulifunga ndoa Septemba 24, 1960 (24/9/1960). Ni baraka kama nini kuishi kwa miaka 47 pamoja na mwanamume mzuri wa kiroho! Kwa miaka 58, Merton amekuwa akifanya kazi katika Idara ya Utumishi ambayo inatoa usaidizi na mwongozo kwa makutaniko ya Mashahidi wa Yehova katika Marekani yote. Kwa zaidi ya miaka 30, kazi yangu huko Brooklyn ilikuwa kupamba vyumba vya wageni na baadaye Majumba makubwa ya Kusanyiko katika New York City. Kisha, mwaka wa 1995, mimi na Merton tulihamishwa kwenda kutumikia kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, kilomita 110 hivi kaskazini ya New York City.

Nilipotoka nyumbani nikiwa na umri wa miaka 12, sikufikiri kamwe kwamba siku moja nitazungukwa na familia kubwa ya kiroho, kutia ndani ndugu na dada zangu. Ninatamani sana wakati ambapo katika ulimwengu mpya wa Mungu, tutaweza kumzunguka Mama na kumweleza kile kilichotukia alipokuwa amekufa, na hasa jinsi Yehova Mungu alivyotutimizia kwa upendo mahitaji yetu ya kiroho. Tunashangilia kama nini kwamba Yehova ametuongoza katika “mapito ya uadilifu”!—Zaburi 23:3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Kwa sababu ya msimamo wa Mashahidi wa Yehova wa kutounga mkono upande wowote katika siasa, serikali ilipiga marufuku tengenezo lao Julai 4, 1940 (4/7/1940).

^ fu. 23 Kwa habari zaidi kuhusu mateso ya kidini huko Quebec, ona gazeti la Amkeni! la Aprili 22, 2000 (22/4/2000), ukurasa wa 20-23.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Wazazi wangu na nyumba tulimoishi pamoja nao na ndugu na dada zangu saba

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikiwa pamoja na wenzangu katika utumishi huko Ottawa, 1952

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikiwa na ndugu na dada zangu (kushoto hadi kulia) Ann, Mary, Fred, Doris, John, mimi, Bill, na Emily

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikiwa na Merton leo