Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawatumii Msalaba Katika Ibada Yao?

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawatumii Msalaba Katika Ibada Yao?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawatumii Msalaba Katika Ibada Yao?

Mashahidi wa Yehova wanaamini kabisa kwamba kifo cha Yesu Kristo kilikuwa dhabihu ya ukombozi ambayo inafungua njia ili wale wanaomwamini wapate uzima wa milele. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16) Hata hivyo, hawaamini kwamba Yesu alikufa kwenye msalaba, kama picha nyingi za kidini zinavyoonyesha. Wanaamini kwamba Yesu alikufa kwenye mti ulionyooka na si kwenye msalaba.

Matumizi ya msalaba yalianza zamani huko Mesopotamia, miaka elfu mbili kabla ya Kristo. Kulikuwa hata na misalaba kwenye miamba ya Skandinavia wakati wa Enzi ya Shaba Nyekundu, karne nyingi kabla ya Yesu kuzaliwa. Watu hao wasiokuwa Wakristo walitumia msalaba “kuwa ishara ya uchawi . . . ambayo iliwalinda, na kuleta bahati nzuri,” akaandika, Sven Tito Achen, mtaalamu wa ishara na mwanahistoria kutoka Denmark, katika kitabu kimoja (Symbols Around Us). Haishangazi kwamba kitabu fulani (New Catholic Encyclopedia) kinasema hivi: “Msalaba unapatikana katika tamaduni za kabla ya Ukristo na za watu wasio Wakristo, ambako unawakilisha vitu vingi vya asili angani.” Kwa nini, basi, makanisa yamechagua msalaba kuwa ishara yao takatifu zaidi?

W. E. Vine, msomi Mwingereza mwenye kuheshimika, anatoa hoja hizi zenye nguvu: “Kufikia katikati ya karne ya 3 W.K. . . . wapagani walikubaliwa kanisani . . . na waliruhusiwa kuendelea kutumia ishara na mifano mingi ya kipagani. Kwa hiyo, Tau au T, . . . ikiwa na vipande viwili vya msalaba vinavyokingamana, ilikubaliwa.”—Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words.

Zaidi ya hayo, Vine anasema kwamba neno “msalaba” na kitenzi “kusulubisha” vinarejelea “mti . . . ulio tofauti na muundo unaokubaliwa na makanisa, yaani, msalaba wenye miti miwili inayokingamana.” Kikikubaliana na wazo hilo, kitabu kimoja (Companion Bible, cha Chuo Kikuu cha Oxford) kinasema hivi: “Uthibitisho ni . . . kwamba Bwana aliuawa juu ya mti ulionyooka, bali si juu ya vipande viwili vya mbao vilivyokingamana kwa njia yoyote ile.” Ni wazi kwamba makanisa yamekubali desturi ambayo si ya Kibiblia.

Mwanahistoria Achen, aliyenukuliwa hapo juu, anasema hivi: “Inaelekea kwamba karne mbili baada ya kifo cha Yesu, Wakristo hawakutumia ishara ya msalaba.” Anaongeza kwamba kwa Wakristo wa karne ya kwanza, haikosi msalaba “uliwakilisha hasa kifo na uovu, kama vizazi vya baadaye vinavyoona mashini ya kukata kichwa au kiti cha umeme cha kuua.”

Jambo la maana zaidi ni kwamba haidhuru ni kitu gani kilichotumiwa kumtesa na kumuua Yesu, ishara au mfano wa kitu hicho haupaswi kuabudiwa au kutumiwa na Wakristo katika ibada. Biblia inaamuru: “Ikimbieni ibada ya sanamu.” (1 Wakorintho 10:14) Yesu mwenyewe alionyesha jambo ambalo lingewatambulisha wafuasi wake wa kweli. Alisema hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”—Yohana 13:35.

Katika mambo yote yanayohusu ibada, Mashahidi wa Yehova, kama vile Wakristo wa karne ya kwanza, wanajitahidi kufuata Biblia badala ya desturi. (Waroma 3:4; Wakolosai 2:8) Kwa sababu hiyo, hawatumii msalaba katika ibada yao.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Mchoro ukionyesha mfalme mpagani Mwashuru akiwa amevaa msalaba, karibu mwaka wa 800 K.W.K.

[Hisani]

Photograph taken by courtesy of the British Museum