Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Kinachohusika Katika Kulijua Jina la Mungu?

Ni Nini Kinachohusika Katika Kulijua Jina la Mungu?

Ni Nini Kinachohusika Katika Kulijua Jina la Mungu?

UUMBAJI unaoonekana unaonyesha kwamba kuna Mungu, lakini haufunui jina la Mungu. (Zaburi 19:1; Waroma 1:20) Ili mtu alijue jina la Mungu, anahitaji kujua mengi zaidi ya jina lenyewe. (2 Mambo ya Nyakati 6:33) Kulijua jina hilo kunamaanisha kumjua Mungu mwenyewe—kusudi lake, kazi zake, na sifa zake kama zinavyofunuliwa katika Neno lake. Jambo hilo linaonyeshwa katika kisa cha Musa, mtu ambaye Yehova ‘alimjua kwa jina,’ yaani, kwa ukaribu. (Kutoka 33:12) Musa alipata pendeleo la kuona utukufu wa Yehova na pia kusikia ‘jina la Yehova likitangazwa.’ (Kutoka 34:5) Tangazo hilo halikurudia-rudia tu jina Yehova, bali lilionyesha sifa na kazi za Mungu. “Yehova, Yehova, Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli, anayehifadhi fadhili zenye upendo kwa ajili ya maelfu, anayesamehe kosa na ubaya na dhambi, lakini kwa vyovyote hatakosa kuadhibu, anayeleta adhabu kwa ajili ya kosa la akina baba juu ya wana na juu ya wajukuu, juu ya kizazi cha tatu na juu ya kizazi cha nne.”—Kutoka 34:6, 7.

Yesu Kristo alipokuwa duniani, ‘aliwajulisha wanafunzi wake jina la Baba yake.’ (Yohana 17:6, 26) Ingawa tayari wanafunzi hao walijua jina hilo na kazi za Mungu ambazo ziliandikwa katika Maandiko ya Kiebrania, walipata kumjua Yehova vizuri zaidi kupitia Yule aliye “kifuani pa Baba.” (Yohana 1:18) Kristo Yesu alimwakilisha Baba yake kwa njia kamilifu, kwa kufanya kazi za Baba yake na kusema maneno ya Baba yake, bali si maneno yake mwenyewe. (Yohana 10:37, 38; 12:50; 14:10, 11, 24) Hiyo ndiyo sababu Yesu angeweza kusema, “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”—Yohana 14:9.

Hilo linaonyesha wazi kwamba ni watumishi wa Mungu watiifu peke yao ndio wanaojua jina la Mungu kikweli. (Linganisha na 1 Yohana 4:8; 5:2, 3.) Hivyo, uhakikisho ambao Yehova anatoa katika Zaburi 91:14, unawahusu watu hao: “Nitamlinda kwa sababu amelijua jina langu.” Jina hilo si hirizi, hata hivyo, Yule anayeitwa kwa jina hilo anaweza kuwalinda watu wake waaminifu. Kwa hiyo, jina hilo linamwakilisha Mungu mwenyewe. Ndiyo sababu methali moja ya Biblia inasema: “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi.” (Methali 18:10) Watu wanaomtupia Yehova mizigo yao wanafanya hivyo.—Zaburi 55:22.

Yehova analionea wivu jina lake, naye havumilii ushindani wowote wala ukosefu wa uaminifu katika mambo ya ibada. (Kutoka 34:14; Ezekieli 5:13) Waisraeli waliamuriwa hata wasiyataje majina ya miungu mingine. (Kutoka 23:13) Kwa kuwa majina ya miungu ya uwongo yako katika Biblia, inaonekana kwamba hilo linahusu kutaja majina ya miungu ya uwongo katika ibada.

Waisraeli, ambao waliitwa kwa jina la Mungu, walilichafua au kulitia unajisi jina lake waliposhindwa kuishi kulingana na amri zake za uadilifu. (Ezekieli 43:8; Amosi 2:7) Kwa kuwa Mungu aliwaadhibu Waisraeli kwa sababu ya kutokuwa waaminifu, hilo lilifanya mataifa mengine yalidharau jina la Mungu. (Linganisha na Zaburi 74:10, 18; Isaya 52:5.) Kwa kuwa mataifa hayo hayakutambua kwamba adhabu hiyo inatoka kwa Yehova, yalifikiri kimakosa kwamba Waisraeli wanapatwa na misiba kwa sababu Yehova hana uwezo wa kuwalinda watu wake. Ili kulisafisha jina lake, Yehova alichukua hatua ya kulitetea jina lake na kuwarudisha mabaki ya Waisraeli katika nchi yao.—Ezekieli 36:22-24.

Ni pendeleo kama nini kulijua jina la Mungu na hata kumwakilisha!—Isaya 43:10-12.