Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Sheria Imekuwa Mtunzaji Wetu”

“Sheria Imekuwa Mtunzaji Wetu”

“Sheria Imekuwa Mtunzaji Wetu”

NI WATOTO wangapi ambao wanatambua umuhimu wa sheria na nidhamu? Si wengi. Watoto hawapendi vizuizi. Hata hivyo, wale walio na wajibu wa kuwasaidia watoto, wanajua kwamba ni lazima watoto wasimamiwe kwa njia inayofaa. Na kadiri miaka inavyopita, huenda vijana wengi wakatambua umuhimu wa mwongozo waliopokea. Mtume Paulo alitumia mfano wa mtu aliyewalinda watoto ili kuonyesha jambo fulani kuhusu uhusiano kati ya Yehova Mungu na watu wake.

Wakristo fulani wa karne ya kwanza katika jimbo la Roma la Galatia walisisitiza kwamba Mungu aliwapenda tu wale ambao walitii Sheria aliyowapa Waisraeli kupitia Musa. Mtume Paulo alijua kwamba hilo si kweli, kwa kuwa Mungu aliwapa roho takatifu watu fulani ambao hawakufuata kamwe sheria ya Wayahudi. (Matendo 15:12) Hivyo, Paulo alisahihisha maoni hayo yasiyo ya kweli kwa kutoa mfano mmoja. Katika barua yake kwa Wakristo Wagalatia, aliandika hivi: “Sheria imekuwa mtunzaji wetu kutuongoza kwa Kristo.” (Wagalatia 3:24) Msomi mmoja anasema kwamba mfano wa mtunzaji ni wa “zamani na wenye maana sana.” Kuelewa maana ya mfano huo kunatusaidia kufahamu jambo ambalo mtume Paulo alikuwa akizungumzia.

Mtunzaji na Wajibu Wake

Watunzaji walitumiwa sana katika familia tajiri za Wagiriki, Waroma, na hata labda za Wayahudi ili kusimamia shughuli za watoto tangu walipokuwa wachanga mpaka walipobalehe. Kwa kawaida, mtunzaji alikuwa mtumwa ambaye alitumainiwa, na mara nyingi alikuwa mtu mwenye umri mkubwa, aliyetumika akiwa mtumishi ili kuhakikisha kuwa mtoto alikuwa salama na kwamba maagizo ya baba kumhusu mtoto huyo yalifuatwa. Mchana kutwa, mtunzaji alimsindikiza mtoto popote alipoenda, alimtunza, alimpeleka shuleni, na mara nyingi alimbebea vitabu na vifaa vingine, na kuhakikisha kwamba mtoto huyo anajifunza.

Kwa kawaida, mtunzaji hakuwa mwalimu wa shule. Badala ya kutoa mafunzo rasmi, mtunzaji alikuwa tu mlinzi wa mtoto na alihakikisha kwamba maagizo ya baba yanafuatwa. Hata hivyo, alitoa maagizo kwa njia isiyo ya moja kwa moja kwa kumwongoza mtoto na kumtia nidhamu. Hiyo ilitia ndani kumfundisha mtoto jinsi ya kujiendesha, kumkaripia, na hata kumwadhibu mtoto kwa kiboko akijiendesha isivyofaa. Bila shaka, mama na baba ndio waliokuwa hasa walimu wa mtoto. Hata hivyo, mvulana alipoendelea kukua, mtunzaji wake alimfundisha jinsi ya kutembea vizuri barabarani, jinsi ya kuvaa joho lake, kukaa na kula kwa njia inayofaa, na alimfundisha kwamba alipaswa kusimama mbele ya watu wanaomzidi umri, kuwapenda wazazi wake, na kadhalika.

Mwanafalsafa Mgiriki Plato (428-348 K.W.K.) alikazia kwamba tamaa za kitoto zinapaswa kuzuiwa. Aliandika hivi: “Kama vile tu kondoo au mnyama mwingine anayelisha hawezi kuishi bila mchungaji, vivyo hivyo watoto hawawezi kuishi bila mtunzaji, wala watumwa bila bwana.” Huenda maoni hayo yakaonekana kuwa yenye kupita kiasi. Lakini, hivyo ndivyo Plato alivyoona mambo.

Kuwapo daima kwa watunzaji kuliwafanya wawe na sifa ya kuwa walinzi wenye kuonea na watoa-nidhamu wakali, jambo ambalo lilitokeza mashtaka mengi madogo-madogo yenye kulemea, na yasiyo na maana. Hata hivyo, mtunzaji alimlinda mtoto kiadili na pia kimwili. Appian, mwanahistoria Mgiriki wa karne ya pili W.K. anaeleza kuhusu mtunzaji mmoja ambaye akiwa njiani kwenda shuleni alimshika mtoto ili kumlinda na wauaji. Alipokataa kumwachilia mvulana huyo, wote wawili waliuawa.

Maadili mapotovu yalienea sana katika Ugiriki ya kale. Watoto, hasa wa kiume, walihitaji kulindwa ili wasinyanyaswe kingono. Hivyo, watunzaji walikuwepo watoto walipokuwa wakifundishwa kwa sababu walimu wengi hawakutumainika. Msemaji Mgiriki, Libanius, wa karne ya nne W.K. hata alisema kwamba watunzaji walipaswa kuwa “walinzi wa vijana wanaokua,” ili “kuzuia wapenzi wasiotakikana, kuwazuia wasiwe na uhusiano wa karibu sana na wanafunzi wengine, wala wasichangamane na wavulana.” Watunzaji wengi waliheshimiwa na wale ambao walilinda. Mawe ya ukumbusho yanaonyesha jinsi watu fulani wazima walivyowathamini watunzaji wapendwa waliokufa.

Sheria Ikiwa Mtunzaji

Kwa nini mtume Paulo alilinganisha Sheria ya Musa na mtunzaji? Ni nini kinachofanya mfano huo ufae kabisa?

Jambo la kwanza ni kwamba Sheria ilitoa ulinzi. Paulo alieleza kwamba Wayahudi ‘walilindwa chini ya sheria.’ Ni kana kwamba walilindwa na mtunzaji. (Wagalatia 3:23) Sheria ilikuwa na uvutano katika kila sehemu ya maisha yao. Ilizuia tamaa zao zisizofaa na za kimwili. Sheria iliongoza mwenendo wao na iliwakaripia daima kwa sababu ya makosa yao, na hivyo kumfanya kila Mwisraeli atambue kutokamilika kwake.

Pia, Sheria iliwalinda Waisraeli kutokana na uvutano mbalimbali mpotovu, kama vile mazoea machafu kiadili na mazoea ya kidini ya mataifa yaliyowazunguka. Kwa mfano, Mungu aliwakataza Waisraeli wasioane na wapagani ili taifa lote liwe na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. (Kumbukumbu la Torati 7:3, 4) Sheria hizo zililinda usafi wa kiroho wa watu wa Mungu na kuwatayarisha wamtambue Masihi. Kwa kweli, hayo yalikuwa maandalizi yenye upendo. Musa aliwakumbusha Waisraeli wenzake hivi: “Kama vile mtu anavyomrekebisha mwana wake, ndivyo Yehova Mungu wako alikuwa akikurekebisha.”—Kumbukumbu la Torati 8:5.

Hata hivyo, jambo la maana katika mfano wa mtume Paulo ni kwamba mtunzaji alikuwa na mamlaka ya muda tu. Mtoto alipokuwa mtu mzima, hakulindwa tena na mtunzaji. Mwanahistoria Mgiriki Xenophon (431-352 K.W.K.) aliandika hivi: “Wakati ambapo mvulana si mtoto tena, na anapoanza kuwa kijana, watu wengine wanamweka huru kutokana na [mtunzaji] wake na pia [mwalimu] wake; hawi tena chini ya uongozi wao, lakini anaruhusiwa kujitegemea maishani.”

Ndivyo ilivyokuwa kuhusiana na mamlaka ya Sheria ya Musa. Mamlaka yake yalikuwa ya muda tu, “ili kufanya makosa yawe wazi, mpaka ufike uzao [Yesu Kristo].” Mtume Paulo alieleza kwamba kwa Wayahudi, Sheria ilikuwa ‘mtunzaji ili kuwaongoza kwa Kristo.’ Ili Wayahudi wa siku za Paulo wapate kibali cha Mungu, walipaswa kutambua daraka la Yesu katika kusudi la Mungu. Wayahudi fulani walipotambua daraka hilo, kazi ya mtunzaji ilikwisha.—Wagalatia 3:19, 24, 25.

Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilikuwa kamilifu. Ilitimiza kabisa makusudi ya Mungu, yaani, kuwalinda watu wake na kuwaonyesha kwamba viwango vyake ni vya hali ya juu. (Waroma 7:7-14) Sheria ilikuwa mtunzaji mzuri. Hata hivyo, huenda watu fulani ambao waliishi chini ya ulinzi wa Sheria, waliona matakwa yake kuwa mzigo mzito. Hivyo, Paulo angeweza kuandika kwamba wakati uliowekwa na Mungu ulipofika, “Kristo kwa kutununua alituachilia huru kutoka katika laana ya Sheria.” Sheria hiyo ilikuwa “laana” katika maana ya kwamba iliwatiisha Wayahudi wasio wakamilifu chini ya viwango ambavyo hawangeweza kuvifuata kwa ukamilifu. Walipaswa kufuata kwa makini desturi nyingi. Myahudi alipokubali dhabihu ya ukombozi iliyotolewa na Yesu, hakuhitaji tena kuwa chini ya vizuizi vya mtunzaji.—Wagalatia 3:13; 4:9, 10.

Hivyo, Paulo alipolinganisha Sheria ya Musa na mtunzaji, alikuwa akikazia kwamba Sheria hiyo ilipaswa kuwaongoza Wayahudi na kwamba ilikuwa ya muda tu. Tunapata kibali cha Yehova si kwa kutii Sheria hiyo, bali kwa kumtambua Yesu na kumwamini.—Wagalatia 2:16; 3:11.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

“WATU WENYE KUSIMAMIA” NA “WASIMAMIZI-NYUMBA”

Mbali na kuandika kuhusu mtunzaji, mtume Paulo alitumia pia mfano wa “watu wenye kusimamia” na mfano wa “wasimamizi-nyumba.” Tunasoma hivi katika Wagalatia 4:1, 2: “Wakati mrithi anapokuwa angali mtoto mchanga hatofautiani hata kidogo na mtumwa, ingawa yeye ni bwana wa vitu vyote, bali yeye yuko chini ya watu wenye kusimamia na chini ya wasimamizi-nyumba mpaka siku ambayo baba yake aliiweka kimbele.” Kazi za “watu wenye kusimamia” na “wasimamizi-nyumba” zilitofautiana na zile za watunzaji, lakini Paulo alitaka kukazia jambo lilelile.

Chini ya sheria ya Waroma, ‘mtu mwenye kusimamia’ aliwekwa rasmi kisheria ili kumlinda mtoto mchanga aliyekuwa yatima na kusimamia masuala ya kifedha ya mtoto huyo mpaka wakati ambapo angekuwa mtu mzima. Hivyo, Paulo anasema kwamba hata ingawa mtoto huyo kwa njia fulani alikuwa ndiye “bwana” wa urithi wake, maadamu alikuwa bado mtoto, sawasawa na mtumwa, hakuwa na haki yoyote ya urithi huo.

Kwa upande mwingine, ‘msimamizi-nyumba,’ alisimamia masuala ya kifedha ya mali za mtoto huyo. Flavio Yosefo, mwanahistoria Myahudi, anasema kwamba kijana aliyeitwa Hyrcanus alimwomba baba yake barua ya kumwagiza msimamizi-nyumba wake ampe pesa za kununua kitu chochote alichohitaji.

Hivyo, sawa na mtoto aliyekuwa chini ya mtunzaji, mtoto aliyekuwa chini ya ‘mtu mwenye kusimamia’ au ‘msimamizi-nyumba’ hakuwa na uhuru. Maisha ya mtoto huyo yaliongozwa na watu wengine mpaka wakati uliowekwa na baba yake ulipofika.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Mchoro kwenye chombo cha zamani cha Ugiriki unaoonyesha mtunzaji akiwa na fimbo yake

[Hisani]

National Archaeological Museum, Athens

[Picha katika ukurasa wa 19]

Mchoro wa karne ya tano K.W.K. kwenye kikombe unaoonyesha mtunzaji (akiwa na fimbo) akimtazama mtoto akifundishwa mashairi na muziki

[Hisani]

Bildarchiv Preussischer Kulturbesitz/Art Resource, NY