Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Sijawahi Kamwe Kuhisi Upendo Kama Huu”

“Sijawahi Kamwe Kuhisi Upendo Kama Huu”

Barua Kutoka Jamhuri ya Dominika

“Sijawahi Kamwe Kuhisi Upendo Kama Huu”

NIURKA alitoa hotuba ya Biblia kwa mara ya kwanza katika kutaniko letu juma hili. Alitayarisha hotuba hiyo kwa kuiandika katika maandishi ya vipofu, kisha akaiweka akilini. Nilikuwa jukwaani pamoja naye, nikijifanya kuwa mtu aliyetaka kujifunza kweli ya Biblia. Nilitumia kikuza-sauti ambacho kilipeleka sauti yangu kwenye vifaa vya kusikia alivyovaa kwenye masikio. Tulipomaliza, wahudhuriaji wenye mshangao walipiga makofi kwa nguvu sana hivi kwamba aliweza kuyasikia makofi hayo. Tabasamu yake ilionyesha jinsi alivyofurahi na kutosheka. Nilifurahi pia. Ni baraka kama nini kuwa mmishonari!

Ninakumbuka mara ya kwanza nilipokutana na Niurka. Ilikuwa miaka miwili iliyopita. Siku hiyo, baada ya kuendesha gari kwa dakika 30 kwenye barabara za vumbi, nilimwona kwa mara ya kwanza. Alikuwa ameketi kwenye varanda ya nyumba ndogo iliyojengwa kwa mbao na matofali, na iliyoezekwa mabati yenye kutu. Kulikuwa na sauti na harufu ya mbuzi, sungura, na mbwa. Niurka aliketi akiwa ameinamisha kichwa chini, ishara ya upweke na kushuka moyo. Alionekana mzee sana ingawa alikuwa na umri wa miaka 34.

Nilimgusa-gusa kwenye bega, na aliinua kichwa chake kutuelekea. Alikuwa amepofuka miaka 11 iliyopita. Nilimwambia kwa sauti kubwa katika sikio jina langu na jina la yule niliyekuwa nikihubiri naye. Baadaye, tulijua kwamba Niurka alipatwa na ugonjwa wa Marfan unaorithiwa, ambao ulimletea maumivu makali. Pia, Niurka alikuwa na ugonjwa mbaya wa sukari ambao ulimlazimu kupima mara nyingi viwango vya sukari katika damu kwa kuwa vinabadilika-badilika.

Nilipoweka Biblia mikononi mwake, aliitambua na kusema kwamba kabla ya kuwa kipofu alipenda sana kusoma Maandiko. Basi, ningemfundisha jinsi gani msichana huyu mnyonge, mpweke, na mnyenyekevu, kweli zenye kuburudisha za Neno la Mungu? Kwa kuwa alijua alfabeti, nilianza kwa kuweka mikononi mwake herufi za plastiki. Punde si punde, alianza kuzitambua. Kisha, kwa kugusa mikono yangu nilipokuwa nikisema kwa ishara, alijifunza kuhusianisha kila herufi na herufi inayolingana nayo katika Lugha ya Ishara ya Marekani. Hatua kwa hatua alijifunza ishara nyingine. Kwa sababu nilikuwa nimeanza tu kujifunza peke yangu lugha ya ishara, nilihitaji kutayarisha kila somo kwa saa nyingi. Hata hivyo, mimi na Niurka tulifanya maendeleo ya haraka katika lugha ya ishara kwa sababu tulijitahidi sana.

Niurka alifanya maendeleo makubwa hata zaidi wakati shirika moja la misaada lilipompa vifaa vya kuwasaidia watu kusikia. Vifaa hivyo vilimsaidia sana ingawa havikuwa vya hali ya juu. Baada ya kuishi kwa zaidi ya miaka kumi bila kuona na katika hali ya ukimya kabisa, alijitenga na watu. Lakini roho ya Yehova ilichochea akili na moyo wake na kuujaza ujuzi, tumaini, na upendo. Punde si punde, kwa kutumia fimbo ya kutembelea, Niurka alikuwa akitembelea maeneo ya karibu na kuwahubiria wengine kweli za Biblia.

Niurka anawafundisha Biblia shangazi yake na binamu wake wawili. Anatayarisha vizuri kila somo, na kuliweka akilini. Wanafunzi wake wanasoma fungu halafu Niurka anasoma swali katika kitabu chake cha maandishi ya vipofu. Mtu anayehubiri naye anamwambia Niurka majibu kwa kusema kwa sauti kubwa masikioni mwake au kufanya ishara mikononi mwake.

Kutaniko lote linamsaidia na kumtia moyo Niurka. Baadhi ya ndugu zake Wakristo wanamsaidia kwa kumpeleka kwenye mikutano na makusanyiko. Wengine wanaenda naye kuhubiri. Hivi karibuni Niurka aliniambia hivi: “Sijawahi kamwe kuhisi upendo kama huu.” Anatumaini kubatizwa kwenye kusanyiko letu la wilaya lijalo.

Tunapopitia mahali ambapo Niurka anaishi, tunamwona akiwa ameketi katika varanda akiota jua huku akiwa ameinua kichwa chake na kutabasamu. Ninamuuliza kwa nini anatabasamu. Niurka anasema: “Nilikuwa nikitafakari kuhusu wakati ujao dunia itakapokuwa paradiso. Na nilijiwazia nikiwa huko tayari.”

[Picha katika ukurasa wa 25]

Niurka pamoja na washiriki fulani wa kutaniko letu mbele ya Jumba la Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 25]

Niurka anawaambia wengine yale ambayo amejifunza