Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kupata Furaha Hata Ukivunjika Moyo

Unaweza Kupata Furaha Hata Ukivunjika Moyo

Unaweza Kupata Furaha Hata Ukivunjika Moyo

NI NANI ambaye hajawahi kuvunjwa moyo? Hata Baba yetu wa mbinguni, Yehova Mungu, amewahi kupatwa na maumivu ya kukatishwa tamaa. Kwa mfano, aliwakomboa Waisraeli kutoka utumwani huko Misri na kuwabariki sana. Lakini, Biblia inasema: “Wakawa wakimjaribu Mungu tena na tena, nao wakamtia uchungu Mtakatifu wa Israeli.” (Zaburi 78:41) Hata hivyo, sikuzote Yehova ni “Mungu mwenye furaha.”—1 Timotheo 1:11.

Kwa kweli, kuna mambo mengi yanayoweza kutuvunja moyo. Tunaweza kufanya nini ili mambo hayo yasitunyang’anye furaha? Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yehova Mungu alivyoshughulikia hali zenye kukatisha tamaa?

Mambo Yanayovunja Moyo

Neno la Mungu linasema kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” linatupata sote. (Mhubiri 9:11) Uhalifu, msiba, au ugonjwa unaweza kutokea ghafula na kutuhuzunisha kwelikweli, ndiyo, unaweza kutuvunja moyo. Pia, Biblia inasema: “Tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa.” (Methali 13:12) Tunakuwa na furaha sana tunapotazamia kwa hamu jambo zuri, lakini linapokawia, tunaweza kushuka moyo. Kwa mfano, Duncan * alitamani sana kuwa mmishonari. Lakini baada ya yeye na mke wake kufanya utumishi wa umishonari kwa miaka mingi, walilazimika kurudi nyumbani. Duncan alisema hivi: “Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu, nilipoteza mwelekeo. Sikuwa na miradi tena. Mambo yote yalionekana kuwa hayana maana tena.” Maumivu ya kuvunjika moyo yanaweza kudumu kwa muda mrefu, kama ilivyokuwa katika kisa cha Claire. Anasema hivi: “Nilikuwa na mimba ya miezi saba, lakini mimba hiyo ikaharibika. Sasa miaka mingi imepita, lakini hata leo, ninapomwona mvulana yeyote akitoa hotuba jukwaani, ninajiambia hivi, ‘Mwana wangu angekuwa kama huyu.’”

Pia, unaweza kuumia mtu fulani anapokuvunja moyo, kama vile wakati uchumba unapovunjika, ndoa inapovunjika, mtoto anapoasi, rafiki akikosa kuwa mshikamanifu au akionyesha kwamba hakuthamini. Kwa kuwa tunaishi na watu wasio wakamilifu na katika nyakati ngumu, tunaweza kuvunjwa moyo mara kwa mara.

Zaidi ya hayo, tunaweza kuvunjika moyo tusipofanikiwa. Kwa mfano, tusipopita mtihani, tusipopata kazi, au tunaposhindwa kumvutia mtu fulani tunayempenda, tunaweza kujihisi kwamba hatufai. Pia, tunaweza kujilaumu wakati mtu tunayempenda anapoanguka kiroho. Mary anasema: “Binti yangu alionekana kuwa Mkristo mwenye maendeleo. Nilifikiri kwamba nimemwekea mfano mzuri. Lakini alipomwasi Yehova Mungu na kuacha kufuata kanuni zetu za familia, nilijiona sifai kamwe. Hata mafanikio mengine niliyopata maishani hayangeondoa huzuni yangu. Nilivunjika moyo sana.”

Tunaweza kufanya nini tunapovunjika moyo kwa sababu ya hali kama hizo? Ili tupate jibu, acheni tuchunguze mfano uliowekwa na Yehova katika kushughulikia hali zinazokatisha tamaa.

Kazia Fikira Suluhisho

Kwa upendo, Yehova Mungu aliwapa wenzi wa ndoa wa kwanza kila kitu walichohitaji, lakini hawakuthamini maandalizi hayo, nao wakaasi. (Mwanzo, sura ya 2 na 3) Kisha, mwana wao Kaini akaanza kusitawisha mtazamo mbaya. Kaini alipuuza onyo la Yehova, naye akamuua ndugu yake. (Mwanzo 4:1-8) Je, unaweza kuwazia jinsi Yehova alivyokatishwa tamaa?

Kwa nini jambo hilo halikumnyang’anya Mungu furaha? Kwa sababu alikuwa amekusudia wanadamu wakamilifu waijaze dunia, naye aliendelea kufanya kazi ili kutimiza kusudi hilo. (Yohana 5:17) Akiwa na lengo hilo, aliandaa dhabihu ya ukombozi na Ufalme wake. (Mathayo 6:9, 10; Waroma 5:18, 19) Yehova Mungu alikazia fikira suluhisho, bali si tatizo.

Neno la Mungu linatutia moyo tukazie fikira mambo tunayoweza kufanya badala ya yale ambayo yangetokea au yale ambayo tulikosa kufanya. Linasema: “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa lililoko, endeleeni kuyafikiria mambo hayo.”—Wafilipi 4:8.

Maoni Yanayofaa Kuhusu Mambo Yenye Kuvunja Moyo

Maisha yetu yanaweza kubadilika ghafula. Kwa mfano, tunaweza kufutwa kazi ghafula, kupoteza mwenzi wa ndoa, au mapendeleo yetu. Tunaweza kuwa wagonjwa, kupoteza nyumba, au marafiki. Tunaweza kufanya nini mabadiliko kama hayo yakitokea?

Wengine wameona kwamba kuna faida ya kutanguliza mambo fulani. Duncan, aliyetajwa mwanzoni, anasema: “Mimi na mke wangu tulipotambua kwamba hatungeweza tena kuwa wamishonari, tulivunjika moyo sana. Mwishowe, tuliamua kutanguliza mambo mawili: kumtunza Mama na ikiwezekana, kuendelea katika utumishi wa wakati wote. Tunapohitaji kufanya maamuzi, tunafikiria ikiwa maamuzi hayo yatavuruga mambo hayo tunayotanguliza. Hivyo, inakuwa rahisi zaidi kufanya maamuzi.”

Kwa kawaida, wengi wetu tunapovunjika moyo, tunakazia fikira kupita kiasi mambo mabaya. Kwa mfano, huenda tusifanikiwe katika jitihada zetu za kumlea mtoto, kupata kazi, au kuhubiri habari njema katika eneo la kigeni. Labda tunaweza kusema, ‘Sifai hata kidogo.’ Lakini, mambo yaliyotukia mwanzoni mwa historia ya wanadamu hayakumfanya Mungu ajione hafai, nasi hatupaswi kuona kwamba hatufai tusipofanikiwa mwanzoni.—Kumbukumbu la Torati 32:4, 5.

Ni rahisi kukasirika sana watu wanapotuvunja moyo. Lakini Yehova hafanyi hivyo. Mfalme Daudi alifanya jambo lenye kukatisha tamaa alipofanya uzinzi pamoja na mwanamke na kuagiza mume wake auawe. Hata hivyo, Yehova aliona kwamba Daudi ametubu kikweli, naye akaendelea kumtumia Daudi kuwa mtumishi wake. Vivyo hivyo, Mfalme Yehoshafati mwaminifu alikosea alipofanya mapatano na maadui wa Mungu. Nabii wa Yehova alisema: “Kwa sababu hiyo kuna ghadhabu juu yako inayotoka mbele za uso wa Yehova. Hata hivyo, kuna mambo mema ambayo yameonekana kwako.” (2 Mambo ya Nyakati 19:2, 3) Yehova alitambua kwamba kosa moja halikumfanya Yehoshafati awe msaliti. Vivyo hivyo, hatutapoteza marafiki tukiepuka kukasirika kupita kiasi wanapotukosea. Huenda marafiki wanaotuvunja moyo bado wana sifa nzuri.—Wakolosai 3:13.

Tunaweza kuwa na maoni ya kwamba ili tufanikiwe, ni lazima tuvunjwe moyo mara kwa mara. Huenda tukajilaumu tunapotenda dhambi. Hata hivyo, tunaweza kurudia hali yetu tukichukua hatua inayofaa na kusonga mbele. Mfalme Daudi alipojuta sana kwa sababu ya mambo aliyofanya, aliandika hivi: “Mifupa yangu ilichakaa kwa sababu ya kuugua kwangu mchana kutwa. . . . Mwishowe niliungama dhambi yangu kwako [Yehova] . . . , nawe mwenyewe ukanisamehe kosa la dhambi zangu.” (Zaburi 32:3-5) Tukitambua kwamba hatujatimiza matakwa ya Mungu, tunapaswa kumwomba msamaha na kufanya mabadiliko na kuazimia kufuata mashauri yake kwa ukaribu zaidi wakati ujao.—1 Yohana 2:1, 2.

Jitayarishe Sasa kwa Ajili ya Hali Zenye Kuvunja Moyo

Hakuna shaka kwamba sisi sote tutavunjika moyo kwa njia moja au nyingine. Tunaweza kufanya nini ili tujitayarishe kwa ajili ya hali hiyo? Bruno, Mkristo mmoja mwenye umri mkubwa ambaye alivunjwa moyo na mabadiliko fulani yaliyotokea maishani mwake, anatoa maelezo haya mazuri. Anasema: “Jambo kuu lililonisaidia kushughulikia hali ya kuvunjika moyo ni kwamba niliendelea kujijenga kiroho. Nilikuwa nimejifunza kwa nini Mungu anaruhusu ulimwengu huu mkatili uendelee. Nilisitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kwa miaka mingi. Ninafurahi kwamba nilifanya hivyo. Kujua kwamba alikuwa pamoja nami kulinisaidia kuvumilia niliposhuka moyo.”

Tunapotafakari kuhusu wakati ujao, tunaweza kuwa na hakika kuhusu jambo hili: Ingawa tunaweza kujivunja moyo au kuvunjwa moyo na wengine, Mungu hatatuvunja moyo kamwe. Kwa hakika, Mungu alisema kwamba jina lake, Yehova, linamaanisha “nitakuwa kile nitakachokuwa.” (Kutoka 3:14) Hilo linatupa uhakika wa kwamba atakuwa chochote kinachohitajiwa ili kutimiza ahadi zake. Ameahidi kwamba kupitia Ufalme wake, mapenzi yake yatatendeka “duniani kama ilivyo mbinguni.” Ndiyo sababu mtume Paulo aliandika hivi: “Nimesadiki kwamba wala kifo wala uzima wala malaika wala serikali . . . wala uumbaji mwingine wowote havitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu.”—Mathayo 6:10; Waroma 8:38, 39.

Tunaweza kuwa na hakika kwamba ahadi hii ya Mungu iliyotolewa kupitia nabii Isaya itatimia: “Tazama, mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya; na mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.” (Isaya 65:17) Inatia moyo kama nini kujua kwamba wakati unakuja ambapo hatutakumbuka tena mambo yote ya zamani yenye kuvunja moyo!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Majina fulani yamebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Hatupaswi kuona kwamba hatufai tusipofanikiwa mwanzoni

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Neno la Mungu linatutia moyo tukazie fikira mambo tunayoweza kufanya badala ya yale ambayo yangetokea

[Picha katika ukurasa wa 15]

Hata ingawa wanadamu wanakosea, Mungu ana furaha kwa sababu kusudi lake litatimia hakika

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kutanguliza mambo ya kiroho kutatusaidia kuvumilia hali zenye kuvunja moyo