Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walioshambuliwa Watetewa

Walioshambuliwa Watetewa

Walioshambuliwa Watetewa

MNAMO Mei 3, 2007, (3/5/2007) Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu huko Strasbourg, Ufaransa, ilifanya uamuzi bila kupingwa ambao uliunga mkono Mashahidi wa Yehova katika Jamhuri ya Georgia. Mahakama hiyo ilithibitisha kwamba Mashahidi katika nchi hiyo walikuwa wametendewa kinyama na kwamba haki yao ya kuabudu kwa uhuru ilikuwa imeingiliwa. Pia, Mahakama hiyo ilishutumu serikali ya zamani ya Georgia kwa kutochukua hatua ya kuwashtaki waliofanya uhalifu huo. Kwa nini mahakama hiyo ilifikia uamuzi huo?

Mnamo Oktoba 17, 1999 (17/10/1999), washiriki 120 hivi wa Kutaniko la Gldani la Mashahidi wa Yehova katika mji mkuu, Tbilisi, walikutana kwa amani ili kuabudu. Kwa ghafula, mkutano huo ulikatizwa na umati ambao uliongozwa na Vasili Mkalavishvili, ambaye aliachishwa ukasisi katika kanisa la Othodoksi. Umati huo, ambao ulibeba marungu na misalaba ya chuma, uliwashambulia vikali wahudhuriaji, na wengine wakaumizwa sana. Mwanamke mmoja aliumizwa sana jicho hivi kwamba haliwezi kupona. Watu 16 hivi walihitaji matibabu. Mashahidi fulani walipoenda kuomba msaada kwenye kituo cha polisi, walimkuta ofisa mkuu wa polisi, naye akawaambia kwamba ikiwa yeye ndiye angeongoza mashambulizi hayo basi wangeona cha mtema kuni! Mmoja wa watu waliokuwa katika umati huo alirekodi tukio lote kwenye video, na baadaye vituo vya televisheni vya kitaifa vilionyesha tukio hilo, na washambulizi walionekana waziwazi. *

Mashahidi walioshambuliwa waliwashtaki washambulizi, lakini hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa. Mpelelezi mmoja wa polisi aliyeagizwa kufanya uchunguzi alisema kwamba yeye ni muumini wa kanisa la Othodoksi, hivyo angeonyesha upendeleo katika kesi hiyo. Kwa kuwa wenye mamlaka hawakuchukua hatua, watu hao wenye msimamo mkali wa kidini waliazimia hata zaidi kutekeleza mashambulizi mengine kama hayo zaidi ya mia moja.

Basi, Juni 29, 2001 (29/6/2001), Mashahidi wa Yehova walipeleka kesi hiyo kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu. * Mahakama hiyo ilipokuwa ikitoa uamuzi wake wa mwisho Mei 3, 2007, ilieleza waziwazi kuhusu mashambulizi hayo na kuwashutumu maofisa wa serikali kwa sababu ya kutochukua hatua yoyote. Mahakama hiyo ilisema hivi: “Wenye mamlaka . . . walipaswa kuchukua hatua haraka ili kuhakikisha ukweli” kuhusu mashambulizi hayo. Kisha ikaongeza: “Kwa kuwa wenye mamlaka waliachilia matendo hayo, hilo linafanya raia watilie shaka ikiwa kuna haki na ikiwa serikali inaweza kutetea sheria zilizopo.”

Mahakama hiyo ilimalizia kwa kusema: “Kwa kuwa mashambulizi yaliyofanywa Oktoba 17, 1999 juu ya waliofikisha mashtaka ndiyo mashambulizi ya kwanza makubwa juu ya Mashahidi wa Yehova, tendo la wenye mamlaka la kupuuza jambo hilo lilifanya washambulizi hao wawe na ujasiri wa kutekeleza tena matendo kama hayo ya jeuri juu ya dini katika maeneo yote ya Georgia.”

Hivyo, wale walioshambuliwa vikali walitetewa, na serikali ya Georgia iliagizwa kulipa Kutaniko la Gldani gharama za kesi na hasara zozote zilizosababishwa. Ingawa Mashahidi wa Yehova nchini Georgia wanafurahi kwamba jeuri na ukatili vimepungua sana, kinachowafurahisha zaidi ni kwamba uamuzi wa Mahakama unatetea haki yao ya kukutana kwa amani ili kuabudu. Kwa sababu hiyo, wanamshukuru sana Baba yao wa mbinguni, Yehova Mungu, ambaye amekuwa akiwaongoza na kuwalinda katika kipindi hicho chote cha majaribu.—Zaburi 23:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Unaweza kupata habari zaidi katika gazeti la Amkeni! la Januari 22, 2002 (22/1/2002), ukurasa wa 18-24, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 5 Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu ni shirika la Baraza la Ulaya ambalo linatoa maamuzi kunapokuwa na mashtaka kuhusu uvunjaji wa Mkataba wa Ulaya wa Kulinda Haki za Kibinadamu na Haki za Msingi. Georgia ilitia sahihi mkataba huo Mei 20, 1999, na hivyo ikakubali kuunga mkono matakwa yake.