Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wokovu Unahitajiwa!

Wokovu Unahitajiwa!

Wokovu Unahitajiwa!

KWA ghafula, maji mengi sana yalifurika katika mgodi mmoja wa makaa ya mawe karibu na Pittsburgh, Pennsylvania, Marekani. Wachimba-migodi tisa walikwama mita 73 chini ya ardhi katika sehemu ndogo yenye hewa. Siku tatu baadaye, walitoka ndani ya mgodi huo wakiwa salama salimini. Waliokolewa jinsi gani?

Wakitumia ramani za mgodi huo na Mfumo wa Kupokea Habari Kutoka kwa Setilaiti, waokoaji walichimba shimo lenye upana wa sentimita 65 na kuwateremshia kifaa cha kuwaokolea. Wachimba-migodi hao waliokolewa mmoja baada ya mwingine kutoka katika mgodi huo ambao ungekuwa kaburi lao. Wote walifurahi na kushukuru sana baada ya kuokolewa.

Wengi wetu hatutakwama kamwe chini ya ardhi au kuchungulia kaburi kama wachimba-migodi hao tisa. Hata hivyo, sote tunahitaji kuokolewa, kwa kuwa hatuwezi kuepuka magonjwa, uzee, na mwishowe kifo. Mzee mwaminifu Ayubu alisema hivi: “Mwanadamu, aliyezaliwa na mwanamke, ana maisha mafupi na yenye kujaa msukosuko. Amechanuka kama ua na kukatiliwa mbali, naye hukimbia kama kivuli wala haendelei kuwako.” (Ayubu 14:1, 2) Leo, baada ya miaka 3,500 hivi kupita, maneno hayo bado ni ya kweli, kwa kuwa ni nani kati yetu anayeweza kuepuka kifo? Hata iwe tunaishi wapi au tuwe tunatunza afya yetu kadiri gani, tunahitaji kuokolewa kutoka katika minyororo ya mateso, uzee, na kifo.

Wanasayansi na watu wengine wanajitahidi sana kurefusha maisha kupita kiwango ambacho watu leo wanaona kuwa cha kawaida. Shirika moja linasema kwamba kusudi lake ni “kushinda tatizo la kifo cha mapema” na “kuwasaidia washiriki wake wafaulu kupata njia ya kuuzuia mwili wa mwanadamu usife.” Hata hivyo, kufikia sasa maendeleo ya kisayansi pamoja na tamaa ya kurefusha maisha ya wanadamu hayajawawezesha kupita miaka 70 au 80 ambayo Musa alitaja miaka 3,500 iliyopita.—Zaburi 90:10.

Iwe unakubali au hukubali maoni ya Ayubu kuhusu maisha na kifo, huwezi kuepuka uhakika wa kwamba miaka inaposonga, wewe pia ‘utakimbia kama kivuli,’ mbali sana kutoka kwa marafiki wako, familia yako, nyumbani kwenu, na kuacha vitu vyote ulivyotimiza—utakapokufa. Mfalme Sulemani mwenye hekima wa Israeli la kale aliandika hivi: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe, wala hawana malipo tena, kwa maana kumbukumbu lao limesahauliwa.”—Mhubiri 9:5.

Kama Biblia inavyoonyesha jambo la kuhuzunisha ni kwamba kifo ‘kimetawala kama mfalme,’ mfalme mkatili juu ya wanadamu. Ndiyo, kifo ndiye adui wa mwisho ambaye wanadamu wanahitaji kuokolewa kutoka kwake. (Waroma 5:14; 1 Wakorintho 15:26) Wafanyakazi waliozoezwa vizuri zaidi kukabiliana na hali ya hatari na vifaa bora zaidi ulimwenguni haviwezi kukuzuia usife. Lakini, Muumba wa wanadamu, Yehova Mungu, amefanya mpango wa kutuokoa.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

Photo by Gene J. Puskar-Pool/Getty Images