Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yule Anayerudisha Uhai

Yule Anayerudisha Uhai

Mkaribie Mungu

Yule Anayerudisha Uhai

Luka 7:11-15

JE, UMEWAHI kufiwa na mpendwa wako? Ikiwa ndivyo, basi umepitia wakati wenye huzuni zaidi maishani. Muumba wetu anaelewa huzuni yako. Zaidi ya hayo, Mungu anaweza kuondoa madhara ya kifo. Katika Biblia, ametupa habari kuhusu watu waliofufuliwa zamani ili kuonyesha kwamba Yeye si Mpaji wa uhai tu, bali pia ni Mrudishaji wa uhai. Acheni tuchunguze ufufuo mmoja ambao alimwezesha Mwana wake, Yesu Kristo, kufanya. Andiko la Luka 7:11-15 linasimulia muujiza huo.

Ulikuwa mwaka wa 31 W.K. Yesu alifunga safari ya kwenda Naini, jiji la Galilaya. (Mstari wa 11) Inaelekea ilikuwa ikikaribia jioni alipofika kwenye mipaka ya jiji hilo. Biblia inasema hivi: “Alipokaribia lango la jiji, kumbe! tazama! kulikuwa na mfu akiwa anapelekwa nje, mwana mzaliwa-pekee wa mama yake. Mbali na hilo, alikuwa ni mjane. Pia umati mkubwa kutoka jijini ulikuwa pamoja naye.” (Mstari wa 12) Je, unaweza kuwazia huzuni ya mama huyo mjane? Baada ya kufiwa na mwana wake wa pekee, hakuwa na mtu yeyote wa kumtunza na kumlinda.

Yesu alimkazia fikira mama huyo mwenye huzuni, ambaye inaelekea alikuwa akitembea kando ya sanduku lililokuwa na mwili wa mwana wake aliyekufa. Simulizi hilo linasema hivi: “Bwana alipomwona akamsikitikia, akamwambia: ‘Acha kulia.’” (Mstari wa 13) Yesu alisikitishwa sana na hali za mjane huyo. Labda alikuwa akimfikiria mama yake mwenyewe, ambaye inaelekea wakati huo alikuwa mjane, na ambaye angehuzunika pia kwa ajili yake.

Yesu alikaribia, lakini hakuwa na nia ya kujiunga na msafara huo. Lakini kwa ishara yenye mamlaka ‘aligusa sanduku’ na hivyo kuufanya umati huo usimame. Kisha, kwa sauti ya mtu aliyepewa uwezo juu ya kifo, alisema: “‘Kijana, ninakuambia, Inuka!’ Na huyo mfu akaketi na kuanza kusema, naye akamkabidhi kwa mama yake.” (Mstari wa 14 na 15) Alipokufa, kijana huyo hakuwa tena mwana wa mama yake. Hivyo, Yesu ‘alipomkabidhi kwa mama yake,’ waliunganishwa tena na kuwa familia. Bila shaka, badala ya kuhuzunika, mjane huyo alitokwa na machozi akiwa na shangwe kubwa.

Je, unatamani sana kupata shangwe kama hiyo kwa kuunganishwa tena na mpendwa wako aliyekufa? Uwe na hakika kwamba Mungu anajua huzuni yako. Huruma ya Yesu kuelekea mjane huyo mwenye huzuni ilionyesha huruma ya Mungu mwenyewe, kwa kuwa Yesu aliiga utu wa Baba yake kikamilifu. (Yohana 14:9) Biblia inatufundisha kwamba Mungu anatamani sana kuwafufua wafu walio katika kumbukumbu yake. (Ayubu 14:14, 15) Neno lake, Biblia, linatupa tumaini zuri ajabu, yaani, tarajio la kuishi katika paradiso duniani na kuwaona wapendwa wetu wakifufuliwa. (Luka 23:43; Yohana 5:28, 29) Kwa nini usijifunze mengi zaidi kuhusu yule Anayerudisha uhai na jinsi unavyoweza kuwa na tumaini hilo?

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Huyo mfu akaketi na kuanza kusema, naye akamkabidhi kwa mama yake”