Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

How Jesus’ Death Can Save You

How Jesus’ Death Can Save You

KARIBU miaka 2,000 iliyopita, wakati wa Pasaka ya Kiyahudi mwaka wa 33 W.K., mtu fulani asiye na hatia alikufa ili wengine waishi. Ni mtu gani huyo? Ni Yesu wa Nazareti. Ni nani wanaoweza kufaidika kutokana na tendo hilo zuri? Ni wanadamu wote. Andiko la Biblia ambalo linajulikana sana linaeleza kwa ufupi kuhusu dhabihu hiyo inayookoa uhai: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16, Union Version.

Ingawa watu wengi wanafahamu andiko hilo, ni wachache wanaoelewa maana yake. Wanajiuliza hivi: ‘Kwa nini tunahitaji dhabihu ya Kristo? Kifo cha mtu mmoja kinaweza kuwaokoa wanadamu namna gani kutokana na kifo cha milele?’ Biblia inajibu maswali hayo kwa njia iliyo wazi na yenye kuridhisha.

Jinsi Kifo Kilivyoanza Kuwatawala Wanadamu

Watu fulani wanaamini kwamba wanadamu waliumbwa waishi kwa muda mfupi tu duniani, wateseke, wafurahi kwa kadiri fulani, kisha wafe na kwenda mahali pazuri zaidi. Kulingana na maoni hayo, kifo ni sehemu ya kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba wanadamu wanakufa kwa sababu tofauti na hiyo. Inasema: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Mstari huo unaonyesha kwamba watu wanakufa kwa sababu ya dhambi. Lakini ni nani huyo “mtu mmoja” ambaye aliwaletea wanadamu madhara hayo mabaya ya dhambi?

Kitabu kimoja (The World Book Encyclopedia) kinasema kuwa wanasayansi wengi wanaamini kwamba wanadamu wote wametokana na chanzo kimoja, na Biblia inaonyesha waziwazi kuwa chanzo hicho ni yule “mtu mmoja.” Tunasoma hivi katika Mwanzo 1:27: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.” Hivyo, Biblia inasema kwamba wanadamu wawili wa kwanza walikuwa kazi bora zaidi ya uumbaji wa Mungu Mweza-Yote.

Masimulizi ya kitabu cha Mwanzo yanaeleza mengi zaidi kuhusu maisha ya wanadamu baada ya Yehova Mungu kumuumba mwanadamu wa kwanza. Kwa kweli, katika masimulizi hayo yote, Mungu hakutaja kifo isipokuwa tu alipozungumzia matokeo ya kutotii. (Mwanzo 2:16, 17) Alitaka wanadamu waishi katika paradiso maridadi duniani, wakiwa na furaha na afya nzuri milele. Hakutaka wazeeke, wateseke, kisha wafe. Basi, kifo kilianza kuwatawala wanadamu jinsi gani?

Andiko la Mwanzo sura ya 3 linaeleza jinsi wanadamu wawili wa kwanza walivyoamua kimakusudi kutomtii Mpaji-Uhai wao, Yehova Mungu. Kwa hivyo, Mungu alitekeleza hukumu ambayo alikuwa amewajulisha mapema. Alimwambia hivi huyo mwanamume: “Wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” (Mwanzo 3:19) Mwishowe, wanadamu hao wawili waliokosa kutii walikufa kama Mungu alivyosema.

Hata hivyo, madhara hayo hayakuwapata wanadamu hao wawili wa kwanza peke yao, yaliwapata wengine pia. Kutotii kwao kuliwafanya wazao wao wapoteze tumaini la kufurahia maisha makamilifu. Yehova aliwatia ndani ya kusudi lake wanadamu hao ambao hawakuwa wamezaliwa alipowaambia Adamu na Hawa hivi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.” (Mwanzo 1:28) Baada ya muda, familia ya wanadamu ingejaa duniani na kuwa na maisha yenye furaha kabisa bila kifo. Lakini babu yao Adamu, yule “mtu mmoja,” aliwauza kuwa watumwa wa dhambi ambao walitazamia tu kifo. Mtume Paulo, mzao wa mwanadamu wa kwanza, aliandika hivi: “Mimi ni wa kimwili, nimeuzwa chini ya dhambi.”—Waroma 7:14.

Kama vile ambavyo watu fulani wameharibu michongo au picha zenye thamani hivi karibuni, ndivyo Adamu alivyoharibu uumbaji mzuri ajabu wa Mungu—wanadamu—alipotenda dhambi. Watoto wa Adamu walipata watoto, kisha wajukuu, nao wakaendelea kuzaana. Vizazi vilizaliwa, vikakua, vikazaa watoto, kisha vikafa. Kwa nini wote wamekufa? Kwa sababu wote wametoka kwa Adamu. Biblia inasema hivi: “Kwa kosa la mtu mmoja wengi walikufa.” (Waroma 5:15) Magonjwa, uzee, mwelekeo wa kukosea, na kifo ni matokeo yenye kuhuzunisha ya hatua ya Adamu ya kuisaliti familia yake mwenyewe. Sisi sote ni washiriki wa familia hiyo.

Katika barua yake kwa Wakristo huko Roma, mtume Paulo aliandika kuhusu hali yenye kusikitisha ya wanadamu wasio wakamilifu, kutia ndani yeye, na jinsi wanavyopambana na matokeo ya dhambi. Alisema hivi: “Maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?” Hilo ni swali zuri, sivyo? Ni nani ambaye angemwokoa Paulo pamoja na wengine wote wanaotamani kuokolewa kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo? Paulo mwenyewe alijibu swali hilo: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Waroma 7:14-25) Ndiyo, Muumba wetu amefanya mpango wa kutuokoa kupitia Mwana wake, Yesu Kristo.

Daraka la Yesu Katika Mpango wa Mungu wa Kuwaokoa Wanadamu

Yesu alieleza daraka lake katika kuwaokoa wanadamu kutoka katika utumwa mbaya sana wa dhambi. Alisema hivi: “Mwana wa binadamu alikuja . . . kutoa uhai wake kuwa fidia kwa ajili ya wengi.” (Mathayo 20:28, King James Version) Uhai wa Yesu ni fidia au malipo ya ukombozi kwa njia gani? Kifo chake kinatuletea faida gani?

Yesu alitoa uhai wake ili kuondoa matokeo ya dhambi ya Adamu

Biblia inasema kwamba Yesu ‘hakuwa na dhambi’ na ‘alitengwa kutoka kwa watenda-dhambi.’ Katika maisha yake yote, Yesu alitii Sheria ya Mungu kwa ukamili. (Waebrania 4:15; 7:26) Kwa hiyo, Yesu hakufa kwa sababu ya dhambi na kutotii kama Adamu. (Ezekieli 18:4) Badala yake, Yesu alikubali kifo ambacho hakustahili ili atimize mapenzi ya Baba yake ya kuwaokoa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo. Kama ilivyotajwa mwanzoni, Yesu alikubali kuja “kutoa uhai wake kuwa fidia.” Akichochewa na upendo usio na kifani, Yesu alikubali ‘kuonja kifo kwa ajili ya kila mwanadamu.’—Waebrania 2:9.

Uhai ambao Yesu alidhabihu ulilingana kabisa na uhai ambao Adamu alipoteza alipotenda dhambi. Kifo cha Yesu kilikuwa na matokeo gani? Yehova alikubali dhabihu hiyo kuwa “fidia inayolingana kwa ajili ya wote.” (1 Timotheo 2:6) Hivyo, Mungu alitumia thamani ya uhai wa Yesu kuwanunua, au kuwakomboa wanadamu kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo.

Biblia inataja tena na tena tendo hilo kubwa la upendo la Muumba wa wanadamu. Paulo aliwakumbusha Wakristo kwamba ‘walinunuliwa kwa bei.’ (1 Wakorintho 6:20; 7:23) Petro aliandika kwamba Mungu hakutumia dhahabu wala fedha kuwakomboa Wakristo kutoka katika maisha yao yanayoongoza kwenye kifo, bali alitumia damu ya Mwana wake. (1 Petro 1:18, 19) Kupitia dhabihu ya fidia ya Kristo, Yehova alifanya mpango wa kuwaokoa wanadamu ili wasipate kifo cha milele.

Je, Utafaidika Kutokana na Fidia ya Kristo?

Mtume Yohana aliandika hivi kuhusu faida kubwa za fidia ya Kristo: “[Yesu Kristo] ni dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu, lakini si kwa ajili ya zetu tu bali pia kwa ajili ya zile za ulimwengu wote.” (1 Yohana 2:2) Ndiyo, fidia ya Kristo inaweza kuwaletea wanadamu wote faida. Je, hilo linamaanisha kwamba kila mtu atafaidika kutokana na uandalizi huo wenye thamani bila kufanya jitihada yoyote? Hapana. Kumbuka kazi ya uokoaji iliyozungumziwa katika habari iliyotangulia. Watu waliokuwa wakiwaokoa wachimba-migodi waliokwama waliteremsha kifaa cha kuwaokolea, lakini kila mtu aliyekuwa ndani ya mgodi huo alihitaji kuingia ndani ya kifaa hicho. Vivyo hivyo, wale wanaotaka kufaidika kutokana na dhabihu ya fidia ya Kristo hawawezi kukaa kitako tu na kungoja baraka za Mungu. Wanahitaji kuchukua hatua.

Mungu anataka wachukue hatua gani? Andiko la Yohana 3:36 linatuambia hivi: “Yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele; yule asiyemtii Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu hukaa juu yake.” Mungu anataka tuwe na imani katika dhabihu ya Kristo. Lakini kuna jambo lingine analotaka tufanye. “Kwa jambo hili tunajua kwamba tumemjua [Yesu], yaani, tukiendelea kuzishika amri zake.” (1 Yohana 2:3) Basi, ni wazi kwamba ili tuokolewe kutoka katika dhambi na kifo ni lazima tuwe na imani katika fidia ya Kristo na kutii amri za Kristo.

Njia moja ya maana ya kuonyesha imani katika fidia ya Yesu ni kuonyesha kwamba tunathamini kifo chake kwa kukiadhimisha, kama alivyoamuru. Kabla hajafa, Yesu alianzisha mlo wa mfano pamoja na mitume wake waaminifu, akawaambia hivi: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Mashahidi wa Yehova wanathamini sana urafiki wao pamoja na Mwana wa Mungu, nao wanatii amri hiyo. Mwaka huu, Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo utaadhimishwa Jumamosi (Siku ya Posho), Machi 22, baada ya jua kushuka. Tunakualika kwa uchangamfu uhudhurie mkutano huo wa pekee na hivyo kutii amri ya Yesu. Mashahidi wa Yehova wa eneo lenu wanaweza kukuambia wakati na mahali pa maadhimisho hayo. Ukihudhuria Ukumbusho utajifunza mengi kuhusu yale unayohitaji kufanya ili fidia ya Kristo iweze kukuweka huru kutokana na madhara ya dhambi ya Adamu.

Ni watu wachache leo wanaothamini sana dhabihu kubwa ambayo Muumba na Mwana wake wameandaa ili kuwaokoa wasiangamie. Wale walio na imani katika dhabihu hiyo wanapata furaha ya pekee. Mtume Petro aliandika hivi kuhusu Wakristo wenzake: “Mnaonyesha imani katika [Yesu] na mnashangilia sana kwa shangwe isiyosemeka na iliyotukuzwa, huku mkipokea tokeo la mwisho la imani yenu, ule wokovu wa nafsi zenu.” (1 Petro 1:8, 9) Ukisitawisha upendo kumwelekea Yesu Kristo na kuwa na imani katika dhabihu ya fidia, unaweza kupata shangwe nyingi sasa na kutazamia kuokolewa kutoka katika dhambi na kifo.