Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Kwa nini mafuta yenye marashi ambayo Maria alitumia yalikuwa ya bei ghali sana?

Siku chache kabla ya kifo cha Yesu, Maria, dada ya Lazaro, ‘alikuja na chupa ya alabasta iliyo na mafuta yenye marashi, nardo halisi, ghali sana,’ na kuyamimina juu ya Yesu. (Marko 14:3-5; Mathayo 26:6, 7; Yohana 12:3-5) Masimulizi ya Marko na Yohana yanasema kwamba marashi hayo yalikuwa na thamani ya dinari 300—bei iliyolingana na mapato ya mwaka mzima ya mfanyakazi wa kawaida.

Marashi hayo ghali yalitoka wapi? Inasemekana kwamba nardo hiyo inayotajwa katika Biblia inatokana na mmea mdogo wenye manukato (Nardostachys jatamansi) unaopatikana katika Milima ya Himalaya. Mara nyingi nardo hiyo ya bei ya juu ilichanganywa na kiungo kingine cha bei ya chini na hata iliuzwa ikiwa nardo bandia. Hata hivyo, Marko na Yohana wanatumia maneno “nardo halisi.” Kwa kuwa mafuta hayo yenye marashi yalikuwa ghali sana, hiyo inaonyesha kwamba huenda yalitoka India.

Kwa nini simulizi la Marko linasema kwamba Maria ‘alivunja chupa ya alabasta’? Kwa kawaida, chupa ya alabasta ilikuwa na shingo nyembamba ambayo ilizibwa kabisa ili kuzuia harufu ya marashi isitoke. Katika kitabu chake (Discoveries From the Time of Jesus), Alan Millard anasema hivi: “Ni rahisi kuwazia jinsi ambavyo mwanamke huyo aliyesisimuka angevunja [shingo ya chupa hiyo] bila kuifungua taratibu, na hivyo kumimina marashi yote mara moja.” Huenda ndiyo sababu ‘nyumba hiyo ilijaa harufu ya mafuta yenye marashi.’ (Yohana 12:3) Kwa kweli, ilikuwa zawadi ya bei ghali sana, lakini ilifaa. Kwa nini? Mwanamke huyo mwenye uthamini alikuwa ametoka tu kumwona Yesu akimfufua ndugu yake mpendwa, Lazaro.—Yohana 11:32-45.

Yeriko lilikuwa jiji moja au majiji mawili?

Mathayo, Marko, na Luka wanasimulia muujiza wa kuponya uliotukia karibu na Yeriko. (Mathayo 20:29-34; Marko 10:46-52; Luka 18:35-43) Mathayo na Marko wanasema kwamba Yesu alifanya muujiza huo ‘alipokuwa akitoka’ Yeriko. Hata hivyo, Luka anasema kwamba Yesu alifanya muujiza huo “alipokuwa akikaribia” Yeriko.

Katika siku za Yesu, je, kulikuwa na jiji moja tu lililoitwa Yeriko au majiji mawili? Kitabu kimoja (Bible Then & Now) kinatoa jibu: “Kufikia nyakati za Agano Jipya, Yeriko lilikuwa limejengwa upya kilomita 1.6 hivi kusini mwa jiji la kale. Herode Mkuu alikuwa amejenga huko jumba la kifalme la majira ya baridi kali.” Jambo hilo linathibitishwa na kitabu kingine (Archaeology and Bible History), kinachosema hivi: “Yeriko la siku za Yesu lilikuwa jiji lenye sehemu mbili. . . . Jiji la kale la Kiyahudi lilikuwa kilomita 1.6 hivi kutoka kwenye jiji la Kiroma.”

Kwa hiyo, huenda Yesu alifanya muujiza huo alipokuwa akitoka jiji la Kiyahudi na kukaribia jiji la Kiroma au wakati alipokuwa akitoka jiji la Kiroma na kukaribia jiji la Kiyahudi. Bila shaka, kujua jinsi hali zilivyokuwa wakati masimulizi hayo yalipoandikwa kunatusaidia kuelewa habari hiyo inayoonekana kuwa yenye kupingana.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Chupa ya Alabasta yenye marashi

[Hisani]

© Réunion des Musées Nationaux/Art Resource, NY