Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuona Ni Kuamini

Kuona Ni Kuamini

Kuona Ni Kuamini

“Mtu anayeamini kwamba mambo ya Mungu hayawezi kujulikana anafikiri haiwezekani kujua ukweli kumhusu Mungu na maisha ya wakati ujao ambayo dini ya Ukristo na dini nyingine zinaamini. Au, ikiwa yanaweza kujulikana, basi hayawezi kujulikana wakati huu.”—MWANAFALSAFA BERTRAND RUSSELL, 1953.

MTAALAMU wa wanyama anayeitwa Thomas Huxley ndiye aliyeanzisha imani hiyo. Huxley aliyezaliwa mwaka wa 1825, na ambaye aliunga mkono fundisho la mageuzi, aliishi wakati mmoja na Charles Darwin. Mwaka wa 1863, Huxley aliandika kwamba hakuona uthibitisho wa kwamba kuna Mungu “anayetupenda na kutujali kama Wakristo wanavyodai.”

Leo, huenda watu wengi wakakubaliana na maoni ya watu hao maarufu, na kusema kwamba wanaamini tu kile wanachoona. Huenda wakasema kwamba ni upumbavu kumwamini mtu au kitu fulani bila uthibitisho.

Je, Biblia inasema tunapaswa kumwamini Mungu bila uthibitisho wowote wa kuwapo kwake? Haisemi hivyo. Biblia inaonyesha kwamba ni upumbavu kuamini yale ambayo watu wanasema bila kuwa na uthibitisho wowote. Biblia inasema hivi: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Methali 14:15.

Namna gani kuhusu kumwamini Mungu? Je, kweli kuna uthibitisho wowote wa kwamba kuna Mungu, na kwamba anatupenda na kutujali?

Sifa za Mungu Zinafunuliwa

Paulo, mwandikaji wa Biblia, alipokuwa akizungumza na kikundi cha wasomi huko Athene, alisema kwamba Mungu ‘aliufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo.’ Alipokuwa akizungumza na wasikilizaji wake wasioamini, Paulo aliwaambia kwamba Mungu anapendezwa na wanadamu na kwamba, kwa kweli, “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:24-27.

Kwa nini Paulo alikuwa na uhakika kwamba kuna Mungu na kwamba anapendezwa na wanadamu ambao Aliumba? Paulo alionyesha sababu moja alipowaandikia Wakristo wenzake katika jiji la Roma. Alisema hivi kumhusu Mungu: “Sifa zake ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa.”—Waroma 1:20.

Kurasa zinazofuata zinazungumzia sifa tatu za Mungu ambazo zinaweza kuonekana waziwazi katika vitu alivyoumba. Unapochunguza mifano hiyo, jiulize hivi: ‘Ninahisi jinsi gani ninapojifunza kuhusu sifa hizi za Mungu?’

[Blabu katika ukurasa wa 3]

Biblia haisemi tunapaswa kumwamini Mungu bila uthibitisho wowote wa kuwapo kwake