Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nyota Zinafunua Nguvu za Mungu

Nyota Zinafunua Nguvu za Mungu

Nyota Zinafunua Nguvu za Mungu

“Inueni macho yenu juu, mwone. Ni nani ameviumba vitu hivi? Ni Yeye anayelileta jeshi lake kulingana na hesabu, ambaye zote anaziita kwa jina. Kutokana na wingi wa nguvu zenye msukumo, yeye pia akiwa hodari katika nguvu, hakuna hata moja kati ya hizo inayokosekana.”—ISAYA 40:26.

JUA letu ni nyota yenye ukubwa wa kadiri tu. Hata hivyo, ukubwa wake unazidi ukubwa wa dunia kwa mara 330,000. Nyota nyingi ambazo ziko karibu na dunia ni ndogo zaidi kuliko jua. Hata hivyo, nyota nyingine, kama ile inayoitwa V382 Cygni, ni kubwa angalau mara 27 kuliko jua letu.

Jua letu linatoa nishati au nguvu nyingi kadiri gani? Fikiria joto ambalo ungehisi ikiwa ungekuwa umbali wa kilomita 15 kutoka kwenye moto. Kwa wastani, jua liko umbali wa kilomita milioni 150 kutoka duniani. Hata hivyo, siku yenye jua kali, joto lake linaweza kuchoma ngozi! Inashangaza kwamba yapata sehemu moja tu ya bilioni ya nishati ya jua ndiyo inayofika duniani. Hata hivyo, sehemu hiyo ndogo ya nguvu za jua inatosha kutegemeza uhai kwenye sayari yetu.

Wanasayansi wamegundua kwamba jumla ya nishati inayotoka kwenye jua letu tu inatosha kutegemeza sayari zipatazo trilioni 31 zilizo kama dunia. Au tukihesabu nguvu hizo kwa njia nyingine: Ikiwa nguvu zote ambazo jua linatoa kwa sekunde moja tu zingekusanywa, Marekani ingepata “nishati ya kutosha, kwa ajili ya miaka 9,000,000 ijayo,” kinasema kituo kimoja cha Intaneti (cha Space Weather Prediction Center, SWPC).

Nishati ya jua inatoka kwenye kiini cha jua, yaani, ndani kabisa ya tanuru ya nyuklia ambayo inagonganisha atomi na kutokeza nguvu. Jua ni kubwa sana na kiini chake ni kizito sana hivi kwamba inachukua mamilioni ya miaka ili nishati iliyo ndani ya kiini hicho itokee nje. “Ikiwa Jua lingeacha kutoa nishati leo,” kinasema kituo cha Intaneti kilichotajwa juu, “ingechukua miaka 50,000,000 ili kuhisi mabadiliko makubwa duniani!”

Sasa fikiria uhakika huu: Unapoinua macho yako juu usiku usiokuwa na mawingu, unaweza kuona maelfu ya nyota, kila moja ikitoa nishati nyingi sana, kama jua letu. Wanasayansi wanakadiria kwamba kuna mabilioni na mabilioni ya nyota katika ulimwengu wote!

Nyota zote hizo zilitoka wapi? Watafiti wengi sasa wanaamini kwamba kwa sababu ambazo hawajaelewa, ulimwengu wote ulitokea ghafula miaka bilioni 14 hivi iliyopita. Biblia inasema hivi kwa ufupi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Bila shaka, inaweza kusemwa kwamba Yule ambaye aliumba mashini hizo kubwa za nishati ambazo tunaita nyota ni “hodari katika nguvu.”—Isaya 40:26.

Jinsi Mungu Anavyotumia Nguvu Zake

Yehova Mungu anatumia nguvu zake kuwategemeza wale wanaofanya mapenzi yake. Kwa mfano, mtume Paulo alitumia nguvu zake ili kuwafundisha wengine kumhusu Mungu. Paulo hakuwa malaika, lakini alitimiza kazi nyingi nzuri ingawa alikabili upinzani mkali. Jinsi gani? Alikiri kwamba alipokea “nguvu zinazopita zile za kawaida” kutoka kwa Mungu.—2 Wakorintho 4:7-9.

Pia, Yehova Mungu ametumia nguvu zake kuwaharibu wale wanaovunja kimakusudi viwango vyake vya maadili. Yesu Kristo alizungumza kuhusu uharibifu wa Sodoma na Gomora na Gharika ya siku za Noa kuwa mifano ya jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake ili kuwaharibu waovu tu. Yesu alitabiri kwamba hivi karibuni Yehova atatumia tena nguvu zake kuwaharibu wale wanaopuuza viwango Vyake.—Mathayo 24:3, 37-39; Luka 17:26-30.

Unahisi Jinsi Gani?

Baada ya kutafakari juu ya nguvu za Mungu zinazoonekana wazi katika nyota, huenda ukahisi kama Mfalme Daudi aliyesema hivi: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba umweke akilini, na mwana wa mtu wa udongo hivi kwamba umtunze?”—Zaburi 8:3, 4.

Ndiyo, ni jambo linalonyenyekeza kutambua jinsi tulivyo wadogo tunapolinganishwa na ukubwa wa ulimwengu. Hata hivyo, hatuhitaji kuogopa nguvu za Mungu. Yehova alimwongoza nabii Isaya kuandika maneno haya yenye kufariji: “Yeye [Mungu] anampa nguvu mtu aliyechoka; naye huzijaza nguvu kamili kwa mtu asiye na nguvu zenye msukumo. Wavulana watachoka na pia kuzimia, na vijana hakika watajikwaa, lakini wale wanaomtumaini Yehova watapata nguvu mpya. Wataruka juu kwa mabawa kama tai. Watakimbia wala hawatazimia; watatembea wala hawatachoka.”—Isaya 40:29-31.

Ikiwa unatamani kufanya mapenzi ya Mungu, unaweza kuwa na hakika kwamba atakupa roho yake takatifu ili ikutegemeze. Lakini unapaswa kumwomba Mungu akupe roho hiyo. (Luka 11:13) Kwa msaada wa Mungu, unaweza kuvumilia jaribu lolote na kupata nguvu za kutenda mambo yaliyo sawa.—Wafilipi 4:13.

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Kwa msaada wa Mungu, unaweza kupata nguvu za kutenda mambo yaliyo sawa

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kuanzia kushoto juu na kuzunguka kulia: Galaksi ya Whirlpool, kikundi cha nyota kinachoitwa Pleiades, Orion Nebula, galaksi ya Andromeda

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ukubwa wa jua unazidi ukubwa wa dunia kwa mara 330,000

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 7]

Pleiades: NASA, ESA and AURA/Caltech; all others above: National Optical Astronomy Observatories