Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafundishe Watoto Wako

Alitaka Kusaidia

Alitaka Kusaidia

JE, UMEWAHI kumwona mtu fulani aliye mgonjwa sana?— Je, ulitamani kumsaidia?— Namna gani ikiwa alikuwa wa taifa au dini nyingine? Je, bado ungetaka kumsaidia apone?— Msichana mdogo aliyeishi katika nchi ya Israeli miaka 3,000 hivi iliyopita alifanya hivyo. Acha tuzungumzie yaliyotukia.

Msichana huyo anaishi Israeli. Mara nyingi kumekuwa na vita kati ya nchi hiyo na nchi jirani ya Siria. (1 Wafalme 22:1) Siku moja Wasiria wanakuja na kumteka nyara msichana huyo mdogo. Anapelekwa Siria, ambako anakuwa kijakazi wa mkewe Naamani, mkuu wa Jeshi la Siria. Naamani ana ugonjwa mbaya sana unaoitwa ukoma. Ugonjwa huo unaweza kufanya nyama ya mwili wa mtu ikatike-katike.

Kijakazi huyo anamwambia mkewe Naamani jinsi mume wake anavyoweza kuponywa. Anasema hivi: ‘Ikiwa Naamani angekuwa Samaria, Elisha nabii wa Yehova angemponya ukoma wake.’ Kijakazi huyo anazungumza kumhusu Elisha kwa njia inayomfanya Naamani aamini kwamba kwa kweli nabii huyo anaweza kumponya. Hivyo, akiwa na ruhusa ya Ben-hadadi, mfalme wa Siria, Naamani na watumishi wake wanafunga safari ndefu ya kilomita 150 hivi kumtafuta Elisha.

Kwanza, wanamwendea Yehoramu, mfalme wa Israeli. Wanamwonyesha barua ya Mfalme Ben-hadadi ya kuomba msaada kwa ajili ya Naamani. Lakini Yehoramu hamwamini Yehova wala nabii Elisha. Yehoramu anafikiri kwamba Ben-hadadi anajaribu kuanzisha vita naye. Elisha anaposikia jambo hilo, anamwambia Mfalme Yehoramu: “Tafadhali, mwache aje kwangu.” Elisha anataka kuonyesha kwamba Mungu ana nguvu za kumponya Naamani ugonjwa wake mbaya.—2 Wafalme 5:1-8.

Naamani anapofika nyumbani kwa Elisha akiwa na farasi na magari ya kukokotwa, Elisha anamtuma mjumbe akamwambie hivi: ‘Unapaswa kuoga mara saba katika Mto Yordani, nawe utaponywa.’ Naamani anakasirika. Alitazamia kwamba Elisha angekuja nje na kutikisa mkono wake huku na huku juu ya mahali penye ukoma na kupaponya. Badala yake, anamwona mjumbe tu! Hivyo, Naamani anageuka kwa ghadhabu na kuanza kurudi nyumbani.—2 Wafalme 5:9-12.

Ungefanya nini ikiwa ungekuwa mmoja wa watumishi wa Naamani?— Watumishi wake wanamuuliza hivi: ‘Ikiwa Elisha angekwambia ufanye jambo gumu, je, hungefanya? Hivyo, kwa nini usifanye jambo hili rahisi—kuoga tu na kuwa safi?’ Naamani anawasikiliza. ‘Anashuka na kuanza kujitumbukiza katika Yordani mara saba kisha nyama yake inakuwa kama nyama ya mvulana mdogo.’

Naamani anarudi kwa Elisha na kusema: “Tazama, sasa, hakika ninajua kwamba hakuna Mungu yeyote mahali pengine popote duniani isipokuwa katika Israeli.” Anamwahidi Elisha kwamba “hatatoa tena toleo la kuteketezwa wala dhabihu kwa miungu mingine yoyote isipokuwa kwa Yehova.”—2 Wafalme 5:13-17.

Je, ungependa kumsaidia mtu fulani kujifunza kumhusu Yehova na kuhusu yale anayoweza kufanya, kama msichana huyo mdogo alivyofanya?— Yesu alipokuwa duniani, mtu fulani aliyekuwa na ukoma alimwamini na kusema: ‘Kwa kweli ikiwa unataka, unaweza kunisaidia.’ Je, unajua jinsi Yesu alivyomjibu?— “Nataka.” Na Yesu akamponya, kama tu Yehova alivyomponya Naamani.—Mathayo 8:2, 3.

Je, unajua kwamba Yehova ataumba ulimwengu mpya ambamo watu wote watakuwa na afya na wataweza kuishi milele?— (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Ikiwa ndivyo, hapana shaka kwamba ungetaka kuwajulisha wengine mambo hayo mazuri ajabu!