Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Njia Fulani Hususa Tunayopaswa Kumtumikia Mungu?

Je, Kuna Njia Fulani Hususa Tunayopaswa Kumtumikia Mungu?

Je, Kuna Njia Fulani Hususa Tunayopaswa Kumtumikia Mungu?

“DINI ni sehemu muhimu sana ya asili ya mwanadamu.” Ndivyo anavyosema Profesa Alister Hardy katika kitabu chake (The Spiritual Nature of Man). Matokeo ya uchunguzi wa karibuni yanaelekea kuunga mkono maoni hayo. Uchunguzi huo ulionyesha kwamba asilimia 86 hivi ya idadi ya watu ulimwenguni wanadai kushirikiana na dini fulani.

Pia uchunguzi huo ulionyesha kwamba waumini hao wanatoka katika dini 19 kuu na kwa kushangaza wale wanaodai kuwa Wakristo ni wa dini 37,000 tofauti-tofauti. Je, hilo halikufanyi ujiulize ikiwa Mungu anakubali njia hizo zote tofauti za kumwabudu? Kwa kweli, je, ni muhimu kufikiria njia tunayotumia kumwabudu?

Kuhusu jambo hili muhimu, inapatana na akili kwamba hatuwezi kutegemea hisia au maoni ya kibinafsi. Kwa wazi, tunahitaji kuchunguza Mungu ana maoni gani kuhusu jambo hilo. Ili kujua maoni yake tunapaswa kuchunguza Neno la Mungu, Biblia. Kwa nini? Kwa sababu Yesu Kristo alisali hivi kwa Mungu: “Neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Na mtume mwaminifu Paulo alisema hivi: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.”—2 Timotheo 3:16.

Biblia inaonyesha kwamba Mungu hakubali ibada ya aina zote. Tunaweza kupata mifano ya kihistoria ya aina ya ibada iliyokubaliwa na Mungu na ile ambayo hakukubali. Kwa kuchunguza kwa uangalifu mifano kama hiyo, tunaweza kujifunza kile tunachopaswa kufanya na kile tusichopaswa kufanya ili ibada yetu impendeze Mungu.

Mfano wa Zamani

Kupitia kwa nabii Musa, Yehova Mungu aliwapa Waisraeli sheria ambazo ziliwaonyesha jinsi ya kumwabudu Mungu kwa njia inayofaa. Watu walipotii kile kilichosemwa na sheria hizo, zinazojulikana kama Sheria ya Musa, walikubaliwa na Mungu kuwa watu wake naye akawabariki. (Kutoka 19:5, 6) Hata hivyo, ingawa Mungu alikubali taifa la Israeli, taifa hilo halikushikamana na ibada ambayo ilimpendeza. Tena na tena, walimpa Yehova kisogo na kufuata mazoea ya kidini ya watu katika mataifa yaliyowazunguka.

Katika karne ya saba K.W.K., siku za manabii Ezekieli na Yeremia, Waisraeli wengi walipuuza Sheria ya Mungu na kusitawisha uhusiano wa karibu na watu wa mataifa yaliyowazunguka. Kwa kufuata desturi zao na kushiriki katika sherehe zao, Waisraeli walichanganya dini. Waisraeli wengi walikuwa wakisema: “Na tuwe kama mataifa, kama familia za nchi mbalimbali, katika kuhudumia miti na mawe.” (Ezekieli 20:32; Yeremia 2:28) Walidai kwamba wanamtumikia Yehova Mungu, lakini wakati huohuo, walitukuza “sanamu zao za mavi,” na hata wakawatoa watoto wao dhabihu kwa sanamu hizo.—Ezekieli 23:37-39; Yeremia 19:3-5.

Wachimbuaji wa vitu vya kale wanasema kwamba aina hii ya ibada ni ile ambayo watu wanachanganya ibada kwa miungu mbalimbali. Au wanasema kuwa ni aina ya ibada inayopendwa na watu wengi. Leo, watu wengi wanasema kwamba kwa kuwa tunaishi katika jamii yenye watu wenye imani mbalimbali, tunapaswa kuwa na maoni yaliyopanuka katika mambo yote, kutia ndani dini. Kwa hiyo, wanahisi kwamba hakuna tatizo kumwabudu Mungu katika njia yoyote ambayo wanataka. Je, hiyo ni kweli? Je, tunapaswa tu kuvumiliana na kupanuka? Hebu ona mambo fulani yaliyofanywa katika dini ambazo Waisraeli wasio waaminifu walijihusisha nazo na uone mambo hayo yalitokeza nini.

Waisraeli Wachanganya Ibada

Vituo ambapo Waisraeli walichanganya ibada vilikuwa “mahali pa juu,” au vihekalu vilivyokuwa na madhabahu, nguzo za mawe, na miti mitakatifu, ambayo inaelekea ilikuwa mifano ya mbao ya Ashera, mungu wa kike wa uzazi wa Kanaani. Kulikuwa na vituo vingi kama hivyo huko Yuda. Andiko la 2 Wafalme 23:5, 8 linataja kuhusu “mahali pa juu katika majiji ya Yuda na ujirani wa Yerusalemu, . . . kuanzia Geba [mpaka wa kaskazini] mpaka Beer-sheba [mpaka wa kusini].”

Katika mahali pa juu, Waisraeli ‘walifukiza moshi wa dhabihu kwa Baali, kwa jua na kwa mwezi na kwa makundi-nyota ya unajimu na kwa jeshi lote la mbinguni.’ Walikuwa na nyumba kwa ajili ya “wanaume makahaba wa hekaluni . . . katika nyumba ya Yehova” na waliwatoa watoto wao kwa ‘kuwapitisha motoni kwa Moleki.’—2 Wafalme 23:4-10.

Waakiolojia wamepata sanamu nyingi za udongo huko Yerusalemu na Yuda, hasa katika magofu ya nyumba za watu binafsi. Nyingi kati ya hizo, zilionyesha wanawake wakiwa uchi na matiti yaliyofanywa kuwa makubwa. Wasomi wanasema kwamba sanamu hizo zinafanana na miungu ya kike Ashtorethi na Ashera. Sanamu hizo zinasemekana kuwa “hirizi zinazosaidia kutunga mimba na kuzaa.”

Waisraeli walikuwa na maoni gani kuhusu vituo hivyo vya kuchanganya ibada? Profesa Ephraim Stern wa Chuo Kikuu cha Hebrew, alisema kwamba nyingi kati ya mahali pa juu huenda “paliwekwa wakfu kwa Yahweh [Yehova].” Maandishi katika maeneo ya akiolojia yanaonekana kuwa yanaunga mkono wazo hilo. Kwa mfano, bamba moja linasema, “Ninakubariki kupitia Yahweh wa Samaria na kwa ashera wake,” nalo lingine linasema, “Ninakubariki kupitia Yahweh wa Teman na kwa ashera wake!”

Mifano hiyo inaonyesha jinsi Waisraeli walivyochanganya ibada safi ya Yehova Mungu na mazoea yenye kuaibisha ya kipagani. Matokeo yalikuwa kuzorota kwa maadili na giza la kiroho. Mungu alikuwa na maoni gani kuhusu aina hiyo ya kuchanganya ibada?

Mungu Alifanya Nini Kuhusu Ibada Hiyo?

Mungu alionyesha hasira yake na kushutumu ibada ya Waisraeli iliyozorota kupitia nabii wake Ezekieli, akisema: “Katika makao yenu yote majiji yataharibiwa na mahali pa juu patafanywa ukiwa, ili padumu katika uharibifu na madhabahu zenu zikae ukiwa na kuvunjwa nazo sanamu zenu za mavi zikomeshwe na vinara vyenu vya uvumba vikatwe na kazi zenu zifutiliwe mbali.” (Ezekieli 6:6) Hapana shaka kwamba Yehova aliona ibada hiyo kuwa isiyokubalika na akaikataa.

Yehova Mungu alitabiri jinsi uharibifu huo ungetokea. “Tazama, ninatuma . . . Nebukadreza mfalme wa Babiloni, mtumishi wangu, nami nitawaleta wao juu ya nchi hii na juu ya wakaaji wake na juu ya haya mataifa yote kuzunguka pande zote; nami nitawaangamiza . . . Na nchi hii yote itakuwa mahali palipoharibiwa.” (Yeremia 25:9-11) Kupatana na maneno hayo, mnamo 607 K.W.K., Wababiloni walikuja dhidi ya Yerusalemu na kuliharibu kabisa jiji hilo pamoja na hekalu lake.

Profesa Stern aliyetajwa hapo juu alipozungumza kuhusu kuharibiwa kwa Yerusalemu, alisema kwamba mabaki ya akiolojia “yanaunga mkono waziwazi maandiko ya kibiblia (2 Wafalme 25:8; 2 Mambo ya Nyakati 36:18-19) yanayofafanua uharibifu, kuteketezwa, na kuanguka kwa nyumba na kuta.” Anaongezea hivi: “Uthibitisho wa kiakiolojia wa sehemu hii ya historia ya Yerusalemu . . . unaweza kusemwa kuwa moja kati ya maeneo ya kibiblia yaliyochimbuliwa yenye uthibitisho ulio wazi sana.”

Tunajifunza Nini?

Jambo kuu tunalojifunza ni kwamba Mungu hakubali ibada inayojaribu kuchanganya mafundisho ya Biblia na imani, desturi, au mila za dini nyingine. Hilo ni jambo ambalo mtume Paulo alielewa na kulikubali. Alikuwa Farisayo Myahudi, alifunzwa na kuzoezwa katika sheria ya madhehebu hayo. Alipojifunza na kukubali kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa, alifanya nini? Alisema hivi: “Vitu vilivyokuwa faida kwangu, hivyo nimeviona kuwa hasara kwa sababu ya Kristo.” Paulo aliacha njia zake za zamani na akawa mfuasi wa Kristo mwenye bidii.—Wafilipi 3:5-7.

Akiwa mmishonari anayesafiri, Paulo alifahamu vizuri mazoea ya kidini na falsafa za watu mbalimbali. Kwa hiyo, aliwaandikia hivi Wakristo huko Korintho: “Nuru ina ushirika gani na giza? Na zaidi, kuna upatano gani kati ya Kristo na Beliali? Au mtu mwaminifu ana fungu gani na asiye mwamini? Na hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu? . . . ‘Kwa hiyo tokeni katikati yao, na mjitenge,’ asema Yehova, ‘na mwache kugusa kitu kilicho najisi’; ‘nami nitawakaribisha ndani.’”—2 Wakorintho 6:14-17.

Tunapotambua kwamba Mungu anajali njia tunayotumia kumwabudu, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Ni aina gani ya ibada inayokubaliwa na Mungu? Ninaweza kumkaribia Mungu jinsi gani? Na ninapaswa kufanya nini ili nimwabudu Mungu kwa njia inayokubalika?’

Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia upate majibu kwa maswali haya na mengine yanayohusiana na Biblia. Twakualika uwasiliane na Mashahidi kwenye Jumba la Ufalme au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili na uombe funzo la Biblia bila malipo kwa wakati na mahali panapokufaa.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kihekalu cha kale cha ibada ya sanamu, Tel Arad, Israeli

[Hisani]

Garo Nalbandian

[Picha katika ukurasa wa 10]

Sanamu za Ashtorethi kutoka nyumba za zamani za Yudea

[Hisani]

Photograph © Israel Museum, Jerusalem; courtesy of Israel Antiquities Authority