Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni “Jina Lisilopaswa Kutamkwa”?

Je, Ni “Jina Lisilopaswa Kutamkwa”?

Je, Ni “Jina Lisilopaswa Kutamkwa”?

TAO la Gateway lililo kando ya mto huko St. Louis, Missouri, lenye kimo cha mita 192, ndio mnara mrefu zaidi nchini Marekani. Karibu na tao hilo kuna kanisa fupi linalojulikana kama Kanisa Kuu la Zamani.

Kikifafanua jinsi mwingilio wa kanisa hilo ulivyo, kijitabu (The Story of the Old Cathedral) kilichochapishwa na kanisa hilo kinasema hivi: “Roshani imefunikwa kwa paa maridadi ambayo ina lile jina lisilopaswa kutamkwa la Mungu likiwa limenakshiwa katikati kwa herufi kubwa za Kiebrania.” Kama picha inavyoonyesha, zile herufi nne za Kiebrania יהוה (YHWH), au Tetragramatoni, zinazowakilisha jina la Mungu, zinaonekana waziwazi.

Kanisa hilo kuu lilipojengwa mnamo 1834, lazima wale waliokuwa katika dayosisi ya St. Louis wawe walihisi kwamba jina hilo lililoandikwa kwa herufi nne za Kiebrania linapaswa kuwekwa mahali muhimu. Basi kwa nini, jina la Mungu lionwe kuwa jina “lisilopaswa kutamkwa”?

Kitabu fulani (New Catholic Encyclopedia) kinaeleza kile kilichotukia baada ya Wayahudi kurudi kutoka uhamishoni Babiloni katika karne ya sita K.W.K. Kinasema hivi: “Jina Yahweh [yaani herufi za Tetragramatoni zinapoongezwa vokali] lilianza kuonwa kwa njia ya pekee, na zoea la kulibadili na neno ADONAI [Bwana] au ELOHIM [Mungu] likaanza. . . . Baada ya muda zoea hilo liliwafanya watu wasahau jinsi jina Yahweh linavyopaswa kutamkwa.” Hivyo, watu wakaacha kutumia jina la Mungu. Mwishowe, watu hawakujua jinsi lilivyotamkwa zamani na kwa maoni yao jina la Mungu likawa jina lisilopaswa kutamkwa.

Ingawa hatuwezi kuwa na uhakika kabisa jinsi jina la Mungu lilivyokuwa likitamkwa, jambo muhimu ni kwamba kutumia jina lake hutufanya tumkaribie. Je, ungependa rafiki zako wakuite “bwana” au “bibi,” au ungependa wakuite kwa jina lako la kibinafsi? Hata ikiwa wanazungumza lugha tofauti na yako na hawatamki jina lako vizuri kabisa, bila shaka ungependelea zaidi watumie jina lako, sivyo? Hilo ni kweli pia kumhusu Mungu. Yeye pia angependelea tumwite kwa jina lake la kibinafsi, Yehova.

Katika Kiswahili, jina “Yehova” ndilo linalojulikana zaidi. Je, haingefaa kwa wote wanaompenda Mungu wamwite kwa jina hilo na hivyo wamkaribie? “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi,” inasema Biblia.—Yakobo 4:8.