Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Noa Alipata Kibali cha Mungu—Je, Hilo Linatuhusu?

Kwa Nini Noa Alipata Kibali cha Mungu—Je, Hilo Linatuhusu?

Kwa Nini Noa Alipata Kibali cha Mungu—Je, Hilo Linatuhusu?

WENGI wetu tunakumbuka pindi fulani tuliposikia habari muhimu. Tunakumbuka mambo mengi, kama vile mahali tulipokuwa, tulichokuwa tukifanya, na pia jinsi tulivyoitikia. Bila shaka, Noa hakusahau siku ambayo alipewa habari na Yehova Mungu, Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu. Na ni habari gani ingeweza kuwa muhimu kuliko hiyo? Yehova alisema alikuwa ameamua kuangamiza “wote wenye mwili.” Noa alipaswa kujenga safina kubwa sana ya kumhifadhi hai yeye, familia yake, na wanyama wa kila aina.—Mwanzo 6:9-21.

Noa aliitikia jinsi gani? Je, alifurahi aliposikia habari hizo, au alilalamika? Alimpasha habari jinsi gani mke na familia yake? Biblia haituelezi. Inatueleza tu hivi: “Noa akafanya kulingana na yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru. Alifanya vivyo hivyo.”—Mwanzo 6:22.

Kwa kweli hilo ndilo jambo muhimu, kwa kuwa maneno hayo yanatueleza sababu moja iliyomfanya Noa apate kibali cha Mungu; Noa alikuwa tayari kufanya kile ambacho Mungu alimwomba afanye. (Mwanzo 6:8) Ni nini kingine kilichomfanya Noa akubaliwe na Mungu? Jibu la swali hilo ni muhimu kwa kuwa tunapaswa kutenda kama Noa ili tuokoke wakati Mungu atasafisha tena uovu kutoka duniani. Hata hivyo, acheni kwanza tuchunguze jinsi maisha yalivyokuwa siku za Noa kabla ya Gharika.

Roho Waovu Waja Duniani

Noa aliishi mapema katika historia ya wanadamu. Alizaliwa miaka elfu moja hivi baada ya mwanamume wa kwanza kuumbwa. Watu wa wakati huo hawakuwa kama wengi wanavyofikiri, eti watu wanaoishi katika mapango, wenye miili iliyofunikwa kwa nywele nyingi, wasio na akili, na wanaotembea wakiwa wameinama huku wakibeba rungu mkononi. Kulikuwa na vifaa vilivyotengenezwa kwa chuma na shaba, na huenda Noa alitumia vifaa hivyo kujenga safina. Pia kulikuwa na vyombo vya muziki. Watu walioana, wakawa na familia, wakapanda mimea, na kufuga wanyama. Waliuza na kununua vitu. Katika njia hizo, maisha ya wakati huo yalikuwa tu kama ya leo.—Mwanzo 4:20-22; Luka 17:26-28.

Katika njia nyingine, mambo yalikuwa tofauti. Tofauti moja ni kwamba watu waliishi muda mrefu zaidi. Haikuwa ajabu kwa mtu kuishi zaidi ya miaka 800. Noa aliishi miaka 950; Adamu akaishi miaka 930; na Methusela, babu ya Noa akaishi miaka 969. *Mwanzo 5:5, 27; 9:29.

Tofauti nyingine inafafanuliwa katika Mwanzo 6:1, 2 inayosema hivi: “Sasa ikawa kwamba hesabu ya wanadamu ilipoanza kuongezeka usoni pa nchi nao wakazaa mabinti, ndipo wana wa Mungu wa kweli wakaanza kuwaona mabinti wa wanadamu, kwamba ni wenye sura ya kupendeza; nao wakajichukulia wake, yaani, wote waliowachagua.” Hawa “wana wa Mungu wa kweli” walikuwa malaika kutoka mbinguni ambao walivaa miili ya kibinadamu na kutembea duniani kama wanadamu. Hawakuwa wametumwa na Mungu; wala hawakuja kwa faida ya wanadamu. Badala yake, ‘waliyaacha makao yao wenyewe yanayofaa’ huko mbinguni ili wafanye ngono na wanawake warembo duniani. Wakawa roho waovu.—Yuda 6.

Malaika hao waovu walikuwa na uvutano mbaya sana juu ya wanadamu kwa kuwa walikuwa waasi, waliopotoka, na walikuwa na nguvu na akili zinazozidi zile za kibinadamu. Inaelekea kwamba walidhibiti na kutawala jamii ya wanadamu. Hawakutenda kwa siri, kama mhalifu anayetenda uovu kwa siri huku akijificha asitambuliwe. Badala yake, waliasi waziwazi mpango wa Mungu.

Wana hao wa kimalaika wa Mungu walifanya ngono na wanawake, na wanawake hao wakazaa watoto ambao walikua wakawa na nguvu za ajabu. Waliitwa katika Kiebrania “Wanefili.” Tunaelezwa hivi: “Wanefili walikuwa duniani siku hizo, na pia baada ya hapo, wakati wana wa Mungu wa kweli walipoendelea kulala na binti za wanadamu nao wakawazalia wana, hao ndio waliokuwa watu wenye nguvu wa kale, wanaume wenye sifa.” (Mwanzo 6:4) Wanefili waliogopwa sana. Neno “Wanefili” linamaanisha “Waangushaji,” wale wanaowaangusha wengine. Walikuwa wauaji ambao huenda matendo yao ya jeuri yanaelezewa katika hekaya nyingi za kale.

Huzuni ya Waadilifu

Biblia inafafanua kizazi hicho kuwa kilichojaa ufisadi. Inasema hivi: “Ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani na kila mwelekeo wa fikira za moyo wake ulikuwa mbaya tu wakati wote. . . . Dunia ikajaa jeuri. . . . Kila mwenye mwili alikuwa amejiharibia njia yake duniani.”—Mwanzo 6:5, 11, 12.

Huo ndio ulimwengu ambamo Noa aliishi. Tofauti na wale waliomzunguka, “Noa alikuwa mtu mwadilifu” ambaye “alitembea pamoja na Mungu wa kweli.” (Mwanzo 6:9) Si rahisi kwa mtu mwadilifu kuishi katika jamii yenye ukosefu wa uadilifu. Lazima Noa awe alihuzunishwa sana na mambo ambayo watu walisema na kufanya! Huenda alihisi kama Loti, mwanamume mwingine mwadilifu aliyeishi baada ya Gharika. Loti, ambaye aliishi kati ya wakaaji wa Sodoma waliotenda kwa ukosefu wa maadili, ‘alitaabishwa sana na kule kujitia mno katika mwenendo mpotovu kwa watu wanaokaidi sheria na pia yale ambayo aliona na kusikia alipokuwa akikaa katikati yao siku baada ya siku yalimfanya aitese nafsi yake yenye uadilifu kwa sababu ya vitendo vyao vya kuasi sheria.’ (2 Petro 2:7, 8) Bila shaka, Noa alihisi vivyo hivyo.

Je, unahuzunishwa na habari za matukio yenye kushtua au mwenendo wa kutomwogopa Mungu unaofuatwa na watu wanaokuzunguka? Ikiwa ndivyo, basi unaweza kuelewa jinsi Noa alivyohisi. Wazia jinsi ilivyokuwa vigumu kwake kuvumilia kuishi katika ulimwengu usio na uadilifu kwa miaka 600, umri aliokuwa nao Gharika ilipokuja. Alitamani kama nini kupata kitulizo!—Mwanzo 7:6.

Noa Alikuwa na Ujasiri wa Kuwa Tofauti

Noa “alionekana kuwa mtu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake.” (Mwanzo 6:9) Ona kwamba Biblia inasema alikuwa asiye na kosa kati ya, si kwa maoni ya, watu wa siku zake. Kwa maneno mengine, Noa alikuwa asiye na kosa kwa maoni ya Mungu, lakini machoni pa watu walioishi katika ulimwengu wa kabla ya Gharika, Noa alikuwa mtu asiye na akili timamu. Tunaweza kuwa na hakika kwamba hakukubaliana na maoni ya watu wengi, wala hakujihusisha katika burudani zinazomshushia Mungu heshima na shughuli za kijamii za wakati huo. Wazia jinsi watu walivyomwona alipoanza kujenga safina! Huenda walimcheka na kumdhihaki. Hawakufikiri kwamba mambo aliyosema yangetendeka.

Zaidi ya hayo, Noa alikuwa na imani za kidini zenye kina na aliwaambia wengine kuzihusu. Biblia inasema kwamba alikuwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5) Bila shaka, Noa alitarajia upinzani. Babu yake wa kale Enoko alikuwa mwanamume mwadilifu ambaye alitabiri kwamba Mungu angetekeleza hukumu juu ya waovu. Kwa wazi, hilo lilimfanya Enoko ateswe, ingawa Mungu hakuwaruhusu wapinzani wake wamuue. (Mwanzo 5:18, 21-24; Waebrania 11:5; 12:1; Yuda 14, 15) Kwa kuwa Shetani, roho waovu, Wanefili, na watu wengi walionyesha ama ubaridi ama walimpinga, Noa alihitaji kuwa na ujasiri na pia imani katika uwezo wa Yehova wa kumlinda.

Sikuzote wale wanaomtumikia Mungu wamepingwa na wale wasiomtumikia. Hata Yesu Kristo alichukiwa, na hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa wafuasi wake. (Mathayo 10:22; Yohana 15:18) Noa alikuwa na ujasiri wa kumtumikia Mungu, ingawa wengi hakupendezwa na jambo hilo. Alielewa kwamba kupata kibali cha Mungu ni muhimu zaidi kuliko kupata kibali cha wanaompinga Mungu. Naye Noa alipata kibali cha Mungu.

Noa Alijali

Kama tulivyoona, Noa aliwahubiria wengine kwa ujasiri. Waliitikia jinsi gani ujumbe aliowapa? Biblia inasema kwamba kabla ya Gharika watu walikuwa “wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.” Walikosa kutii onyo.—Mathayo 24:38, 39.

Yesu alisema kwamba mambo yatakuwa hivyo pia katika siku zetu. Kwa zaidi ya miaka 100, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakionya kwamba Yehova atachukua hatua madhubuti za kutimiza ahadi yake ya kutokeza ulimwengu mpya wenye uadilifu. Ingawa mamilioni ya watu wameitikia kwa njia inayofaa, mabilioni ya wakaaji wa dunia hawajali. “Kulingana na kupenda kwao,” wanapuuza uhakika na umuhimu wa ile Gharika.—2 Petro 3:5, 13.

Hata hivyo, Noa alijali. Aliamini kile ambacho Yehova Mungu alimwambia. Kutii huko kulimfanya aokolewe. Mtume Paulo aliandika: “Kwa imani Noa, baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo ambayo yalikuwa bado hayajaonekana, alionyesha woga wa kimungu na kujenga safina kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake.”—Waebrania 11:7.

Mfano wa Kuiga

Safina ambayo Noa alijenga ilikuwa kubwa sana, ndefu kuliko uwanja wa mpira na ilikuwa na kimo kinacholingana na jengo la orofa tatu. Ilikuwa ndefu kwa mita 30 kuliko meli ya mbao inayosemekana kuwa ndefu zaidi kuwahi kujengwa. Bila shaka, safina haikuwa meli; ilihitaji tu kuelea. Hata hivyo, ilihitaji kujengwa kwa mbinu za hali ya juu. Ilihitaji kufunikwa ndani na nje kwa lami. Huenda ilichukua zaidi ya miaka 50 kuijenga.—Mwanzo 6:14-16.

Lakini si hilo tu. Noa alihitaji kuhifadhi chakula cha mwaka mmoja kwa ajili ya familia yake na wanyama. Kabla ya Gharika, wanyama walihitaji kukusanywa na kuingizwa ndani ya safina. “Noa akafanya kulingana na yote ambayo Yehova alikuwa amemwamuru.” Noa alipata kitulizo kama nini kila kitu kilipokuwa tayari na Yehova akafunga mlango wa safina!—Mwanzo 6:19-21; 7:5, 16.

Kisha Gharika ikaja. Mvua ilinyesha kwa siku 40, mchana na usiku. Wote walihitaji kukaa katika safina kwa mwaka mzima hadi maji yalipopungua. (Mwanzo 7:11, 12; 8:13-16) Waovu wote walikufa. Noa na familia yake tu ndio waliookoka na kuingia katika dunia iliyosafishwa.

Biblia inasema kwamba Gharika ya ulimwenguni pote ya siku za Noa ilikuwa ‘kielelezo cha mambo yatakayokuja.’ Kwa njia gani? Tunasoma hivi: “Mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zinahifadhiwa mpaka ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.” Hata hivyo, kama tu ilivyokuwa katika siku za Noa, kuna watu watakaookoka. Uwe na hakika kwamba “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.”—2 Petro 2:5, 6, 9; 3:7.

Noa alikuwa mwanamume mwenye ujitoaji-kimungu, mtu mwadilifu kati ya kizazi kiovu. Alimtii Mungu kabisa. Alikuwa na ujasiri wa kufanya yaliyo sawa hata ingawa alijua kwamba hilo lingemfanya adharauliwe na kuchukiwa na wale ambao hawakutaka kumtumikia Mungu. Tukimwiga Noa katika njia hizo, sisi pia tutapata kibali cha Mungu na kupata taraja la kuokolewa kuingia katika ulimwengu mpya utakaokuja karibuni.—Zaburi 37:9, 10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona makala “Je, Ni Kweli Waliishi Miaka Mingi Hivyo?” katika Amkeni! la Julai 2007 ukurasa wa 30.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Huenda matendo ya jeuri ya Wanefili yanaelezewa katika hekaya nyingi za kale

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kwa kuiga imani ya Noa, tunaweza kupata kibali cha Mungu

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]

Alinari/Art Resource, NY