Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Msichana Mwisraeli” wa Kisasa

“Msichana Mwisraeli” wa Kisasa

“Msichana Mwisraeli” wa Kisasa

MNAMO 2006, majuma mawili kabla ya Ukumbusho wa kifo cha Yesu, kila mshiriki wa familia ya Sales huko Praia Grande nchini Brazili, aliandika orodha ya wale aliotaka kuwaalika. Abigayl, mwenye umri wa miaka sita alipewa mwaliko na kuulizwa angependa kumpa nani.

“Yule mtu anayetabasamu akiniona,”akajibu.

“Ni nani huyo?” wazazi wake wakamwuliza.

“Yule anayetumia kiti cha magurudumu,” akajibu.

Siku nne baadaye, Abigayl aliwaonyesha wazazi wake mtu huyo. Mtu huyo anayeitwa Walter, aliishi karibu sana na Jumba la Ufalme. Zaidi ya miaka 15 iliyopita, alipokuwa na umri wa miaka 28, alihusika katika msiba wa barabarani na akapooza kuanzia kiunoni kwenda chini. Alikuwa na walinzi wawili kwa sababu alikuwa tajiri. Baada ya Abigayl kupewa ruhusa azungumze na Walter, wazazi wake walimweleza kwamba binti yao alitaka kumpa mwaliko.

Akimalizia, Abigayl alisema: “Wengine wote katika Jumba letu la Ufalme walipata mialiko mingi, lakini mimi nina mwaliko mmoja tu. Kwa hiyo, ni wewe tu ninayekualika. Ukikosa kuja, sitakuwa na mtu yeyote. Lakini ukija, nitafurahi sana, na Yehova atafurahi hata zaidi.”

Siku ya Ukumbusho, Mashahidi, kutia ndani Abigayl waliosha Jumba la Ufalme wakijitayarishia programu ya Ukumbusho jioni hiyo. Alasiri hiyo, Walter alikuwa akipita, na alipomwona Abigayl, alimwambia dereva wake asimamishe gari. Dirisha la gari lilifunguliwa, na akamwuliza Abigayl alikuwa akifanya nini. Abigayl alimwambia kwamba walikuwa wakiosha jumba ili liwe nzuri kwa ajili yake.

Jioni hiyo, Abigayl alikuwa na wasiwasi mwingi. Hotuba ilianza, na aligeuka mara kwa mara ili aone ikiwa Walter alikuwa amewasili. Ghafula, Walter na walinzi wake wakaingia. Alitabasamu kwa furaha sana. Baada ya hotuba, Walter alikiri kwamba alikuwa ameanza safari ya kwenda jiji lingine lakini akabadili maoni yake na akaenda kuhudhuria Ukumbusho, kwa sababu tu ya Abigayl. Kisha akaongezea: “Hotuba hiyo hasa ndiyo niliyohitaji kusikiliza.” Aliomba apewe Biblia na ameanza kujifunza na kuhudhuria mikutano.

Katika kipindi hicho, dada ya Walter alisema kwamba angependa kukutana na Abigayl, ambaye ndugu yake alimtaja mara nyingi sana. Walipokutana, alifurahi kujua jinsi Abigayl alivyokuwa msichana mzuri sana. Alisema hivi: “Sasa ninajua ni kwa nini ndugu yangu ana furaha hivyo.”

Walter anaendelea kujifunza na kuhudhuria mikutano. Hata anatoa maelezo na anawaambia wengine mambo anayojifunza. Kwa kweli, Abigayl anatukumbusha yule msichana Mwisraeli ambaye alimsaidia Naamani kumjua Mungu wa kweli, Yehova.—2 Wafalme 5:2-14.