Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Aliye Tayari Kusamehe

Mungu Aliye Tayari Kusamehe

Mkaribie Mungu

Mungu Aliye Tayari Kusamehe

Yohana 21:15-17

“WEWE, Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Kwa maneno hayo yenye kutia moyo, Biblia inatuhakikishia kwamba Yehova Mungu anasamehe sana. Tukio fulani katika maisha ya mtume Petro linaonyesha waziwazi kwamba Yehova anasamehe “kwa njia kubwa.”—Isaya 55:7.

Petro alikuwa mmoja wa waandamani wa karibu zaidi wa Yesu. Hata hivyo, katika usiku wa mwisho wa maisha ya Yesu duniani, Petro aliingiwa na woga na akatenda dhambi nzito. Akiwa katika ua uliokuwa karibu na mahali ambapo Yesu alijaribiwa kinyume cha sheria, Petro alikana kumjua Yesu—si mara moja tu bali mara tatu. Baada ya Petro kumkana mara ya tatu, Yesu ‘aligeuka na kumtazama Petro.’ (Luka 22:55-61) Je, unaweza kuwazia jinsi Petro alivyohisi Yesu alipomtazama? Akitambua uzito wa dhambi yake, Petro ‘alianza kulia.’ (Marko 14:72) Huenda mtume huyo aliyetubu alijiuliza ikiwa kumkana Yesu mara tatu kungemfanya asiweze kusamehewa na Mungu.

Baada ya kufufuliwa, Yesu alizungumza na Petro, na mazungumzo hayo yalionyesha wazi kwamba Petro alikuwa amesamehewa. Yesu hakutumia maneno makali wala kumshutumu. Badala yake, alimwuliza Petro: “Je, unanipenda?” Petro akamjibu: “Ndiyo, Bwana, unajua ninakupenda.” Yesu akamwambia: “Lisha wana-kondoo wangu.” Yesu alirudia swali hilo mara ya pili, na Petro akamjibu vilevile, huenda akisisitiza zaidi. Yesu alisema: “Chunga kondoo wangu wadogo.” Kisha Yesu alimwuliza swali lilelile mara ya tatu: “Je, unanipenda?” Sasa “Petro akahuzunika” na kusema: “Bwana, wewe unajua mambo yote; unajua kwamba ninakupenda.” Yesu akamwambia: “Lisha kondoo wangu wadogo.”—Yohana 21:15-17.

Kwa nini Yesu aliuliza maswali ambayo tayari alijua majibu yake? Yesu angeweza kusoma mioyo, kwa hiyo alijua kwamba Petro alimpenda. (Marko 2:8) Kwa kuuliza maswali hayo, Yesu alimpa Petro nafasi ya kuthibitisha upendo wake mara tatu. Maneno ya Yesu: “Lisha wana-kondoo wangu. . . . Chunga kondoo wangu wadogo. . . . Lisha kondoo wangu wadogo,” yalimhakikishia mtume huyo aliyetubu kwamba bado alitegemewa. Yesu alimpa Petro mgawo wa kusaidia katika kutunza mali zenye thamani zaidi, yaani, wafuasi wapendwa wa Yesu walio kama kondoo. (Yohana 10:14, 15) Bila shaka, Petro alihisi vizuri kujua kwamba bado anategemeka machoni pa Yesu!

Ni wazi kwamba Yesu alimsamehe mtume wake aliyetubu. Kwa sababu Yesu anaiga sifa na njia za Baba yake kwa ukamilifu, tunaweza kukata kauli kwamba Yehova pia alimsamehe Petro. (Yohana 5:19) Yehova hasiti kusamehe, badala yake yeye ni Mungu wa rehema aliye “tayari kusamehe” mtenda-dhambi anayetubu. Hilo ni wazo la kufariji kama nini!