Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nimepata Shangwe Maishani kwa Kufanya Mapenzi ya Mungu

Nimepata Shangwe Maishani kwa Kufanya Mapenzi ya Mungu

Nimepata Shangwe Maishani kwa Kufanya Mapenzi ya Mungu

Limesimuliwa na Bill Yaremchuk

Mnamo Machi (Mwezi wa 3) 1947, majuma machache tu baada ya kuhitimu nikiwa mmishonari katika darasa la nane la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead), huko South Lansing, New York, Marekani, nilifunga safari kuelekea mgawo wangu mpya—nchi iliyo mbali ya Singapore.

NILIPEWA mgawo pamoja na Mkanada mwenzangu Dave Farmer, aliyekuwa amehitimu katika darasa la saba la Shule ya Gileadi. Tuliabiri meli inayoitwa Marine Adder kutoka San Francisco, California, iliyotumiwa jeshini hapo zamani.

Mahali pa kwanza ambapo meli yetu ilisimama katika nchi za Mashariki ni Hong Kong. Mambo tuliyoona huko yalitushtua sana. Kila mahali tuliona madhara ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, watu walikuwa wamelala kandokando ya njia, wakiwa na njaa na wakionekana kama wanaelekea kufa. Muda si muda tulirudi ndani ya meli na kuelekea Manila, mji mkuu wa Filipino.

Huko pia, tuliona madhara ya vita. Bandari ilijaa milingoti ya meli zilizozamishwa na majeshi ya Muungano, na umaskini ulienea. Tulikutana na Mashahidi kadhaa wa Yehova, waliotupeleka katika Jumba lao la Ufalme. Ingawa walikuwa na matatizo, walikuwa na furaha.

Baada ya hapo, tulisimama katika bandari ya Batavia (leo inaitwa Jakarta) huko Indonesia. Vita vya wenyewe kwa wenyewe vilikuwa vikiendelea, na kulikuwa na mapambano hapo karibu, hivyo hatukuruhusiwa kutoka melini. Tulipoondoka kuelekea Singapore, nilianza kujiuliza tutapata hali gani huko. Kwani kila kitu chenye kupendeza tulichokuwa tumesoma katika magazeti ya utalii kilikuwa kimepotea?

Baada ya siku kadhaa, niliacha kuwa na wasiwasi. Mambo fulani yangetendeka na kuthibitisha kabisa kwamba mimi na Dave tulikuwa tunafanya kazi iliyo na kibali cha Mungu.

Tulivyoruhusiwa Kuishi Singapore

Mwezi mmoja hivi baada ya kutoka San Francisco, meli yetu ilitia nanga katika kisiwa cha St. John, eneo la Singapore ambako meli zilikaa kabla ya kuruhusiwa kuingia bandarini. Maofisa wa uhamiaji walikuja melini kuwakagua wasafiri, na pasipoti zetu zilitiwa muhuri uliosema “Umeruhusiwa Kuingia Nchini.” Asubuhi iliyofuata, meli ilitia nanga kando ya eneo la kupakia na kupakua mizigo. Baada ya hati zetu kukaguliwa na ofisa wa meli, tukashuka.

Siku iliyofuata, tulirudi bandarini kuwaaga wamishonari tuliokuwa tukisafiri nao. Walikuwa wakiendelea na safari hadi India na Ceylon (leo inaitwa Sri Lanka). Kapteni wa meli alipotuona, alikuja bandarini na kutushutumu. Alikuwa amekasirika na akasema kwamba hatukupaswa kutoka melini. Mapema tulipokuwa safarini, mkuu wa uhamiaji, Bw. Haxworth, alimwagiza asituruhusu tutoke kwenye meli tutakapofika bandarini. Hatukujua kulikuwa na agizo kama hilo na ofisa aliyeturuhusu tutoke melini hakujua jambo hilo pia.

Bw. Haxworth alikasirika sana tulipofikishwa mbele yake. Alifoka akisema kwamba tulikuwa tumekatazwa kuingia Singapore. Kwa kuwa hatukujua kwamba hatukupaswa kuingia, tulimwonyesha pasipoti zetu zikiwa na muhuri rasmi uliosema “Umeruhusiwa Kuingia Nchini.” Kwa hasira alichukua pasipoti hizo kutoka mikononi mwetu na akafuta maneno hayo. Lakini tayari meli ilikuwa imeondoka! Bw. Haxworth alibaki na pasipoti zetu kwa mwaka mzima, mwishowe akaturudishia zikiwa zimetiwa muhuri uliosema “Umeruhusiwa Kuingia Nchini.”

Utumishi Wenye Matokeo Nchini Singapore

Tulipowasili Singapore mnamo Aprili 1947, Joshua ndiye aliyekuwa Shahidi pekee nchini. Alitumika akiwa mhudumu wa wakati wote, au painia, mpaka kifo chake mwanzoni mwa miaka ya 1970. Baada ya muda, baadhi ya wale waliokuwa wakijifunza kweli za Biblia walianza kuwahubiria wengine. Sala zetu za kupata wafanyakazi zaidi katika mavuno ya kiroho zilianza kujibiwa.—Mathayo 9:37, 38.

Mnamo 1949, Bw. Haxworth alipokuwa na likizo ndefu huko Uingereza, wamishonari sita waliokuwa wamehitimu katika darasa la 11 la Shule ya Gileadi waliwasili nchini Singapore. Katika kipindi hichohicho, Dave ambaye alikuwa mmishonari mwenzi kwa miaka fulani, aliona ni muhimu atoke Singapore kwa sababu ya matatizo ya afya. Alihamia Australia, ambako alitumika kwa uaminifu mpaka kifo chake katika 1973. Mmoja wa wamishonari hao sita alikuwa Aileen Franks, ambaye nilimwoa mnamo 1956.

Kwa miaka mingi, tumejifunza Biblia na watu wengi ambao wamekuwa Mashahidi pamoja na watoto wao. Hata leo, wengine wao ni watumishi wa wakati wote katika nchi nyingine. Jambo moja lililoonwa ambalo lilitutia moyo linawahusu Lester and Joanie Haynes, wenzi wa ndoa Wamarekani walioishi Singapore. Tulianza kujifunza nao Biblia katika miaka ya 1950. Wenzi hao walifanya maendeleo ya kiroho haraka na baada ya kurudi Marekani wakabatizwa. Baadaye, Lester na Joanie walifurahia utumishi wenye matokeo. Waliwasaidia watu wengi kuwa Mashahidi, kutia ndani watoto wao watatu.

Joanie aliandika hivi: “Ninapoufikiria mwaka huo tulipokuwa Singapore, kwa kweli ulibadili jinsi tulivyokuwa tukiishi. Ikiwa hamngetutunza huenda bado tungekuwa tukiranda-randa kote ulimwenguni. Ninafurahi kwamba wewe ndiye uliyemfundisha Les kweli kwa sababu tangu mwanzoni, amekuwa na mwalimu aliyekazia ndani yake upendo kwa Yehova na kwa ndugu zetu Wakristo. Hajaacha upendo huo.”

Kutumika Tukiwa Familia Nchini Singapore

Katika 1962 jambo lisilotazamiwa lilibadili kabisa maisha yetu. Daktari wetu alimwambia Aileen kwamba alikuwa na mimba. Tulitaka kubaki katika kazi ya umishonari, lakini tungeweza jinsi gani kuwa wamishonari huku tukimlea mtoto? Nathan H. Knorr, aliyekuwa akisimamia kazi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, alituandikia, akinitia moyo nitafute kazi ili tuendelee kuishi Singapore. Hilo halikuwa jambo rahisi.

Watu wengi kutoka nchi za kigeni walikuwa na madaraka katika kampuni za kigeni. Sikuwa na uzoefu wowote katika biashara kwani nilianza utumishi wa wakati wote baada ya kumaliza shule miaka 23 mapema. Kwa hiyo nilililipa pesa shirika la kuwatafutia watu kazi huko London ili wanitengenezee hati yenye muhtasari kuhusu elimu na ufundi wangu ikitegemea kazi yangu kama mhudumu wa kidini katika nchi ya kigeni, kisha wakaituma kwa makampuni mengi ya kimataifa nchini Singapore.

Lakini mara nyingi nilipata jibu hili, “Tunasikitika kwamba hatujapata kazi inayoweza kufanywa na mtu wa ustadi wako.” Waliona kuwa nina ustadi mwingi kupita kiasi! Miezi ilisonga, na mtoto wetu, Judy, akazaliwa. Wakati huo, ndugu Knorr alikuwa akitembelea Singapore, na alienda kumwona Judy na mama yake hospitalini. Alituhakikishia, “Mnaweza kukaa katika makao ya wamishonari kwa muda wowote mtakaohitaji mpaka Bill apate kazi.”

Miezi michache baadaye, nilipata kazi ya kuwa mwakilishi wa uuzaji katika shirika moja la ndege la kimataifa. Mshahara ulitosheleza tu mahitaji yetu. Miaka miwili baadaye, nilipata kazi katika shirika la Marekani la kusafirisha mizigo nao wakanipa mshahara maradufu. Mwishowe, nilijulikana katika biashara ya usafiri, na hivyo nikaweza kutenga wakati zaidi kwa ajili ya familia yangu na utumishi wa Kikristo.

Tulikazia utumishi kwa Yehova maishani mwetu, tukitanguliza mambo ya kiroho. Hilo limeniwezesha kuwa na mapendeleo mengi katika tengenezo. Aileen alirudia utumishi wa wakati wote tena. Wakati huohuo, kazi ya kuhubiri Ufalme ilisitawi nchini Singapore. Katikati ya miaka ya 1960, tulinunua jengo zuri la orofa mbili karibu na mji lililotumika kama Jumba la Ufalme. Makutaniko manne yalikutana hapo.

Kazi Yetu Yapigwa Marufuku!

Baada ya muda, dalili za mateso zilionekana. Januari 14, 1972 (14/1/1972), kama kawaida tulienda kwenye Jumba la Ufalme ili kuhudhuria mkutano wetu. Lakini lango lilikuwa limefungwa kwa mnyororo na kufuli. Kulikuwa na karatasi iliyosema kwamba Kutaniko la Singapore la Mashahidi wa Yehova limeondolewa kwenye orodha. Tulikuwa tumepigwa marufuku! *

Kufungwa kwa Jumba la Ufalme hakukusimamisha ibada yetu kwa Yehova, lakini swali nililojiuliza ni, ‘Mapenzi ya Mungu kuhusu familia yangu ni nini?’ Nilifikiria kwamba ikiwa tutatimuliwa kutoka Singapore, hatutaweza kamwe kurudi na kuwatembelea marafiki wetu. Kwa hiyo nimwuliza meneja wa kampuni yetu ikiwa ningeweza kufanya kazi Kuala Lumpur, Malasia. Hilo lingeturuhusu kuzuru maeneo yote mawili bila usumbufu. Alinishangaza kwa kunipa kazi ya umeneja katika ofisi ya Kuala Lumpur ambapo ningepata mshahara maradufu na marupurupu mengine.

Kisha nilijiuliza, ‘Je, ni mapenzi ya Mungu kwamba tutoke Singapore na kuwaacha ndugu zetu?’ Tukiwa familia, tulizungumza na Yehova katika sala. Tulikata kauli kwamba ni Yehova aliyetuingiza nchini. Kwa hiyo nilifanya uamuzi wa mwisho kwamba tutakaa. Meneja wangu alishangaa sana nilipokataa kazi mpya aliyotaka kunipa.

Halikuwa jambo rahisi kuishi na kufanya kazi chini ya marufuku, kwa kuwa wakati wowote mtu angeshikwa au kufungwa. Kulikuwa na pindi fulani zilizotufanya tuthamini maneno ya Zaburi 34:7: “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa, na yeye huwaokoa.”

Mgawo Mpya

Mwishowe mnamo 1993, baada ya kutumika nchini Singapore kwa miaka 46, tuliombwa tuhamie New Zealand, ambako tungetumika bila mkazo na wasiwasi. Bila shaka, tulihuzunika kuwaacha marafiki wetu ambao tulikuwa tumekuja kuwapenda sana huko Singapore. Hata hivyo, tulitiwa moyo kujua kwamba imani yao ilikuwa imejengwa kwenye msingi thabiti kwa vifaa visivyoshika moto. Hilo limewawezesha kusimama imara dhidi ya majaribu wanayoendelea kuvumilia.—1 Wakorintho 3:12-14.

Sasa, baada ya kuwa New Zealand kwa zaidi ya miaka 14, ingawa miaka yetu imesonga, mimi na Aileen bado tunafurahia utumishi wetu kama mapainia wa pekee. Ndugu zangu wawili—Mike, ambaye ana umri wa miaka 94, and Peter, 90—wangali hai, wakitumikia Yehova kwa uaminifu nchini Kanada.

Mnamo 1998, binti yetu, Judy, alihamia Mashariki na ametumika huko kwa miaka fulani. Katika barua moja aliyotuandikia, alisema hivi: “Ninamshukuru Yehova sana kila siku kwa pendeleo la kutumika hapa! Asanteni nyote wawili pia kwa mazoezi ya upendo na jinsi mlivyojidhabihu na mnavyoendelea kujidhabihu ili kuwezesha mambo haya yote.” Katika mwaka wa 2003 alirudi New Zealand ili kutupa mimi na Aileen msaada tuliohitaji. *

Tunamshukuru Yehova kwamba hali zetu zimeturuhusu kuitikia mwito wa Bwana wa kutuma wafanyakazi zaidi katika mavuno. Kufanya hivyo kumetuletea furaha isiyo na kifani. Na kama Biblia inavyosema ‘ulimwengu utakapopitilia mbali,’ tutatimiziwa ahadi hii nzuri ajabu kutoka kwa Mungu: “Yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 25 Ona Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 1972 (1/6/1972), ukurasa wa 341-349 la Kiingereza.

^ fu. 32 Dada yetu mpendwa Aileen alikufa Januari 24, 2008 (24/1/2008), makala hii ilipokuwa ikikamilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Joshua ndiye aliyekuwa Shahidi pekee huko Singapore tulipofika mnamo 1947

[Picha katika ukurasa wa 29]

Pamoja na Dave Farmer huko Hong Kong, tukiwa njiani kwenda Singapore, 1947

[Picha katika ukurasa wa 29]

Pamoja na Aileen, 1958

[Picha katika ukurasa wa 31]

Pamoja na binti yetu, Judy

[Hisani]

Kimroy Photography

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 28]

Kimroy Photography