Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumia Vizuri Udadisi Wako

Tumia Vizuri Udadisi Wako

Tumia Vizuri Udadisi Wako

“Mwanadamu ni kiumbe anayeuliza maswali. Tangu tunapozaliwa tunaanza kuuliza maswali . . . Hata inaweza kusemwa kwamba historia ya mwanadamu ni historia ya maswali na majibu yetu sisi wanadamu.” —Octavio Paz, mshairi kutoka Mexico.

NI NINI kinachomchochea mpishi abuni mapishi mapya? Ni nini kinachomsukuma mvumbuzi atembelee maeneo ya mbali? Ni nini kinachofanya mtoto aulize maswali mengi sana? Mara nyingi sana ni udadisi.

Namna gani wewe? Je, mawazo mapya au tamaa ya kupata majibu ya maswali yenye kusisimua inachochea udadisi wako? Kwa mfano, Uhai unatoka wapi? Kwa nini tupo hapa? Je, kuna Mungu? Tangu utotoni, wengi wetu tumekuwa tukichochewa na udadisi kuuliza maswali kama hayo na kujitahidi kuelewa kwa nini mambo yako jinsi yalivyo. Jambo linapotupendeza, tunajitahidi juu chini kulielewa kabisa. Hivyo, udadisi unaweza kuleta matokeo mazuri ajabu. Lakini unaweza pia kuleta matatizo, au hata msiba.

Tahadhari na Usawaziko Unahitajiwa

Kwa kweli, tusipojihadhari udadisi unaweza kutuhatarisha. Kwa mfano, kwa sababu ya udadisi mtoto anaweza kushika jiko lenye moto, na matokeo yatakuwa mabaya. Kwa upande mwingine, udadisi unaweza kutuchochea kuongeza ujuzi wetu, na kutafuta majibu ya maswali yetu. Lakini je, lingekuwa jambo la hekima kuchunguza kila kitu kinachotusisimua au kuamsha udadisi wetu?

Kwa wazi, kuna ujuzi usiopendeza kwa sababu unadhuru. Udadisi kuhusu ponografia (picha au habari za ngono), uchawi, mafundisho ya madhehebu au vikundi vyenye msimamo mkali unaweza kutuingiza matatani. Kuhusu mambo hayo na mengineyo, inafaa tumwige mtunga-zaburi Mwebrania aliyesali hivi: “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa.”—Zaburi 119:37.

Pia, kuna ujuzi ambao huenda usiwe na madhara lakini hauna thamani na hauhitajiwi. Kwa mfano, kuna faida gani kupata habari zote kuhusu maisha ya kibinafsi ya wasanii au waigizaji maarufu wa sinema, kuchunguza takwimu za kila timu ya mchezo na wachezaji, au kujua kila kitu kuhusu vifaa vya karibuni au magari mapya zaidi? Kwa watu wengi, kuwa “wataalamu” katika mambo hayo hakuwaletei manufaa yoyote.

Mfano Unaochochea

Bila shaka, udadisi una faida zake. Fikiria kisa cha Mjerumani Alexander von Humboldt, mtaalamu wa vitu vya asili na mvumbuzi aliyeishi katika karne ya 19 ambaye Mto Humboldt huko Amerika Kusini uliitwa jina lake.

Pindi moja maishani mwake, Humboldt alisema: “Tangu ujana wangu nilitamani sana kutembelea maeneo ya mbali, ambayo watu wa Ulaya waliyatembelea mara chache sana.” Anasema kwamba tamaa ya kutembelea maeneo hayo ilianza alipohisi, “akili yake ikimchochea kwa njia zisizozuilika.” Akiwa na umri wa miaka 29, alienda Amerika ya Kati na ya Kusini katika safari yake ya uvumbuzi ya miaka mitano. Habari aliyokusanya aliiandika katika mabuku 30 ya rekodi ya matukio ya safari zake.

Mambo yote yalimvutia Humboldt, kutia ndani kiwango cha joto la bahari, samaki wanaoishi humo, hata mimea aliyoona. Alipanda milima, akavumbua mito, na kuabiri bahari. Utafiti wa Humboldt uliwekea msingi nyanja mbalimbali za sayansi ya kisasa. Yote hayo yalitokana na udadisi wake mwingi, na katika maisha yake yote aliendelea kuwa na tamaa isiyotoshelezwa ya kupata ujuzi. Mwandikaji Mmarekani, Ralph Waldo Emerson, alisema hivi kumhusu: “Humboldt alikuwa mmoja wa watu wa ajabu . . . wanaotokea mara kwa mara, kana kwamba wanataka kutuonyesha yale ambayo akili ya mwanadamu inaweza kufanya, nguvu na uwezo wake mbalimbali.”

Jambo Linalostahili Kuchunguzwa

Bila shaka, ni wachache sana miongoni mwetu wanaoweza kuwa wavumbuzi wa ulimwengu au kuchangia uvumbuzi wa kisayansi. Hata hivyo, tunaweza kutumia uwezo wetu wa akili kuchunguza ujuzi fulani na hivyo kupata thawabu kubwa kuliko zote. Yesu Kristo alizungumzia ujuzi huo aliposali hivi kwa Baba yake wa kimbingu: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Ujuzi juu ya Mungu wa kweli anayeitwa Yehova, na ujuzi juu ya Mwana wake, Yesu Kristo, unaweza kumletea mtu mwenye udadisi thawabu kubwa kuliko habari yoyote ile. Kumbuka maswali kuhusu maisha ambayo yalizushwa mapema. Tunaweza pia kuongeza maswali haya: Kwa nini kuna kuteseka kwingi sana ulimwenguni? Je, wanadamu wataiharibu, na hata kuiangamiza dunia? Mungu atafanya nini ili kuzuia jambo kama hilo lisitukie? Kupata majibu ya maswali hayo hakutatosheleza tu udadisi wako. Kama Yesu alivyosema, hilo litamaanisha “uzima wa milele.” Kwa nini tuamini hilo?

Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Mtume Mkristo Paulo aliandika hivi kuihusu: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17.

Hebu wazia—mtume alisema kwamba Biblia inaandaa ujuzi unaoweza kutupa vifaa au uwezo wa kufanya mambo yote yaliyo mema. Inaweza kutusaidia kuwa na maoni sawa na ya Yehova. Na tunajua kwamba ujuzi na hekima ya Mungu inapita kwa mbali ujuzi na hekima ya mtu awaye yote. Nabii Isaya aliongozwa na roho kuandika taarifa hii muhimu sana kutoka kwa Mungu: “‘Mawazo yenu si mawazo yangu, wala njia zangu si njia zenu,’ asema Yehova. ‘Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu kuliko dunia, ndivyo njia zangu zilivyo juu kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.’”—Isaya 55:8, 9.

Je, ungependa kujifunza kuhusu njia na mawazo yaliyokwezwa ya Mungu? Je, udadisi wako unakuchochea uchunguze yale ambayo Neno la Mungu, Biblia, inafundisha kuhusu njia na mawazo ya Mungu? Je, una hamu ya kujua yale ambayo Mungu atafanya ili kukomesha kuteseka kote, na pia mema atakayowafanyia wanadamu watiifu? Biblia inatoa mwaliko huu: “Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema; mwenye furaha ni mwanamume ambaye humkimbilia.”—Zaburi 34:8.

Kweli zenye nguvu za Neno la Mungu zinaweza kuwa na uvutano mkubwa juu ya moyo mnyoofu kama vile tu nuru inavyoweza kuwa na uvutano mkubwa kwa mtu anayepata kuona kwa mara ya kwanza. Mtume Paulo alisukumwa kutangaza hivi: “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika!” (Waroma 11:33) Ukweli ni kwamba kwa umilele wote hatutapata kufahamu kikamili utajiri wa ujuzi na hekima ya Mungu. Tuna tarajio lenye kusisimua la maisha yasiyochosha, kwa kuwa sikuzote tutakuwa na mambo mapya ya kujifunza.

Usiache Kuwa Mdadisi!

Ni kweli kwamba wengi wetu hawatakuwa wavumbuzi na wagunduzi maarufu. Na huenda katika maisha yetu ya wastani hatutaelewa kamwe mambo yote ambayo tungependa kuelewa. Hata hivyo, usiache kuwa mdadisi. Endelea kuchochea kiu ya ujuzi ambayo kwa upendo Mungu alituumba tukiwa nayo.

Itumie vizuri zawadi hiyo nzuri ajabu kutoka kwa Mungu, na utafute uelewaji sahihi wa Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Ukifanya hivyo, utakuwa na kusudi na shangwe maishani sasa, na utakuwa na taraja la kufanya hivyo kwa umilele wote. “[Mungu] amefanya kila kitu kiwe chenye kupendeza kwa wakati wake,” yasema Biblia. “Tena wakati usio na kipimo ameuweka ndani ya moyo wao, ili mwanadamu asiweze kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.”—Mhubiri 3:11.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

Je, Unajua Kwamba ...

• Karne nyingi kabla umbo la dunia halijatajwa na Columbus na Magellan, Biblia ilisema kwamba sayari yetu si tambarare bali ni duara?—Isaya 40:22.

• Muda mrefu kabla ya wanaanga kuitazama dunia ikining’inia angani, Biblia ilisema kwamba imetundikwa pasipo na kitu?—Ayubu 26:7.

• Angalau miaka 2,500 kabla ya daktari Mwingereza William Harvey kuvumbua mfumo wa kuzungusha damu katika mwili wa mwanadamu, Biblia iliutaja moyo kuwa chemchemi, au chanzo, cha uzima?—Methali 4:23.

• Miaka 3,000 hivi iliyopita, Biblia ilifafanua kwa maneno rahisi mzunguko wa maji kuwa mojawapo mifumo ya ekolojia inayowezesha uhai kuwepo duniani?—Mhubiri 1:7.

Je, haistaajabishi kwamba mambo hayo hakika ya kisayansi yalizungumziwa na Biblia muda mrefu sana kabla ya wanadamu kuyaelewa au kuyavumbua? Kwa kweli, katika Biblia kuna hazina yenye thamani ya habari zilizo muhimu kwa uhai, zinazosubiri tu uzivumbue.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Alexander von Humboldt