Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Amenionyesha Rehema

Mungu Amenionyesha Rehema

Mungu Amenionyesha Rehema

Limesimuliwa na Bolfenk Moc̆nik

“Jikaze sasa.” Hayo yalikuwa maneno thabiti ya Mama aliponikumbatia. Baada ya wanamgambo kututenganisha, kesi ikaanza. Mwishowe nilihukumiwa kifungo cha miaka mitano gerezani. Huenda watu wengi wangevunjika moyo. Lakini kwa kweli, mwishowe nilihisi amani nyingi ya moyoni. Acheni niwaeleze.

MATUKIO yanayotajwa hapo juu yalitukia mnamo 1952 huko Slovenia. * Lakini simulizi langu linaanza zaidi ya miaka 20 kabla, katika 1930. Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, walipanga ubatizo kwa ajili ya kikundi cha kwanza katika nchi yetu. Wazazi wangu, Berta na Franz Moc̆nik, walikuwa miongoni mwa wale waliobatizwa. Nilikuwa na umri wa miaka sita, na dada yangu, Majda, alikuwa na umri wa miaka minne. Nyumba yetu ilikuwa kituo cha utendaji wa Kikristo katika jiji la Maribor.

Adolf Hitler alianza kutawala nchini Ujerumani mnamo 1933 na akaanza kuwatesa Mashahidi. Ili kusaidia kazi ya kuhubiri, Mashahidi wengi Wajerumani walihamia Yugoslavia. Wazazi wangu walifurahia kuwakaribisha wageni waaminifu kama hao. Mgeni mmoja ninayekumbuka vizuri ni Martin Poetzinger, ambaye baadaye alifungwa kwa miaka tisa katika kambi za mateso za Nazi. Baadaye, kuanzia 1977 mpaka kifo chake katika 1988, alitumika akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.

Sikuzote alipotutembelea, Martin alilala katika kitanda changu, na mimi na dada yangu tulilala kwenye chumba kimoja na wazazi wetu. Alikuwa na ensaiklopidia ndogo yenye rangi mbalimbali ambayo ilinipendeza sana nikiwa mtoto. Nilifurahia kuangalia kurasa mbalimbali za kitabu hicho.

Wakati wa Majaribu Makali

Mnamo 1936, utawala wa Hitler ulipokuwa ukiongezeka, wazazi wangu walihudhuria kusanyiko muhimu sana la kimataifa huko Lucerne, Uswisi. Kwa kuwa Baba alikuwa na sauti tamu, wakati huo alichaguliwa arekodi hotuba za Biblia ambazo baadaye zilisikilizwa na wenye nyumba kotekote nchini Slovenia. Muda mfupi baada ya kusanyiko hilo, Mashahidi huko Ulaya walianza kuteswa vibaya. Wengi waliteswa na kufa wakiwa katika kambi za mateso za Nazi.

Katika Septemba (Mwezi wa 9) 1939, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilianza, na kufikia Aprili (Mwezi wa 4) 1941, majeshi ya Wajerumani yalikuwa yamechukua maeneo fulani ya Yugoslavia. Shule za Kislovenia zilifungwa na watu wakakatazwa kuzungumza lugha hiyo hadharani. Kwa sababu Mashahidi wa Yehova hawaungi mkono upande wowote katika mizozo ya kisiasa, walikataa kuunga mkono vita. * Kwa sababu hiyo, wengi walifungwa gerezani na wengine waliuawa—kutia ndani kijana anayeitwa Franc Drozg, ambaye nilimfahamu vizuri. Kwa kawaida, askari wa Nazi waliwapiga watu risasi karibu na nyumba yetu. Bado ninaweza kumkumbuka Mama akifunga masikio yake na kitambaa, akijaribu kuziba kelele za risasi. Maneno ya mwisho katika barua ya Franc aliyomwandikia rafiki wa karibu yalikuwa, “Tutaonana katika Ufalme wa Mungu.”

Jambo Ninalojutia Sana

Nilikuwa na umri wa miaka 19 wakati huo. Hata ingawa nilipendezwa na Franc kwa msimamo wake thabiti, niliogopa. Je, mimi pia ningekufa? Imani yangu haikuwa yenye nguvu, na sikuwa na uhusiano wa karibu na Yehova Mungu. Kisha nikaitwa niende jeshini. Woga wangu ulikuwa mwingi kuliko imani yangu, kwa hiyo nikakubali kwenda jeshini.

Nilitumwa nikapigane dhidi ya Urusi. Baada ya muda niliwaona wenzangu wakifa kwa wingi. Vita vilitisha na vilikuwa vyenye ukatili. Dhamiri yangu ilinisumbua zaidi na zaidi. Nilimwomba Yehova msamaha na nguvu ili niweze kutembea katika njia inayofaa. Shambulizi kali la kivita liliposababisha mvurugo kambini mwetu, nilipata fursa ya kutoroka.

Nilijua kwamba ikiwa ningekamatwa, ningeuawa. Katika miezi saba iliyofuata, nilijificha katika maeneo mbalimbali. Hata nilifaulu kumtumia Majda kadi yenye maneno haya: “Nimemwacha mwajiri wangu na sasa ninamfanyia mwajiri mwingine kazi.” Nilimaanisha kwamba nilitaka kumfanyia Mungu kazi sasa, lakini muda ulipita kabla ya kufanya hivyo.

Mnamo Agosti (Mwezi wa 8) 1945, miezi mitatu baada ya Wajerumani kushindwa na Majeshi ya Muungano, nilifaulu kurudi Maribor. Jambo la kupendeza ni kwamba sisi sote, yaani, baba, mama, na dada yangu, tuliokoka vita hivyo vibaya. Hata hivyo, kufikia wakati huo, Wakomunisti walikuwa mamlakani, na walikuwa wakiwatesa Mashahidi wa Yehova. Kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku, lakini Mashahidi waliendelea kuhubiri kwa siri.

Katika Februari (Mwezi wa 2) 1947, Mashahidi watatu waaminifu—Rudolf Kalle, Dus̆an Mikić, na Edmund Stropnik—walihukumiwa kifo. Hata hivyo, baadaye hukumu hiyo ilibadilishwa na kuwa kifungo cha miaka 20. Mashirika ya habari yalionyesha hayo kwa undani, na hivyo kuwafanya watu wengi wajue jinsi Mashahidi walivyotendwa isivyo haki. Baada ya kusoma habari hizo, nilichomwa moyoni. Nilitambua nilichopaswa kufanya.

Napata Nguvu za Kiroho

Nilijua vizuri sana kwamba nilihitaji kuchukua msimamo kwa ajili ya kweli za Biblia, kwa hiyo niliongeza jitihada za kutumiwa katika kazi yetu ya kuhubiri kwa siri. Kwa sababu ya kusoma Biblia kwa uangalifu, nilipata nguvu za kiroho zilizoniwezesha kuacha tabia chafu, kama vile kuvuta sigara.

Mnamo 1951, nilibatizwa ili kuonyesha wakfu wangu kwa Mungu, na hivyo nikarudia njia ya maisha niliyoacha miaka kumi hivi mapema. Mwishowe, nilianza kuhisi kwamba Yehova ni Baba wa kweli—mwaminifu, mshikamanifu, na mwenye upendo usiokoma. Ingawa nilikuwa nimefanya uamuzi mbaya nikiwa kijana, niliguswa sana na uhakikisho wa Biblia wa msamaha wa Mungu. Akiwa Baba mwenye upendo, Mungu aliendelea kunivuta “kwa kamba za upendo.”—Hosea 11:4.

Katika kipindi hicho kigumu, tulifanya mikutano ya Kikristo kwa siri katika nyumba za Mashahidi kadhaa, na tuliendelea na kazi ya kuhubiri isivyo rasmi. Hata kabla ya mwaka mmoja kwisha baada ya ubatizo wangu, nilikamatwa. Mama aliniona kwa muda mfupi kabla ya kesi yangu. Kama nilivyotaja mwanzoni, alinikumbatia kwa upendo na kunihimiza: “Jikaze sasa.” Nilipopewa hukumu ya kufungwa gerezani kwa miaka mitano, nilibaki mtulivu na thabiti.

Nilifungiwa katika chumba kidogo pamoja na wafungwa wengine watatu, kwa hiyo niliweza kushiriki kweli ya Biblia na watu ambao hawangefikiwa kwa njia nyingine. Ingawa sikuwa na Biblia au vichapo vya Biblia, nilishangaa kwamba niliweza kukumbuka maandiko na ufafanuzi wake kutokana na saa nilizotumia katika kujifunza Biblia kibinafsi. Niliwaambia wafungwa wenzangu mara kwa mara kwamba ikiwa nilihitaji kutumika gerezani kwa miaka mitano, Yehova angenipa nguvu za kufanya hivyo. Hata hivyo, huenda angefungua njia mapema. Nilijiambia, ikiwa angefanya hivyo, ni nani angeweza kufunga njia hiyo?

Kutumika Tukiwa na Uhuru wa Kadiri

Mnamo Novemba (Mwezi wa 11) 1953, serikali ilitoa msamaha; Mashahidi wa Yehova wote waliokuwa gerezani waliachiliwa. Kisha niligundua kwamba marufuku dhidi ya kazi yetu ilikuwa imeondolewa miezi miwili mapema. Mara moja tulianza kupanga upya makutaniko na kazi yetu ya kuhubiri. Tulipata mahali pa kukutania katika chumba cha chini katika jengo katikati ya Maribor. Tulibandika ishara kwenye ukuta iliyosema: “Mashahidi wa Yehova—Kutaniko la Maribor.” Shangwe ya kumtumikia Yehova kwa uhuru ilifanya mioyo yetu ifurike kwa uthamini.

Mwanzoni mwa 1961, nilianza utumishi wa wakati wote nikiwa painia. Miezi sita hivi baadaye, nilialikwa kufanya kazi katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Yugoslavia. Ilikuwa katika eneo la Zagreb, Kroatia. Wakati huo, ofisi hiyo ya tawi ilikuwa ya chumba kimoja kidogo na ndugu watatu. Wakristo wenzetu walioishi karibu walikuja mchana ili kusaidia katika kutokeza Mnara wa Mlinzi katika lugha za kienyeji.

Wanawake Wakristo walioishi karibu pia walisaidia kufanya kazi. Kati ya mambo mengine, walishona kurasa za magazeti pamoja. Nilifanya kazi mbalimbali, kutia ndani kukagua chapa, kutafsiri, kusafirisha vichapo, na kukusanya rekodi.

Mgawo Mpya

Katika 1964, nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko, kazi ambayo ilihusisha kutembelea kwa kawaida makutaniko kadhaa ya Mashahidi ili kuwaimarisha kiroho. Nilifurahia sana kazi hiyo. Wakati mwingi, nilisafiri kutoka kutaniko moja hadi lingine kwa basi au gari-moshi. Ili kuwafikia Mashahidi walioishi katika vijiji vidogo zaidi, mara nyingi nilitumia baiskeli au nikatembea, mara nyingine katika matope yaliyonifikia kwenye vifundo vya miguu.

Lakini pia kuna mambo yaliyonichekesha. Wakati mmoja, ndugu Mkristo alinipeleka kwenye kutaniko lililofuata akitumia gari lililokokotwa na farasi. Tulipokuwa tukienda kwenye barabara ya mchanga, gurudumu moja lililegea na kuanguka. Tulijikuta mchangani. Tulipokuwa tumeketi mchangani tukimtazama farasi, alituangalia kana kwamba tulikuwa tumemshangaza. Hata miaka mingi baadaye, bado tulicheka tulipokumbuka kisa hicho. Upendo usio na unafiki wa ndugu hao kwenye maeneo ya vijijini ulinipa shangwe ambayo sikuzote ninaithamini.

Katika mji wa Novi Sad, nilifahamiana na Marika ambaye alikuwa painia. Upendo wake kwa kweli ya Biblia na bidii yake katika utumishi ilinipendeza sana hivi kwamba nilitaka kumwoa. Muda fulani baada ya kuoana, tulianza kutumikia makutaniko pamoja katika kazi ya kuzunguka.

Familia yetu ilikuwa imevumilia majaribu wakati wa marufuku. Baba yangu alishtakiwa kwa uwongo kwamba alishirikiana na maadui wakati wa vita na hivyo alipoteza kazi yake. Alijaribu kwa muda mrefu bila mafanikio kurudishwa kazini na hilo lilimfanya avunjike moyo sana. Kwa muda imani yake ilififia, lakini aliifanya iwe yenye nguvu kabla ya kufa. Kufikia wakati wa kifo chake mnamo 1984, bado alikuwa mwenye bidii kutanikoni. Mama yangu mnyenyekevu na mwaminifu alikufa kabla yake katika 1965. Majda bado anatumika katika kutaniko huko Maribor.

Utumishi Nchini Austria

Katika 1972, mimi na Marika tulipata mwaliko wa kwenda nchini Austria ili kuwahubiria Wayugoslavia wengi waliohamia na kufanya kazi huko. Tulipofika Vienna, mji mkuu, hatukujua kwamba huo ungekuwa mgawo wetu wa kudumu. Muda si muda, makutaniko na vikundi vipya vilivyotumia lugha za Yugoslavia vilianzishwa kotekote nchini Austria.

Baada ya muda, nilikuwa tena mwangalizi wa mzunguko nchini humo na nikatembelea idadi iliyokuwa ikiongezeka ya makutaniko na vikundi vya lugha hizo nchini kote. Baadaye, tuliombwa tutembelee makutaniko ya lugha hizo nchini Ujerumani na Uswisi. Nilipanga makusanyiko mengi ya mzunguko na ya wilaya katika nchi hizo.

Mara kwa mara, makusanyiko hayo makubwa yalitembelewa na washiriki wa Baraza Linaloongoza, na nilikutana na Martin Poetzinger tena. Tulikumbushana matukio ya miaka 40 hivi mapema, alipokuwa akitutembelea mara nyingi nyumbani. Nilimwuliza, “Unakumbuka jinsi nilivyopenda kusoma ensaiklopidia yako ndogo?”

“Ngoja kidogo,” alisema na kuondoka. Alirudi na kitabu hicho na kunipa akisema, “Hebu shika. Hii ni zawadi kutoka kwa rafiki.” Bado ensaiklopidia hiyo ni sehemu muhimu ya maktaba yangu.

Bidii Ijapokuwa Matatizo ya Afya

Mnamo 1983, iligunduliwa kwamba nina kansa. Muda mfupi baada ya hapo, niliambiwa kwamba singepona ugonjwa wangu. Hicho kilikuwa kipindi kigumu hasa kwa Marika, lakini kwa sababu ya utunzaji wake wa upendo na msaada wa ndugu wengi Wakristo, bado ninafurahia maisha yenye kuridhisha.

Mimi na Marika tunaendelea na utumishi wa wakati wote huku Vienna. Mara nyingi, ninaenda kwenye ofisi ya tawi saa za asubuhi na kutafsiri, na Marika anakuwa na shughuli nyingi katika kuhubiri mjini. Inanifurahisha sana kuona jinsi kikundi kidogo cha wahamiaji kutoka Yugoslavia wanaoishi nchini Austria ambao wamekuwa Mashahidi kimekua na kufikia zaidi ya watu 1,300. Mimi na Marika tumekuwa na pendeleo la kusaidia wengi wao kujifunza kweli ya Biblia.

Katika miaka ya karibuni, nimekuwa na pendeleo la kushiriki katika programu za kuweka wakfu ofisi za tawi katika nchi zilizokuwa chini ya jamhuri ya Yugoslavia—moja huko Kroatia katika 1999 na nyingine huko Slovenia mnamo 2006. Nilikuwa mmoja wa Mashahidi wa zamani walioombwa washiriki mambo waliyokumbuka kuhusu mwanzo wa kazi ya kuhubiri katika nchi hizo miaka 70 hivi iliyopita.

Kwa kweli, Yehova ni Baba mwenye upendo aliye tayari kusamehe kwa njia kubwa udhaifu na makosa yetu. Ninashukuru sana kwamba haangalii makosa! (Zaburi 130:3) Ni kweli kwamba amenionyesha fadhili na rehema. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Wakati huo jamhuri sita, kutia ndani Slovenia, zilifanyiza nchi ya Yugoslavia.

^ fu. 9 Ili kujua sababu za Kimaandiko zinazowafanya Mashahidi wa Yehova wasiende vitani, ona makala “Wasomaji Wetu Wanauliza” katika ukurasa wa 22 wa gazeti hili.

^ fu. 39 Bolfenk Moc̆nik alikufa Aprili 11, 2008, makala hii ilipokuwa ikikamilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Kuanzia kushoto kuelekea kulia: Wazazi wangu, Berta na Franz Moc̆nik, Majda, na mimi, huko Maribor, Slovenia, katika miaka ya 1940

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikiwa na mke wangu, Marika