Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Kitu Kinachoweza “Kututenga na Upendo wa Mungu”?

Je, Kuna Kitu Kinachoweza “Kututenga na Upendo wa Mungu”?

Mkaribie Mungu

Je, Kuna Kitu Kinachoweza “Kututenga na Upendo wa Mungu”?

Waroma 8:38, 39

NI NANI kati yetu ambaye hahitaji kupendwa? Kwa kweli, sisi tunajihisi vizuri tunapopendwa na watu wa familia na marafiki. Hata hivyo, inasikitisha kwamba mahusiano kati ya wanadamu yanaweza kuvunjika kwa urahisi au kubadilika kulingana na hali. Wapendwa wetu wanaweza kutuumiza, kutuacha, au hata kutukataa. Lakini, kuna mtu ambaye ana upendo wa kudumu. Upendo ambao Yehova Mungu anawaonyesha waabudu wake unaelezewa vizuri katika Waroma 8:38, 39.

“Nimesadiki,” anasema mtume Paulo. Amesadiki nini? Kwamba hakuna kitu kinachoweza “kututenga na upendo wa Mungu.” Paulo hakuwa akisema kuhusu yeye mwenyewe tu bali pia kuhusu sisi, yaani, kuhusu wote wanaomtumikia Mungu kwa ushikamanifu. Ili kukazia jambo hilo, Paulo anaorodhesha mambo kadhaa ambayo hayawezi kuuzuia upendo wa Yehova usiwafikie watumishi wake wenye bidii.

“Wala kifo wala uzima.” Yehova haachi kuwapenda watu wake wanapokufa. Ili kuthibitisha upendo wake, Mungu anahifadhi watu hao katika kumbukumbu lake, naye atafanya wawe hai katika ulimwengu mpya unaokuja wenye uadilifu. (Yohana 5:28, 29; Ufunuo 21:3, 4) Kwa sasa, upendo wa Mungu kwa waabudu wake waaminifu haubadiliki hata wanapokabili hali mbalimbali katika mfumo huu.

“Wala malaika wala serikali.” Wanadamu wanaweza kuathiriwa na uvutano kutoka kwa watu wenye nguvu au wenye mamlaka, lakini Yehova hawezi. Viumbe wa roho wenye nguvu, kama malaika aliyekuja kuwa Shetani, hawawezi kumshawishi Mungu aache kuwapenda waabudu wake. (Ufunuo 12:10) Hata serikali ambazo huenda zikawapinga Wakristo wa kweli, haziwezi kubadili maoni ya Mungu kuhusu watumishi wake.—1 Wakorintho 4:13.

“Wala mambo yaliyopo sasa wala mambo yatakayokuja.” Upendo wa Mungu haufifii kadiri wakati unavyopita. Hakuna kitu kinachoweza kuwapata watumishi wake sasa au wakati ujao kitakachomfanya Mungu aache kuwapenda.

“Wala nguvu.” Tayari Paulo amezungumza kuhusu uvutano wa kimbingu na wa kidunia, yaani, “malaika” na “serikali,” lakini sasa anataja kuhusu “nguvu.” Neno la Kigiriki linalotumiwa hapa lina maana pana. Hata liwe linamaanisha nini, jambo moja ni hakika: Hakuna nguvu mbinguni au duniani inayoweza kufanya upendo wa Yehova usiwafikie watu wake.

“Wala kimo wala kina.” Yehova anawapenda watu wake ingawa wana viwango mbalimbali vya maisha, iwe wanaishi maisha ya hali ya juu au ya chini.

“Wala uumbaji mwingine wowote.” Kwa maneno hayo yanayotia ndani kila kitu, Paulo anasema kwamba hakuna kitu chochote kinachoweza kuwatenga waabudu washikamanifu na upendo wa Yehova.

Tofauti na upendo wa mwanadamu ambao unaweza kubadilika au kufifia, upendo wa Mungu kuelekea wale wanaomwamini kabisa hauwezi kubadilika; upendo huo ni wa milele. Bila shaka, kujua hilo kunatuchochea kumkaribia Yehova na kutufanya tujitahidi kabisa kuthibitisha kwamba tunampenda.