Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Karibuni Dunia Itakuwa Paradiso!

Karibuni Dunia Itakuwa Paradiso!

Karibuni Dunia Itakuwa Paradiso!

“Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10, Union Version.

SALA hiyo maarufu inayojulikana na wengi kuwa sala ya Baba Yetu au Sala ya Bwana, inawatolea wanadamu tumaini. Jinsi gani?

Kama vile Sala ya Bwana inavyoonyesha, Ufalme wa Mungu utafanya mapenzi ya Mungu yatimizwe duniani kama yanavyotimizwa mbinguni sasa. Na ni mapenzi ya Mungu kwamba dunia ifanywe tena kuwa Paradiso. (Ufunuo 21:1-5) Ufalme wa Mungu ni nini hasa, na utarudisha Paradiso duniani jinsi gani?

Serikali Halisi

Ufalme wa Mungu ni serikali halisi. Ili serikali ifanye kazi, inahitaji kuwa na watawala, sheria, na raia. Je, Ufalme wa Mungu una mambo hayo yote? Hebu ona jinsi Biblia inavyojibu maswali haya matatu:

Ni nani watawala wa Ufalme wa Mungu? (Isaya 33:22) Yehova Mungu amemweka rasmi Mwana wake, Yesu Kristo, asimamie Ufalme huo. (Mathayo 28:18) Chini ya uongozi wa Yehova, Yesu amechagua idadi ndogo ya watu kutoka “kila kabila na lugha na watu na taifa” ambao watatawala pamoja naye wakiwa “wafalme juu ya dunia.”—Ufunuo 5:9, 10.

Ufalme wa Mungu umewawekea raia zake sheria gani? Baadhi ya sheria au amri hizo zinadai kwamba raia wafanye matendo fulani. Yesu alitaja sheria muhimu zaidi kati ya hizo aliposema: “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza. Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’”—Mathayo 22:37-39.

Sheria nyingine zinadai kwamba raia wa Ufalme wa Mungu wajiepushe na matendo fulani. Kwa mfano, Biblia inasema hivi waziwazi: “Msidanganyike! Watu wanaoishi maisha ya uasherati, wanaoabudu sanamu, wazinzi, au walawiti, wezi, wachoyo, walevi, wasengenyaji, wanyang’anyaji, hao wote hawataushiriki ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10, Biblia Habari Njema.

Ni nani raia wa Ufalme wa Mungu? Yesu aliwafananisha raia wa Ufalme wa Mungu na kondoo. Alisema: “Wataisikiliza sauti yangu, nao watakuwa kundi moja, mchungaji mmoja.” (Yohana 10:16) Ili awe raia wa Ufalme wa Mungu, mtu hapaswi tu kusema kwamba anamfuata Mchungaji Mwema, Yesu, bali anapaswa pia kufanya yale anayoamuru. Yesu alisema: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia.”—Mathayo 7:21.

Hivyo, wale ambao ni raia wa Ufalme wa Mungu wanatumia na kuheshimu jina la Mungu, Yehova, kama Yesu alivyofanya. (Yohana 17:26) Wanatii amri ya Yesu ya kuwafundisha wengine kuhusu “hii habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Na wanaonyeshana upendo wa kweli.—Yohana 13:35.

“Kuwaharibu Wale Wanaoiharibu Dunia”

Hali za ulimwengu zinaonyesha kwamba Ufalme wa Mungu utachukua hatua hivi karibuni ili kutokeza mabadiliko makubwa duniani. Tunajua jambo hilo jinsi gani? Miaka elfu mbili iliyopita, Yesu alitaja ishara yenye mambo mengi ambayo ingeonyesha kwamba “ufalme wa Mungu uko karibu.” (Luka 21:31) Kama tulivyoona katika habari iliyotangulia, sehemu mbalimbali za ishara hiyo zinaonekana wazi ulimwenguni pote.

Ni nini kitakachotukia baada ya hapo? Yesu anajibu hivi: “Ndipo kutakapokuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:21) Huo si msiba unaoletwa na wanadamu. Badala yake, ni tendo la Mungu la “kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia.” (Ufunuo 11:18) Watu waovu ambao matendo yao ya ubinafsi karibu yaiharibu dunia, “watakatiliwa mbali kutoka duniani.” Lakini wasio na lawama ambao wanamtumikia Mungu kwa njia inayofaa “ndio watakaobaki ndani yake.”—Methali 2:21, 22.

Yehova Mungu ana haki ya kuchukua hatua hiyo kali. Kwa nini? Fikiria mfano huu: Wazia una nyumba za kukodisha. Wapangaji fulani wana adabu na ufikirio; wanalipa kodi na wanatunza nyumba vizuri. Hata hivyo, wapangaji wengine wanavuruga na ni wenye ubinafsi; wanakataa kulipa kodi na wanaharibu nyumba. Ingawa unawaonya mara kadhaa, wanaendelea na mwenendo wao mbaya. Ungefanya nini? Ukiwa mwenye nyumba, bila shaka ungewafukuza.

Vivyo hivyo, Yehova Mungu akiwa Muumba wa dunia na vyote vilivyomo, ana haki ya kuamua ni nani atakaowaruhusu waishi kwenye sayari hii. (Ufunuo 4:11) Kusudi la Yehova lililofunuliwa ni kuwaondoa watu waovu ambao wanapuuza mapenzi yake na kuingilia haki za wengine.—Zaburi 37:9-11.

Kurudishwa kwa Paradiso

Hivi karibuni, Ufalme wa Mungu ukiongozwa na Yesu Kristo utatawala dunia. Yesu aliuita mwanzo huo mpya “kutengenezwa upya [kwa] ulimwengu.” (Mathayo 19:28, Verbum) Hali zitakuwa namna gani? Hebu fikiria ahadi zifuatazo za Biblia:

Zaburi 46:9. “Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.”

Isaya 35:1. “Nyika na nchi isiyo na maji itafurahi; na nchi tambarare ya jangwani itakuwa na shangwe na kuchanua maua kama zafarani.”

Isaya 65:21-23. “Watu wangu waliochaguliwa wataitumia kazi ya mikono yao wenyewe kikamilifu. Hawatafanya kazi ya bure, wala hawatazaa kwa ajili ya kupata usumbufu.”

Yohana 5:28, 29. “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Yesu] na kutoka.”

Ufunuo 21:4. “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”

Sababu za Kuamini

Je, unaamini ahadi za Biblia? Biblia ilitabiri kwamba watu wengi hawangeziamini. Inasema: “Katika siku za mwisho watakuja wadhihaki . . . wakiendelea kulingana na tamaa zao wenyewe na kusema: ‘Huku kuwapo kwake kulikoahidiwa kuko wapi? Kwani, tangu siku mababu zetu walipolala katika kifo, mambo yote yanaendelea sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.’” (2 Petro 3:3, 4) Lakini wadhihaki hao wamekosea kama nini! Fikiria sababu nne tu kwa nini unaweza kuamini kile ambacho Biblia inasema:

(1) Wakati uliopita Mungu aliingilia mambo ya dunia. Mfano mzuri ni Gharika ya siku za Noa.—2 Petro 3:5-7.

(2) Neno la Mungu lilitabiri kwa usahihi hali tunazoona duniani.

(3) Mambo yote ‘hayaendelei sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.’ Sayari yetu inaharibiwa kijamii, kiadili, na kimazingira kwa kiwango ambacho hakijawahi kutukia tena.

(4) “Habari njema ya ufalme” inahubiriwa duniani pote, na hilo linaonyesha kwamba ‘ule mwisho utakuja’ karibuni.—Mathayo 24:14.

Mashahidi wa Yehova wanakualika ujifunze Neno la Mungu, Biblia, pamoja nao ili ujifunze mengi kuhusu tumaini la uzima wa milele chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. (Yohana 17:3) Ndiyo, wanadamu wanatarajia kuwa na wakati ujao mzuri. Hivi karibuni kutakuwa na hali nzuri ajabu! Je, utakuwapo wakati huo?

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Wale ambao sikuzote wamesema kwamba mambo hayatabadilika wamekosea sana

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Je, utakuwapo chini ya hali hizi nzuri?