Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Baba Yetu wa Mbinguni Ana Utu wa Aina Gani?

Baba Yetu wa Mbinguni Ana Utu wa Aina Gani?

Baba Yetu wa Mbinguni Ana Utu wa Aina Gani?

WATU wengi wanaweza kukariri sala ya Baba Yetu au Sala ya Bwana, sala ambayo Yesu aliwafunza wanafunzi wake. (Mathayo 6:9-13) Kila wakati wanaposema sala hiyo, wanamwita Mungu “Baba Yetu.” Hata hivyo, ni wangapi wanaoweza kusema wanamfahamu vizuri?

Namna gani wewe? Unamfahamu Mungu vizuri kadiri gani? Je, una uhusiano wa karibu pamoja naye, unaongea naye, na kumweleza mambo yanayokufurahisha na yale yanayokuhuzunisha? Kwa kweli, kumfahamu kunahusisha nini?

“Yehova Ndilo Jina Lake”

Huenda jambo pekee ambalo mtoto akawa anajua kumhusu baba yake ni kwamba anaitwa Baba. Hata hivyo, anapoendelea kukua, anafahamu jina na sifa za baba yake na inaelekea anajivunia kuwa mwana wake. Namna gani kuhusu Mpaji-Uhai wetu aliye mbinguni? Je, unajua jina lake la kibinafsi na maana ya jina hilo?

Ingawa wengi wanasema “Jina lako litukuzwe” wanapokariri Sala ya Bwana, huenda wasiweze kujibu wanapoulizwa, “Hilo ni jina gani?” (Union Version) Tunapata uthibitisho wa kuwepo kwa Mungu tunapotazama mbingu zenye nyota nyingi, mlima mkubwa, au matumbawe yenye rangi zinazopendeza zilizo na viumbe wengi. Lakini, vitu hivyo havituambii jina lake. Ili tujifunze jina hilo, tunahitaji kuichunguza Biblia. Inasema hivi kwa usahihi: “Yehova ndilo jina lake.”—Kutoka 15:3.

Mungu anataka tumjue kwa jina lake, Yehova. Kwa nini? Kwa sababu jina lake linawakilisha utu wake. Jina hilo linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Kwa maneno mengine, anakuwa chochote kinachohitajika ili kutimiza kusudi lake. Ili tuelewe jambo hilo, fikiria mfano huu: Ili kutunza familia yake, baba anatafuta riziki, anakuwa mshauri, hakimu, mpatanishi, mlinzi, na mwalimu, ikitegemea mahitaji na hali za familia yake. Kwa njia hiyohiyo, jina Yehova linatuhakikishia kwamba Mungu ana uwezo kamili wa kutekeleza mapenzi yake ili kuwabariki wote wanaomtumikia chini ya hali zozote zile.

Acheni tuchunguze majukumu mbalimbali ambayo Mungu wetu mwenye upendo anatimiza kupatana na maana ya jina lake. Hilo litakusaidia kuthamini Yehova ni Mungu wa aina gani, na pia kujifunza kile unachopaswa kufanya ili umkaribie.

“Mungu wa Upendo na wa Amani”

Mtume Paulo alimwita Mtengenezaji wetu “Mungu wa upendo na wa amani.” (2 Wakorintho 13:11) Kwa nini? Yesu Kristo alikuwa amesema hivi mapema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Kwa sababu aliwapenda wanadamu sana, Mungu alimtoa Mwana wake mpendwa kuwa fidia na hivyo kuwawezesha wale wanaomwamini kufurahia maisha yasiyo na mwisho bila maumivu na mateso yanayotokana na dhambi. Hiyo ndiyo sababu Paulo alisema hivi pia: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 6:23) Je, hilo halipaswi kutuchochea tumpende Mungu na kumkaribia?

Mungu haonyeshi upendo wake tu kwa wanadamu wote kwa ujumla, bali pia kwa watu mmoja-mmoja waaminifu. Musa aliwaambia hivi Waisraeli wa kale ambao mara nyingi walipotoka: “Je, Yehova ndiye mnayeendelea kumfanyia hivi, Enyi watu wajinga na ambao hawana hekima? Je, yeye si Baba yenu aliyewazaa, yeye aliyewafanyiza ninyi na kuwaimarisha?” (Kumbukumbu la Torati 32:6) Je, unaelewa maana ya maneno hayo? Kama Baba mwenye upendo, Yehova aliwajali watu wake ingawa alijua udhaifu wao. Naye aliwatimizia mahitaji yao ya lazima, ya kimwili, ya kihisia, na ya kiroho.

Maishani, sisi sote tunakabili matatizo mbalimbali na mara nyingine tunafadhaika, au hata kushuka moyo. Tunahitaji mtu anayeweza kutusaidia kuelewa hali na matatizo yetu. Ni nani anayeweza kutusaidia? Kupitia Neno lake Biblia, Yehova anathibitika kuwa Mshauri na Mtunzaji mwenye upendo. Kitabu hicho Kitakatifu kinaeleza kwa nini tunateseka na jinsi tunavyoweza kukabiliana kwa mafanikio na matatizo hayo. Kama vile tu baba mwenye upendo anavyomsaidia mwanaye ambaye ameanguka na kujiumiza, kwa upendo wake mkubwa, Yehova anainama kitamathali na kutupa msaada tunaohitaji. Kwa kweli, mkono wa Yehova si mfupi kuelekea watu wanaomwamini.—Isaya 59:1.

Mungu pia anatuonyesha upendo wake kwa kuwa “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Jinsi gani? Mtume Paulo anaeleza hivi: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Unaposali kwa Mungu kutoka moyoni na kufuata mwongozo anaotoa katika Neno lake, wewe pia unaweza kuhisi “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.”

“Mungu wa Ujuzi”

Biblia inamfafanua Yehova Mungu kuwa “mkamilifu katika ujuzi.” Akiwa “Mungu wa ujuzi,” anaelewa vizuri utu wa wanadamu na mahitaji yao kuliko mtu mwingine yeyote. (Ayubu 36:4; 1 Samweli 2:3) Kupitia mtumishi wake Musa, aliwajulisha watu kwamba “mwanadamu haishi kwa mkate tu bali mwanadamu huishi kwa kila neno la kinywa cha Yehova.” (Kumbukumbu la Torati 8:3; Mathayo 4:4) Hiyo inamaanisha kwamba ili turidhike kikweli maishani, hatuhitaji vitu vya kimwili tu.

Muumba wetu anatuandalia mwongozo na mashauri yenye thamani kupitia Neno lake, Biblia. Tunapojifunza Biblia na kutumia shauri lake maishani mwetu, tunafaidika kutokana na “kila neno la kinywa cha Yehova.” Kwa mfano, Zuzanna, mwanamke Mkristo, alisema hivi kuhusu familia yake: “Ndoa yetu iliimarika kwa sababu tulisoma Biblia pamoja, tukahudhuria mikutano ya Kikristo pamoja, na tukawaambia wengine mambo tuliyojifunza. Kwa sababu ya mwongozo wa kiroho kutoka kwa Mungu, tuna miradi inayofanana na tunafurahia uhusiano wenye nguvu zaidi.”

Je, ungependa kufaidika na mashauri ya kiroho na mwongozo kutoka kwa Mungu? Kwa kujifunza Biblia kwa ukawaida na kutumia mashauri yake, utapata baraka nyingi za kiroho kutoka kwa Mungu.—Waebrania 12:9.

‘Mungu wa Wokovu’

Kuna matatizo mengi sana ulimwenguni leo. Hatujui maisha yatakuwa namna gani kesho. Ikiwa unaishi katika nchi yenye vita, huenda unatamani kuwe na amani. Katika sehemu nyingine nyingi za ulimwengu, watu wanaishi wakiogopa uhalifu na jeuri, hali mbaya za kiuchumi, na ugaidi. Ni nani atakayetukomboa kutokana na mambo yote hayo? Sasa, kuliko wakati mwingine wowote, wanadamu wanahitaji ulinzi na ukombozi.

“Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi,” inasema Biblia. (Methali 18:10) Kufahamu jina la Mungu na kulitegemea kunaweza kutufanya tufikirie kile alichofanya na kile atakachofanya ili kuwakomboa wale wanaomwamini. Yehova Mungu amethibitisha kwamba bila shaka anaweza kuwakomboa watu wake. Kwa mfano, aliwakomboa Waisraeli kwa kuharibu magari ya Farao ya vita na majeshi yake. Yehova alithibitika kuwa Mungu wa uaminifu, Mungu anayewakumbuka wanaoteseka, na anayetamani kuwakomboa.—Kutoka 15:1-4.

Pia, wakati wetu ujao wa milele unategemea kumwamini Yehova Mungu kuwa Mwokozi. Mfalme Daudi wa Israeli la kale, ambaye alikabili matatizo mengi, alionyesha imani ya aina hiyo alipoandika hivi kumhusu Yehova: “Wewe ni Mungu wangu wa wokovu.” (Zaburi 25:5) Mtume Petro aliandika hivi kwa uhakika: “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.”—2 Petro 2:9.

Kuhusu mtu anayemtegemea ili kupata msaada, Mungu ameahidi hivi: “Nitamlinda kwa sababu amelijua jina langu.” (Zaburi 91:14) Watumishi wa Mungu wa nyakati za sasa wamejionea ahadi hiyo ikitimia. Licha ya hali ngumu na mateso, Henryk anayeishi Poland, amemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka 70. Henryk alipokuwa na umri wa miaka 16, baba yake alifungwa katika kambi ya mateso ya Auschwitz. Henryk na ndugu yake walipelekwa kwenye shule ya Wanazi ya kurekebisha tabia za watoto. Baada ya hapo, alifungwa katika kambi mbalimbali za mateso. Kuhusu matukio ya siku hizo, Henryk anakumbuka: “Katika hali zangu zote ngumu, Yehova hakuniacha kamwe. Sikuzote alinisaidia kubaki mwaminifu, hata ingawa nyakati fulani nilikuwa karibu kufa.” Ndiyo, Yehova anawapa watumishi wake imani na nguvu za kuvumilia.

Hivi karibuni, Mungu atathibitika kuwa Mwokozi kwa wale wanaomwamini na wanaomtegemea awaokoe. Anasema hivi: “Mimi ni Yehova, na zaidi ya mimi hakuna mwokozi.” (Isaya 43:11) Katika “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” atawaangamiza waovu wote kutoka duniani na kuwakomboa wanyoofu. (Ufunuo 16:14, 16; Methali 2:21, 22) Yehova anatuhakikishia hivi: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.

Kuwa “Watoto wa Mungu”

Katika siku za nabii Malaki, Waisraeli walidai kwamba Yehova ni Baba yao. Hata hivyo, walipohitajiwa kumwonyesha heshima na ujitoaji, wao walimtolea dhabihu mkate uliotiwa unajisi na wanyama waliokuwa vipofu na vilema. Hiyo ndiyo sababu Yehova aliwauliza hivi: “Ikiwa mimi ni baba, iko wapi heshima yangu?”—Malaki 1:6.

Usifanye kosa lilelile ambalo Waisraeli hao wasio waaminifu walifanya. Badala yake, tunakutia moyo ujifunze kumhusu Yehova Mungu na umkaribie. “Mkaribieni Mungu,” akahimiza mwanafunzi Yakobo, “naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.

Ikiwa unataka Yehova awe Baba yako ni lazima utimize wajibu fulani. Ukijitahidi kumheshimu Mungu kwa kufuata viwango vyake kwa uaminifu katika kila sehemu ya maisha yako, hatasahau kamwe jitihada zako. Badala yake, atakusaidia utembee kwenye barabara iliyonyooka inayoongoza kwenye ulimwengu mpya ulioahidiwa ambamo “kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Wakati huo, wanadamu wote watiifu ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’—Waroma 8:21.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Mungu anataka tumjue kwa jina lake, Yehova, ambalo linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa”

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Katika hali zangu zote ngumu, Yehova hakuniacha kamwe.”—HENRYK

[Blabu katika ukurasa wa 7]

“Ndoa yetu iliimarika kwa sababu tulisoma Biblia pamoja, tukahudhuria mikutano ya Kikristo pamoja, na tukawaambia wengine mambo tuliyojifunza.”—ZUZANNA