Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dunia Ina “Homa” Je, Kuna Tiba?

Dunia Ina “Homa” Je, Kuna Tiba?

Dunia Ina “Homa” Je, Kuna Tiba?

DALILI zinaonekana, joto linaongezeka. Mfano mmoja ni kijiji cha Newtok huko Alaska, kilicho upande wa kusini wa Mzingo wa Aktiki. Udongo uliokuwa umeganda wa kijiji cha Newtok umeanza kuyeyuka. “Sitaki kuishi [tena] kwenye eneo lililo na udongo uliogandamana,” akalalamika mkaaji anayeitwa Frank. “Kuna matope mengi sana.” Uchunguzi unaonyesha kwamba katika muda wa miaka kumi, huenda kijiji hicho cha pwani kitafagiliwa mbali.

Kamati ya Serikali Mbalimbali Kuhusu Mabadiliko ya Hali ya Hewa (IPCC) ilifikia kauli hii: “Hatuwezi kupinga kwamba joto linaongezeka katika mfumo wa hali ya hewa.” Hilo linaonekana kutokana na kuongezeka kwa kiwango cha joto duniani. Kile ambacho wanasayansi wanaita badiliko la hali ya hewa kimetokeza hali mbaya sana ya hewa kutia ndani, ukame, mvua nyingi sana, vipindi vya joto kali, na vimbunga ulimwenguni pote. Ni nini kitakachoipata sayari yetu? Je, kuna tiba?

Kupima “Ugonjwa” wa Dunia

Kama mgonjwa aliye hospitalini, dalili muhimu za dunia zinachunguzwa kwa makini na wanasayansi wa hali ya hewa. Satelaiti zinachunguza kupungua kwa miamba ya barafu, vituo vya hali ya hewa vinapima na kurekodi kiwango cha mvua, boya zinapima kiwango cha joto cha sehemu za ndani sana za bahari, ndege zinachunguza viwango vya gesi hewani. Habari hizo nyingi za hali ya hewa zinaingizwa kwenye kompyuta zenye uwezo mkubwa. Mfumo wa hali ya hewa ya wakati uliopita unachunguzwa ili kutabiri mambo yatakayotokea makumi ya miaka, hata karne kadhaa, zinazokuja.

Vipimo vinasema nini? Watu fulani wanaamini kwamba anga limejaa gesi zinazoongeza kiwango cha joto. Katika mwaka wa 2006 peke yake, kiwango cha kaboni dioksidi kilichotokezwa duniani “kilikuwa karibu tani bilioni 32,” linasema gazeti moja (Time). Kama vioo vinavyotumiwa kwenye banda la kukuzia maua, gesi hizo zinanasa joto la dunia, na kulizuia lisipenye angani, hivyo kuchangia katika ongezeko la joto duniani. Ni nini kitakachotukia wakati ujao? Kulingana na IPCC, ikiwa kiwango cha gesi kitaendelea kutokezwa kama ilivyo wakati huu, kutakuwa na “mabadiliko mengi katika hali ya hewa ya dunia,” ambayo yatakuwa mabaya zaidi kuliko yale yametokea. Wengi wanaamini kwamba suluhisho ni kudhibiti kiwango cha kaboni dioksidi kinachotokezwa. Hata hivyo, ikiwa kiwango cha gesi zinazotokezwa kitadhibitiwa, matokeo ya kompyuta yanaonyesha kwamba huenda “ongezeko la kiwango cha joto linasababisha kuongezeka kwa kiwango cha maji baharini na hilo linaweza kuendelea kwa karne kadhaa.”

Majibu Yanapatikana Wapi?

Ni kweli kwamba elimu ya kutabiri hali ya hewa ni tata. “Kwa mfano, kiwango cha joto Duniani kinapoendelea kuongezeka kitaathiri namna gani mawingu? Je, mawingu yaliyo juu sana yanayofyonza joto ambayo huenda yakaongeza kiwango cha joto yatakuwa mengi kuliko mawingu mazito yanayozuia miale ya jua?” kinauliza kichapo kimoja (Earth Observatory). Jibu ni nini? “Kwa sasa, wanasayansi hawawezi kujibu maswali hayo.”

Kwa upande mwingine, Biblia inatuhakikishia kwamba Yehova Mungu ndiye “aliyezitokeza mbingu na dunia,” kutia ndani “mawingu makubwa yaliyo juu.” (Mwanzo 14:19; Methali 8:28) Alijifafanua kwa njia ya kitamathali kuwa ameweka “hekima katika tabaka za mawingu.” Ndiyo, Yehova anaelewa vizuri mambo ambayo wanasayansi hawawezi.—Ayubu 38:36.

Kuhusu hali ya anga ya dunia, hebu ona yale ambayo Mungu alisema, kama ilivyorekodiwa kwenye Biblia miaka 2,700 hivi iliyopita: “Mvua inayonyesha hushuka . . . kutoka mbinguni nayo hairudi mahali pale, mpaka kwa kweli iwe imeinywesha dunia.” (Isaya 55:10) Hilo linafafanua vizuri kama nini mzunguko wa maji! Mvuke wa maji katika mawingu yanabadilika na kuwa matone kisha yananyesha kama mvua, ambayo ‘inainywesha dunia.’ Joto la jua linafanya unyevunyevu uvukizwe na ‘kurudi mahali pale,’ yaani, angani, ili kuanza tena mzunguko wa maji. Neno la Yehova lilitoa habari zenye kusisimua kuhusu mfumo wa hali ya hewa wa dunia karne nyingi kabla ya wanadamu kuandika vitabu kuhusu jambo hilo. Je, hilo halikufanyi uwe na hakika katika Muumba na uwezo wake? Kwa hiyo, kuhusu matokeo ya hali ya hewa ya wakati huu, je, si jambo linalopatana na akili kwetu kumtegemea “Muumba wa upepo,” na ‘baba wa mvua,’ ambaye anajua muundo wa sayari yetu?—Amosi 4:13; Ayubu 38:28.

Dunia Iliumbwa kwa Kusudi

Ingawa maoni ya watu yanatofautiana kuhusu wakati ujao wa dunia, jambo moja ni hakika: Dunia ni ya pekee. Tofauti na sayari zingine, ina unamna-namna wa uhai. Ni nini kinachowezesha hilo? Wanasayansi wanatoa sababu kadhaa. Zinatia ndani, dunia ina kiwango kikubwa cha maji; iko kwenye umbali unaofaa kutoka kwa jua; na ina mchanganyiko unaofaa wa gesi kwenye anga lake, kutia ndani kiwango kikubwa cha oksijeni.

Huenda ukashangaa kujua kwamba kitabu cha Biblia cha Mwanzo kinarejelea mambo hayo katika simulizi la uumbaji. Kwa mfano, Mwanzo 1:10 inafafanua Mungu akikusanya ‘maji aliyoyaita Bahari’—maneno hayo yakionyesha wazi maji mengi sana. Kwenye Mwanzo 1:3, tunasoma hivi: “Mungu akasema: ‘Kuwe na nuru.’” Sayari yetu iko umbali unaofaa kutoka kwa jua hivi kwamba maji yake mengi hayagandi, lakini haiko karibu sana hivi kwamba maji yote yavukizwe angani.

Mwanzo 1:6 inasema kwamba Mungu alitokeza “anga.” Kisha, mistari ya 11 na 12 inaeleza Mungu akitokeza nyasi, mimea, na miti. Mambo yote hayo ni uthibitisho wa kuwepo kwa oksijeni ambayo baadaye ingewezesha wanadamu na wanyama waendeleze uhai wao kwa kupumua.

Kwa hiyo, tunaweza kufikia mkataa gani? Mungu alipoiumba dunia ikiwa na maji mengi, ikiwa umbali unaofaa kutoka kwa jua, na ikiwa na mchanganyiko unaofaa wa gesi, bila shaka alikuwa na sababu na kusudi. Biblia inatuambia: “[Mungu] hakuiumba [dunia] tu bila sababu, . . . aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) “Mbingu ni mbingu za Yehova,” inasema Zaburi 115:16, “bali dunia amewapa wana wa binadamu.” Ndiyo, dunia iliumbwa ili ikaliwe na wanadamu.

Kulingana na Maandiko, Mungu aliumba mwanamume na mwanamke wa kwanza na kuwaweka katika bustani ya Edeni, paradiso maridadi sana. Walipaswa ‘kuilima na kuitunza.’ (Mwanzo 2:15) Mungu pia aliwaambia: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” (Mwanzo 1:28) Hebu fikiria taraja zuri walilokuwa nalo! Walipaswa kupanua mipaka ya Paradiso duniani pote na kuishi milele ndani yake. Ulikuwa wakati ujao mzuri kama nini!

Kwa kusikitisha, badala ya kumtii Mungu, wanadamu hao wa kwanza walichagua kumwasi na kufuata mwendo wa kujitegemea ambao wanadamu wengi wanafuata hadi leo. (Mwanzo 3:1-6) Matokeo yamekuwa nini? Badala ya kuilima na kuitunza, wanadamu ‘wanaiharibu dunia’ kwa kiwango kikubwa sana. (Ufunuo 11:18) Hata hivyo, tunaweza kufarijika kujua kwamba kusudi la Mungu kwa dunia halijabadilika. Biblia inatuhakikishia hivi: “[Mungu] ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Na Yesu mwenyewe aliahidi hivi kwenye Mahubiri ya Mlimani: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Hilo litatimizwa jinsi gani?

Tunatarajia Wakati Ujao Mzuri

“Mabadiliko ya hali ya hewa ni tatizo la duniani pote,” alisema rais mmoja wa zamani wa Marekani. Je, hukubali kwamba suluhisho la duniani pote linahitajika? Yesu Kristo alisema kwamba suluhisho hilo ni Ufalme wa Mungu. Aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Ufalme wako na uje.” (Mathayo 6:9, 10) Kulingana na unabii wa Biblia, Ufalme huo wa mbinguni ni serikali ya duniani pote ambayo hivi karibuni ‘itazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [serikali zilizopo].’ (Danieli 2:44) Zaidi ya hilo, ‘itawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Ni wazi kwamba wale wanaoiharibu dunia na kutumia vibaya mali zake za asili watahukumiwa na kuharibiwa.

Hata hivyo, ni nini kitakachoipata sayari yetu iliyochafuliwa? Jambo moja tunalopaswa kutambua ni kwamba Yesu alipokuwa duniani alitumia nguvu za kimuujiza kudhibiti nguvu za asili, kama vile upepo na bahari. Alinyamazisha dhoruba kali kwa maneno machache. (Marko 4:35-41) Akitawala mbinguni akiwa “Bwana wa mabwana na Mfalme wa wafalme,” Yesu ataidhibiti dunia na nguvu zake za asili kwa njia kubwa zaidi. (Ufunuo 17:14) Yesu hata aliufafanua utawala wake kuwa “uumbaji-mpya.” (Mathayo 19:28) Tafsiri nyingine inasema “kutengenezwa upya ulimwengu.” (Verbum Bible) Yesu ataumba upya, au kutengeneza upya hali za dunia, akizifanya ziwe kama zile zilizokuwako katika bustani ya Edeni. Paradiso itarudishwa. (Luka 23:43) “Homa” ya dunia itaponywa na Ufalme wa Mungu.

Hata sasa, unaweza kunufaika kutokana na utawala wa Ufalme. Jinsi gani? Yesu alitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Kwa sababu ya kazi hiyo ya kuhubiri, mamilioni wanatenda kupatana na habari njema. Maisha ya watu wengi yanabadilishwa. Watu wameachana na uraibu unaohatarisha. Maisha ya familia yameboreshwa. Watu wameanza kuwapenda watu wa rangi tofauti badala ya kuwachukia. Kwa kweli, Ufalme wa Mungu unatimiza kile ambacho hakuna serikali ya wanadamu inaweza kutimiza. Ufalme huo umeunganisha karibu watu milioni saba kutoka nchi zaidi ya 235 kuwa undugu wa kweli wa kimataifa! Ndiyo, wakiwa raia wa Ufalme wa Mungu, wao wanatayarishwa waishi milele katika Paradiso juu ya sayari hii.

Wakati ujao wa dunia ni salama. Tunatumaini kwamba hata wewe utakuwa na wakati ujao kama huo!

[Picha katika ukurasa wa 27]

Biblia ilifafanua mzunguko wa maji wa dunia karne nyingi kabla ya wanadamu kuandika vitabu kuhusu jambo hilo

[Picha katika ukurasa wa 28]

Yesu “akaukemea upepo na kuiambia bahari: ‘Nyamaza, utulie!’ Na upepo ukapunguka, kukawa utulivu mkubwa”

[Picha katika ukurasa wa 29]

Paradiso itakaporudishwa, “homa” ya dunia itaponywa

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]

Godo-Foto