Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Wakristo wa Mapema Walivyoandika Maandishi Matakatifu

Jinsi Wakristo wa Mapema Walivyoandika Maandishi Matakatifu

Jinsi Wakristo wa Mapema Walivyoandika Maandishi Matakatifu

VIZAZI vingi sana vya waamini vimetumia saa nyingi sana kusoma, kujifunza, na kuchunguza baadhi ya maandishi maarufu zaidi kuwahi kuandikwa, yaani, Agano Jipya, kama watu wengi wanavyoyaita Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Maandishi hayo, pamoja na Biblia nzima, yamekuwa na uvutano mkubwa ulimwenguni, yakasaidia kuonyesha maadili na kanuni, na kuchochea watu kuandika vitabu na kutokeza vitu vya sanaa. Zaidi ya yote, maandishi hayo yamewasaidia mamilioni ya watu, na labda hata wewe, kupata ujuzi sahihi kuhusu Mungu na Yesu.—Yohana 17:3.

Vitabu vya Injili, na pia Maandiko mengine ya Kigiriki ya Kikristo, hayakuandikwa mara tu baada ya kifo cha Yesu. Inaelekea kwamba Mathayo aliandika Injili yake miaka 7 au 8 hivi baadaye, na Yohana aliandika Injili yake miaka 65 hivi baadaye. Ni nini kilichowawezesha kurekodi maneno na matendo ya Yesu kwa usahihi kabisa? Ni wazi kwamba roho takatifu ya Mungu ilitimiza fungu muhimu katika kuwaongoza. (Yohana 14:16, 26) Hata hivyo, mafundisho ya Yesu yalipitishwa jinsi gani kwa usahihi na hatimaye kuwa sehemu ya Maandiko Matakatifu?

“Hawakujua Kusoma na Kuandika”?

Katika karne iliyopita, watu fulani wamekisia kwamba inaelekea wanafunzi wa mapema wa Yesu hawakuandika mafundisho na matendo ya Yesu bali waliyapitisha kwa maneno. Kwa mfano, msomi mmoja anasema hivi: “Kulikuwa na pengo la makumi ya miaka kati ya huduma ya Yesu ya hadharani na wakati waandikaji wa Injili walipoandika maneno yake. Wakati huo mambo yaliyojulikana kumhusu Yesu yalipitishwa kwa maneno.” Watafiti fulani hata wanasema kwamba wanafunzi wa mapema wa Yesu “hawakujua kusoma na kuandika.” * Zaidi ya hayo, wanasema kuwa kwa makumi ya miaka ambayo ujumbe ulipitishwa kwa maneno, masimulizi ya huduma ya Yesu yaliongezwa, yakabadilishwa, au kutiwa chumvi. Wanadai kwamba matokeo hayakuwa sahihi hata kidogo.

Wasomi wengine wanasema kwamba wanafunzi wa karibu wa Yesu waliokuwa Wayahudi huenda walifuata mbinu ya Kirabi ya kufundisha ambayo ilichangia usahihi wa ujumbe uliopitishwa, yaani, kukariri na kurudia. Je, wanafunzi walitegemea njia ya kupitisha ujumbe kwa maneno? Au je, kabla ya kuandika Biblia inawezekana kwamba walikuwa wamenakili mambo fulani kuhusu masimulizi ya huduma ya Yesu? Ingawa hatuwezi kusema kwa uhakika kabisa, inawezekana kwamba maandishi yalitumiwa.

Jinsi Maandishi Yalivyotumiwa Kila Siku

Katika karne ya kwanza, watu kutoka matabaka mbalimbali ya jamii walijua kusoma na kuandika. Alan Millard profesa wa Kiebrania na lugha za Kisemiti za awali alisema hivi: “Maandishi ya Kigiriki, Kiaramu, na Kiebrania yalikuwa yameenea na yaliweza kupatikana katika matabaka yote katika jamii.” Anaongeza hivi: “Hizo ndizo hali zilizokuwapo wakati wa Yesu.”

Kuhusu wazo la kwamba maandishi ya Injili “yalitokana na jamii ya watu wasiojua kabisa kusoma na kuandika,” Profesa Millard anaandika hivi: “Hilo si wazo la kweli, [kwa kuwa] karibu kila mahali watu walijua kuandika . . . Hivyo, kulikuwa na watu ambao wangeweza kuandika jambo walilosikia, labda kwa ajili ya matumizi yao au ili kuwaeleza wengine.”

Inaonekana kwamba mabamba yenye nta yalipatikana kwa urahisi na yangetumiwa kuandika habari. Mfano mmoja wa jambo hilo unaonekana katika sura ya kwanza ya Luka. Zekaria, ambaye alikuwa amepoteza uwezo wake wa kuzungumza kwa muda, aliulizwa alitaka mwana wake aitwe jina gani. Mstari wa 63 unasema hivi: “Akaomba bamba [huenda kwa kutumia ishara] na kuandika: ‘Yohana ndilo jina lake.’” Kamusi za Biblia zinaeleza kwamba neno “bamba” huenda lilirejelea ubao wa kuandika uliofunikwa kwa nta. Huenda mtu fulani hapo alikuwa na ubao ambao Zekaria angeweza kuandikia.

Kuna mfano mwingine unaoonyesha kwamba vibao vya kuandika na matumizi yake yalijulikana wakati huo. Katika kitabu cha Matendo, tunasoma kwamba Petro alipokuwa akizungumza na umati kwenye eneo la hekalu aliwahimiza hivi: “Tubuni . . . dhambi zenu zipate kufutwa.” (Matendo 3:11, 19) Maneno “zipate kufutwa” yanatokana na kitenzi cha Kigiriki kinachomaanisha “futa.” Kamusi moja (The New International Dictionary of New Testament Theology) inaeleza hivi: “Inawezekana kwamba wazo linalotolewa na kitenzi hicho hapo na kwingineko ni lile la kulainisha sehemu ya juu ya ubao wa kuandika wenye nta ili utumike tena.”

Masimulizi ya Injili yanaonyesha pia kwamba wafuasi na wasikilizaji wa Yesu walitia ndani watu ambao yaelekea walitumia maandishi katika shughuli zao za kila siku. Kwa mfano, kulikuwa na wakusanya-kodi Mathayo na Zakayo (Mathayo 9:9; Luka 19:2); ofisa wa sinagogi (Marko 5:22); ofisa-jeshi (Mathayo 8:5); Yoana, mke wa ofisa aliyekuwa na cheo kikubwa chini ya Herode Antipa (Luka 8:3); na vilevile waandishi, Mafarisayo, Masadukayo, na washiriki wa Sanhedrini. (Mathayo 21:23, 45; 22:23; 26:59) Bila shaka, wengi, ikiwa si wote, kati ya mitume na wanafunzi wa Yesu waliweza kuandika.

Wanafunzi, Walimu, na Waandikaji

Ili wawe walimu Wakristo, wanafunzi hawakuhitaji tu kujua yale ambayo Yesu alifanya na kusema lakini pia walihitaji kujua jinsi Sheria na unabii mbalimbali katika Maandiko ya Kiebrania ulivyotimia katika Kristo. (Matendo 18:5) Kwa kupendeza, Luka alirekodi pindi moja ambapo Yesu alikutana na baadhi ya wanafunzi wake muda mfupi baada ya kufufuliwa. Yesu alifanya nini? ‘Akianzia Musa na Manabii wote, akawafasiria mambo yanayomhusu yeye mwenyewe katika Maandiko yote.’ Muda mfupi baadaye, Yesu aliwaambia wanafunzi hao: “‘Haya ndiyo maneno yangu niliyowaambia nilipokuwa ningali pamoja nanyi, kwamba mambo yote yaliyoandikwa katika sheria ya Musa na katika Manabii na Zaburi juu yangu lazima yatimizwe.’ Ndipo akafungua akili zao ili kuifahamu maana ya Maandiko.” (Luka 24:27, 44, 45) Baadaye, wanafunzi ‘walikumbuka’ habari ambayo Yesu alikuwa amewaambia.—Yohana 12:16.

Masimulizi hayo yanadokeza kwamba ni lazima mitume na wanafunzi walijitahidi kufanya utafiti na kujifunza Maandiko ili waweze kuelewa kabisa maana ya mambo waliyoona na kusikia kuhusu Bwana wao, Yesu Kristo. (Luka 1:1-4; Matendo 17:11) Harry Y. Gamble, profesa wa masomo ya kidini kwenye Chuo Kikuu cha Virginia, anaandika hivi: “Haiwezi kutiliwa shaka kwamba tangu mwanzoni kulikuwa na Wakristo, huenda hata vikundi vya wakristo ambao walijitoa ili kujifunza kwa uangalifu na kufasiri maandiko ya Kiyahudi, na kuonyesha uthibitisho wa imani ya Kikristo kutokana na maandishi hayo na kuyafanya yaweze kutumiwa katika mahubiri ya Kikristo.”

Yote hayo yanaonyesha kwamba badala ya kutegemea tu mambo yanayopitishwa kwa mdomo, wanafunzi wa mapema wa Yesu walikuwa na bidii ya kujifunza, kusoma, na kuandika. Walikuwa wanafunzi, walimu, na waandikaji. Zaidi ya yote walikuwa wanaume wa kiroho ambao walitegemea mwongozo wa roho takatifu. Yesu aliwahakikishia kwamba ‘roho ya kweli ingewakumbusha mambo yote aliyowaambia.’ (Yohana 14:17, 26) Ni roho takatifu ya Mungu iliyowasaidia kukumbuka na kuandika mambo yote ambayo Yesu alifanya na kusema, kutia ndani manukuu marefu, kama vile Mahubiri ya Mlimani. (Mathayo, sura ya 5-7) Pia, roho hiyo iliwaongoza waandikaji wa Injili warekodi jinsi Yesu alivyohisi nyakati fulani na mambo aliyosema katika sala.—Mathayo 4:2; 9:36; Yohana 17:1-26.

Kwa hiyo, ingawa waandikaji wa Injili walitumia mambo yaliyopitishwa kwa mdomo na maandishi, habari walizorekodi zilitoka katika chanzo kinachotegemeka na kilichotukuka zaidi, yaani, Yehova Mungu mwenyewe. Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu” na linaweza kutufundisha na kutuongoza tufanye mambo yanayompendeza yeye.—2 Timotheo 3:16.

[Maelezo ya Chini]

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Wafuasi wa Yesu walitia ndani watu ambao yaelekea walitumia maandishi katika shughuli zao za kila siku

[Blabu katika ukurasa wa 15]

Roho takatifu ya Mungu iliwasaidia wanafunzi wa mapema wa Yesu kukumbuka na kuandika mambo aliyofanya na kusema

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

 Je, Mitume Hawakujua Kusoma na Kuandika?

Watawala na wanaume wazee wa Yerusalemu “walipoona maneno ya waziwazi ya Petro na Yohana, na kufahamu kwamba walikuwa watu wasio na elimu na wa kawaida tu, wakaanza kustaajabu.” (Matendo 4:13) Je, kweli mitume walikuwa watu wasio na elimu? Kitabu fulani kuhusu Biblia (The New Interpreter’s Bible) kinasema hivi kuhusu dai hilo: “Inaonekana kwamba maneno hayo hayafai kuchukuliwa kihalisi kana kwamba Petro [na Yohana] hawakuwa na elimu na hawangeweza kusoma au kuandika. Yanaonyesha tu tofauti ya kijamii iliyokuwapo kati ya wale waliowahukumu na mitume.”

[Picha katika ukurasa wa 13]

“Akaomba bamba na kuandika: ‘Yohana ndilo jina lake’”

[Picha katika ukurasa wa 13]

Bamba lililo na nta likiwa na vifaa vya kuandikia vya karne ya kwanza au ya pili W.K.

[Hisani]

© British Museum/Art Resource, NY