Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilijifunza Thamani ya Uhai

Nilijifunza Thamani ya Uhai

Nilijifunza Thamani ya Uhai

ILIKUWA NI ASUBUHI YA APRILI 16, 2007. Nikiwa nimejikunyata kwenye kona moja ya ofisi iliyo kwenye orofa ya tatu ya jengo la Norris Hall kwenye Chuo Kikuu cha Virginia, nilikumbushwa kwa mara nyingine kwamba tunapaswa kuthamini uhai wetu kila siku.

Nilikuwa kwenye ofisi yangu nikijitayarisha kwenda kwenye orofa ya pili kuchukua barua zangu. Profesa mmoja alikuja na kuniomba nimsaidie kusuluhisha tatizo la kompyuta katika ofisi yake. Tulipokuwa tukiingia ofisini mwake, tulisikia milio kadhaa ya risasi kwenye orofa ya pili. Kwa sababu hatukujua kilichokuwa kikiendelea, tuliharakisha na kuingia katika ofisi yake, tukafunga mlango, na kungoja kwa wasiwasi bila kujua kitakachotukia. Nilijificha kwenye kona fulani na kummiminia Yehova Mungu moyo wangu katika sala nikimwomba mwongozo ili nikabiliane na chochote ambacho kingetupata.

Tulipokuwa tukingoja, nilikumbuka tukio lililonipata miaka 15 mapema. Nilikuwa fundi wa magari katika kituo kimoja cha kurekebisha magari. Mfanyakazi mwenzangu alikuwa ameshika chombo fulani kidogo kilichokuwa na mafuta, nacho kikawaka moto. Kwa woga, alinitupia chombo hicho usoni bila kukusudia! Nilipumua mafuta hayo yaliyokuwa yamewaka moto na nikaungua sana katika sehemu ya juu ya mwili wangu. Nilipelekwa kwa helikopta katika hospitali inayoshughulikia watu walioungua na nikawa katika wodi ya kuwatunzia wagonjwa mahututi kwa miezi mitatu na nusu, nilikuwa nikichungulia kaburi. Baada ya kutibiwa kwa miezi mitano, nilirudi nyumbani, nikishukuru tu kwamba nilikuwa hai. Tukio hilo lilinifundisha kuona kila siku niliyo hai kuwa yenye thamani. Pia liliimarisha azimio langu la kutumia maisha yangu kumtumikia yule aliyenipa uhai, Yehova Mungu nikiwa mmoja wa Mashahidi wake.—Zaburi 90:12; Isaya 43:10.

Singeweza tena kufanya kazi ya kurekebisha magari kwa sababu ya majeraha niliyopata, hivyo nikajifunza jinsi ya kufanya kazi ya kompyuta na nikaajiriwa kwenye Chuo Kikuu cha Virginia. Hiyo ndiyo sababu nilikuwa kwenye jengo la Norris Hall asubuhi hiyo.

Milio ya risasi ilipokuwa ikiendelea, hatukutambua kuwa mauaji mabaya zaidi katika historia ya Marekani ya kuwapiga watu wengi risasi kwa kipindi kimoja yalikuwa yakiendelea kwenye orofa iliyokuwa chini yetu. Mauaji hayo yalikoma wakati mtu aliyekuwa akifyatua risasi alipojiua, baada ya kuwaua watu 32 wasio na hatia. Dakika 20 hivi baada ya milio hiyo kuanza, tuliwasikia polisi wakitembea nje ya ofisi tulimokuwa. Tuliwaita na wakatusindikiza nje.

Tukio hilo lenye kusikitisha limenifundisha jinsi ilivyo rahisi sana kufa. (Yakobo 4:14) Ni jambo muhimu kwetu kumtegemea Mpaji wa uhai, Yehova Mungu, na kuiona kila siku kuwa zawadi yenye thamani kutoka kwake!—Zaburi 23:4; 91:2.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 30]

AP Photo/The Roanoke Times, Alan Kim