Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Usisahau Kamwe Kuhubiri Nyumba kwa Nyumba”

“Usisahau Kamwe Kuhubiri Nyumba kwa Nyumba”

“Usisahau Kamwe Kuhubiri Nyumba kwa Nyumba”

Limesimuliwa na Jacob Neufeld

“Hata kutukie nini, usisahau kamwe kuhubiri nyumba kwa nyumba.” Huku maneno hayo yakiwa wazi akilini, nilitembea kilomita tano hivi hadi kwenye kijiji kilichokuwa karibu. Nilipowasili, sikuwa na ujasiri wa kubisha nyumba ya kwanza. Baada ya kujaribu mara kadhaa, niliingia msituni na kusali kwa Mungu kwa bidii ili anipe ujasiri wa kuhubiri. Mwishowe, nilifaulu kurudi kwenye nyumba ya kwanza na kuhubiri.

NILIFIKA namna gani kwenye kijiji hicho kilicho kwenye jangwa nchini Paraguai ambako nilikuwa nikijaribu kuhubiri nikiwa peke yangu? Acha nianze kusimulia kutoka mwanzo. Nilizaliwa Novemba (Mwezi wa 11) 1923 katika kijiji cha Kronstalʹ huko Ukrainia, katika koloni ya Wameno waliotoka Ujerumani. Mwishoni mwa miaka ya 1700, Wameno walikuwa wamehama Ujerumani na kwenda Ukrainia na walikuwa wamepewa mapendeleo mengi kutia ndani, uhuru wa ibada (lakini si wa kuwageuza watu imani), haki ya kujitawala, na kutohusishwa katika utumishi wa kijeshi.

Mapendeleo hayo yote yaliondolewa Chama cha Kikomunisti kilipoanza kutawala. Mwishoni mwa miaka ya 1920, mashamba makubwa ya Wameno yaliwekwa chini ya usimamizi wa serikali. Watu walinyimwa chakula hadi walipojitiisha kwa serikali, na waasi wowote walishughulikiwa kwa ukatili. Katika miaka ya 1930, hasa wakati wa usiku, wanaume wengi walichukuliwa na KGB (Shirika la Usalama wa Kitaifa la Sovieti), hadi vijiji vingi vikabaki na wanaume wachache sana. Hivyo ndivyo nilivyompoteza baba yangu mnamo 1938, nikiwa na umri wa miaka 14 na sikuwahi kumwona au kusikia kutoka kwake tena. Miaka miwili baadaye, ndugu yangu mkubwa akachukuliwa pia.

Kufikia mwaka wa 1941, majeshi ya Hitler yaliteka Ukrainia. Hilo lilituweka huru kutoka kwa utawala wa Kikomunisti. Hata hivyo, kwa ghafula familia nane za Wayahudi zilizokuwa zikiishi katika kijiji chetu zilitoweka. Mambo yote hayo yalinifanya nijiulize maswali mengi. Kwa nini mambo hayo yalitendeka?

Unyoofu Waokoa Uhai Wangu

Mnamo 1943, majeshi ya Ujerumani yaliondoka yakiwa na familia nyingi za Wajerumani, kutia ndani washiriki waliobaki wa familia yetu, ili wakategemeze vita. Kufikia wakati huo, nilikuwa nimeandikishwa na kutumwa katika SS ya Ujerumani (Schutzstaffel, walinzi bora zaidi wa Hitler) nchini Rumania. Tukio dogo wakati huo lilikuwa na matokeo makubwa maishani mwangu.

Kapteni wa kikundi chetu alitaka kujaribu unyoofu wangu. Aliniambia nimpelekee sare yake kwa dobi. Alikuwa ameweka pesa katika mfuko mmoja, nami nikazipata. Nilipomrudishia pesa hizo, aliniambia kwamba hakuwa ameacha chochote katika sare hiyo. Nilisisitiza kwamba nilikuwa nimezitoa mfukoni mwake. Muda mfupi baada ya hapo, nilifanywa kuwa msaidizi wake na nikapewa kazi za ofisini, kuwapa walinzi migawo, na kutunza pesa za kikundi chetu.

Usiku mmoja, jeshi la Urusi liliteka kikundi chetu chote isipokuwa mimi; nilikuwa nimeachwa ili nimalizie kazi fulani ya kapteni. Ninachojua ni kwamba ni mimi tu ambaye sikutekwa, na hiyo ni kwa sababu nilikuwa mnyoofu na nikapewa mgawo huo wa pekee. Kama sivyo, mimi pia ningetekwa.

Hivyo, mnamo 1944, niliruhusiwa kuondoka kwa kipindi kisichojulikana. Nilirudi nyumbani kumtembelea mama yangu. Nilipokuwa nikisubiri mgawo mwingine, nilifanya kazi pamoja na mjenzi fulani na ujuzi huo ulinisaidia baadaye. Mnamo Aprili (Mwezi wa 4) 1945 majeshi ya Marekani yaliteka mji wetu ulio karibu na Magdeburg. Mwezi mmoja baadaye vita vilikwisha kirasmi. Tulikuwa hai. Wakati wetu ujao ulionekana kuwa mwangavu.

Siku moja katika Juni (Mwezi wa 6), tulisikia tangazo kutoka kwa mpiga-mbiu wa mji, “Majeshi ya Marekani yaliondoka jana usiku, na majeshi ya Urusi yatawasili leo saa 5:00 asubuhi.” Tulivunjika moyo tulipotambua kwamba tulikuwa tena katika eneo la Kikomunisti. Mara moja, mimi na binamu yangu tukaanza kupanga jinsi tungetoroka. Kufikia katikati ya msimu wa kiangazi, tulikuwa tumeingia katika eneo la Wamarekani. Kisha, mnamo Novemba, kupitia hali ngumu na tukihatarisha maisha yetu, tuliingia tena eneo la Warusi na kuwavusha mpaka kwa siri washiriki wa familia zetu.

“Sikiliza kwa Makini Sana, na Ulinganishe”

Tuliishi katika nchi iliyoitwa wakati huo Ujerumani Magharibi. Baada ya muda, nilianza kuipenda biblia. Jumapili (Siku ya Yenga), ningeenda msituni kusoma Biblia, lakini sikuelewa mambo niliyosoma kwani yalionekana kuwa ya zamani. Pia, nilikuwa nikihudhuria masomo ya katekisimu nikijitayarisha ili nibatizwe kuwa Mmeno. Nilishangaa niliposoma katika kitabu cha katekisimu maneno haya: “Baba ni Mungu, Mwana ni Mungu, na Roho Mtakatifu ni Mungu,” halafu yakafuatwa na swali: “Je, kuna Miungu mitatu?” Jibu liliandikwa baada ya swali hilo: “Hapana, hao watatu ni mmoja.” Nilimwuliza kasisi huyo hilo lingewezekana jinsi gani. Alijibu hivi, “Kijana, mtu hapaswi kufikiria sana mambo hayo; watu fulani wamerukwa na akili kwa sababu ya kutafakari sana kuyahusu.” Papo hapo, nikaamua kwamba sitabatizwa.

Siku kadhaa baadaye, nilisikia mgeni fulani akizungumza na binamu yangu. Nikitamani kujua walichokuwa wakizungumzia, nilijiunga nao na kuuliza maswali kadhaa. Wakati huo sikujua kwamba mgeni huyo alikuwa Erich Nikolaizig, ambaye aliokoka kambi ya mateso ya Wewelsburg. Aliniuliza kama nilitaka kuielewa Biblia. Nilipokubali, alinihakikishia kwamba kila kitu ambacho angenifundisha kingethibitishwa katika Biblia yangu mwenyewe.

Baada ya kunitembelea mara kadhaa, Erich alinialika kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova ambalo ninafikiri lilikuwa moja ya makusanyiko ya kwanza kufanywa baada ya vita. Nilifurahia sana na nikaandika kila andiko lililosomwa au kutajwa na wasemaji. Baada ya muda nilitambua kwamba kujifunza Biblia kunaleta madaraka fulani, kwa hiyo, nikaamua kuacha. Pia, ilikuwa vigumu kwangu kuamini kwamba kuna dini moja tu ya kweli. Erich alipoona kwamba nimeamua kurudi kwenye kanisa langu la zamani, alinishauri hivi, “Sikiliza kwa makini sana, na ulinganishe.”

Nilihitaji kuwatembelea makasisi wangu mara mbili tu ili kutambua kwamba hawakujua walichozungumzia na hawakuijua kweli. Niliwaandikia makasisi kadhaa na kuwauliza maswali ya Biblia. Mmoja wao alinijibu, “Hupaswi kuchunguza Maandiko kwa sababu hujazaliwa mara ya pili.”

Msichana mmoja ambaye nilikuwa nikimchumbia alinilazimisha nifanye uamuzi mgumu. Alikuwa mshiriki wa madhehebu moja ya Wameno waliozaliwa mara ya pili. Kwa sababu ya mkazo kutoka kwa watu wa familia yake ambao waliwachukia Mashahidi wa Yehova, alinifahamisha kwamba ikiwa singeacha dini hiyo mpya, uchumba wetu ungekoma. Kufikia wakati huo, kweli ilikuwa wazi kwangu hivi kwamba nilijua kuna uamuzi mmoja tu sahihi, yaani, kukomesha uchumba huo.

Muda mfupi baadaye, Erich alikuja kunitembelea. Alisema kwamba kuna ubatizo uliopangiwa juma lililofuata na akaniuliza ikiwa ningependa kubatizwa. Nilikuwa nimefikia mkataa kwamba Mashahidi wa Yehova walifundisha kweli, na nilitaka kumtumikia Yehova Mungu. Kwa hiyo, nilikubali mwaliko wake na nikabatizwa kwenye beseni ya kuogea mnamo Mei (Mwezi wa 5) 1948.

Muda mfupi baada ya ubatizo wangu, familia yetu iliamua kuhamia Paraguai, huko Amerika Kusini, na Mama akanisihi niandamane nao. Nilisitasita kwa sababu nilihitaji kujifunza Biblia zaidi na kuzoezwa. Nilipotembelea ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Wiesbaden, nilikutana na August Peters. Alinikumbusha kwamba nilikuwa na jukumu la kuitunza familia yetu. Alinihimiza hivi pia: “Hata kutukie nini, usisahau kamwe kuhubiri nyumba kwa nyumba. Ukisahau, utakuwa kama tu mshiriki wa dini nyingine zinazodai kuwa za Kikristo.” Hadi leo, ninatambua umuhimu wa shauri hilo na uhitaji wa kuhubiri “nyumba kwa nyumba,” au mlango kwa mlango.—Matendo 20:20, 21.

“Nabii wa Uwongo” Nchini Paraguai

Muda mfupi baada ya kukutana na August Peters, nilipanda meli iliyokuwa ikielekea Amerika Kusini nikiwa na familia yangu. Tuliwasili katika eneo la Gran Chaco nchini Paraguai, eneo ambalo pia lilikuwa na koloni ya Wameno. Majuma mawili baada ya kuwasili, nilifunga ile safari ngumu kuelekea kwenye kijiji kilichokuwa karibu ili kuhubiri nikiwa peke yangu. Ujumbe ulienezwa haraka kwamba kulikuwa na “nabii wa uwongo” ambaye alikuwa amewasili.

Katika kipindi hicho ujuzi wangu wa kazi ya ujenzi ulinifaidi sana. Kila familia ya wahamiaji ilihitaji kuwa na nyumba, na nyumba hizi zilijengwa kwa matofali na kuezekwa kwa nyasi. Kwa miezi sita iliyofuata, nilijenga nyumba nyingi na nilipata nafasi ya kuhubiri isivyo rasmi. Watu walikuwa na heshima, lakini mara tu nilipomaliza kujenga kuta za nyumba yao, walifurahi kwa kuwa hawakunihitaji tena.

Wakati huohuo, meli nyingine zilileta wakimbizi zaidi Wameno kutoka Ujerumani. Kati yao kulikuwa na mwanamke kijana aliyeitwa Katerina Schellenberg ambaye alikuwa amekutana na Mashahidi kwa muda mfupi na alikuwa ametambua kweli. Ingawa hakuwa amebatizwa, alikuwa amejitambulisha kuwa Shahidi wa Yehova alipokuwa ndani ya meli. Kwa sababu hiyo, alinyimwa ruhusa ya kufika kwenye koloni ya Ujerumani. Akiwa ameachwa peke yake huko Asunción, mji mkuu wa Paraguai, alipata kazi ya kuwa yaya, akajifunza Kihispania, akawapata Mashahidi, na kubatizwa. Mnamo Oktoba (Mwezi wa 10) 1950, nilimwoa msichana huyo jasiri. Amenitegemeza sana na kunisaidia katika mambo yote ambayo tumepitia maishani.

Katika muda mfupi, nilikuwa nimekusanya pesa za kutosha kununua gari la kukokotwa na farasi wawili, na nikatumia vitu hivyo katika kazi ya kuhubiri, kila wakati nikikumbuka mashauri ya Ndugu Peters. Wakati huo, dada yangu ambaye alikuwa amejifunza na kuwa Shahidi, alijiunga nasi. Mara nyingi, sisi sote tuliamka saa 10:00 alfajiri, tukasafiri kwa saa nne, tukahubiri kwa saa mbili au tatu, kisha tukarudi nyumbani.

Nilikuwa nimesoma katika vichapo vyetu kwamba hotuba za watu wote zilikuwa zikitolewa, kwa hiyo, nikapanga kutoa moja. Sikuwa nimewahi kuhudhuria mkutano huko Ujerumani, kwa hiyo, nilikisia tu jinsi hotuba inavyopaswa kutolewa na nikazungumzia Ufalme wa Mungu. Watu wanane walihudhuria mkutano huo na jambo hilo liliwaudhi sana makasisi wa Kanisa la Meno. Walipanga kampeni ya kukusanya kila kichapo cha Biblia ambacho tulikuwa tumewaachia watu na kuwaagiza wasitusalimu kamwe.

Kisha, niliitwa mbele ya makao makuu ya usimamizi wa koloni hiyo na nikahojiwa kwa saa kadhaa na msimamizi pamoja na makasisi wawili waliokuwa wamezuru kutoka Kanada. Mwishowe, mmoja wao akasema, “Kijana, unaweza kuamini jambo lolote unalotaka, lakini lazima uahidi kwamba hutazungumza na mtu yeyote kuhusu imani yako.” Hiyo ni ahadi ambayo singetoa. Kwa hiyo, wakaniambia niondoke kwenye koloni hiyo kwa sababu hawakutaka “nabii wa uwongo” kati ya “ndugu waaminifu.” Nilipokataa, walisema wangelipa nauli kwa ajili ya familia yangu yote. Nilishikilia uamuzi wangu na nikakataa kuondoka.

Katika msimu wa kiangazi mnamo 1953, nilihudhuria kusanyiko huko Asunción. Nikiwa huko nilizungumza na Nathan Knorr, aliyekuwa ametoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York. Alipendekeza kwamba nihamie kwenye mji mkuu na kufanya kazi pamoja na kikundi kidogo cha wamishonari waliokuwa huko, hasa kwa sababu kazi ya kuhubiri katika koloni ya Wameno haikuwa na matokeo makubwa.

Kutanguliza Ufalme

Wakati huo kulikuwa na Mashahidi 35 hivi nchini Paraguai. Nilizungumza na mke wangu na ingawa hakupendezwa na wazo la kuhamia jiji kubwa, alikuwa tayari kuanza maisha mapya. Mnamo 1954, mimi na Katerina tulijenga nyumba ya matofali, tukiwa peke yetu wakati wa mapumziko. Hatukukosa mkutano wowote, na tulizungumza na watu kuhusu Biblia mwishoni mwa juma.

Pendeleo moja nililopewa lilikuwa kuandamana na mwangalizi wa mzunguko, mhudumu anayesafiri, alipokuwa akizuru baadhi ya koloni za Kijerumani nchini Paraguai ili kumtafsiria. Kwa kuwa sikujua Kihispania vizuri, huenda mgawo mgumu zaidi ambao nimewahi kupokea ulikuwa kutafsiri kwa mara ya kwanza hotuba kutoka Kihispania hadi Kijerumani.

Kwa sababu ya afya ya mke wangu, tulihamia Kanada mnamo 1957. Kisha, mnamo 1963, tukahamia Marekani. Popote ambapo tumekuwa, sikuzote tumejaribu kutanguliza Ufalme maishani. (Mathayo 6:33) Ninamshukuru sana Yehova Mungu kwa kuniruhusu nijifunze kweli ya Neno lake, Biblia, nilipokuwa kijana. Mazoezi ya kiroho niliyopata yamenisaidia katika njia nyingi sana maishani mwangu!

Limekuwa pendeleo kubwa kuwasaidia wengine wajifunze kweli nzuri za Biblia ambazo zimenifariji sana. Shangwe yangu kubwa ni kwamba watoto na wajukuu wangu wote wamefaidika tangu utotoni na mafundisho ya Biblia. Wote wanafuata mashauri ya Ndugu Peters, aliyeniambia hivi zamani, “Hata kutukie nini, usisahau kamwe kuhubiri nyumba kwa nyumba.”

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Shangwe yangu kubwa ni kuona kwamba watoto na wajukuu wangu wote wamefaidika tangu utotoni na mafundisho ya Biblia

[Picha katika ukurasa wa 21]

Mimi na Katerina muda mfupi kabla ya arusi yetu mnamo 1950

[Picha katika ukurasa wa 21]

Tukiwa nyumbani na mtoto wetu wa kwanza huko Paraguai, mnamo 1952

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na watoto na wajukuu wangu leo

[Hisani]

Photo by Keith Trammel © 2000

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 19]

Photo by Keith Trammel © 2000