Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Alikata “Kauli Moyoni Mwake”

Alikata “Kauli Moyoni Mwake”

Igeni Imani Yao

Alikata “Kauli Moyoni Mwake”

MARIA aliketi bila kustarehe juu ya punda. Alikuwa amesafiri kwa muda mrefu. Mbele yake, Yosefu alikuwa akitembea akiwaelekeza Bethlehemu iliyo mbali sana. Kwa mara nyingine, Maria alihisi kitoto kikicheza ndani yake.

Biblia inasema kwamba wakati huo Maria alikuwa “karibu kuzaa.” (Luka 2:5) Wenzi hao walipopita shamba moja baada ya lingine, huenda wakulima fulani waliwatazama na kujiuliza kwa nini mwanamke aliye katika hali kama hiyo angeamua kusafiri. Ni nini kilichomfanya Maria asafiri mbali hivyo kutoka nyumbani kwao Nazareti?

Matukio hayo yalianza miezi kadhaa mapema wakati mwanamke huyo Myahudi alipopata mgawo wa pekee zaidi katika historia yote ya wanadamu. Angezaa mwana ambaye angekuwa Masihi, Mwana wa Mungu! (Luka 1:35) Alipokaribia kuzaa, walihitaji kusafiri. Wakati wa safari hiyo, Maria alikumbwa na mambo mbalimbali yaliyoijaribu imani yake. Hebu tuone ni nini kilichomsaidia kubaki imara kiroho.

Safari ya Kwenda Bethlehemu

Si Yosefu na Maria peke yao waliokuwa wakisafiri. Kaisari Augusto alikuwa ametoa amri kwamba watu wote katika nchi waandikishwe na watu walihitaji kusafiri hadi kwenye mji waliozaliwa ili waandikishwe. Yosefu alifanya nini? Simulizi hilo linasema: “Yosefu pia akapanda kutoka Galilaya, kutoka jiji la Nazareti, akaingia Yudea, kwenye jiji la Daudi, linaloitwa Bethlehemu, kwa sababu alikuwa mshiriki wa nyumba na familia ya Daudi.”—Luka 2:1-4.

Halikuwa jambo lisilotarajiwa kwamba Kaisari alitoa amri yake wakati huo. Unabii ulioandikwa karne saba hivi mapema ulitabiri kwamba Masihi angezaliwa Bethlehemu. Kulikuwa na mji unaoitwa Bethlehemu kilomita 11 tu kutoka Nazareti. Hata hivyo, unabii ulitaja kihususa kwamba Masihi angetoka “Bethlehemu Efratha.” (Mika 5:2) Kijiji hicho kidogo kilicho upande wa kusini kiko umbali wa kilomita 150 hivi kutoka Nazareti ukitumia barabara za siku hizi za mlimani. Hiyo ndiyo Bethlehemu ambayo Yosefu aliamriwa aende kwani hilo ndilo lililokuwa chimbuko la ukoo wa Mfalme Daudi. Yosefu na mke wake walikuwa wa ukoo huo.

Je, Maria angeunga mkono uamuzi wa Yosefu wa kutii amri hiyo? Hiyo ingekuwa safari ngumu kwake. Huenda huo ulikuwa msimu wa mvua ndogo kwa kuwa msimu wa kiangazi ulikuwa ukiisha. Isitoshe, maneno “akapanda kutoka Galilaya” yanafaa, kwa kuwa mji wa Bethlehemu ulikuwa zaidi ya mita 760 juu ya usawa wa bahari. Baada ya kutembea kwa siku kadhaa, huo ungekuwa mwinuko mkubwa sana wenye kuchosha. Huenda safari hiyo ingechukua muda mrefu zaidi kwa kuwa Maria angehitaji kupumzika mara nyingi kwa sababu ya hali yake. Wakati kama huo, huenda mwanamke angetaka kukaa karibu na watu wa familia na marafiki wake ambao wangekuwa tayari kumsaidia wakati ambapo uchungu wa kuzaa ungeanza. Bila shaka, alihitaji kuwa na ujasiri ili asafiri.

Hata hivyo, Luka anaandika kwamba Yosefu alienda “kuandikishwa pamoja na Maria.” Pia anasema kwamba Yosefu ‘alikuwa amemwoa Maria kama ilivyoahidiwa.’ (Luka 2:4, 5) Yosefu alikuwa na uvutano mkubwa sana juu ya maamuzi ya Maria kwa kuwa sasa Maria alikuwa mke wake. Maria alimwona mume wake kuwa kichwa chake kuhusiana na mambo ya kiroho, na alikubali jukumu lake alilopewa na Mungu la kuwa msaidizi wake kwa kuunga mkono maamuzi yake. * Kwa hiyo, alishinda kipingamizi hicho cha imani yake kwa kutii.

Ni nini kingine kilichomchochea Maria atii? Je, alijua unabii wa kwamba Masihi angezaliwa Bethlehemu? Biblia haisemi. Hatuwezi kupuuza uwezekano huo, kwa maana jambo hilo lilijulikana na viongozi wa kidini na watu kwa ujumla. (Mathayo 2:1-7; Yohana 7:40-42) Maria pia aliyajua Maandiko. (Luka 1:46-55) Vyovyote vile, iwe Maria alisafiri ili kumtii mumewe, kutii Kaisari, au kwa sababu ya unabii wa Yehova au iwe alichochewa na mambo hayo yote matatu, aliweka mfano bora. Yehova anathamini sana roho ya unyenyekevu na utii inayoonyeshwa na wanaume na wanawake. Siku hizi ambapo kujitiisha ni mojawapo ya sifa zinazodharauliwa, mfano wa Maria ni kielelezo kizuri kwa watu waaminifu kila mahali.

Kuzaliwa kwa Kristo

Lazima Maria awe alifurahi sana walipokaribia Bethlehemu. Walipopanda milima na kupita mashamba ya mizabibu, mojawapo ya mimea ya mwisho kuvunwa, huenda Maria na Yosefu walifikiri kuhusu historia ya kijiji hicho kidogo. Kilikuwa kidogo sana kuhesabiwa kuwa kati ya majiji ya Yuda kama nabii Mika alivyosema; hata hivyo, huko ndiko walikozaliwa Boazi, Naomi, na baadaye Daudi, zaidi ya miaka elfu moja mapema.

Maria na Yosefu walipata kijiji hicho kikiwa kimejaa watu. Wengi walikuwa wamefika mapema kabla yao ili kuandikishwa, kwa hiyo, hakukuwa na nafasi katika chumba cha kukaa. * Walilazimika kulala kwenye zizi. Tunaweza kuwazia jinsi Yosefu alivyohangaika alipomwona mke wake akiwa na uchungu mkali uliozidi kuongezeka. Uchungu wake wa kuzaa ulianzia papo hapo zizini.

Wanawake ulimwenguni pote wanaweza kuelewa jinsi Maria alivyohisi. Miaka 4,000 hivi mapema, Yehova alikuwa ametabiri kwamba wanawake wangehisi uchungu walipokuwa wakizaa kwa sababu ya kurithi dhambi. (Mwanzo 3:16) Hakuna uthibitisho unaoonyesha kwamba Maria hakupata uchungu wa kuzaa. Simulizi la Luka halitaji uchungu ambao Maria alipata, linasema tu: “Akamzaa mwana wake, mzaliwa wa kwanza.” (Luka 2:7) Ndiyo, alikuwa amemzaa mwana “mzaliwa wa kwanza,” kati ya watoto wake saba hivi. (Marko 6:3) Hata hivyo, mwana huyu angekuwa wa pekee. Si eti alikuwa mwana wake mzaliwa wa kwanza tu bali pia alikuwa kwa Yehova “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu!—Wakolosai 1:15.

Sasa simulizi hilo linataja jambo linalojulikana sana: “Akamfunga vitambaa na kumlaza katika hori.” (Luka 2:7) Ulimwenguni pote michezo ya kuigiza, michoro, na mandhari zinazoonyesha kuzaliwa kwa Yesu zinakazia sana tukio hilo. Hata hivyo, fikiria mambo haya ya hakika. Hori ni chombo cha kuweka chakula kwa ajili ya mifugo. Kwa hiyo, familia hiyo ilikuwa ikilala katika zizi ambalo kwa kawaida halina hewa au mazingira safi. Ni wazazi gani ambao wangechagua kumzaa mtoto wao mahali kama hapo ikiwa kungekuwa na mahali bora? Wazazi wengi wanataka kuwapa watoto wao vitu bora zaidi. Basi lazima Maria na Yosefu wawe walitaka kumzaa Mwana wa Mungu mahali bora zaidi!

Hata hivyo, hawakuruhusu hali zao ziwakatishe tamaa; walifanya yote wawezayo. Kwa mfano, ona kwamba Maria alimtunza mtoto huyo na kumfunga kwa vitambaa ili awe na joto, kisha akamlaza kwa uangalifu ndani ya hori ili alale akihakikisha kwamba atakuwa salama. Maria hangeruhusu wasiwasi kuhusu hali yake imkengeushe asimwandalie mtoto wake kilicho bora. Pia, yeye na Yosefu walijua kwamba kumtunza mtoto huyo kiroho ndilo lingekuwa jambo muhimu zaidi ambalo wangeweza kumfanyia. (Kumbukumbu la Torati 6:6-8) Leo, wazazi wenye hekima wanatanguliza mambo ya kiroho wanapowalea watoto wao katika ulimwengu huu uliopotoka.

Ziara Iliyotia Moyo

Kwa ghafula amani ikavurugwa. Wachungaji wa kondoo wakaingia katika zizi wakiwa na hamu ya kuiona familia na hasa yule mtoto. Wanaume hao walikuwa wamesisimuka sana, nyuso zao zikiwa zimeng’aa kwa shangwe. Walikuja haraka kutoka milimani walikokuwa wakiishi na kondoo zao. * Waliwaambia wazazi hao waliokuwa wameshangaa kuhusu jambo la ajabu lililokuwa limewapata. Walipokuwa wakichunga kondoo usiku, malaika alikuwa amewatokea ghafula. Utukufu wa Yehova ulikuwa umemulika pande zote na malaika akawaambia kwamba Kristo, au Masihi alikuwa amezaliwa Bethlehemu. Wangempata mtoto huyo akiwa amelala kwenye hori, akiwa amefungwa vitambaa. Kisha, jambo lenye kupendeza zaidi likatokea. Umati wa malaika ukatokea, wakiimba kuhusu utukufu wa Yehova!

Si ajabu kwamba wanaume hao wanyenyekevu walikuja wakikimbia kuingia Bethlehemu! Lazima wawe walisisimuka sana kumwona mtoto huyo mchanga akiwa amelala hapo kama tu malaika walivyosema. Walieneza habari hizo njema. “Wakasema mambo yaliyokuwa yamesemwa . . . Na wote waliosikia wakastaajabu juu ya mambo waliyoambiwa na wachungaji.” (Luka 2:17, 18) Inaelekea kwamba viongozi wa kidini wa siku hizo waliwadharau wachungaji. Lakini ni wazi kwamba Yehova aliwathamini wanaume hao wanyenyekevu na waaminifu. Hata hivyo, ziara hiyo ilikuwa na matokeo gani kwa Maria?

Bila shaka, Maria alikuwa amechoka sana baada ya kuzaa, hata hivyo, alisikiliza kila neno kwa makini. Lakini si hilo tu: “Maria akaanza kuyahifadhi maneno hayo yote, akikata kauli moyoni mwake.” (Luka 2:19) Kwa kweli, mwanamke huyu alikuwa mtu anayefikiria mambo kwa uzito. Alijua kwamba ujumbe huo kutoka kwa malaika ulikuwa muhimu. Mungu wake, Yehova, alimtaka ajue mwana wake alikuwa nani na alikuwa mtu muhimu. Lakini hakusikiliza tu. Alihifadhi maneno hayo moyoni mwake ili ayatafakari tena na tena katika miezi na miaka ambayo ingefuata. Hilo lilichangia sana katika ukuzi wa imani ya Maria ambayo ilionekana muda wote wa maisha yake.

Je, utafuata mfano wa Maria? Yehova amezijaza kurasa za Neno lake kweli muhimu za kiroho. Hata hivyo, kweli hizo haziwezi kutufaidi tusipozithamini. Tunafanya hivyo kwa kusoma Biblia kwa ukawaida, si kama kitabu tu cha hadithi bali kama Neno la Mungu lililoongozwa na roho ya Mungu. (2 Timotheo 3:16) Kisha, kama Maria, tunahitaji kuyahifadhi mambo ya kiroho moyoni na kujitahidi kuyaelewa vizuri zaidi. Tukitafakari mambo tunayosoma katika Biblia, na kufikiria njia tunazoweza kutumia mashauri ya Yehova zaidi, tutakuza imani yetu.

Maneno Zaidi ya Kuhifadhi

Mtoto alipokuwa na siku nane, Maria na Yosefu walimtahiri kulingana na Sheria ya Musa, na wakamwita Yesu kama walivyoagizwa. (Luka 1:31) Kisha, siku ya 40, walimpeleka kutoka Bethlehemu hadi kwenye hekalu huko Yerusalemu, lililokuwa umbali wa kilomita kadhaa, na kutoa matoleo ya kujitakasa ambayo Sheria iliwaruhusu maskini kutoa, yaani, njiwa-tetere wawili au hua wawili. Hata kama waliaibika kwa sababu hawangeweza kutoa kondoo-dume na njiwa-tetere kama wazazi wengine waliokuwa na uwezo, walipuuza hisia hizo. Vyovyote vile, walitiwa moyo sana walipokuwa huko.—Luka 2:21-24.

Mwanamume mzee anayeitwa Simeoni aliwakaribia na kumwambia Maria mambo zaidi aliyopaswa kuhifadhi moyoni mwake. Alikuwa ameahidiwa kwamba angemwona Masihi kabla ya kufa, na roho takatifu ya Yehova ikamwonyesha kwamba Yesu angekuwa Mwokozi aliyeahidiwa. Pia, Simeoni alimwonya Maria kuhusu uchungu ambao siku moja angehitaji kuvumilia. Alisema kwamba angehisi kana kwamba upanga mrefu umemchoma. (Luka 2:25-35) Hata maneno hayo yenye kuogopesha huenda yakawa yalimsaidia Maria kuvumilia wakati mgumu aliokabili zaidi ya miaka 30 baadaye. Baada ya Simeoni, nabii wa kike anayeitwa Ana alimwona Yesu na akaanza kumwambia kila mtu aliyekuwa na tumaini la kukombolewa kwa Yerusalemu kumhusu Yesu.—Luka 2:36-38.

Yosefu na Maria walikuwa wamefanya uamuzi mzuri kama nini walipomleta mtoto wao katika hekalu la Yehova huko Yerusalemu! Kwa mwana wao, matukio hayo yalikuwa mwanzo wa kwenda kwenye hekalu la Yehova kwa ukawaida. Walipokuwa huko walifanya yote waliyoweza katika utumishi wa Yehova na wakapata maagizo na kutiwa moyo. Bila shaka, siku hiyo Maria alitoka hekaluni akiwa ameimarishwa imani zaidi na moyo wake ukiwa umejaa mambo ya kiroho aliyohitaji kutafakari na kuwaambia wengine.

Ni jambo linalopendeza kuwaona wazazi leo wakifuata mfano huo. Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, wazazi wanawapeleka watoto wao kwa uaminifu kwenye mikutano ya Kikristo. Wazazi hao wanafanya yote wanayoweza, na kuwatia moyo waamini wenzao. Wanatoka katika mikutano hiyo wakiwa na nguvu na furaha zaidi, na wakiwa na mambo mengi mazuri ya kuwaambia wengine. Unakaribishwa kwa moyo mkunjufu uhudhurie mikutano hiyo. Ukifanya hivyo, imani yako itaimarika zaidi kama ile ya Maria.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ona tofauti kati ya andiko hilo na simulizi la safari ya mapema zaidi: “Maria akaondoka . . . akaenda” kumtembelea Elisabeti. (Luka 1:39) Wakati huo, akiwa mwanamke anayechumbiwa ambaye hakuwa ameolewa, Maria angeweza kusafiri bila kumwuliza Yosefu. Lakini baada ya kuolewa, ingawa walisafiri pamoja inasemekana kwamba Yosefu ndiye aliyefanya uamuzi wa kusafiri, si Maria.

^ fu. 14 Ilikuwa kawaida kwa miji kuwa na chumba cha kulala kwa ajili ya wasafiri.

^ fu. 19 Kwa kuwa wachungaji hao walikuwa wakiishi nje na mifugo yao, hilo linathibitisha kile ambacho kinasemwa na kronolojia ya Biblia: Kristo hakuzaliwa Desemba (Mwezi wa 12) wakati ambapo mifugo ingekuwa imefungiwa nyumbani, bali alizaliwa mwanzoni mwa Oktoba.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Simeoni alibarikiwa kwa kumwona Mwokozi aliyeahidiwa