Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ikiwa Adamu Alikuwa Mkamilifu, Angeweza Jinsi Gani Kufanya Dhambi?

Ikiwa Adamu Alikuwa Mkamilifu, Angeweza Jinsi Gani Kufanya Dhambi?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Ikiwa Adamu Alikuwa Mkamilifu, Angeweza Jinsi Gani Kufanya Dhambi?

Iliwezekana kwa Adamu kufanya dhambi kwa sababu Mungu alimuumba akiwa na uhuru wa kuchagua. Zawadi hiyo haikupingana na uhakika wa kwamba Adamu alikuwa mkamilifu. Kwa kweli, ni Mungu tu aliye mkamilifu katika maana kamili. (Kumbukumbu la Torati 32:3, 4; Zaburi 18:30; Marko 10:18) Ukamilifu wa mtu au kitu kingine una mipaka. Kwa mfano, kisu ni kikamilifu kwa kukata nyama, lakini unaweza kukitumia kunywa supu? Kitu ni kikamilifu ikiwa kinatumiwa kwa kusudi linalokifaa.

Basi Mungu alimuumba Adamu kwa kusudi gani? Kusudi la Mungu lilikuwa kwamba Adamu atokeze jamii ya watu wenye akili walio na uhuru wa kuchagua. Wale waliotaka kumpenda Mungu na njia zake wangeonyesha hivyo kwa kuchagua kutii sheria zake. Hivyo, utii haukutiwa ndani ya akili ya mwanadamu bali ungetoka moyoni bila kulazimishwa. (Kumbukumbu la Torati 10:12, 13; 30:19, 20) Hivyo, akiwa mwanadamu aliyepewa uhuru wa kuchagua, ikiwa Adamu angekosa uwezo wa kuchagua kutotii, hangekuwa kamili, yaani, angekuwa asiyekamilika. Biblia inatuambia kwamba Adamu aliamua kutumia uhuru wake wa kuchagua kumfuata mke wake na hivyo akakosa kutii sheria ya Mungu kuhusiana na “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.”—Mwanzo 2:17; 3:1-6.

Basi je, Mungu alimuumba Adamu bila uwezo wa kuchagua kati ya mema na mabaya, hivi kwamba hangeweza kufanya maamuzi mazuri au hangeweza kushinda vishawishi? Kabla ya kutotii kwa Adamu, Yehova Mungu alikuwa amechunguza uumbaji wake wote wa kidunia, kutia ndani wanadamu wa kwanza, na kusema kwamba ulikuwa ‘mzuri sana.’ (Mwanzo 1:31, ZSB) Hivyo, Adamu alipofanya dhambi, Muumba hakuhitaji kusahihisha kasoro fulani ya katika uumbaji lakini kwa kufaa alimlaumu Adamu mwenyewe. (Mwanzo 3:17-19) Adamu hakumtii Mungu kwa sababu alishindwa kuchochewa na upendo wa Mungu na kanuni zinazofaa.

Pia, kumbuka kwamba Yesu alipokuwa duniani alikuwa mwanadamu mkamilifu kama Adamu. Hata hivyo, Yesu, tofauti na wazao wengine wa Adamu, alizaliwa kupitia roho takatifu na hivyo hakuwa na udhaifu ambao ungemzuia asishinde kishawishi. (Luka 1:30, 31; 2:21; 3:23, 38) Kwa kupenda kwake mwenyewe, Yesu alidumu akiwa mshikamanifu kwa Baba yake ijapokuwa alikabili mikazo mingi. Kwa kutumia uhuru wake mwenyewe wa kuchagua, Adamu alipaswa kulaumiwa kwa kukosa kutii amri ya Yehova.

Kwa nini Adamu alichagua kutomtii Mungu? Je, aliamini kwamba angeboresha hali yake kwa njia fulani? Hapana, kwa sababu mtume Paulo aliandika kwamba “Adamu hakudanganywa.” (1 Timotheo 2:14) Hata hivyo, Adamu aliamua kufuata mapendezi ya mke wake ambaye alikuwa ameshachagua kula kutokana na mti uliokuwa umekatazwa. Tamaa yake ya kumpendeza ilikuwa kubwa kuliko tamaa ya kumpendeza Muumba wake. Kwa kweli, alipopewa tunda lililokatazwa, Adamu alipaswa kutua na kufikiria kuhusu matokeo ambayo kutotii kwake kungetokeza katika uhusiano wake pamoja na Mungu. Bila upendo wenye kina kwa Mungu usioweza kuvunjwa, Adamu angeweza kushinikizwa na mtu yeyote, kutia ndani mke wake.

Adamu alifanya dhambi kabla ya kupata watoto, hivyo tangu wanapozaliwa wazao wake wote si wakamilifu. Hata hivyo, kama Adamu tuna uhuru wa kuchagua. Na tuchague kutafakari kwa uthamini kuhusu wema wa Yehova na kusitawisha upendo wenye kina kwa Mungu ambaye anastahili utii na ibada yetu.—Zaburi 63:6; Mathayo 22:36, 37.