Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Kwa nini Wayahudi walianza maadhimisho ya Sabato jioni?

Yehova alipowapa watu wake sheria kuhusu Siku ya Upatanisho, alisema hivi: “Hamtafanya kazi ya aina yoyote siku hiyo . . . Ni sabato ya pumziko kamili kwenu . . . Toka jioni mpaka jioni mtaishika sabato.” (Mambo ya Walawi 23:28, 32) Sheria hiyo ilionyesha kwamba siku ilianza jioni, baada ya jua kushuka, na kumalizika jioni iliyofuata baada ya jua kushuka. Hivyo, kwa Wayahudi, siku ilianza jioni hadi jioni.

Njia hiyo ya kuhesabu siku inafuata kielelezo kilichowekwa na Mungu mwenyewe. Kuhusu siku ya kwanza ya uumbaji ya mfano, simulizi linasema: “Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya kwanza.” “Siku” zilizofuata zilihesabiwa kwa njia hiyohiyo, kuanzia “jioni.”—Mwanzo 1:5, 8, 13, 19, 23, 31.

Si Wayahudi peke yao waliohesabu siku kwa njia hiyo. Waathene, Wafoinike, na Wanumidi walifanya hivyo. Wababiloni nao waliona kuwa siku ilianza jua lilipochomoza, huku Wamisri na Waroma wakihesabu kuwa siku ilianza saa sita usiku hadi saa sita usiku, kama ilivyo leo. Hata hivyo, Wayahudi wa siku zetu bado wanaanza na kumaliza maadhimisho ya Sabato baada ya jua kushuka.

“Safari ya siku ya sabato” ilikuwa umbali gani?

Baada ya kuona Yesu akipaa mbinguni kutoka kwenye Mlima wa Mizeituni, wanafunzi wake walirudi Yerusalemu, “umbali wa safari ya siku ya sabato.” (Matendo 1:12) Msafiri angeweza kutembea umbali wa kilomita 30 au zaidi kwa siku. Hata hivyo, Mlima wa Mizeituni ulikuwa karibu na Yerusalemu. Kwa hiyo, “safari ya siku ya sabato” ilikuwa umbali gani?

Sabato ilikuwa siku ambayo Waisraeli walipaswa kupumzika kutokana na shughuli zao za kawaida. Hata hawakupaswa kuwasha moto ndani ya nyumba zao siku hiyo. (Kutoka 20:10; 35:2, 3) “Endeleeni kukaa kila mmoja mahali pake,” Yehova akaamuru. “Mtu yeyote asitoke mahali pake siku ya saba.” (Kutoka 16:29) Sheria hiyo iliwapa Waisraeli nafasi ya kupumzika kutokana na shughuli za kawaida na kukazia fikira mambo ya kiroho.

Kwa kuwa hawakutosheka na kanuni zilizowekwa na Sheria ya Yehova, marabi wenye kushikilia sana sheria waliweka umbali hususa ambao mtu angeweza kutembea katika siku ya Sabato, kwa mfano, ili kuhudhuria ibada. Kuhusu jambo hilo, kitabu fulani (Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature) kinasema: “Kwa sababu ya sheria kali kuhusu maadhimisho ya Sabato . . . , sheria ziliwekwa ili Mwisraeli yeyote asitembee siku ya Sabato zaidi ya umbali fulani, ulioitwa safari ya siku ya Sabato.” Umbali huo uliwekwa kuwa mikono 2,000, ambao ni kati ya mita 900 hadi kilomita moja.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Yerusalemu kama inavyoonekana kutoka Mlima wa Mizeituni