Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutabiri Kuhusu Masihi

Kutabiri Kuhusu Masihi

Kutabiri Kuhusu Masihi

WAKIJUA kile ambacho Isaya na manabii wengine waliandika kumhusu Masihi, Wayahudi walikuwa wamemtazamia kwa muda mrefu. Kwa kweli, kufikia wakati wa Yesu, Wayahudi wengi “walikuwa wakitarajia” kuja kwa Masihi. (Luka 3:15) Ni muhimu kwamba unabii wa Biblia unatia ndani habari hususa kuhusu maisha ya Masihi. Hakuna mwanadamu yeyote ambaye angeweza kutabiri matukio kama hayo au kupanga ili Yesu apatwe na mambo hayo yote.

Habari Kuhusu Kuzaliwa kwa Masihi. Isaya alitabiri kwamba Masihi, au Kristo, angezaliwa na bikira. Baada ya kuzungumzia hali za kimuujiza kuhusiana na kuzaliwa kwa Yesu, mtume Mathayo aliandika hivi: “Yote haya kwa kweli yalitukia ili litimizwe lile lililosemwa na Yehova kupitia nabii wake, akisema: ‘Tazama! Bikira atapata mimba naye atazaa mwana.’” (Mathayo 1:22, 23; Isaya 7:14) Pia, Isaya alitabiri kwamba Kristo angekuwa mwana wa Daudi, na alimtaja kihususa Yese, baba ya Daudi. Ni kweli kwamba Yesu alikuwa mzao wa Daudi moja kwa moja. (Mathayo 1:6, 16; Luka 3:23, 31, 32) Hivyo, kabla ya Yesu kuzaliwa, malaika Gabrieli alimwambia hivi Maria, mama ya Yesu: “Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake.”Luka 1:32, 33; Isaya 11:1-5, 10; Waroma 15:12.

Habari Kuhusu Maisha ya Masihi. Katika sinagogi huko Nazareti, Yesu akiwa mtu mzima alisoma kwa sauti unabii wa Isaya uliotia ndani maneno haya: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kuwatangazia maskini habari njema.” Akitumia unabii huo kujihusu, Yesu alisema: “Leo andiko hili ambalo mmesikia sasa hivi limetimizwa.” (Luka 4:17-21; Isaya 61:1, 2) Pia, Isaya alitabiri kwamba Yesu angewaponya wagonjwa kwa fadhili, upole, na unyenyekevu. Mathayo anaandika hivi: “Wengi pia wakamfuata, naye akawaponya wote, lakini akawaagiza kwa kusisitiza wasifunue habari zake; ili lipate kutimizwa lililosemwa kupitia nabii Isaya . . . ‘Hatagombeza, wala hatapaaza sauti kubwa . . . Hakuna tete lililovunjika ambalo ataliponda.’”—Mathayo 8:16, 17; 12:10-21; Isaya 42:1-4; 53:4, 5.

Habari Kuhusu Kuteseka kwa Masihi. Pia, Isaya alitabiri kwamba Masihi hangekubaliwa na wengi katika Israeli lakini badala yake wangemwona kuwa “jiwe la kukwaza.” (1 Petro 2:6-8; Isaya 8:14, 15) Na kwa kweli licha ya miujiza mingi ya Yesu, watu “hawakuwa wanamwamini, hata kwamba neno la nabii Isaya likatimizwa ambalo alisema: ‘Yehova, ni nani aliyeliamini jambo ambalo tumesikia?’” (Yohana 12:37, 38; Isaya 53:1) Jambo moja lililowafanya Wayahudi wasimwamini Yesu, ni imani ya uwongo kwamba Masihi angekomboa taifa hilo mara moja kutoka kwa utawala wa Waroma na kurudisha ufalme wa Kidaudi hapa duniani. Kwa sababu Yesu aliteseka na kufa, Wayahudi wengi hawakukubali kwamba alikuwa Masihi. Lakini kwa kweli, Isaya alikuwa ametabiri kwamba Masihi angeteseka kabla ya kuwa Mfalme.

Katika kitabu cha Isaya, Masihi alisema hivi kwa njia ya unabii: “Mgongo wangu niliwapa washambuliaji . . . Uso wangu sikuuficha kutoka kwa mambo yenye kufedhehesha na mate.” Mathayo anaripoti kilichotendeka Yesu alipokuwa akijaribiwa: “Wakamtemea mate usoni na kumpiga ngumi. Wengine wakampiga makofi usoni.” (Isaya 50:6; Mathayo 26:67) Isaya aliandika hivi: “Alijiachilia ateswe; ingawa hivyo hakufungua kinywa chake.” Hivyo, Pilato alipomwuliza Yesu kuhusu mashtaka ya Wayahudi, Yesu “hakumjibu, hata neno moja, hivi kwamba gavana akastaajabu sana.”—Isaya 53:7; Mathayo 27:12-14; Matendo 8:28, 32-35.

Habari Kuhusu Kifo cha Masihi. Unabii wa Isaya uliendelea kutimizwa wakati wa kifo cha Yesu na hata baadaye. Isaya alitabiri hivi: “Atafanya kaburi lake liwe pamoja na waovu, na pamoja na jamii ya matajiri katika kifo chake.” (Isaya 53:9) Unabii huo unaoonekana kama kwamba unajipinga ungetimizwa namna gani? Yesu alipokufa, alitundikwa katikati ya wezi wawili. (Mathayo 27:38) Lakini baadaye, Yosefu wa Arimathea aliyekuwa tajiri aliulaza mwili wa Yesu katika kaburi lake jipya alilokuwa amechimba katika mwamba. (Mathayo 27:57-60) Hatimaye, kifo cha Yesu kilitimiza mojawapo ya mambo muhimu katika unabii wa Isaya. Akizungumza kuhusu Masihi, Isaya anasema: “Mtu mwadilifu, mtumishi wangu, atawaletea watu wengi msimamo wa uadilifu; naye mwenyewe atayachukua makosa yao.” Kwa kweli, kifo cha Yesu kiliandaa fidia ili mzigo wa dhambi uondolewe kutoka kwa watu wote waaminifu.—Isaya 53:8, 11; Waroma 4:25.

Unabii Ulitimizwa Hakika

Ili kumtambulisha Masihi Kimaandiko, mitume na Yesu mwenyewe walinukuu mara nyingi zaidi kutoka katika unabii wa Isaya kuliko vitabu vingine vya Biblia. Hata hivyo, si kitabu cha Isaya tu kilichotabiri kuhusu wakati ujao. Unabii mwingi wa Maandiko ya Kiebrania unatimizwa katika Yesu, Ufalme wake, na mambo mazuri ambayo Ufalme huo utatimiza wakati ujao. * (Matendo 28:23; Ufunuo 19:10) Kulikuwa na uhakika gani kwamba unabii huo ungetimizwa? Yesu aliwaambia wasikilizaji wake Wayahudi hivi: “Msifikiri nilikuja kuharibu Sheria au Manabii [yaani, Maandiko ya Kiebrania]. Sikuja kuharibu, bali kutimiza; kwa maana kwa kweli ninawaambia ninyi kwamba mbingu na dunia zingepitilia mbali upesi zaidi kuliko herufi moja ndogo zaidi au nukta moja ya herufi kupitilia mbali kutoka katika Sheria na mambo yote yasitukie.”—Mathayo 5:17, 18.

Pia Yesu alizungumzia kutimizwa kwa unabii mbalimbali uliohusiana na matukio ya wakati wake na wakati ujao. (Danieli 9:27; Mathayo 15:7-9; 24:15) Isitoshe, Yesu na wanafunzi wake walitabiri matukio ambayo yangetukia baada ya siku zao, kutia ndani mambo yanayotukia leo. Habari inayofuata itazungumzia mambo hayo na unabii mwingine wa Biblia ambao utatimia wakati ujao.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kwa habari zaidi kuhusu unabii uliotimizwa na Yesu, ona kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? ukurasa wa 200, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 4]

“Bikira . . . atazaa mwana”

[Picha katika ukurasa wa 5]

“Uso wangu sikuuficha kutoka kwa mambo yenye kufedhehesha”